Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 - Ofisi ya Waziri Mkuu

Hon. Jitu Vrajlal Soni

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Babati Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 - Ofisi ya Waziri Mkuu

MHE. JITU V. SONI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Awali ya yote naomba nichukue fursa hii kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa siku ya leo, lakini pia nichukue fursa hii kumpongeza Rais wetu kwa kazi kubwa na nzuri anayofanya, lakini pia Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa kazi kubwa na nzuri na Wizara yake inavyofanya.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia nichukue fursa hii kumpongeza Mheshimiwa Rais kwa kuanzisha Wizara ya Uwekezaji, lakini pia kuhamisha Kituo cha Uwekezaji (TIC) katika Ofisi ya Waziri Mkuu. Jambo hili tulikuwa tumelisemea kwa muda mrefu sana kwamba lazima pawe na chombo Serikalini ambacho kitakuwa kinaratibu, kinaunganisha Wizara mbalimbali na ndiyo kinaelekeza ili Serikali iweze kufanya kazi kama Serikali moja.

Mheshimiwa Naibu Spika, siku zote tulikuwa tunasema huko nyuma hakuna uratibu ndani ya Serikali, kila Wizara ilikuwa inajitahidi ifanye mema katika sekta yake, lakini bila kuwa na uratibu na kufanya kazi kwa pamoja, Serikali kama Serikali isingefanikiwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru na ninawapongeza Waheshimiwa Mawaziri wote katika Ofisi ya Waziri Mkuu, tena ni akina mama wote wawili, Mheshimiwa Jenister na Mheshimiwa Kairuki. Ni akina mama ambao wanajiamini na wanaweza kuchukua maamuzi magumu. Pia Manaibu Waziri, Makatibu Wakuu na timu nzima kwa kazi nzuri wanayofanya. Mimi ombi langu ni moja, naomba Waziri wa Uwekezaji ndio awe mratibu mkuu kwa shughuli zote hasa katika biashara inayofanyika hapa nchini katika sekta zote.

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kwa sababu hili suala tunalozungumza kuhusu urahisi wa kufanya biashara Tanzania, umekuwa mgumu kutokana na kodi, tozo, ada na urasimu mwingi. Hiyo inaweza kuondolewa na Wizara ya Uwekezaji; siyo kwa wawekezaji wa nje tu, lakini pia kwa uwekezaji wa ndani uwe mkubwa au mdogo. Wizara hii inaweza kufanya kazi kubwa.

Mhshimiwa Naibu Spika, nilipitia bajeti yao lakini bado naona bajeti waliyopewa ni ndogo. Nilikuwa naomba kama inawezekana Wizara hii iongezewe bajeti ili wawe na fedha ya kutosha kufanya utafiti lakini pia waweze kufanya kazi ambazo zinaweza kuunganisha Wizara nyingine zote. Ni vizuri sasa Mawaziri wengine kupitia Wizara zao watoe ushirikiano wa karibu sana na Waziri wa Uwekezaji ili mambo yetu yaweze kwenda vizuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, muhimu kwenye suala hili, ili pawe na urahisi wa kufanya biashara, tunahitaji kuwa na One Stop Center. Sheria inasema, kutokujua sheria siyo kinga. Hivi kila Mtanzania, kama wako milioni 20 wanafanyabiashara, hivi kila mmoja atajua sheria zote? Leo hii tunakwama kwa sababu sekta ambayo ni rasmi inazidi kupungua na sekta isiyokuwa rasmi inazidi kuongezeka kutokana na urasimu na utaratibu ambao ni mbovu.

Mheshimiwa Naibu Spika, Sekta isiyokuwa rasmi inazidi kukua kutokana na tozo, ada, kodi mbalimbali ambazo zinatokana na taasisi za udhibiti (Regulatory Boardies) charges zao zimekuwa kubwa. Leo hii wote sasa wanashindana kukusanya mapato kwa kupitia fine au tozo mbalimbali ili kuonekana Wizara zao zinakusanya mapato makubwa. Mapato yalitakiwa yatokane na faida inayopatikana na kodi ya hiari watu walipe, hapo ndiyo utaona uchumi umekua na watu wanafanya biashara na wanaridhika kulipa kodi.

Mheshimiwa Naibu Spika, zile tozo ni kubwa mno. Mheshimiwa Rais juzi alisema kwamba liangaliwe na kama ni sheria ziletwe. Huu ndiyo wakati wa kubadilisha hizo sheria na tozo mbalimbali ili ziendane na viwango. Cost of production ikiwa kubwa hata tukiwekeza; kama sukari yetu au mafuta gharama ya kuzalisha ndani ya nchi ikiwa kubwa, hatuwezi kushindana na ile inayotoka nje. Mtu akitoka nje, akilipa kodi zote hata ukiweka mara mbili, bado ni rahisi kuliko ile ya ndani. Ni vizuri sasa ile blueprint tuifanyie kazi; na siyo kuifanyia kazi kwa kuleta tu Bungeni kwa kuturidhisha sisi, lakini ifanyiwe kazi ili iwe na mafanikio makubwa, ili biashara zetu zikue, viwanda vikue na hali ya ufanyaji wa biashara uwe mzuri hapa nchini.

Mheshimiwa Naibu Spika, muhimu ni kuangalia namna ya kupunguza zile tozo na kodi mbalimbali. Sasa tukija kwenye kila sekta, tutaleta hasa kwenye Finance Bill kwamba hivi ni vitu ambavyo vinatakiwa viondolewe au vipunguzwe ili tuweze kuzalisha bidhaa zetu kwa gharama nafuu, bidhaa ambazo tunaweza kuzalisha humu humu nchini.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kupitia Wizara ya Uwekezaji, sisi tuna bidhaa kama nne au tano, tungeweka muda kwamba ndani ya miaka mitatu tunataka tuwe tunazalisha nchini na tusiagize kutoka nje, tutakuwa na mafanikio makubwa, moja ni mbegu ambayo kwa asilimia 76 tunaagiza kutoka nje ya nchi ambayo hata usalama wa chakula hakuna; lakini pia mafuta ya kula, sukari, maziwa, nyama, samaki lakini pia mboga mboga na matunda. Ni vitu hivyo tu ambavyo tunaweza kuzalisha hapa nchini, hivyo ni vizuri kwa kupitia Wizara ya Uwekezaji tufanye hiyo kazi na Serikali iwekeze katika hayo maeneo tuweze kufanikiwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali isipowekeza kwenye utafiti, bado hatutafanikiwa kwa sababu bila utafiti hatutakuwa na maendeleo. Ni vizuri tuwekeze kwenye suala la utafiti.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia asilimia kubwa ya Watanzania wako kwenye Sekta ya Kilimo, zaidi ya asilimia 75. Vijana wetu wanaosoma, wengi sasa hivi ajira hakuna kutokana na fani walizosomea ajira hizo hakuna. Ni vizuri Serikali sasa ikubali maombi yetu ya muda mrefu kwamba huko nyuma tuliondoa Skill Development Levy, ile 4% tukaipungua 2% kwenda kwenye Loans Board. Naomba asilimia mbili ile ambayo tumeipeleka kwenye Loans Board sasa irudi kwenye Skills Development Levy iende VETA ili tuwekeze kwenye shule zetu hizi za ufundi ili watu wengi waweze kusoma ufundi kwa kuwa ajira zao zipo na hizo kazi uhitaji wao ni mwingi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo namna ya kuongeza ajira ni kuwekeza kwenye shule zetu za ufundi ili tupate vijana wengi ambao wanaweza wakapata ajira za kawaida ambao uhitaji ni mkubwa; iwe kwenye sekta yoyote, iwe kilimo, mifugo, hata kwenye Sekta ya Madini, tukitaka value addition bila kuwekeza kwenye Vocational Training watu ambao watajua kusanifu na kuchonga madini yetu ili tuzalishe bidhaa hapa hapa, hatutafanikiwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, naomba ile 2% ambayo tuliipeleka katika kipindi tulichokuwa na dharura, hatukuwa na fedha ya mikopo, basi turudishe irudi kwenye VETA. Mbali na hiyo, ni vizuri pia tukaangalia namna ya kuhakikisha kuwa hiyo One Stop Center iwe na mafanikio makubwa kwa biashara kubwa na ndogo, lakini pia Ofisi ya Uwekezaji iweze kukaa na Wizara mbalimbali. Leo hii ili waonekane wanafanya kazi kubwa, wanaanza kudai tozo na ada ya miaka kumi nyuma. Unakuta mtu wa TFDA anakuja anakudai vitu vya miaka kumi nyuma. Unakuta OSHA, Regulatory Boardies, yaani Taasisi za Udhibiti, zinakuja kukudai vitu vya miaka 10 nyuma. Je, siku zote walikuwa wapi? Sasa ni vizuri tukafutilia mbali madeni ya nyuma, wakaanza leo kwa sababu waliolala usingizi walikuwa ni wao, sio wafanyabiashara. Mfanyabiashara kutokujua sheria, siyo kosa lake. Sasa ni vizuri haya yakafanyiwa kazi na ninaamini kabisa kwamba hali ya ufanyaji biashara itakuwa na unafuu.

Mheshimiwa Naibu Spika, mbali na hiyo, ni vizuri pia sekta binafsi kwa kupitia Baraza la Uwezeshaji lakini pia kwa kupitia Baraza la Biashara Taifa ambalo iko chini ya Ofisi ya Waziri Mkuu, liweze kufanya kazi kubwa na kuunganisha na kuangalia kwamba nini kinahitajika ili kazi iweze kwenda vizuri.

Mheshimiwa Naibu Spika watu wamezungumzia urasimu, namshukuru Waziri wa Uwekezaji, juzi kulikuwa na vibali ambavyo vilitakiwa vitolewa ili mtu aanze kuwekeza kwenye Kiwanda cha Sukari. Aliweza kupiga simu mbili na ndani ya wiki moja kibali kikatoka, lakini yule mtu alihangaika zaidi ya miezi sita, ilikuwa hapati. Sasa ni vizuri pawe na mfumo au website ili hata kama mtu anaomba katika Wizara nyingine aweze kutoa taarifa hiyo kwa Waziri wa Uwekezaji ili Ofisi yake iweze kufanya kazi ya uratibu kwamba kwa nini hiki kitu hakijatoka kwa muda maalum? Kwa sababu watu wakipata vibali kwa muda maalum, nina uhakika watu watawekeza na mambo yetu yataenda vizuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna jambo lingine ambalo ni muhimu sana, kwamba tukija kwenye Finance Bill kwa kupitia Waziri wa Uwekezaji na Waziri wa Kazi, ni vizuri tukaangalia hizi kodi mbalimbali ambazo ni kubwa, tuzipunguze lakini tukizipunguza hatutapata tatizo lolote kwenye ukusanyaji kwa sababu compliance itakuwa kubwa. Leo hii kama kodi ni kubwa watu wengi wanaendelea kukwepa, juzi Mheshimiwa Rais amezungumza vizuri sana, naamini muda huu ni muafaka, amezungumzia kipindi cha Bunge la Bajeti, tutaweza kufanikiwa kwa sehemu kubwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, mbali na hiyo, wengi wamezungumzia suala la vibali; upatikanaji wa permit. Kwa watu ambao wanawekeza, kuna aina mbili; kuna wale ambalo ni skilled labour ambao wana vyeti vyao vyote, lakini pia kuna unskilled labour, lakini ana uzoefu mkubwa. Vile vile mwangalie wale ambao ni unskilled lakini wana uzoefu, vibali hivyo viwe vinatoka kwa urahisi zaidi ili biashara hizo ziweze kufanyiwa kazi na Serikali itapata kodi kubwa na watu wetu wa humu ndani pia wataweza kujifunza kutokana na suala hilo.

Mheshimiwa Naibu Spika, mbali na hayo, napongeza tu kwa kuanzishwa kwa Wizara hii ya Uwekezaji na ninaamini kabisa kwamba kwa kupitia Ofisi ya Waziri Mkuu, Wizara zote hizi zikifanya kazi vizuri kwa ushirikiano, tutakuwa na mafanikio makubwa na tutaweza kuhakikisha kwamba nchi yetu inapata viwanda vingi, biashara inakua na uchumi wetu unakua. Wananchi wa…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)