Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 - Ofisi ya Waziri Mkuu

Hon. Amina Saleh Athuman Mollel

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 - Ofisi ya Waziri Mkuu

MHE. AMINA S. MOLLEL: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ili niweze kuchangia hotuba ya Waziri Mkuu kwa mwaka huu wa fedha 2019/2020. Awali ya yote namshukuru sana Mwenyezi Mungu kwa kutujaalia uzima na kuwepo hapa, bila yeye tusingekuwepo hapa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kipekee kabisa naomba na naonesha kutokana na jinsi ambavyo Ofisi hii ya Waziri Mkuu na pia Rais kupitia Serikali hii ya Awamu ya Tano kwa jinsi ambavyo wamekuwa wakifanya kazi na hasa katika masuala ya watu wenye ulemavu yalivyopewa kipaumbele. Hii inaonesha kwamba Serikali yetu ni sikivu, inasikiliza wanyonge na inasikiliza hoja mbalimbali ambazo zinatolewa na kwenda kuzifanyia kazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, ningependa kwa kuanza kuzungumzia Mfuko wa Watu Wenye Ulemavu; tarehe 2 Februari, 2017 niliuliza swali kuhusiana na Mfuko huu na nilisema kwamba kwa sababu Mfuko huu na masuala yote ya watu wenye ulemavu yapo pia katika mkataba wa Kimataifa wa watu wenye ulemavu wa mwaka 2006, lakini pia Sera ya Watu Wenye Ulemavu ya mwaka 2004 inazungumzia pia haki za watu wenye ulemavu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa muda mrefu tumekuwa tukizungumzia na kuishauri Serikali kuona ni kwa jinsi gani wanatatua changamoto mbalimbali zinazowakabili watu wenye ulemavu na tulidai Mfuko kuhusiana na watu wenye ulemavu lakini pia tukadai bajeti kuhusiana na Wizara hii kwamba tayari tunaye Naibu Waziri na kama tunaye Naibu Waziri tulihitaji kwamba kuwepo na bajeti maalum. Kwa mfano mfuko huu kwa mwaka 2017 haukutengewa fedha, lakini mabadiliko makubwa tumeyaona katika bajeti hii ya mwaka 2019/2020.

Mheshimiwa Naibu Spika, kipekee kabisa nampongeza mwenzangu Mheshimiwa Naibu Waziri, Ikupa Alex, kwa ushauri mzuri ambao ameweza kuutoa kwa kushirikiana kwa pamoja hatimaye sasa kwa kweli tunajivunia kuona kwamba kitengo cha watu wenye ulemavu kimetengewa fedha. Kwa kuanza kwa mwaka huu ambayo ni subvote 2034 na imetengewa zaidi ya bilioni moja na naamini kabisa huu ni mwanzo, tunapokwenda ni pazuri na tutaweza kuongezewa pia hiyo bajeti. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hili kwa kweli nampongeza sana Waziri mwenye dhamana, dada yangu Mheshimiwa Jenista Mhagama yeye ni jembe lakini pia niwapongeze Manaibu Waziri, Mheshimiwa Mavunde na Mheshimiwa Ikupa. Jembe lingine ambalo limeongezeka katika Ofisi hii nimpongeze sana Mheshimiwa Angella Kairuki, lakini pia naamini kabisa ni kutokana pia na Makatibu Wakuu waliopo ambao na wao kwa kweli kipekee nawapongeza sana kwa mchango wao katika kuwasimamia na kuwashauri vizuri Mawaziri hatimaye tunakwenda pamoja sasa. Nawapongeza sana na nimpongeze sana Katibu Mkuu baba yangu Massawe. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na pongezi hizo na kazi nzuri ambazo kwa kweli zimefanywa na Serikali ya Awamu ya Tano, napenda kushauri mambo mawili, matatu ili basi kuona kwamba ni kwa jinsi gani na kama ilivyo sisi ni kiunganishi katika ya Serikali na wanachi na wajibu wetu ni kuisimamia Serikali na kuishauri. Napenda kuishauri Serikali katika mambo yafuatayo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa kwamba tumeona tunacho kitengo na tayari tumekwishatengewa fedha. Naishauri Serikali kuona umuhimu sasa kutoka kwenye kitengo na kwenda kwenye idara kamili ambayo idara hii ndiyo itakuwa Idara ya Watu Wenye Ulemavu na siyo kitengo. Huu ni ushauri wangu naomba sana watakapoendelea basi waone kwamba ni kwa jinsi gani tunakwenda kufikia huko na kuwa Idara ya Watu Wenye Ulemavu.

Mheshimiwa Naibu Spika, miundombinu bado siyo rafiki katika majengo mengi na hata ya Serikali pia kwa watu wenye ulemavu. Bado miundombinu siyo rafiki na hata baadhi ya majengo mengine watu hawazingatii. Nawaomba waliopewa dhamana ya kulisimamia hili kuona kwamba tunaweza kuondoa changamoto zote hizi ambazo zinawakwamisha watu wenye ulemavu kuweza kushindwa kutimiza majukumu yao au kwenda maeneo ambayo wanapaswa kwenda kufuatilia haki zao au kushughulikia yale mambo ambayo ni muhimu kabisa.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia naomba nimpongeze Naibu Waziri wa Kazi, Ajira pamoja na Mkurugenzi wa Ajira, Bwana Msaki kwa kazi nzuri wanayofanya. Mimi ni Mjumbe wa Kamati ya Katiba na Sheria na tunaisimamia Ofisi ya Waziri Mkuu. Tumeshuhudia ni kwa jinsi gani ambavyo Waziri mwenye dhamana, kwa ujumla Ofisi hii kwa jinsi ambavyo wanafanya kazi na tumesikia kwamba watu wakilalamika kuhusu suala la ajira na tunapoelekea hata Marekani bado tatizo la ajira lipo na ni nchi zilizoendelea. Kwa kuona kwamba Serikali haiwezi pia kuwatimizia wananchi wake wote kuwapa ajira, Ofisi ya Waziri Mkuu, Kazi na Ajira wao wameandaa utaratibu mzuri ambao wanakusanya maoni na hasa vijana mbalimbali ambao wamemaliza Chuo Kikuu, wanatuma maoni na maombi hatimaye Ofisi hii kwa utaratibu mzuri ulioandaliwa wanapelekwa katika Taasisi mbalimbali ikiwemo mabenki. Kule wanakwenda wanapata ujuzi na wengi tayari hivi sasa kule walikopelekwa wamekwishapata ajira na kuchukuliwa na mabenki na maeneo mengine tofauti tofauti. Hii ni kazi nzuri inayofanywa na Ofisi ya Waziri Mkuu.

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile bado utaratibu mzuri ambao umeandaliwa katika suala zima la kilimo na tumekuwa tukizungumza hapa kilimo cha kutegemea msimu wa mvua siyo kilimo ambacho kitaweza kutukomboa. Serikali yetu imekuja na utaratibu mzuri wa kuona ni kwa jinsi gani tunalima katika kilimo biashara, kilimo chenye tija kwa kuona ni kwa jinsi gani tunalima kwenye kilimo cha kutumia maji hasa kilimo cha umwagiliaji. Ofisi hii utaratibu mzuri iliyoandaa katika Halmashauri zetu hivi sasa katika kila Halmashauri vijana wanatakiwa zaidi ya 100, Halmashauri zetu zimeandaa baadhi ya maeneo na vijana hawa wanapewa ujuzi, wanajengewa nyumba-vitalu yaani green house ambazo wanapewa ujuzi kuweza kujua ni kwa jinsi gani wataweza kulima mazao ya kule ndani kwenye bustani hizo.

Mheshimiwa Naibu Spika, mazao hayo yatakuwa ni mazao ambayo kwanza ni yenye ubora, ni mazao ambayo yataweza kuuzwa katika maeneo tofauti tofauti na yataweza kuwakwamua vijana wale na vijana hao watakaokuwa wamepata huo ujuzi watatoka sasa pale. Tunayo mabenki yetu, naamini kabisa Serikali itawawezesha vijana hawa ili basi waweze kujitegemea badala ya kutegemea hasa ajira kutoka Serikalini. Huu ni utaratibu mzuri unaoandaliwa na Ofisi ya Waziri Mkuu na tayari vijana wapo site wanafanya kazi hiyo. Halmashauri zetu tunaziomba sana zihakikishe kwamba zinasimamia zoezi hili na kutoa ushirikiano kwa walengwa ili waweze kufanyia kazi hili.

Mheshimiwa Naibu Spika, nitakuwa mchoyo wa fadhila kama kweli sitawazungumzia OSHA pamoja na Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi. Tulikuwa na malalamiko mengi kwa OSHA, lakini hivi sasa OSHA wameondoa vipengele vingi ambavyo vilikuwa ni kero kwa wawekezaji na vipengele hivyo vimeondolewa hivi sasa na tumeona kwamba, pamoja na kuondoa vipengele hivyo, wawekezaji sasa wengi wamekwenda, vibali vinatolewa kwa muda muafaka, lakini pia wanapata fedha kutokana na vibali hivyo. Kwa hiyo, napongeza sana huu utaratibu unaofanywa na nimpongeze sana Mkurugenzi wa OSHA, Bi.Khadija kwa kazi nzuri sana anayofanya.

NAIBU SPIKA: Muda wako umekwisha Mheshimiwa, ahsante sana.

MHE. AMINA S. MOLLEL: Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja na naishukuru sana Serikali.