Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Masuala ya UKIMWI kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018

Hon. Susan Anselm Jerome Lyimo

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Masuala ya UKIMWI kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018

MHE. SUSAN A.J. LYIMO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipatia nafasi ili niweze kuchangia katika hoja hizi muhimu kimsingi ndiyo ambazo zinaleta maendeleo katika jamii zetu.

Mheshimiwa Spika, nianze kwa kusema kwamba kuna mtaalam mmoja ambaye alikuwa Rais wa Chuo Kikuu cha Harvard, alisema hivi: “if education is expensive, try ignorance”. Huyu siyo mwingine bali Derek Bok.

Mheshimiwa Spika, tuko hapa kwa sababu ya elimu, kama elimu yetu ni mbovu hatutapata wataalam na vyovyote vile hatutakuwa na maendeleo. Nimesikia kilio cha watu wengi na mimi siku zote nasema elimu ni mwalimu. Tumeshuhudia jinsi gani tumekuwa na upungufu wa walimu hususani walimu wa sayansi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, utakubaliana nami kwamba bila sayansi hatuwezi kwenda kwenye uchumi wa viwanda. Pamoja na kwamba tuna upungufu mkubwa wa walimu tukawa na lile zoezi la kupunguza walimu wa sekondari hasa wa masomo ya sanaa kwenda kwenye shule za msingi, nakubaliana nao kwamba elimu ya msingi ndiyo msingi kama pale hakuna mwalimu kabisa itakuwa matatizo lakini zoezi lile liligubikwa na matatizo makubwa na wengine wakarudishwa tena kwenye sekondari kutokana labda na fedha au sielewi ilikuwa nini?

Mheshimiwa Spika, nachotaka kuzungumza na hata ukiangalia Goal Na.4 la Sustainable Development linalozungumzia elimu bora, sawa na shirikishi kwa wote, unaona wazi kwamba lengo hili litakuwa vigumu sana Tanzania kulifikia kwa sababu ya tatizo kubwa la walimu, vilevile mazingira ya kufundishia. Hili linajionyesha kwa matokeo ya mitihani tuliyoyapata juzi.

Mheshimiwa Spika, tunajua kwamba Tanzania tuna shule za vipaji maalum, shule za kata na shule za binafsi. Nitoe tu analysis kidogo kwa sample ya shule tatu, tatu; shule za Serikali kwa maana ya shule za kata na shule za binafsi. Wewe mwenyewe unajua kwamba wanaopata division four na division zero siyo rahisi kabisa kuendelea na elimu inayofuata.

Mheshimiwa Spika, nimechukua shule za tatu za binafsi ambazo zina jumla ya wanafunzi 236. Katika hizi shule tatu za binafsi waliopata division one ni 223 sawa na asilimia 95; waliopata division two ni 12 sawa na asilimia tano na waliopata division three ni mmoja sawa na asilimia 0.6, kwa hiyo, ukiangalia hawa wote wataendelea. Ukija kwenye shule za kata kwa hiyo sample niliyochukua, katika shule tatu zenye jumla ya wanafunzi 368 waliopata division zero na four ni 297, sawa na asilimia 80 na waliopata division one mpaka three ni wanafunzi 79 sawa na asilimia 20. Kwa hiyo, unakuta kwamba kundi hili linakuwa ni la wasindikizaji.

Mheshimiwa Spika, niishauri Serikali nini cha kufanya. Ni kweli elimu bure imekuja na changamoto nyingi, wanafunzi wamekuwa wengi lakini sasa nini cha kufanya kwa sababu hatuwezi kuacha hali hii iendelee. Naishauri Serikali iendelee kuboresha miuondombinu kwa sababu unakuta shule hizo hizo za kata za Serikali ndiyo hizo hizi hazina walimu wa kutosha lakini kuna suala la chakula watoto hawa nao hawapati chakula shuleni. Kwa hiyo, unakuta nyumbani anatoka kwenye familia maskini hana chakula, anafika shule nako hamna chakula, ukilinganisha na wale wa binafsi unakuta tofauti ni kubwa sana. Kwa hiyo, naomba sana kwa sample hii na Mheshimiwa Waziri anajua tuone ni jinsi gani ya kuwasaidia watoto hawa wanaosoma kwenye shule za kata kwa sababu nao wanastahili kupata elimu kama wanayopata wengine. Hilo la kwanza. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini ukija hata kwenye shule zile ambazo tunaziita special schools, unakuta kwamba shule ya kwanza ya special schooI Ilboru imekuwa shule ya 36. Zile nyingine za Tabora na kadhalika unakuta ziko kati ya hizo 100 bora wala haziko kwenye 50 bora. Kwa hiyo, nadhani kuna haja pia kama hizi ni special schools na tunaamini wanaokwenda kule ni wale waliofaulu vizuri sana darasa la saba basi wawekewe mazingira ambayo kweli yanafanya wawe special kuliko wale wengine. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nirudie tena kusema kwamba kwa kuwa elimu ni mwalimu naomba maslahi ya walimu yaboreshwe, wapandishwe madaraja, wapate mishahara yao kwa wakati lakini na yale maslahi yao mengine pia wayapate. Kama ambavyo amesema Mheshimiwa Mwijage unaweza ukasomea chini ya mti au kwenye nyasi lakini kama una mwalimu bora, mwalimu mahiri utafaulu tu kuliko kusoma kwenye shule zenye AC lakini hakuna walimu au walimu waliopo hawafai. Kwa hiyo, naomba muwekeze zaidi kwa walimu ili tuweze kuboresha elimu yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nizungumzie suala la Bodi ya Mikopo. Ni kweli kwamba Bodi ya Mikopo imeendelea kutoa mikopo kwa wanafunzi wengi zaidi lakini bado kuna tatizo kubwa la urejeshwaji. Pamoja na urejeshwaji naomba sana Mheshimiwa Waziri na Serikali kwa ujumla inisikilize, kuna wanafunzi waliokuwa wanasoma kwenye vyuo ambavyo TCU iliwaondoa, wamepelekwa kwenye vyuo vingine, mpaka leo napozungumza hawajapata mikopo yao. Kuna waliokwenda SAUT zaidi ya wanafunzi 100 hawajapata kabisa na hawa ni wanafunzi ambao wanasomea ualimu. Pamoja na vyuo vingine lakini hiyo particularly nina majina ya wanafunzi, naomba sana Serikali ifuatilie ili wanafunzi hawa wapate mikopo yao. Haiwezekani kwa miezi minne, mitano kuanzia Novemba walipohamishwa mpaka leo hawajapata single cent na hawa wanastahili mikopo yao. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nataka kuoanisha suala la walimu wa sayansi na COSTECH. Nakumbuka kwamba tulikubaliana ndani ya Bunge hili au kwa sheria, sikumbuki vizuri lakini ilikuwa 1% ya GDP iende COSTECH ili kusaidia uvumbuzi na watoto wetu wanaosoma masomo ya sayansi. Cha ajabu hela hiyo haiendi na hata kile chanzo kingine walichokuwa wanakitegemea wamekuja kwenye Kamati wamesema nacho kimeondolewa. Kwa hiyo, leo tunapozungumza hata watoto wakiwa wabunifu namna gani kama COSTECH haina fedha maana yake tutakuwa tunacheza danadana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nakubaliana na Mheshimiwa Profesa Maghembe alivyosema kwamba hisabati ni jambo la muhimu sana. Ndiyo sababu wanafunzi wanaosoma sayansi wakimaliza form six amepata labda ‘A’ zote inakuwa rahisi kwenda vyuo vikuu kusoma masomo yoyote hata ya Arts. Tuli-test Chuo Kikuu cha Dar es Salaam mwaka 1998, waliosoma PCM wakaja kusoma Law na wakafaulu vizuri sana lakini huwezi mtu wa Arts au tunaita Nguin ukasome sayansi, haiwezekani. Kwa hiyo, ni vyema tukawekeza kwenye sayansi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, inasikitisha, hili ni jambo la ajabu sana, tumeambiwa kwamba Bodi ya Mikopo asilimia 66 ya wanafunzi hawa ni Nguin per-se. Kwa hiyo, kama hiyo asilimia nyingine 30 inakwenda kwa wale accountant na mainjinia au natural sciences then tuna tatizo kubwa sana kwamba ni asilimia 30 tu na hiyo 30 sasa labda natural science inaweza ikawa asilimia 10 au 15 halafu tunategemea tutakuwa na Taifa la viwanda, haiwezekani. Nadhani ni muhimu sana kuwekeza kwa walimu wa sayansi. Hili ni tatizo kubwa kwa sababu hatujawekeza kwenye walimu wa sayansi lakini pia hatuna hata vitendeakazi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pamoja na kwamba Sera ya Elimu inazungumzia masuala ya vitendeakazi, jambo la ajabu…

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. SUSAN A.J. LYIMO: Mheshimiwa Spika, mimi ni dakika 10, hazijakwisha bado.

SPIKA: Hiyo ni kengele ya pili, malizia tu hiyo.

MHE. SUSAN A.J. LYIMO: Mheshimiwa Spika, jambo linaloshangaza, sasa hivi vitendeakazi (teaching aids) walimu wamekuwa wagunduzi kweli kweli, wanatumia miili yao kufundishia wanafunzi. Mimi nimeshangaa na hii itasababisha matatizo huko baadaye kwa sababu Mwalimu anamfundisha mtoto …

SPIKA: Mheshimiwa Susan inabidi uwe makini kidogo.

MHE. SUSAN A.J. LYIMO: Mheshimiwa Spika, kama unamfundisha mwanafunzi kuandika tano kwa kiuno watoto wa darasa la tatu, la pili, hili ni tatizo kubwa sana. Hii inaonyesha kwamba Serikali haina fedha ya kuwasaidia walimu kuwapa teaching aids. Naomba sana wasaidiwe kwa sababu utamuona mtoto wako anakuja nyumbani anatikisa kiuno unadhani ameshaanza mahusiano kumbe…

SPIKA: Hiyo tano inaandikwaje Mheshimiwa Mbunge. (Kicheko/Makofi)

MHE. SUSAN A. J. LYIMO: Mheshimiwa Spika, ningekuwa nimevaa suruali ningekuonesha. (Kicheko)

SPIKA: Ahsante sana Mheshimiwa, dakika zako zimekwisha.

MHE. SUSAN A. J. LYIMO: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana. (Makofi)