Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 - Ofisi ya Waziri Mkuu

Hon. Dr. Stephen Lemomo Kiruswa Mamasita

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Longido

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 - Ofisi ya Waziri Mkuu

MHE. DKT. STEVEN L. KIRUSWA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa fursa hii ili nami niweze kuchangia katika hotuba hii ya bajeti ya Waziri Mkuu. Nitangulize pongezi zangu za dhati kwake yeye Waziri Mkuu na timu yake yote kwa kazi nzuri wanayoifanya na kwa jinsi walivyoiratibu na kuangazia masuala chanya ya maendeleo yanayoendelea katika nchi yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile nitumie fursa hii kwa niaba ya wananchi wa Longido kutoa shukurani zangu za dhati kwa sababu ya maendeleo chanya yaliyoonekana na kushangiliwa na wananchi wa Longido katika Serikali hii ya Awamu ya Tano ambapo mradi mkubwa kabisa wa maji kutoka Mlima Kilimanjaro uliogharamiwa kwa jumla ya shilingi bilioni 15.9 hatimaye umefika Longido, watu wamepata maji safi na salama na mengi na ya kutosha. Wananchi wa Longido wamesherehekea na wanaendelea kufurahia, sasa watu wanaweza wakaoga hata mara tatu kwa siku kwa sababu yale maji yamekuja kwa wingi wake.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia kwa sababu kulikuwa na ahadi za Serikali za kuendeleza maji haya yawafikie na majirani waliko pembezoni mwa bomba hilo kubwa katika vijiji mbalimbali kuanzia kule maji yanapotokea Kata ya Olmolog Kijiji cha Elerai; Kata ya Sinya, Kijiji cha Sinya; Kata ya Tingatinga, Kijiji cha Ngereyani na hivi vijiji vya pembezoni mwa Longido hadi Kimokouwa na Namanga ambapo hata Rais mwenyewe alipokua kuzindua ule mpaka wa pamoja alitolea tamko kwamba nao wamepelekewe maji hayo. Kwa kweli Longido wameona haya maji kama ni uzima, wamepewa maisha na mimi nakumbuka kila nikipita pale Moshi kuna mnara wa Askari ambapo kuna slogan chini yake inasema “maji ni uhai” nikawa najiuliza kwa nini Askari anashika bunduki anaelekeza Mlima Kilimanjaro kumbe analinda uhai. Maji ni uhai, ni ya kulindwa, ni ya kuenziwa na wananchi wa Longido wamefarijika sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia wananchi wa Longido kwa mwaka huu wamepata mgao mkubwa wa fedha za kujengewa hospitali ya Wilaya ambayo hatukuwahi kuwa nayo. Hospitali ya Wilaya imetengewa bilioni moja na nusu bila kuhesabu vituo vya afya viwili ambavyo vimejengwa viko katika hatua ya umaliziaji, japo bajeti imekwisha lakini naamini bajeti hii itawapa watu wa Eworendeke na Engarenaibor fedha za kumalizia na moja ambayo wananchi kwa ari kabisa wa Tarafa ya Ketumbeine nao wameanza kuijenga kwa nguvu yao wenyewe mpaka wamefikia hatua ya kupaua.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya shukrani hizo kwa sababu nataka tu kuonyesha ni kwa jinsi gani Serikali hii inawaenzi wananchi wake tena watu wa Wilaya za pembezoni kama Longido, sasa napenda kuchangia katika hotuba hii ya Waziri Mkuu kwa kudonoa baadhi ya mambo machache ambayo nime-note. Kwa suala la ardhi kuna hii sera ya Serikali inayosema kwamba Mpango wa Taifa kufikia mwaka 2033 ni kuhakikisha kila kipande cha ardhi ya Tanzania kimemilikishwa na kinamilikishwa baada ya kupangwa na kupimwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, natoa angalizo kama Mjumbe wa Kamati ya Ardhi, Maliasili na Utalii kwamba tulivyofanya ziara katika baadhi ya mikoa inayopakana na nchi za jirani tumeona ardhi yetu inavamiwa hovyo kabisa na sisi Watanzania naona ardhi yetu ni kubwa hatujakaribia sana ile mipaka kama wenzetu. Tumetembelea mipaka yetu na Rwanda, Uganda, Kenya upande wa Tanga maeneo ya Horohoro tukashangaa nchi za jirani zimejenga mpaka zimeiinga katika ardhi yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, ukiunganisha suala hilo na hili la barabara, wao wametengeneza barabara za kuzunguka mipaka yao lakini sisi hatuna. Kwa sababu tumedhamiria kufanya hilo zoezi la kupima na kumilikisha kila kipande cha ardhi, naomba kuiasa Serikali ilipe kupaumbele zoezi hilo ili twende kwa kasi kubwa tuweze kuimarisha mipaka yetu na kuilinda hiyo rasilimali muhimu ya ardhi ambayo ndiyo chimbuko letu sisi sote.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia hili suala la barabara ni la muhimu sana katika kuzunguka hii mipaka yetu maana tulikuwa tunaenda mpaka nchi ya jirani ndiyo tuone beacon. Hili jambo siyo salama na ni lazima Serikali sasa ione umuhimu wa kutenga fedha za kutosha ili kuimarisha hiyo yetu mipaka.

Mheshimiwa Naibu Spika, nikija kwenye suala lingine la msingi la mawasiliano, katika hotuba ukurasa wa 51 yameongelewa mawasiliano ya Mkongo wa Taifa lakini kuna kipengele muhimu ambacho sijakiona mawasiliano ambayo nafikiri ni sehemu ya huduma za jamii, mawasiliano ya simu za mkononi. Sasa hivi simu ni kama sehemu ya uhai wetu, ukitaka kujua hebu Waheshimiwa Wabunge wote waambiwe waache kutumia simu kuanzia asubuhi mpaka jioni. Biashara zinaendeshwa kwa simu, mawasiliano na kila kitu kinafanyika kwa simu.

Mheshimiwa Naibu Spika, wananchi wengi katika baadhi ya maeneo nchi hii bado hawana hiyo huduma ya simu. Naomba zaidi Serikali itilie mkazo maeneo ya mpakani. Tumezungumza hiyo mipaka niliyoitaja kila mpaka wenzetu wa nchi tunayopakana nao wao wana minara ya simu na watu wetu wanatumia minara ya simu ya nchi nyingine wakati suala hilo pia ni la kiusalama. Naomba Serikali yetu iwekeze katika kusimamia ule Mfuko wa Mawasiliano kwa Wote, wawekezaji au wadau wa mitandao ya simu minara ijengwe katika vijiji vinavyopakana na mipaka ili kuimarisha ulinzi na ili wananchi wetu walio katika hii mipaka wapate minara.

Mheshimiwa Naibu Spika, ukianzia katika Wilaya yangu ambayo kilomita 300 tumepakana na nchi jirani ya Kenya ukienda Kata ya Kamwanga nusu ya watu wanatumia minara ya Kenya. Ukienda Kata za Matale, Wosiwosi na Kilailungwa wote wanatumia minara iliyoko Kenya na kuna Kata ndani ya Wilaya yangu ambazo hazina mawasiliano na Watanzania wale nao wanaona kwamba sasa ifike wakati wapewe minara ya simu kwambabu tuko karne ya teknolojia ya mawasiliano ya kielektroniki.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia napenda kugusia suala la mifugo. Ni kweli mifugo ni sekta ambayo haijapewa kipaumbele katika nchi hii. Kwa masikitiko niseme kwamba kuna zoezi lilifanyika la kuwadhibiti watu wanaovusha ng’ombe kupeleka Kenya katika mipaka ya Wilaya yangu, wale watu kweli walionewa. Sheria tumeweka sisi tukaweka na faini ambazo siyo za kiulihalisia na wananchi wale walikuwa wanakwenda kule kwa sababu hatuna masoko. Sasa hivi sisi tuna kiwanda cha mwekezaji kinajengwa mpakani kitakamilika mwezi Oktoba basi naomba Serikali
ijihusishe na kuweka mikakati thabiti ya kuhakikisha kwamba masoko ya uhakika yatapatikana. Serikali itoe bei elekezi kama inavyotoa katika mazao ya kilimo, waangalie minada ya nje wapange kabisa bei ambayo itawafanya wafugaji na wafanyabiashara wa mifugo wasipate sababu ya kutaka kuvusha ng’ombe na kuuza kwenye masoko ya ndani. Kwa kufanya hivyo, zile bidhaa nyingine kama ngozi, pembe, mifupa, kwato zitaweza kuongeza mnyororo wa thamani kwa sekta hii ya ufugaji.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Ahsante sana Mheshimiwa muda wako umekwisha.

MHE. DKT. STEVEN L. KIRUSWA: Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, naomba kuunga mkono hoja. (Makofi)