Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Masuala ya UKIMWI kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018

Hon. Jerome Dismas Bwanausi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Lulindi

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Masuala ya UKIMWI kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018

MHE. JEROME D. BWANAUSI: Mheshimiwa Spika, kwanza nianze kukushukuru kwa kunipa nafasi na mimi nichangie hotuba za hizi Kamati ambazo zimewasilishwa hapa. Nianze tu kwa kumpongeza Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Magufuli kwa jinsi anavyofanya kazi na kwa kweli ni mfano wa Marais bora katika Afrika ambao wanafanya kazi nzuri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nianze kwenye afya, pongezi hizi ambazo nimempongeza Mheshimiwa Rais na sisi sote hapa pande zote mbili, upande wa Chama Tawala na wale wenzetu wa Upinzani ni mashahidi kwamba katika miaka ya nyuma haijawahi kutokea tukaweza kutenga fedha kwa ajili ya hospitali 67 na vituo vya afya 350. Hii haijawahi kutokea, tunahitaji kumpongeza Mheshimiwa Rais na Serikali ya Awamu ya Tano kwa kazi nzuri inayoifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kama walivyochangia wengine haya majengo tunayoyajenga, hospitali 67 na vituo vya afya 350, kama havikupata watumishi, kwa kweli vituo hivi vitabaki kama white elephant, yatabaki majengo ambayo hayana tija. Nisisitize sana wanaohusika na maandalizi ya kuwapata watumishi wa Idara ya Afya waweze kufanya jambo hili kwa haraka sana ili tuweze kupata tija katika eneo hili.

Mheshimiwa Spika, pia niiombe tu Serikali, sisi wa Mkoa wa Mtwara kuna ujenzi unaoendelea wa Hospitali ya Rufaa lakini unasuasua sana. Nipongeze kazi kubwa anayofanya Mheshimiwa Waziri Ummy na Naibu wake ndugu yangu Mheshimiwa Dkt. Ndungulile, mnafanya kazi kubwa sana na wala hatuna mashaka na utendaji wenu wa kazi lakini naomba sana mlitupie macho suala la ujenzi wa Hospitali ya Rufaa pale Mtwara. Kwa sasa wananchi wa Mkoa wa Mtwara na Lindi wakihitaji kumpeleka mgonjwa katika Hospitali ya Rufaa wanawajibika kuja Dar es Salaam. Kwa hiyo, naomba sana hili jambo lipewe kipaumbele, najua Mheshimiwa Waziri atakapokuja kutoa mchango wake ataeleza kuhusu jambo hili. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lingine ambalo nilitaka kusema, ni kweli huu utaratibu wa Serikali tuliouanzisha wa kuwaondoa watumishi kwa mfano wa kilimo, maji na ardhi na kuwapeleka kwenye Serikali Kuu ni mzuri. Jambo hili ni jema kwa sababu inawezekana likawa linasaidia kuweka udhibiti wa watumishi wetu. Hata hivyo, kwa maana ya uwakilishi (Madiwani na Wabunge), nikubaliane na hoja na Mheshimiwa Mwamoto kwamba kweli tulipitisha hapa hizo sheria lakini kuna wakati mwingine unaweza ukakuta liko jambo ambalo lina umuhimu sana.

SPIKA: Waheshimiwa wenye kikao pale, nawaombeni sana.


MHE. JEROME D. BWANAUSI: Mheshimiwa Spika, napendekeza Usirudishwe utaratibu wa zamani wa kwamba kila jambo linaongelewa kwenye Baraza lakini lazima kuwe na baadhi ya vikao hata kama ni kwa miezi sita au kwa mwaka ambavyo vitafanyika kwenye Halmashauri ambapo mchango wa Waheshimiwa Madiwani na Wabunge kuhusu barabara, maji na kilimo unaweza kupewa umuhimu. Kwa sababu kama wataachiwa tu watendaji peke yao wakafanya maamuzi sasa ule uwakilishi wa wananchi kutoka kwenye ngazi mbalimbali hautakuwa na maana kabisa. Kwa hiyo, hili naomba sana litazamwe Serikalini na tuone mfumo gani mzuri utakaosaidia kuhakikisha kwamba na wale wawakilishi wa wananchi wanapewa fursa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, limezungumzwa pia suala la TARURA kwenye Kamati ya TAMISEMI na mimi naunga mkono kabisa yote yaliyomo katika taarifa ya Kamati ile. Hata hivyo, kama TARURA haikupata fedha za kutosha, watu watakuja kusema afadhali ya Halmashauri kuliko TARURA. Kwa hiyo, ni muhimu sana kwenye bajeti ijayo TARURA wapate fedha za kutosha. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tuna tatizo kubwa sana la barabara vijijini na madaraja ambayo yanahitaji kujengwa lakini kwa fedha wanazopata TARURA hawawezi kujenga madaraja hayo kabisa. Kwa hiyo, ni vizuri sana TARURA iweze kupata fedha za kutosha ili washirikiane na TANROADS kuhakikisha kwamba suala la barabara na madaraja linapewa kipaumbele.

Mheshimiwa Spika, jambo lingine ambalo ni muhimu sana ni juu ya kuziwezesha Halmashauri zetu zijiendeshe zenyewe. Hali kwenye baadhi ya Halmashauri ni mbaya sana na nitatoa mfano wa Halmashauri yangu ya Wilaya ya Masasi na Halmashauri nyingi ambazo zaidi ya asilimia 80 ya mapato yake zinategemea kutokana na ushuru wa korosho, hali ni mbaya sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Waheshimiwa Madiwani hawajapata posho zao za mwezi sasa takribani miezi nane hata posho za vikao hazijatolewa na miradi mbalimbali hakuna kinachofanyika. Bahati nzuri Mheshimiwa Waziri Mkuu ameshalieleza kwamba Serikali ipo kwenye mpango sasa wa kuhakikisha kwamba ushuru wa korosho kwa ajili ya Halmashauri unapelekwa, kwa kweli fedha zile zinahitajika zipelekwe haraka sana ili kunusuru hali ya Halmashauri zetu ambazo hivi sana hali ni mbaya kuliko maelezo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo lingine ambalo napenda kusisitiza ni kwenye Kamati ya UKIMWI. Wafadhili wetu wamekuwa wakitusaidia sana kwenye eneo hili lakini baadhi ya wafadhili wetu wamekuwa wakijiondoa taratibu katika kuchangia kwenye janga hili la UKIMWI. Niiombe Serikali sasa ione uwezekano wa kuanza kutenga fedha zetu za ndani ili zisaidie katika kupambana na janga hili. Kama hatuwezi kutenga fedha zetu za ndani itatusumbua sana mbele ya safari pale wafadhili wetu watakuwa wameachia kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ili kulinda muda wako, niunge mkono hoja za Kamati zote zilizowasilishwa, nakushukuru kwa kunipa nafasi. (Makofi)