Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Masuala ya UKIMWI kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018

Hon. Stella Ikupa Alex

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Masuala ya UKIMWI kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018

NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, WENYE ULEMAVU: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipatia nafasi hii. Awali ya yote nimshukuru sana Mwenyezi Mungu kwa ajili ya kila mmoja wetu aliyeko mahali hapa. Pia nitumie nafasi hii kuwapongeza sana Wenyeviti wa Kamati zote waliowasilisha taarifa zao leo na kipekee kabisa nitumie nafasi hii kumpongeza Mwenyekiti na Makamu Mwenyekiti pamoja na wajumbe wote wa Kamati ya Kudumu ya Masuala ya UKIMWI.

Mheshimiwa Spika, pia naomba nitumie nafasi hii kumpongeza sana Mheshimiwa Rais wetu mpendwa, Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli. Naendelea kumpongeza kwa sababu ya haya mengi ambayo anaendelea kuyafanya katika nchi yetu ambayo yanatupelekea kuwa Tanzania ya kujitegemea. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, katika maoni ya Kamati ya Masuala ya UKIMWI maeneo mengi imeshauriwa kwamba kama Serikali tuweze kujitegemea kwenye masuala ya UKIMWI. Kwa hiki anachokifanya Mheshimiwa Rais anatupeleka kwenye Tanzania ambayo baadaye tutaweza kuwa ni watu wa kujitegemea. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba nichangie katika maeneo yafuatayo:-

Mheshimiwa Spika, kwanza kabisa naomba nichangie katika eneo la mashirikiano kati Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika eneo la mapambano dhidi ya dawa za kulevya. Niseme tu kwamba ushauri wote ambao umetolewa na Kamati hii ya Masuala ya UKIMWI umepokelewa, lakini naomba nitoe ufafanuzi kidogo. Naomba nilihakikishie Bunge lako Tukufu kwamba kuna mashirikiano mazuri kabisa kati ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika mapambano ya dawa za kulevya kwa njia gani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, upande wa Zanzibar tuna Tume, lakini upande huu wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano tuna Mamlaka. Kwa hiyo hii Mamlaka inashirikiana vizuri kabisa na Tume ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya ya Zanzibar, kuna vikao mbalimbali ambavyo vimekuwa vikifanyika vya Baraza la Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya, Tume imekuwa ikishiriki kikamilifu kabisa. Hata hivyo, pia kumekuwa na jumbe mbalimbali ambazo zinatoka Tanzania kwenda Kimataifa katika eneo hili la madawa ya kulevya. Tume pia imekuwa ikishirikishwa vizuri kabisa.

Mheshimiwa Spika, hivi tunavyozungumza sasa hivi, Tume ya Zanzibar ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya, iko katika mchakato wa kufanya mabadiliko na kuwa Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya. Sambasamba na hilo, Tume pia iko katika mchakato na harakati za mwisho kabisa za kufanya marekebisho ya Sheria ya Kupambana na Dawa za Kulevya ili sasa ile Sheria ya upande wa Zanzibar iweze kufanana na Sheria ya upande wa Tanzania Bara. Ni kwa nini tunafanya hivyo, kwa sababu ilionekana kwamba kuna gape kidogo kati ya upande wa Tanzania Bara na upande wa Tanzania Zanzibar. Kwa hiyo marekebisho hayo yakishafanyika ina maana kwamba sasa udhibiti wa dawa za kulevya utaenda vizuri kabisa.

Mheshimiwa Spika, vile vile kulikuwa na hoja ya kwamba hatuna Sera ya Udhibiti wa Dawa za Kulevya. Ni kweli sera hii haipo, lakini, Tume iko katika hatua za mwisho kabisa za kuandaa huu mchakato wa Sera ya Taifa ya Kudhibiti Dawa za Kulevya. Katika hili pia kwa sababu Serikali yetu, Serikali ambayo inapenda ujumuishi, iliandaa utaratibu mzuri kabisa wa kukusanya maoni na walijiwekea kwamba watakusanya maoni kutoka kwa Wadau wapatao 120, lakini pia kutoka kwenye Kanda zetu zote tano. Mpaka sasa hivi ninavyozungumza tayari tumekwishakusanya maoni kutoka kwenye kanda nne bado kanda moja. Tukishakamilisha kanda zote tano, watakaa chini na ku-compile maoni haya na hatimaye utaratibu wa kupatikana kwa sera utaendelea(Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba pia nichangie katika eneo la kukinzana kwa Sera Mipango na Sheria mbalimbali za UKIMWI, lakini pia kuna mapendekezo ya Kamati ambayo yametolewa kwamba Sheria ifanyiwe mapitio. Niseme kwamba ushauri huu mzuri kabisa umepokelewa, lakini sambamba na hilo, naomba nitoe ufafanuzi kidogo, Serikali kupitia Wizara husika, Wizara ya Afya tayari imekwishaandaa mapendekezo ya marekebisho ya Sheria Na. 28 ya mwaka 2008. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, katika mapendekezo haya ya mabadiliko ya Sheria, kuna baadhi ya vifungu ambavyo vitafanyiwa marekebisho. Vifungu hivi ni kifungu cha 13, 15, pamoja na 27. Katika kifungu cha 13 kinaongelea upimaji wa VVU, katika vituo ambavyo vimethibitishwa. Katika mapendekezo ya Sheria yanasema kwamba sasa hivi upimaji wa VVU uwe ni kwa hiyari lakini mtu aruhusiwe kujipima mwenyewe mahali popote alipo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, katika hili tunaamini kwamba tutapata matokeo mazuri ya ile 90 ya kwanza, kwa sababu inaonekana kwamba katika ile 90 ya kwanza tupo nyuma kidogo tofauti na ile 90 ya pili, ambayo tumefikia asilimia 91 na ile 90 ya tatu ambayo tumefikia asilimia 87.

Mheshimiwa Spika, sambasamba na hilo, pia kuna mapendekezo kwenye umri wa kuweza kupima virusi vya UKIMWI kwa hiari bila ridhaa ya mzazi. Katika sheria yetu, kifungu cha 15(2) kilikuwa kinalazimisha mtu anayepima UKIMWI awe ni yule mtu ambaye anakuwa na umri wa miaka 18 na kuendelea ambapo hapo sasa anakuwa anapima mwenyewe kwa hiari yake bila ridhaa ya mzazi lakini chini ya hapo mtu alikuwa haruhusiwi kupima mwenyewe.

Mheshimiwa Spika, sasa hivi sheria inapendekeza kwamba umri wa mtu kupima kwa hiari bila ridhaa ya mzazi/ mlezi uwe ni miaka 15. Tumesikia Waheshimiwa Wabunge wengi wameliongelea hilo na Serikali yenu sikivu imelisikia na muda siyo mrefu mapendekezo haya yataletwa mbele ya Bunge lako Tukufu ili Waheshimiwa Wabunge waweze kuyafanyia kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia kuna kifungu kingine ambacho pia kinatarajiwa kufanyiwa marekebisho, kifungu cha 27 ambacho kinaelezea adhabu ya kosa la mtu ambaye anatangaza tiba ya UKIMWI kinyume cha sheria. Mwanzoni adhabu ilikuwa ni shilingi milioni moja ama kifungo cha miezi sita lakini sasa hivi inapendekezwa kwamba adhabu iwe shilingi milioni milioni tano au kifungo cha miaka mitatu.

Mheshimiwa Spika, pia kulikuwa na suala la mahusiano kati ya shughuli za kiuchumi na ongezeko la maambukizi ya UKIMWI sanasana kwenye maeneo yale ambayo yanakuwa na msongamano mkubwa ama sehemu za miradi mbalimbali kama barabara, migodini na sehemu nyingine. Pamoja na elimu ambayo inatolewa, Serikali pia imeenda mbali zaidi kwa kutoa dawa kinga kwenye maeneo haya ili kuhakikisha makundi haya yanaendelea kuwa salama. Dawa kinga hii ni Pre-exposure Prophylaxis ambayo inasaidia kwa makundi haya ili yasiweze kuambukizwa na magonjwa ya VVU.

Mheshimiwa Spika, katika jitihada hizo tumefika mbali kwa sababu tulianza kutoa dawa hizi mwezi Machi, 2018 kwa pilot ya mikoa tisa. Machi 2018 mpaka Septemba, tulikuwa tumeshafikia mikoa tisa lakini malengo yetu ilikuwa ni kufikia watu wapatao 16,000 na ndani ya mikoa tisa tulikuwa tumeshafikia watu 9,000. Kuanzia Oktoba tuliongeza mikoa mingine 12 na kufanya jumla ya mikoa kuwa 21. Tunategemea kabisa tutavuka lengo kwa sababu katika mikoa tisa tulikuwa tumefikia watu 9,000 lakini katika mikoa hii mingine iliyoongezeka tunategemea kwamba tutaenda kuvuka lengo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sambamba na hilo, kuna suala la Mfuko wa UKIMWI wa Taifa ambao huu unatupelekea kuondokana na ile dhana ya kutegemea wafadhili. Mfuko huu unafanya vizuri sana ambapo mwaka 2017 tuliweza kununua dawa za Septrin zenye gharama ya shilingi milioni 660. Pia kwa mwaka huu umeidhinishiwa kiasi cha shilingi milioni 455 ambayo inaenda kununua hizi dawa za Septrin. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa sababu ya muda na mimi naomba niunge mkono hoja za Kamati zote hizi tatu ambazo zimewasilisha taarifa mbele ya Bunge lako Tukufu. (Makofi)