Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 - Ofisi ya Waziri Mkuu

Hon. Nuru Awadh Bafadhili

Sex

Female

Party

CUF

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 - Ofisi ya Waziri Mkuu

MHE. NURU A. BAFADHILI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Kwanza, nimshukuru Mwenyezi Mungu kuniwezesha kusimama mbele ya Bunge hili Tukufu na kuweza kuchangia. Vilevile nikushukuru wewe kwa kuweza kunipa nafasi hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, nitajikita kuzungumzia afya na hali ya kisiasa. Kwanza napenda kuipongeza Serikali kwa kujali afya za wananchi wake. Serikali imejitahidi imeweza kujenga zahanati, vituo vya afya na hospitali katika kila mkoa. Cha kusikitisha katika Jiji la Tanga, Kata ya Mianjani, wao wamejengewa zahanati na imemalizika toka mwaka jana lakini mpaka leo haijafunguliwa. Matokeo yake vibaka wanaingia kwenye zahanati ile wanaiba madirisha, milango na taa. Bahati nzuri Mwenyekiti wa Mtaa ametafuta walinzi na anawalipa ili kulinda ile zahanati. Kwa hiyo, naiomba Serikali ihakikishe kuwa zahanati hii inafunguliwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kila siku nikisimama hapa nazungumzia kuhusu hospitali yangu ya Bombo. Hospitali ya Bombo ipo katika Jiji la Tanga, ndiyo Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Tanga. Cha kusikitisha hospitali ile haina lift, wanatumia mabaunsa, sasa mabaunsa wakati mwingine wanawadondosha wagonjwa. Hebu Serikali ifikirie kwa moyo mkunjufu kuipelekea hospitali ile lift na kuweza kuwasaidia wale wagonjwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, katika kujali afya zetu Serikali yetu inatilia mkazo sana kuhusu vijana wanaojihusisha na madawa ya kulevya. Kwa kweli Serikali imejitahidi sana kupunguza hili wimbi la wanaotumia madawa ya kulevya lakini binadamu si sawa na mnyama, binadamu ana kila mbinu ya kuweza kufanya kumshinda mnyama.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa hivi vijana wetu wanapokosa hizi dawa za kulevya wamekuwa wezi wa zile taa zinazowashwa nyumbani zina unga mweupe unaotoka, wanachanganya na maji ya kuchanganyia sindano wanajichoma au wengine wanachukua valium wanasaga wanaweka kwenye sigara wanavuta. Kwa hiyo, Serikali bado ina kazi kubwa kwa hawa vijana ambao ndiyo nguvu kazi ya Taifa letu kwa sababu mimi nasema vijana ni taifa la leo. Sasa tukiwatupa hawa vijana, tukiwaacha wawe wamejihusisha kwenye madawa ya kulevya hatimaye tutajajikuta taifa ambalo linakosa nguvu kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nikizungumza kuhusu hali ya siasa. Tunajua mwaka huu 2019 tutakuwa na Uchaguzi wa Serikali za Mitaa na mwakani tutakuwa na Uchaguzi Mkuu. Katika chaguzi unapotaka kupiga kura unatakiwa uwe na kitambulisho cha uraia na cha kupigia kura. Kuna baadhi ya vijana ambao wakati vitambulisho vya uraia vinatoka walikuwa hawajatimiza miaka 18, sasa hivi tayari wameshatimiza miaka 18 lakini wakati mwingine wanapovifuatilia vitambulisho vile vya uraia inakuwa ni tabu sana kuvipata.

Mheshimiwa Naibu Spika, masikitiko yangu, mimi nashangaa sisi tunaambiwa tuwe na vitambulisho vya uraia au kitambulisho cha kupiga kura ili kiweze kutusaidia wakati wa kupiga kura. Nilikuja kushangaa wakati wa marudio ya Chaguzi za Madiwani katika Kata, Mkurugenzi wangu wa Jiji la Tanga alitoa Waraka kuwa ambaye atakuwa hana kitambulisho cha kupigia kura au cha uraia anaweza kutumia aidha passport au leseni ya udereva. Sasa kumbe kuna leseni za udereva, passport na kadhalika kuna haja gani ya kuwa na vitambulisho hivyo? Hii inasababisha kuleta faulo katika uchaguzi kwa sababu watu wanachukuliwa kutoka mitaa mingine na kuja kupiga kura pale. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kama hiyo haitoshi, tunajua katika kituo cha kupigia kura kuna orodha ya wapiga kura, anayekuja pale anaenda kuangalia jina lake lakini cha kushangaza kituo kile kile cha kupigia kura Msimamizi wa Uchaguzi tena ana karatasi yake nyingine. Kwa hiyo, wale wanaokuja aidha na passport, leseni au birth certificate yake wanapiga kura na unajua hivi hivi kuwa hawa watu si wakazi wa eneo husika, wanachukuliwa kwa magari, wanaletwa wanapiga kura, hii inahatarisha pia amani ya nchi. Kwa hiyo, Serikali ihakikishe kuwa anayepiga kura ni yule anayefuata masharti ya kupiga kura. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile nataka kuzungumzia kuhusu zao la michikichi. Tunashukuru Serikali imeipa kipaumbele zao la michikichi. Kweli michikichi ni zao ambalo litaleta faida sana kwa nchi yetu. Wenzetu Malaysia wameendelea kwa sababu ya zao la michikichi. Katika historia michikichi hiyo ya Malaysia nasikia ilitolewa huku huku Tanzania ikapelekwa kwao.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, naomba Serikali isielekeze kilimo cha michikichi katika Mkoa wa Kigoma peke yake ipeleke pia zao hili katika mikoa ambayo michikichi inaweza ikastawi ili watu waweze kuvuna mafuta ambapo tutakuwa tunatumia mafuta yetu sisi wenyewe kwa afya yetu kuliko kutumia mafuta ambayo yanatuathiri. Kuna mafuta tunayoletewa ambayo siyo mazuri, yana cholesterol ambayo inaweza ikatuletea matatizo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kumalizia naomba kama itawezekana Serikali iangalie sana wazee. Kuna wazee ambao wanaishi katika nyumba za wazee wasiojiweza. Nina hakika Serikali inatenga fungu kwa ajili ya kuwahudumia wazee wale lakini utakuta hali zao ni duni halafu wanarandaranda mitaani kuomba, ile ni aibu kwa taifa letu, kumbe wana vituo vyao.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, katika vituo vyao wangekuwa wanaangaliwa kwa malazi, chakula na kwa afya zao kwa sababu utakuta kwenye vituo vingine vya kulelea wazee wale afya zao sio nzuri, sehemu wanazo lala sio nzuri, utakuta wengine godoro analolalia lina mikojo mpaka wanatoka funza kiasi cha kumkosesha raha yule mzee. Kwa hiyo, Serikali iangalie umuhimu na pia iwasisitize wale wanaohusika kuangalia wale wazee wawe wanapata chakula cha kutosha na tiba na pia wawazuie wasirande mitaani kwa sababu anapokuja mgeni akiona watu wanarandaranda mitaani kwa kweli ni aibu kwa Taifa letu.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, nasema ahsante sana. (Makofi)