Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018

Hon. Prof. Makame Mnyaa Mbarawa

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mkoani

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018

WAZIRI WA MAJI NA UMWANGILIAJI: Mheshimiwa Spika, awali ya yote, napenda kuchukuwa fursa hii kumshukuru sana Mwenyezi Mungu kwa kuniwezesha kusimama mbele yako na kuchangia kwenye hoja hii ya Kamati iliyowasilishwa mbele yetu. Napenda kushukuru sana Kamati yetu kwa kazi nzuri wanayofanya ya kutushauri na kwa kiasi kikubwa Kamati hii imetusaidia sana na tutaendelea kushirikiana nayo kwa maslahi ya Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kama tulivyosikia michango mingi imezungumzwa hapa kuhusu sekta ya maji kwa sababu maji ni jambo muhimu sana na sote tunafahamu maji ni uhai, maji ni afya, kama nilivyosema juzi maji kilimo, maji ni viwanda, maji ni ustaarabu, maji ni kila kitu, bila maji huwezi kufanya jambo lolote.

Mheshimiwa Spika, nitazungumzia kama mambo matano. Jambo la kwanza ambalo Kamati limezungumzia, ni kuhusu huduma ya maji mjini na vijini. Jambo la pili nitazungumzia kuhusu Mfuko wa Maji nitazungumzia na majitaka halafu mwisho nitazungumzia. Miji 25 ambayo inapata wafadhili kutoka Serikali ya India. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kama tulivyoelewa kwenye Ilani ya Chama cha Mapinduzi, imesema waziwazi itapofika mwaka 2020, wananchi wanaokaa kwenye mikoa lazima wapate maji kwa asilimia 95, wanaokaa kwenye miji ya Wilaya lazima wapate maji kwa asilimia 90 na kwenye vijiji lazima wapate maji asilimia 85.

Mheshimiwa Spika, hivi tunavyozungumza, kwa wananchi wanaokaa kwenye vijiji, wanapata maji asilimia 64.8; na hivi tunavyozungumza, miradi takriban 1,652 imekamilika na miradi 500 sasa inaendelea kutekelezwa. Miradi inayotekelezwa sasa hivi, kwa mfano, Mkoa wa Arusha tuna mradi mkubwa pale ambao unagharimu takriban shilingi bilioni 520. Longido tuna mradi mkubwa unagharimu shilingi bilioni 15.

Mheshimiwa Spika, naendelea kwa upande wa Mkoa wa Tabora, Nzega, Igunga, tuna mradi unaogharimu takriban shilingi bilioni 604. Kwa upande Magu, Misungwi na Lamadi, tuna mradi unaogharimu takribani shilingi bilioni 42.6. Mwanza kule maeneo ya milimani tuna mradi unaogharimu shilingi bilioni 39.2. Kama nilivyosema juzi, huko Bariadi tuna mradi unaogharimu takribani shilingi bilioni 491.9; na hapa Dodoma tuna mradi wa maji unaogharimu shilingi takriban bilioni 7.288.

Mheshimiwa Spika, nikitaja miradi ni mingi na sitaweza kuitaja yote, lakini kwa ufupi tu, Serikali tunatumia matrilioni ya pesa kuhakikisha kwamba tunamaliza tatizo la maji katika nchi yetu hii. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kulikuwa na issue ya majitaka. Kweli majitaka miaka ya nyuma ilikuwa siyo kipaumbele, lakini sasa Wizara ya Maji tumeamua kwamba lazima tupambane na tupeleke huduma ya majitaka, kwa sababu ni muhimu na kama tunavyojua majitaka yanaweza kupunguza matatizo mengi kwa mfano, maradhi na mambo mengine.

Mheshimiwa Spika, Dar es Salaam pale tunavyozungumza, tuna miradi miwili ya majitaka, mmoja unagharimu takribani shilingi bilioni 239.3 na mradi mwingine unagharimu shilingi bilioni 149.4; kule Arusha tuna mradi wa maji unagharimu takribani shilingi bilioni 116.99 ambao unaendelea; huko Musoma tuna mradi wa majitaka unagharimu takribani shilingi bilioni 30.

Mheshimiwa Spika, kwa ufupi, katika miradi yetu yote ya maji sasa hivi tunahakikisha component ya majitaka inaingizwa ili kuhakikisha tunaendana na Sera yetu ya maji safi na majitaka.

Mheshimiwa Spika, kulikuwa na hoja nyingine kuhusu Mfuko wa Maji. Tumetengeneza kanuni ambazo zimesema wazi wazi angalau asilimia 65 ya fedha za Mfuko wa Maji lazima ziende vijijini. Kwa sababu vijijini ndiyo kwenye changamoto kubwa sana ya maji. Bila kutatua tatizo la maji huko vijijini, itakuwa hatukuwasaidia Watanzania hasa wanaokaa vijijini. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuanzia mwezi Julai, 2018 mpaka mwezi Desemba, 2018 tumepokea takribani shilingi bilioni 88 za Mfuko wa Maji. Kati ya pesa hizo, shilingi bilioni 61.6 zimekwenda vijijini, yaani asilimia 70; na shilingi bilioni 26.4 asilimia 30 zimekwenda mjini. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, vilevile tumepokea shilingi bilioni 4.73 kutoka pesa za nje kwa ajili ya miradi ya maji. Kwa ujumla, kutoka Julai mpaka Desemba mwaka 2018 tumepokea takribani shilingi bilioni 92.7. Kati ya pesa hizo, Mheshimiwa Pascal aliyosema, kule Jimboni kwake kuna mradi wa maji wa Mloo ambao unajengwa kwa shilingi takribani milioni 465 ambao hivi tunavyozungumza wananchi wanapata maji na Mkandarasi tumemlipa shilingi takriban 265. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuna mradi mwingine wa maji kwenye Jimbo lake vilevile, mradi wa Isaka, Itewe unagharimu takribani shilingi bilioni 1.6 na kila akitoa mgao tunampelekea Mheshimiwa Mbunge kwa kuwa sisi hatuchagui Chama, Watanzania wote ni wamoja na nia yetu ni kuwapelekea Watanzania wote huduma majisafi na salama; kama wako mjini kama wako vijijini, kama wako Chadema au CCM, wote tutawapelekea majisafi na salama.

Mheshimiwa Spika, kulikuwa na issue iliyozungumzwa pia kuhusu madeni makubwa ya Taasisi za Serikali kwa mamlaka. Hili kweli ni changamoto, lakini tumepanga kuanzia sasa hivi, kila tunapopeleka kwenye huduma za maji hizi tunafuatia bili zetu na vile vile tumeamua sasa tuingize vifaa vya kisasa, yaani Pre-paid meter kuhakikisha kwamba kama hukulipa, inapofika mwisho wa mwezi maji yanakatika. Tunaamini tukiweka mfumo huu wa pre-paid meters Wizara zote na Taasisi zote zitaweza kulipa maji au bili za maji bila matatizo.

Mheshimiwa Spika, tunataka kuwekeza kwenye Wizara zote za Serikali; kwenye Mji wa Serikali, Ofisi zote tutaweka pre-paid meters ili tuhakikishe kwamba kama Waziri au Wizara haikulipia maji inakatiwa. Tunaamini tukifanya hivi, kila Wizara italipa bili zake kwa wakati bila kuchelewa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kulikuwa na suala lingine kuhusu taarifa ya mchakato wa kupeleka huduma ya maji miji 26 ambao unafadhiliwa na Benki ya Exim Bank ya India, ambao unagharimu takribani dola za Kimarekani milioni 500 sawa na shilingi za Kitanzania trilioni 1.2. Miji 26 hiyo ni Muheza, Korogwe, Makonda, Pangani, Ifakara, Kilwa Masoko, Makambako, Njombe, Songea, Chunya, Rujewa, Mafinga, Manyoni, Sikonge, Singida, Mpanda, Urambo, Kaliua, na mingineyo.

Mheshimiwa Spika, hatua tuliyofikia sasa hivi, kwanza mchakato ulianza tarehe 17 mwezi wa Nane mwaka 2018; na wakati huo tulitangaza tender. Tender hiyo ilitangazwa huko India na makampuni 10 ya India yaliomba kwa sababu huu ni mradi ambao unafadhiliwa kwa mkopo kutoka India. Mchakato ulifanyika na tukapata makampuni manne; na hivi sasa tumeshafungua zabuni kwa ajili ya kumpata Mkandarasi mmoja. Kesho wataendelea na mchakato wa kupitia Financia Bill kwa ajili ya finally ya kumpata Mkandarasi ambaye ataanza kufanya usanifu na kutengeneza Tender Document kwa ajili ya miji hiyo 26. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Wajumbe wote hawa ama Wabunge wote…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)

SPIKA: Ahsante Profesa.

WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Spika, la mwisho, Waheshimiwa Wabunge wote ambao wana miradi hii ya miji 26 tumetayarisha group la WhatsApp, kila tunalofanya tunawapa taarifa na ninaamini Wabunge wote hawa wanajua nini Serikali inafanya kuhusu miradi hii na tutaendelea kuwafahamisha mpaka pale ambapo miradi hii utakapokamilika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba kuunga mkono hoja, ninai-support sana hoja ya Kamati yangu. Ahsante sana. (Makofi)