Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018

Hon. Luhaga Joelson Mpina

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kisesa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018

WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, nami nishukuru sana kwa nafasi hii ambayo umenipatia ili niweze kuchangia kuhusiana na mapendekezo na maazimio ya Kamati hizi zote mbili. Niipongeze sana Kamati yangu, Kamati ya Kilimo, Mifugo, Maji na Uvuvi kwa kazi nzuri sana waliyoifanya ikiongozwa na Mheshimiwa Mahmood Hassan Mgimwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, utakubaliana na mimi kwamba hata ukisoma tu ripoti yao utajua kwamba hii Kamati ina Mwenyekiti makini na Wabunge makini sana wanaofanya kazi vizuri sana. Niwapongeze sana kwa pongezi walizotupa ukurasa wa 42 kwa kuanzisha Dawati la sekta binafsi kwenye Wizara, tunazipokea pongezi hizo. Dawati hilo limekuwa msaada mkubwa sana kwa wananchi wetu, wazalishaji, wenye viwanda na wafanyabiashara wote na wawekezaji hapa nchini. Pia wamealika vijana wa vyuo vikuu wakiongozwa na Ndugu Peter Nibonye, Rais wa Vyuo Vikuu (TAHLISO) ni mambo mazuri vijana hawa nao waweze kujifunza na kuona jinsi tunavyofanya shughuli zetu humu.

Mheshimiwa Spika, niwashukuru sana Waheshimiwa Wabunge kwa michango yao mizuri sana. Kwa kuanzia nianze kusema kwamba yale mapendekezo na Maazimio ya Kamati yaliyowekwa nakubaliana nayo asilimia 100 na sisi kama Serikali tutayasimamia kuhakikisha kwamba utekelezaji wake unafanyika vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Waheshimiwa Wabunge wengi walipochangia waliniomba na waliniagiza kwenda kutembelea na kukutana na wavuvi hasa katika Ukanda wa Pwani. Napenda tu kusema kwamba nimekubali, nimeandaa ratiba ambayo nitatembelea eneo lote kuanzia Moa hadi Msimbati; kuhakikisha kwamba nakutana na wavuvi wote na kuzungumza nao na kuona changamoto zao na kuzitafutia majawabu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Kamati na Waheshimiwa Wabunge wengi na kwa muda mrefu wamezungumzia sana suala la kufufuliwa kwa Shirika la Uvuvi Tanzania (TAFICO). Nataka niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge kwamba Serikali ya Awamu ya Tano iko kwenye hatua nzuri sana za kulifufua hili Shirika. Moja, tayari mpaka sasa hivi, kama Kamati ilivyozungumza menejimenti tumeiweka, uhakiki wa mali unaendelea ambapo mpaka sasa hivi zaidi ya shilingi bilioni 141, samani, viwanja, maghala, ofisi na nyumba ambazo zilikuwa zinamilikiwa na watu kinyemela na nyingine walikuwa wamejimilikisha tumeshazitaifisha na sasa zimerudi mikononi mwa TAFICO, vitu vyenye thamani ya shilingi bilioni
118. Tunaendelea kwenye maeneo mengine kuhakikisha kwamba assets zote za shirika hili zinarejea.

Mheshimiwa Spika, vilevile tunakwenda kwa kasi kuandaa mipango ya biashara, nayo tunaenda vizuri. Mpaka sasa hivi tayari tumeshapata shilingi bilioni 4.3 kutoka Serikali ya Japan kwa ajili ya kufufua ile miundombinu yetu, kwa maana ya majokofu ya kuhifadhi samaki, gari la barafu, meli moja ya uvuvi na kujenga gati la kuegesha meli za TAFICO, kwa hiyo, tunaenda vizuri sana.

Mheshimiwa Spika, katika huo mpango wetu wa biashara tunaoufanya tunajiandaa kununua meli mbili kubwa ambazo tutaingia kwenye uvuvi wa bahari kuu. Wabunge kwa muda mrefu na mingi sana wamekuwa na kilio kikubwa sana, ya sisi kuingia kwenye maji ya bahari, nataka niwahakikishie Serikali ya Awamu ya Tano tunaingia kuvua katika uvuvi wa bahari kuu na mipango iko vizuri na ndio maana unaona sasa hivi kwa muda mfupi tu tumezipata hizi bilioni 4.3 ambazo zinaturahisishia sana safari yetu kuendelea.

Mheshimiwa Spika, ujenzi wa bandari kama nilivyosema tayari Mtaalam Mwelekezi sasa hivi anafanya anaendelea na zoezi ambalo ni miezi minane tu atakuwa amemaliza suala la upembuzi yakinifu ili tuanze ujenzi wa bandari. Hili nalo limezungumzwa miaka mingi, lakini sasa tunaenda kuanza, rasmi ujenzi wa bandari yetu ya uvuvi.

Mheshimiwa Spika, la nne, Wabunge wengi wamelalamika na nakubaliana nao kabisa, malalamiko yao ni ya haki juu ya viwanda vya kuchakata mazao ya mifugo, viwanda hivyo vingi havipo, ni kweli kabisa nakubaliana nao. Hata hivyo, nataka niwaambie Waheshimiwa Wabunge habari njema za Serikali ya Awamu ya Tano, mipango tuliyonayo, viwanda vingi, tunaenda kuvifufua na sasa hivi ninavyozungumza tunaenda kujenga kiwanda kikubwa sana pale Ruvu. Kiwanda ambacho kitakuwa na machinjio, kiwanda ambacho kitakuwa na uchakataji wa kusindika nyama, kiwanda ambacho kitasindika ngozi, kiwanda ambacho kitasindika mazao ya ngozi, maana yake ukiingiza ngozi mpaka unaenda kutoka na kiatu. Pia tutajenga mnada mkubwa sana wa Kimataifa pale Ruvu na hii mchana Bunge lilipoahirishwa Waziri mwenzangu kwa sababu kiwanda hiki kinajengwa baina ya Kampuni ya NARCO Tanzania na Kampuni ya Misri na fedha zipo. Tunatajia kwamba kuanzia Machi, ujenzi wa kiwanda hiki utaanza, matatizo ya wafugaji wa nchi hii yamefika mwisho. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kiwanda hicho kinajengwa na fedha tunazo. Leo kama ninavyozungumza Waziri mwenzangu wa Mifugo na Uvuvi kutoka Misri tumekutana na tumeazimia kwamba sasa ujenzi uanze kuanzia Machi na kuendelea. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tuna viwanda vingi vinajengwa, kipo Kiwanda kikubwa sana kinajengwa Longido, chenye uwezo wa kuchakata mifugo mingi kwa siku, tuna Tan Choice Kibaha, kinajengwa chenye uwezo wa kuchinja ng’ombe zaidi 1,000 mbuzi zaidi 4,000 na kiko kwenye hatua ya mwisho kukamilishwa, lakini kule Kahama, Chato tunajenga kiwanda kingine.

Mheshimiwa Spika na Waheshimiwa Wabunge napenda niwaambie, Serikali ya Awamu ya Tano, iko kazini, matatizo ya wananchi kukosa soko sasa yamefika mwisho na viwanda hivi, ni tegemeo kubwa sana la uchumi wa nchi yetu ambalo litawawezesha wananchi wetu kuwa na soko la uhakika litawawezesha wananchi wetu kupata manufaa ya mazao haya ya mifugo ambayo muda mrefu wameshindwa kunufaika nayo.

Mheshimiwa Spika, tumeenda tumefanya makubwa ambayo yalikuwa yamesimama kwa muda mrefu, kama uogeshaji wa mifugo, sasa hivi tunaogesha mifugo kila kona, mahali ambapo hawaogeshi mifugo ni mahali tu ambapo hawana josho lakini maeneo yote tumegawa dawa kwenye maeneo yote yenye majosho kwa ajili ya kuweza kuogesha. Kwenye majosho 1,409 yote ninavyozungumza hivi sasa wanaogesha mifugo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tumeazimia kwamba uogeshaji wa mifugo utakuwa ni wa kila siku na Wizara itaendelea kutoa madawa kwa ajili ya uogeshaji. Wafugaji walikuwa wanateswa kuogesha ng’ombe mmoja unadumbukiza unalipa Sh.1,000, Sh.500, Sh.2000 tumesema hapana, watakuwa wanachangia gharama ndogondogo tu ya kujaza maji na kununua zile dawa ndogo ndogo na ng’ombe akiingia majini analipa Sh.50 tu na tutaweka mpaka kwenye Kanuni kwa sababu wafugaji wamedhulumiwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kutokana na hili tatizo kubwa hapa la muda ambalo ninalohangaika nalo, sasa nizungumzie hoja za Waheshimiwa Wabunge, wamezungumza mambo mengi mazuri na hasa pia wakazungumzia suala la doria na wakazungumzia suala la operesheni. Waheshimiwa Wabunge hapa tuelewane, tunazungumza uwekezaji leo, hivi nani anayeweza kuja kwenye uwekezaji kwenye nchi ambayo haiwezi kulinda raslimali zake, hakuna. Nani atakayejenga Kiwanda leo hapa, cha Kusindika Samaki wakati samaki wakati samaki wote wanatoroshwa kwenda nje, bila hata kufata utaratibu unaokubalika, ni nani? Nani atakayekubali kuwekeza kuzalisha vifaranga kuzalisha kuku, kuzalisha ng’ombe wa maziwa katika nchi ambayo maziwa yanatoka nje ya nchi hayana vibali, hayajalipiwa kodi yoyote hayajapimwa ubora na yanauzwa na yanashindana na viwanda vya ndani, nani atakayejenga viwanda hapa nchini.

Mheshimiwa Spika, pia nani atakayejenga viwanda katika nchi ambayo inaruhusu mpaka vitu vilivyokwisha muda wa matumizi, kuuzwa hapa nchini na kushindana na wazalishaji wa ndani, nani atakubali? Ni lazima tukubali, doria zinazoendelea, doria zinazoendelea hapa nchini zinalenga kuwalinda wazalishaji wa ndani ili waweze kuzalisha vizuri. Leo nenda kawaulize wazalishaji wa Viwanda vya maziwa, wameji-commit hata kuongeza uzalishaji kwa sababu kuna ulinzi madhubuti, hakuna mtu anaingiza leo mzaha kutoka nje, mzaha mzaha hapa nchini hakuna.

Mheshimiwa Spika, katika vitu ambavyo nilichukia kuliko vyote, ulikuwa Naibu Spika, lakini wewe ni kiongozi wangu wa muda mrefu nikiwa Mbunge wa kawaida, kitu kilichokuwa kinaniuzi na kupita vyote ni suala hili, watu wanaleta vitu hapa nchini vilivyokwisha muda wa matumizi wamepita njia za panya, halafu Waziri mhusika anakuja kuwasilisha naye analalamika juu ya mambo hayo, wakati yeye ndiyo ana uwezo wa kuwashika. Tutawashika na sisi hatutakubali raslimali zetu kuvuruga wawekezaji wetu hapa nchini. (Makofi)

Mheshimiwa Spika na Waheshimiwa Wabunge, naomba tuungane pamoja tuzilinde hizi rasilimali kwa ajili ya wananchi wetu kwa sababu zikitoweka hata wao hawawezi kunufanika, samaki wakitoweka majini yakabaki maji tu, nani anayewahurumia wavuvi? Mtu ambaye anaruhusu watu wakavue kwa nyavu haramu, halafu baadaye mvuvi anayeenda kuvua kwenye ziwa, anaenda na mafuta yake na gharama kubwa, halafu anarudi bila samaki, nani anayetetea wavuvi, ni yule ambaye analinda mwisho wavuvi wakienda kuvua wakarudi na samaki wengi ili wawe matajiri, ndiyo msingi hasa.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, ninachokitaka nikiseme leo hii kwa Wabunge wenzangu, ni kitu kimoja, zipo baadhi ya changamoto mmezizungumza kwenye sharia nimeziona mimi na wenzangu, ndiyo maana tukaamua kuifumua Sheria ya Uvuvi, Na. 22 ya mwaka 2003 na Kanuni zake za mwaka 2009 ili kukaribisha mwanya wa wananchi wetu wachangie waone mambo yaliyopitwa na wakati tuyaondoe na mimi niko tayari.

Mheshimiwa Spika, nimesema tena kwenye Kanuni kwa sababu uwezo ni wa Waziri wakimaliza kunishauri mambo, nitatengeneza hata task team ya kutengeneza Kanuni haraka ili mambo yanayotukwaza kusonga mbele tuyafute, ili wananchi wetu waweze kunufaika na Sheria zingine ambazo nimeamua tuzifumue ni Sheria ya Hifadhi za Bahari na Maeneo Tengefu, Sheria Na. 29 ya mwaka 1994 ili na yenyewe mambo ambayo yanakwaza wazalishaji, wavuvi wetu, wafanyabiashara wetu na wawekezaji wetu, tuyaondoe pamoja na Sheria za Bahari zote hizi ili kuhakikisha kwamba wananchi wetu tumewaweka vizuri, wanafanya biashara vizuri sana katika maeneo yao. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, vilevile kwenye mifugo nako wameshauri hapa shabaha ya kuwa na tozo za rasilimali za nchi, huwezi ukawa na rasilimali zako hapa zinavunwa, zinaenda nchi nyingine halafu Taifa linaachwa halina chochote, lazima tuweke tozo zinazolingana na thamani ya rasilimali zetu ili zinapozouzwa nje, Taifa linufaike, lakini inapotokea labda tumezidisha sana, ikawa maumivu kwa wafugaji wetu au kwa wafanyabiashara wetu, au kwa wawekezaji wetu, sisi hatuna tatizo, tunakaribisha mawazo yenu, tutafanya review; kama kuna tozo zimezidi upande wa uvuvi au mifugo tutazi-regulate. Lengo letu, ni kuhakikisha kwamba hawa wafugaji wetu wanafuga vizuri, lakini na hawa wavuvi wanavua vizuri na wafanyabiashara na wawekezaji katika eneo hili wanafanya biashara vizuri, lakini bila kuyasahau maslahi ya Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa nafasi uliyonipa. (Makofi)