Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Sheria Ndogo kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018

Hon. Joseph Roman Selasini

Sex

Male

Party

CHADEMA

Constituent

Rombo

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Sheria Ndogo kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018

MHE. JOSEPH R. SELASINI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Nianze kwa kusema kwamba tuko hapa Bungeni kwa ajili ya kumsaidia Rais. Hakuna Mbunge yeyote humu ndani ambaye lengo lake siyo kumsaidia Rais. Mawazo tunayotoa hapa lengo lake ni kusaidia ili nchi hii iweze kuongozwa vizuri. Kwa hiyo, Bunge lisipotoshwe kwamba kuna watu ambao wako hapa wanafanya hujuma dhidi ya uongozi wa Rais. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili nataka nilishauri Bunge na Taifa acheni Mheshimiwa Lissu afanye anachofanya kwa utashi wake. Tunapoteza muda na nguvu kujadili habari ya Mheshimiwa Lissu. Nguvu hizi tungezitumia wakati alipopigwa risasi kama Wabunge ingeonekana tumefanya jambo la busara sana lakini alivyopigwa risasi, alivyokuwa hospitali, alivyokuwa anahangaika na matibabu tulikaa kimya. Sasa hivi Mungu amemjalia pumzi acheni aseme. Kama kuna jambo ambalo atakosea atakuja ahojiwe mbele ya safari. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, limezungumzwa hapa jambo la Uchaguzi Mkuu na Tume ya Uchaguzi. Pia Serikali wiki iliyopita ilijibu maswali kuhusu Tume ya Uchaguzi na maandalizi ya uchaguzi ujao kwamba imeanza taratibu za kuboresha daftari, hili ni jambo zuri. Mwenzangu amechangia juu ya kupitia hata Tume yenyewe na kuhakikisha kwamba watendaji wa Tume wanateuliwa watu huru na watakaosimamia uchaguzi vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, chaguzi katika nchi mbalimbali zimeleta fujo sana na zimesababisha mataifa mengi kuvurugika. Kwa hiyo, naikumbusha na kuiomba Serikali, uchaguzi wa 2020 ni wakufa na kupona, naomba sana maandalizi ambayo mmeamua kuanza kuyafanya yawe shirikishi, wananchi washirikishwe, vyama vishirikishwe na kila mdau ashirikishwe. (Makofi)

T A A R I F A

MHE. JOSEPH R. SELASINI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niendelee. Uchaguzi Mkuu unatanguliwa na uchaguzi wa Serikali za Mitaa. Mwaka huu kila mmoja wetu alitegemea kwamba maandalizi ya uchaguzi wa Serikali za Mitaa yangeshaanza kufanyika. Kama tunavyojuwa maandalizi ya uchaguzi wa Serikali za Mitaa yanaanza na kanuni na kuwashirikisha wadau. Naomba sana maandalizi yawe wazi, wadau wote washirikishwe, kwa sababu uchaguzi wa Serikali za Mitaa uliopita ulikuwa na fujo za hapa na pale.

T A A R I F A

MHE. JOSEPH R. SELASINI: Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme tu wamekuwa wanatukatia muda wetu na Kiti kimekuwa kikipunguza muda wetu. Hakuna mtu huku anachangia dakika kumi hata mmoja ni saba, nane.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba wahusika washirikishe wadau na wadau ni vyama vya siasa na kadhalika, tuweze kuzipitia hizo kanuni ili uchaguzi uweze kwenda vizuri, tuweze kupata viongozi wa kutuongoza sawasawa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya hilo haraka haraka nizungumzie kuhusu yanayotokea katika nchi. Tutafika mahali nchi hii tutaingia kwenye matatizo makubwa. Yapo mauaji na vifo ambavyo hadi sasa hakuna matokeo ya uchunguzi wake na nitataja baadhi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, alichinjwa Mwenyekiti wa CHADEMA wa Arumeru, hakuna taarifa mpaka sasa hivi; Ben Saanane hakuna taarifa; Azori Gwanda hakuna taarifa; David John wa Ananasifu hakuna taarifa; Simon Kangoye, Mwenyekiti wa Halmashauri ya Kibondo kupitia Chama cha Mapinduzi hakuna taarifa; Akwilina Akwilini, Kamanda wa Kanda Maalum anasema faili limefungwa wakati anasema alikamata askari sita ambao walituhumiwa kumpiga risasi; Petro Shemasi wa Itigi ambaye baba yake anasema alishuhudia Mkurugenzi akimlenga risasi ya kichwa, leo Polisi wanaanza kusuasua na kuweka mambo ili kulinda wauwaji; yupo Alphonce Mawazo na Lwena wa huko Kilombero. Siyo hao tu, wapo Watanzania wengi ambao wamekwishauwawa kwa sababu mbalimbali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nchi hii tunauwana hovyo namna hii, tuna Polisi na vyombo vya dola lakini hakuna taarifa tunaona ni jambo la kawaida tu, tukumbuke kwamba familia za hawa waliouawa…

T A A R I F A

MHE. JOSEPH R. SELASINI: Mheshimiwa Mwenyekiti, mtu mmoja akiuawa, ni jambo kubwa sana katika nchi na unachoniambia wewe Mbunge wa CCM ni kwamba Serikali imeshindwa kuchunguza haya mauaji kwa sababu mimi sitetei wauaji wa Kibiti, sitetei wauaji wa sehemu nyingine yoyote, nachosema ni kwamba wajibu namba moja wa Serikali ni kumlinda raia na mali zake, wauaji waue Kibiti…

T A A R I F A

MHE. JOSEPH R. SELASINI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nachosema na kuiomba Serikali, mauaji ya holela katika nchi hii itafute namna ya kuyakomesha. Mimi sizungumzi habari ya kauawa wa CCM au CHADEMA. Nachosema tukiendelea na huu mchezo ni kwamba itafika mahali kisasi kitalipwa. Nasikitika yakizungumzwa mambo kama haya Wabunge wazima wanapiga makofi, wanacheka, wanabeza, wanatoa miongozo na nini kama vile hakuna kitu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nawasihi Wabunge wa CCM shaurini Serikali tutafute namna ya kukomesha haya mauaji kwa sababu leo hii ukinigusa mimi, mimi nina watoto, nina ukoo usitegemee kwamba watoto na ukoo wangu utachekelea tu hivi hivi, pengine ukiniua kuna reaction itatokea huko. Ndiyo maana nasema chonde chonde, Waziri wa Sheria kaka yangu Mheshimiwa Kabudi, kaa na vyombo kwa utulivu na amani kabisa, kaa na DPP, IGP na wengine wote hii ni aibu nimetaja watu karibu 20 wameuawa lakini hakuna uchunguzi, hakuna chochote, ni kama mbuzi tu. Hata hawa wa Kibiti waliokamatwa, nasema lazima washughulikiwe vinginevyo tukienda hivi, nchi hii itafika mahali kisasi kitatembea barabarani na haitakuwa jambo la maana. Rwanda ilianza kidogo kidogo hivi ikachochewa na vyombo vya habari matokeo yake Rwanda ikalipuka, sisi hatuna tofauti na Rwanda. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimalizie kwa kusema, limezungumzwa hapa jambo la walio mahabusu. Hoja hapa ni kwamba walio mahabusu wanaweza kutafutiwa njia nyingine. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa Mzungumzaji)