Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Sheria Ndogo kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018

Hon. Anthony Peter Mavunde

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Dodoma mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Sheria Ndogo kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018

NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU (KAZI, AJIRA NA VIJANA): Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwanza kwa kuunga mkono hoja za Kamati zote mbili. Pia nichukue fursa hii kutoa pongezi zangu za dhati kwa Kamati zote mbili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda nijielekeze moja kwa moja kwenye hoja kama ambavyo zimewasilishwa na Kamati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikianza na eneo la kwanza ambalo limegusiwa na wachangiaji ikiwemo mapendekezo ya Kamati, imezungumzwa hoja ya kuhusu uanzishwaji wa Baraza la Watu wenye Ulemavu na litangazwe mapema.

Ni kweli kwa mujibu wa Sheria Na. 9 ya mwaka 2010 inayozungumzia watu wenye ulemavu, imeweka bayana kwamba kutakuwepo kuna Baraza la Watu wenye Ulemavu. Hivi sasa navyozungumzia tayari Serikali imeshakamilisha zoezi la kutoa mapendekezo la kumpata Mwenyekiti na Wajumbe wa Baraza la Ushauri la Taifa la Watu wenye Ulemavu. Kwa hiyo, muda sio mrefu uteuzi huu utafanyika na litazinduliwa rasmi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia imezungumzwa hoja ya kwamba kuanzishwe kifungu maalumu kwa maana ya kasma ya masuala ya watu wenye ulemavu. Wizara tayari imeshafanyia kazi eneo hili na kifungu hiki kimepatikana. Kwenye bajeti ya mwaka 2019/2020 kifungu hiki kitaonekana na kitatengewa fedha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia imezungumzwa hoja ya kuanzisha Mfuko wa Maendeleo ya Watu wenye Ulemavu. Kama Wizara, kwa maana Ofisi ya Waziri Mkuu, tumeshandaa rasimu ya mwongozo wa Mfuko wa Maendeleo ya Watu wenye Ulemavu na tumeshawashirikisha wadau, tumefanya kikao cha Dar es Salaam na eneo hili, Mheshimiwa Ikupa analisimamia kwa ukamilifu sana. Kwa hiyo, muda siyo mrefu baada ya sehemu hii kukamilika basi tutaona namna bora ya uanzishwaji wa Mfuko huu wa Watu wenye Ulemavu kwa ajili ya maendeleo yao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia ilizungumzwa hoja ya kuweka usimamizi mzuri wa fedha kwa ajili ya watu wenye ulemavu kuhakikisha kwamba fedha hizo zinatengwa na Halmashauri. Ni dhahiri kwamba Serikali imeelekeza kila Halmashauri nchini kutenga asilimia 2 ya mapato yake ya ndani ili kuwawezesha watu wenye ulemavu. Katika eneo hili pia, tumeandaa rasimu ya mwongozo mzuri wa utoaji wa fedha hizi za asilimia 2 kwa watu wenye ulemavu ili ziweze kuwafikia kirahisi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia ilizungumzwa hoja ya namna ya kuwashirikisha watu wenye ulemavu kwenye shughuli za michezo. Niseme tu kwamba kama Wizara tumekuwa tukifanya hivyo pale yanapotokea maombi. Mwaka 2009 tuliwahi kuisaidia Timu ya Watu wenye Ulemavu wa Akili ambao walikwenda katika Bara la Asia kushiriki mashindano ya mpira wa miguu na mbio. Halikadhalika kwa sababu BASATA na Baraza la Michezo Tanzania ziko chini ya Wizara, tutahakikisha kwamba tunafanya ushirikiano wa kutosha ili kundi hili pia liweze kuangaliwa katika masuala ya michezo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, imezungumzwa pia hoja kuhusu Mfuko wa Maendeleo wa Vijana. Eneo hili limezungumziwa sana na moja kati jambo ambalo limezungumzwa ni usimamizi na udhibiti ili kuhakikisha kwamba fedha za mfuko huu zinawafikia walengwa ambao ni vijana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Halmashauri zote ambazo zinadaiwa fedha ya Mfuko wa Maendeleo ya Vijana ambapo vijana wamekopa na fedha hizi zinatakiwa zirudishwe, kupitia Ofisi ya Waziri Mkuu tumeanza kuchukua hatua kuzifuatilia fedha hizi ili ziweze kurudishwa. Wale ambao tumeshawapa taarifa ya kurejesha fedha hizi bado hawajafanya kwa wakati, taratibu za kisheria zitachukuliwa kuhakikisha kwamba fedha hizi zinarudi ili vijana wengi zaidi waweze kukopeshwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa taarifa tu, fedha za Mfuko wa Maendeleo wa Vijana zimelengwa kwa ajili ya vikundi vya vijana ambapo utaratibu wake ni kwamba kila Halmashauri nchi nzima inaandaa SACCOS ya vijana yenyewe ndiyo inayokopa kupitia Halmashauri na ndiyo inayokwenda kukopesha vikundi vya vijana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimesikiliza hoja ya Mheshimiwa Bobali, kwa kweli nimeshindwa kuelewa vizuri Mheshimiwa Bobali na nilitamani angekuwepo hapa Mbunge mwenzangu kijana kabisa anasema kwamba haujui Mfuko wa Maendeleo wa Vijana na vijana wake hawajanufaika. Nataka tu nimpe taarifa Mheshimiwa Bobali kwamba mwaka 2016 nilikwenda mwenyewe katika Wilaya ya Lindi Vijijini ambako nilikuwa na Programu ya Kuwawezesha Vijana Kiuchumi. Katika programu ile walikuwepo vijana 683 wakitoka katika majimbo mawili, la Mchinga na Mtama na Mheshimiwa Nape alikuwepo Mheshimiwa Bobali hakuwepo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika jambo hilo vijana hawa waliwezeshwa kiuchumi lakini pia baada ya kuhitimu mafunzo yao ya kuwezeshwa kiuchumi tulitenga utaratibu mzuri wa kuwakopesha kupitia Mfuko wa Maendeleo ya Vijana. Ninavyozungumza hivi sana, kwenye Wilaya ambayo anatoka Mheshimiwa Bobali, tumeshakopesha vikundi na moja ya kikundi ambacho kimekopeshwa katika mwaka wa fedha 2016/2017 ni kikundi ambacho kinaitwa Juhudi kilichokopa Sh.3,500,000 na kingine kinaitwa Kitongamano walikopa Sh.6,000,000 na kikundi cha Mshikamano. Nikimsikia Mheshimiwa Mbunge anasema kwamba haujui mfuko huu na vijana wake hawajanufaika jambo hili si la kweli, mfuko huu unawafikia vijana wengi nchi nzima na vijana wengi wamenufaika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia yalikuja mapendekezo hapa ya kutaka kuwe na namna bora ya mfuko huu kuwafikia watu nje ya mfumo wa SACCOS. Sheria ya kuratibu mfuko huu ilitungwa mwaka 1994. Sisi kama Wizara tukaona ni miaka mingi imepita, kwa sababu masharti ya mwongozo wa mfuko huu inataka SACCOS ndiyo ikopeshwe, tumeenda mbali zaidi, hivi sasa tumeanza kupitia mwongozo wetu ili baadaye kuruhusu vikundi vya vijana kwa maana ya makampuni na vikundi tofauti tofauti, nje ya SACCOS na wenyewe waweze kukopa. Kwa hiyo, naamini kabisa kwamba mfuko huu utawafikia vijana wengi zaidi na wengi watakopa kwa ajili ya kupata fursa hii ya kiuwezeshaji kiuchumi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia Ofisi ya Waziri Mkuu tunaendesha Programun ya Ukuzaji Ujuzi Nchini ambayo ina lengo la kuwafikia vijana takribani…

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa Mzungumzaji)