Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 - Ofisi ya Waziri Mkuu

Hon. Amb Dr. Diodorus Buberwa Kamala

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nkenge

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 - Ofisi ya Waziri Mkuu

MHE. BALOZI DKT. DIODORUS B. KAMALA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa fursa hii muhimu ya kuchangia hoja muhimu iliyo mbele yetu. Naomba nianze kwa kusema kwamba naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba nianze kwa kujielekeza katika eneo moja muhimu, nalo ni eneo la uwekezaji. Najielekeza katika eneo hili ili Tanzania tuweze kupiga hatua kuingia kati ya nchi zilizo katika uchumi wa kati kama walivyosema walionitangulia kwa vyovyote vile lazima tujitahidi tuhakikishe tunapanua uwekezaji, tunavutia wawekezaji wa ndani na wawekezaji kutoka nje ya nchi.

Mheshimiwa Spika, nichukue nafasi hii kumpongeza Mheshimiwa Rais kwa uamuzi wake wa makusudi wa kuanzisha Kitengo cha Uwekezaji katika Ofisi ya Waziri Mkuu, ni jambo muhimu sana na nampongeza sana. Na siyo tu kwamba kahamasisha kitengo hicho Ofisi ya Waziri Mkuu, lakini pia kateua Waziri wa kusimamia sekta hiyo. Nampongeza sana Mheshimiwa Rais kwa uamuzi huo. (Makofi)

Nimesoma kitabu kilichowasilishwa mbele yetu cha hotuba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu, nikaona kwamba kutoka nje tumeweza kuhamasisha, kuvutia wawekezaji kwa ujumla wake kwa ndani na nje dola bilioni 1.84 lakini pia kwenye kitabu hiki kinatuonesha kwamba Tanzania tumeweza kuvutia kutoka nje kuja Tanzania uwekezaji wenye dola bilioni 1.18; kwa hiyo, kwa hesabu ya haraka haraka, nilipochukua ule uwekezaji kwa ujumla tuliohamasisha wa jumla wa ndani na nje 1.84 billion US dollars, nikaondoa dola bilioni 1.18 ambazo zimetoka nje, nikabaini kwamba ndani ya nchi tumeweza kuhamasisha uwekezaji 0.66 billion dollar.

Mheshimiwa Spika, sasa takwimu hazina maana kama hujazifanyia tafsiri. Tafsiri ya haraka haraka ni kwamba wawekezaji wa ndani bado hatujafanya kazi kubwa ya kuhamasisha uwekezaji wa ndani kwa sababu ili Tanzania tuweze kupiga hatua lazima pia tuwe na wawekezaji wa ndani ya nchi. Sasa ili tuweze kuongeza wawekezaji wa ndani ya nchi kutoka dola bilioni 0.6 angalau tupande angalau ifike dola bilioni moja au dola bilioni mbili lazima tufanye kila kinachowezekana siyo kuhamasisha tu wawekezaji wanaotoka nje, lakini pia na wawekezaji wa ndani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa moja ambalo umelizungumza vizuri ni kuhusu kuangalia hivi vikwazo vilivyopo na tukavifanyia kazi. Sote tunafahamu kwamba kwa muda mrefu Serikali imefanyakazi nzuri kupitia Wizara ya Biashara kuandaa ile blue print. Blue print inaonesha ni changamoto zipi zipo, ni mambo yapi yapo yanatakiwa kufanywa, lakini changamoto kubwa iliyopo ni kwamba ukiisoma ile blue print utagundua kwamba kuna mambo mengi yanahitaji kutungiwa sheria, kuna sheria nyingi zinahitaji kufanyiwa rationalization, sasa naomba kupitia kwako tuishauri Serikali ifanye kila linalowezekana ndani ya muda mfupi ituletee hapa Bungeni sheria zote zinazotakiwa kurekebishwa ili kuendana na blue print ambayo imeandaliwa vizuri na kwa muda mrefu ili hiyo blue print iweze kufanyakazi.

Mheshimiwa Spika, ili tuhamasishe vizuri ndani maana Tanzania kama Tanzania tunasema Tanzania ni gateway ya Afrika Mashariki, lakini nichukue nafasi hii nitangaze ndani ya Bunge hili wakati Tanzania ni gateway ya Afrika Mashariki, Wilaya ya Misenyi na Jimbo la Nkenge ni gateway ya Tanzania kwenda Afrika Mashariki.

Kwa hiyo, nichukue nafasi hii kumshukuru Mheshimiwa Waziri wa Uwekezaji ambaye nimemualika tarehe 05 Julai, 2019 aje kuwa mgeni rasmi katika kongamano kubwa la kimataifa la kutangaza uwekezaji na amenikubalia namshukuru sana na nimuombe Mheshimiwa Waziri Mkuu ukisikia Mheshimiwa Waziri Angellah naomba kwenda Misenyi kufanya kazi hiyo umruhusu aje aifanye kwa sababu ni kazi muhimu sana katika kuvutia wawekezaji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia nichukue nafasi hii nitoe jambo moja la tahadhari. Sote tunafahamu hali ya hewa si nzuri sana kwa sasa, katika maeneo mbalimbali hali ya mvua haikwenda kama tulivyotarajia lakini tuna National Food Reserve Agency taarifa tulizonazo na za uhakika wana tani kati ya 78,000 mpaka 100,000 za chakula tu. Kwa takwimu tulizopewa kwenye kitabu cha Mheshimiwa Waziri Mkuu ameeleza vizuri tu kwamba Tanzania tumezalisha tani milioni 16, matumizi ni tani milioni 13, kwa hiyo, tumebakiza surplus tani milioni 3.32.

Mheshimiwa Spika, hali ya hewa isipokuwa nzuri kama ambavyo imeanza kuonekana maana yake tutakuwa na upungufu wa chakula ndani ya nchi. Kama itakuwa hivyo litakuwa jambo la hatari kama huyu National Food Reserve Agency ataendelea na mipango yake ya kuuza reserve kidogo ya chakula aliyonayo ili kuweza kupata fedha ya kuongeza reserve ya chakula. Kama una tani 78 kama reserve unataka uuze hicho ili upate fedha za kununua kingine ni changamoto. Nichukue nafasi hii kuomba Ofisi ya Mheshimiwa Waziri Mkuu ajaribu kuliangalia eneo hilo ili tuweze kujipanga vizuri kwa sababu ukishakuwa na matatizo ya chakula hata upange mambo yoyote yale hayawezi yakaenda vizuri.

Mheshimiwa Spika, la mwisho, niipongeze Serikali kwa sababu imetoa tangazo maeneo mbalimbali ya Ranchi za Taifa ambayo yalikuwa hayatumiki vizuri sasa yapate wawekezaji wapya, ni jambo jema. Hata hivyo, natahadharisha wale wawekezaji walio wengi wameshindwa kuwekeza kwa sababu ya migogoro mingi kutokana na ukweli kwamba ranchi hizo zilivamia vijiji na kwa hivyo mara kwa mara wawekezaji hao wamejikuta kwenye migogoro ya muda mrefu na migogoro hiyo haijaisha. Kwa hiyo, hata Serikali ikitangaza upya ikapata wawekezaji wapya bila kumaliza migogoro iliyopo yatakuwa yale yale. Kwa hiyo, nishauri tu kwa nia nzuri kwamba ile Kamati iliyoundwa ya Mheshimiwa Rais ifanye kazi yake na ihakikishe ranchi inabaki tu maeneo yake na vijiji vyetu waachiwe wananchi ili hizo ranchi mpya zitakazotangazwa zisianze na migoogoro.

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo, naunga mkono hoja kwa asilimia 100. (Makofi)