Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Sheria Ndogo kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018

Hon. Timotheo Paul Mnzava

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Korogwe Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

3

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Sheria Ndogo kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018

MHE. TIMOTHEO P. MNZAVA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi. Awali ya yote, nitumie nafasi hii kukupongeza wewe na viongozi wengine wote wa Bunge kwa namna mnavyotuongoza. Pia nitumie nafasi hii kuzipongeza sana Kamati zote mbili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukisoma taarifa hizi za Kamati kwenye uchambuzi wao, ukasoma maoni na mapendekezo ya Kamati zote, unaona kabisa kwamba Wajumbe wa Kamati hizi wamelitendea haki Bunge lako Tukufu. Nimezisoma, kazi yao ni nzuri na ni wajibu wangu kuwapongeza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunajadili taarifa za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria, lakini pia na ile ya Sheria Ndogo. Tunapokuja kwenye uwanja kama huu wa Sheria, kwa sisi tunaoipenda nchi yetu pia lazima tutumie nafasi hii kumpongeza sana Mheshimiwa Rais. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nampongeza Mheshimiwa Rais kwa kazi kubwa anayoifanya ya kusaidia utekelezaji na usimamizi mzuri wa sheria ndani ya nchi yetu. Speed, kasi na moyo wa Mheshimiwa Rais kuendelea kuteua Majaji kwa wingi kama anavyofanya sasa hivi ni ishara kwamba Mheshimiwa Rais anataka kuusaidia Mhimili wa Mahakama ufanye kazi zake vizuri na utoe haki kwa wakati jambo ambalo ni wajibu wake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeona ni vyema nichangie mambo machache. Kwa muda mrefu tumekuwa tukisikia na ndiyo msingi wa kuwa na Katiba na kuwa na Sheria, kwamba nchi yetu ni lazima iongozwe na iendeshwe kwa mujibu wa sheria, kanuni na taratibu. Hata mchangiaji aliyetoka, kaka yangu Mheshimiwa Lema amesisitiza jambo hilo na ni jambo zuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kumekuwa na kelele nyingi kwenye uhuru wa watu kutoa maoni, uhuru wa watu kushirikiana; na mambo mengine ya namna hiyo. Wote wanaozungumza, wanasema uhuru huu upo kwa mujibu wa Katiba, kwa hiyo, wanataka uhuru huu uheshimiwe. Hilo ni jambo zuri, nami naliunga mkono kabisa; na ndiyo mtazamo wangu, ndiyo msimamo wangu na ndiyo mawazo yangu kwamba kama Taifa, lazima tuheshimu uhuru na haki zilizotolewa kwenye Katiba yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lazima tukumbushane kwamba hata huu uhuru tunaotaka tuuheshimu, tunaotaka ufuatiliwe, tunaotaka utekelezwe; haki za binadamu tunazotaka watu wapate; hakuna haki bila wajibu. Katiba hii hii ambayo inapigiwa kelele kwamba imetoa haki za binadamu, imetoa uhuru kwa watu kufanya mambo, imetoa na namna ya kutekeleza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiisoma vizuri Katiba yetu ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, pamoja na kwamba ziko haki, uko wajibu, lakini ukienda kwenye Ibara ya 30 ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inatoa masharti, haiachi tu uhuru ukaenda unavyotaka, kila mtu afanye anavyotaka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Katiba inatuambia kabisa, lazima kila mmoja kwenye kutekeleza na kutumia uhuru wake, ahakikishe haingilii uhuru wa mtu mwingine, ahakikishe hautumii katika namna ambayo inakwaza na kuumiza watu wengine. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, wale ambao tunapigania haki, tuko sahihi kabisa, lakini lazima tukumbushane kwamba uhuru huu una mipaka. Ibara ya 30(2) inaipa Bunge mamlaka ya kutunga Sheria kutekeleza huo uhuru na hizo haki ambazo tunazo kwa mujibu wa Katiba.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niliona kwa kuwa tunajadili taarifa za Kamati hizi ni vyema tukakumbushana jambo hilo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye taarifa ya Kamati ya Sheria Ndogo, kwenye ukurasa wa 36 kama sikosei, Kamati ya Sheria Ndogo imetoa maoni na mapendekezo mazuri sana kuhusu Sheria Ndogo ambazo zinatungwa kwenye nchi yetu; ukurasa wa 36 ile (a), (b), (c), (d) na (e).

Mheshimiwa Mwenyekiti, naipongeza sana Kamati kwa sababu ushauri walioutoa ni ushauri wa msingi, nami ninauunga mkono na ninaomba ukafanyiwe kazi. Nasema naipongeza Kamati hii kwa sababu gani? Ushauri walioutoa wenzetu kwenye Kamati, umetuonesha pia tofauti ya ile dhana waliyokuwa nayo watu wengine kwenye mawazo yao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, yako mawazo, dhana na maneno; wako watu ambao wanapinga, wanasema siyo sahihi kuendelea kuiachia Serikali, Taasisi mbalimbali za Serikali kutunga Kanuni. Wako wengine wanasema Kanuni mbalimbali zitungwe ziwekwe ndani ya sheria au zije zijadiliwe Bungeni. Ni dhana zinazungumzwa, lakini ukisoma ushauri huu wa Kamati, unaelewa vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Katiba yetu imelipa Bunge mamlaka ya kutunga sheria, ukisoma Ibara ya 64. Ukienda Ibara ya 97(5) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, inatoa mwanya, baada ya kutunga Sheria inaruhusu kutungwa kwa kutungwa kwa Kanuni na sheria nyingine ndogo ndogo zikiwemo Kanuni, zikiwemo Orders na vitu vingine vya namna hiyo. Kwa hiyo, kwanza, Kanuni kutungwa kwenye Wizara, kutungwa kwenye Taasisi mbalimbali za Umma, kutungwa kwenye vyombo mbalimbali, haikiuki Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Hilo ni jambo la kwanza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili, hatuwezi kuacha Bunge likawa linatunga sheria zote, kanuni zote na orders zote. Tutakuwa nchi ya namna gani? Kazi zitafanyika namna gani? Bunge hili tunakutana kwa mwaka mara ngapi? Tunafanya kazi mara ngapi kwenye Bunge hili? Huwezi ukaacha kila sheria ikatungwa na Bunge.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ili mambo yaende vizuri, tutatunga Sheria ya Bunge, lakini sheria hiyo lazima itoe mwanya kwa Taasisi nyingine au Wizara au Idara kutunga kanuni ili mambo yaweze kwenda vizuri. Hata inapotokea kuna jambo la kurekebisha, pia ni rahisi kurekebisha kanuni kuliko utaratibu wa kurekebisha sheria. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, haya siyo maneno yangu tu peke yangu. Mwanasheria mmoja mbobezi anaitwa John Alder, ameandika Kitabu kinaitwa “Constitutional and Administrative Law”, edition ile ya saba. Kwenye kitabu chake ukurasa wa 147 anajaribu kueleza huo mkanganyiko na hayo mawazo ya watu, lakini mwisho ana-conclude akasema “however, it is difficult to imagine a complex and highly regulated society that could function effectively if all laws had to be made by the Parliament itself.”

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimesema niliseme hili, kwa sababu maoni ya Kamati yamejielekeza vizuri, lakini najua yako mawazo ya watu ya namna hiyo. Mimi nadhani utaratibu uliopo ni mzuri, tuache utaratibu huu uendelee. Sheria zitungwe na kama inavyotukumbusha ile Sheria yetu ya Interpretation of Laws, ukisoma kuanzia section ya 36 inatoa utaratibu, hizi kanuni zitungweje? Ziweje? Zifuatane na kitu gani? Zizingatie vitu gani?

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, utaratibu uliopo uendele, lakini ushauri wa Kamati uzingatiwe ili kuweza kuboresha utaratibu huu wa kutengeneza Kanuni na Sheria nyingine ndogo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna jambo lilitoka kuzungumzwa hapa muda siyo mrefu sana. Tunapokumbushana kuendesha nchi kwa mujibu wa sheria, kanuni na taratibu, lazima tukumbushane kama nilivyosema, haki na wajibu wa kila mmoja wetu. Sheria zetu na taratibu zetu haziruhusu mambo yaliyoko Mahakamani kujadiliwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeona imekuwa ni utaratibu wa kawaida na kwa masikitiko makubwa, nimewahi kuona hata kwenye Bunge lako hili, mtu ana kesi Mahakamani, amepewa dhamana, amekiuka masharti ya dhamana, akafutiwa dhamana, ana kesi Mahakamani, ana- challenge uamuzi wa Mahakama kumfutia dhamana, mtu anakuja na jambo hili kulileta Bungeni. Tunakuja kufanya nini kwenye Bunge hili? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, utaratibu uko wazi. Mtu anasema kuna kesi ya Mashehe; ndiyo ipo kesi ya Mashehe lakini iko Mahakamani. Unataka tuilete Bungeni humu kufanya nini? Ni lazima sisi kama Wabunge tuwe watu wa kwanza kuheshimu sheria.

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante.

MHE. TIMOTHEO P. MNZAVA: Mheshimiwa Mwenyekiti, Waheshimiwa Wabunge tuwe watu wa kwanza kuheshimu misingi na taratibu na Katiba ya…

MWENYEKITI: Mheshimiwa Mnzava, ahsante.

MHE. TIMOTHEO P. MNZAVA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja za Kamati. Ahsante.