Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Azimio la Bunge la Kuridhia Ubadilishaji Hadhi Mapori ya Akiba ya Biharamulo, Burigi, Kimisi, Ibanda na Rumanyika – Orugundu kuwa Hifadhi za Taifa

Hon. Amina Saleh Athuman Mollel

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Azimio la Bunge la Kuridhia Ubadilishaji Hadhi Mapori ya Akiba ya Biharamulo, Burigi, Kimisi, Ibanda na Rumanyika – Orugundu kuwa Hifadhi za Taifa

MHE. AMINA S. MOLLEL: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. Awali ya yote, naipongeza Serikali kwa umamuzi wake wa busara kwa kuleta Azimio hili katika kuyabadilisha Mapori haya ya Akiba ya Biharamulo, Burigi, Kimisi, Ibanda na Rumanyika pamoja na Orugundu kuwa sasa Hifadhi za Taifa. Kwa maana hiyo basi Hifadhi za Taifa zitaongezeka kutokana na upandishwaji wa mapori haya.

Mheshimiwa Spika, naomba nitaje faida zitakazopatikana kutokana na hifadhi hizi zilizoanzishwa. Kwanza kabisa, pato litakalopatikana litaongezeka katika pato la Taifa na vilevile ajira zitapatikana na hivyo vijana wanaoishi katika maeneo yale kwa namna moja au nyingine itawasaidia sana hasa katika zile kazi kwa mfano za kuongoza watalii na shughuli nyingine mahoteli yatakapojengwa wataweza kupata hizo ajira.

Mheshimiwa Spika, miradi ya ujirani mwema inayotekelezwa na TANAPA na nichukue fursa hii kumpongeza Mkurugenzi wa TANAPA kwa jinsi ambavyo wanatekeleza sera ya ujirani mwema. TANAPA wamekuwa wakisaidia wananchi wanaoishi maeneo majirani na hifadhi zetu kwa kujenga hospitali na kuboresha miundombinu ya elimu katika maeneo haya. Kwa hiyo, niwapongeze sana TANAPA. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, uwepo wa Uwanja huu wa Ndege ambao kwa kweli kwa muda mrefu umekuwa ukizungumzwa sasa tunaona busara za Mheshimiwa Rais wetu kwa kuona mbali kwamba sasa watalii wataweza kufika kwa haraka zaidi pale na kuweza kutembelea hizi hifadhi zetu. Tunafahamu Geita imebarikiwa na Mwenyezi Mungu kuwa na madini, kwa hiyo, wawekezaji wataweza kufika kwa urahisi zaidi. Madini haya pia yataweza sasa kutangazwa kwa undani zaidi kutokana na hifadhi hizi kwa hiyo wawekezaji wengi watapenda kwenda kule kuwekeza mahoteli na miradi mbalimbali. Kwa hiyo, kwa kweli tunaona kabisa kwamba Geita itakwenda kubadilika lakini na maeneo mengine jirani na uwanja huu sasa ndiyo utakaokuwa chachu kubwa ya maendeleo. Vilevile uanzishwaji wa hifadhi hizi kutachangia utunzaji wa mazingira. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niende tu haraka katika kuishauri Serikali kwa sababu tunafahamu kwamba faida ni nyingi. Hivi karibuni Mheshimiwa Waziri Mkuu alizindua channel ya kutangaza utalii Channel ya Safari pale TBC na Waheshimiwa Mawaziri walikuwepo. Kwa hiyo, sasa ni wakati muafaka kabisa wa kuitumia hii Safari Channel kuweza kutangaza utalii wetu na hasa hifadhi hizi mpya ili wananchi waweze kutambua na kupata ule muamko wa kwenda kutembelea hifadhi zetu. Kwa maana kwamba wananchi watakapokwenda kutembelea hifadhi hizi, kwanza ni njia mojawapo ya kupunguza msongo wa mawazo unapokwenda kule unasahau mengine na kuona utalii uliopo kule. Kwa hiyo, nashauri sana kuitumia hii channel ili iweze kutagaza huo utalii wetu.

Mheshimiwa Spika, wito wangu vilevile wananchi wanaoishi maeneo jirani na hifadhi hizi kuona kwamba wao ndiyo wanakuwa chachu ya kutunza mazingira na kuhifadhi hifadhi hizi.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)

SPIKA: Ahsante sana Mheshimiwa Amina.

MHE. AMINA S. MOLLEL: Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja hii, Mungu ibariki Tanzania, Mungu mbariki Rais wetu, bariki Baraza la Mawaziri, wewe mwenyewe Spika na Watanzania wote kwa ujumla. A Luta continua, mapambano bado yanaendelea. (Makofi)