Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 - Ofisi ya Waziri Mkuu

Hon. Musa Rashid Ntimizi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Igalula

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 - Ofisi ya Waziri Mkuu

MHE. MUSSA R. NTIMIZI: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kupata nafasi ya kuchangia hotuba ya bajeti ya Ofisi ya Waziri Mkuu. Kwanza kabisa naomba nichukue nafasi hii kumpongeza Waziri Mkuu kwa kazi kubwa anayoifanya na Watanzania wanaiona. Anafanya kazi anajitoa sana, anatembelea kwenye majimbo yetu, anahakikisha kabisa kwamba utekelezaji wa Ilani ya Chama cha Mapinduzi inakwenda sawasawa. Hata hivyo, kwa kufanya kwake kazi vizuri ana wasaidizi wake lazima na wenyewe tuwapongeze, hawalali usiku na mchana kuhakikisha kwamba kazi zinakwenda sawasawa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nimpongeze sana Mheshimiwa Mhagama, dada yangu anafanya kazi nzuri sana; Mheshimiwa Kairuki, anafanya kazi nzuri sana; Mheshimiwa mdogo wangu Mavunde, big up anafanya kazi nzuri sana, hatuangushi vijana wenzake; Mheshimiwa Stella Ikupa anafanya kazi nzuri nzuri sana. Kwa ujumla Ofisi ya Waziri Mkuu inaratibu mambo vizuri na mambo yanakwenda sawasawa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, miaka minne iliyopita tulikuwa tunaiomba Serikali kutekeleza ahadi ambazo tuliziahidi wakati wa uchaguzi. Leo katika kipindi cha miaka minne tuna haki leo Wabunge kusimama hapa na kuipongeza Serikali kwa kazi kubwa iliyoifanya kwa kutekeleza Ilani ya Uchaguzi ambayo tulikuwa tumeahidi. Kwa hiyo sisi Wabunge wa CCM tunajivunia, tunakwenda kwenye uchaguzi mambo yetu yakiwa yako juu sana na kazi hii imefanywa vizuri kwa uratibu wa Ofisi ya Waziri Mkuu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa nini tunasema kwamba tunakwenda vizuri. Naomba niseme maneno machache, hasa mimi natoa mfano kwenye Jimbo langu la Igalula na nchi yetu kwa ujumla, kuna watu wanazungumza ujenzi wa standard gauge hauna faida kwa nchi yetu. Tulikuwa tunalalamika mizigo, sisi ambao tunatoa mikoa ambayo reli ya kati inapita, reli iliyokuwepo ilikuwa ni tatizo kubwa kwa usafiri wa wananchi wa mikoa hiyo, usafirishaji wa mizigo ulishuka kwa asilimia kubwa sana kwa sababu ya reli yenyewe kutobudu uzito wa mizigo inayosafirishwa kwa reli hiyo, leo tunajenga reli ambayo itabeba mizigo mizito na mizigo mingi.

Mheshimiwa Naibu Spika, si hivyo tu, pia tunazungumzia muda wa usafiri utakuwa mchache, maana yake kutoka Dar es Salaam kwenda Tabora unakwenda kwa saa tano, wakati tulikuwa tunakwenda kwa siku tatu, tunaadhirika sana njia. Kwa hiyo sisi tunaotoka katika maeneo yale tunaona umuhimu wa standard gauge kwa maana reli ya kisasa inayokuja, tutakuwa na uhakika wa gharama za usafiri zitakuwa ndogo, tutakuwa na uhakika wa safari yetu kwa sababu zamani treni ilikuwa inadondoka sana, sasa hivi tutakuwa uhakika wa usalama wa safari yetu. Kwa hiyo unapozungumzia standard gauge kwa wananchi wa Igalula tunatarajia itasafirisha tumbaku yetu toka Igalula kwenda sokoni kwa gharama nzuri na kwa muda ambao unategemewa kuwa mdogo sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, sisi katika Igalula tunashukuru, tulikuja tukazungumza kwamba kuna maboma mengi wananchi wamejenga kwa nguvu zao yanatakiwa Serikali itenge fedha kuyakamilisha. Nataka kusema tumepekea milioni 500 kukamilisha ujenzi wa madarasa ya shule za misingi na shule za sekondari katika Jimbo la Igalula ambazo zilianzishwa na nguvu za wananchi. Kwa hiyo katika bajeti hii ya Waziri Mkuu, naomba nifikishe salamu za wananchi wa Igalula zile nguvu zao walizoziweka katika kujenga maboma yale Serikali imeona uwezekano wa kuwasaidia na imetuletea zaidi ya shilingi milioni 500. Ambacho tunakiomba, tuna maboma mengi zaidi, tunaomba tuendelee kuangaliwa ili tuweze kusaidia nguvu za wananchi ambazo wameziwekeza katika maeneo mbalimbali ikiwemo pia kwenye eneo la afya.

Mheshimiwa Naibu Spika, upo upungufu mchache ambao tunaomba Serikali iendelee kuuangalia ili wananchi wa Igalula waendelee kuwa juu kama vile ambavyo Serikali yetu ipo juu katika kutekeleza miradi mbalimbali ya maendeleo. Katika Mkoa wetu wa Tabora tuna takribani kilomita 8,000 za barabara, lakini tunaletewa shilingi bilioni nane kutengeneza zile kilomita 8,000, hazitoshi, mtandao wa barabara ni mkubwa na fedha tunazoletewa ni ndogo.

Mheshimiwa Naibu Spika, niombe Serikali iungalie Mkoa wetu wa Tabora, tuongezewe fedha ili ziweze kusaidia huu mtandao mkubwa wa barabara uliopo katika Mkoa wetu wa Tabora. Hata hivyo, nishauri katika eneo letu la kilimo, miaka yote tunashauri kilimo cha umwagiliaji ndio kitakuwa mkombozi wa wananchi wetu ambao wanalima huko vijijini, tusipowekeza katika kilimo cha umwagiliaji, hatutowasaidia wananchi wetu. Naomba Serikali iliangalie hili ili tuongeze tija katika kilimo, tuweze kupata pato la wananchi wetu na tuweze kupata pato la nchi kwa ujumla wake.

Mheshimiwa Naibu Spika, leo nataka niishukuru sana Serikali kwa kazi kubwa inayoifanya, lakini niombe katika Mkoa wetu wa Tabora, Wilaya yetu ya Uyui ni Wilaya kubwa sana, DC wetu aangaliwe sana. Mwaka wa nne sasa hana gari na wilaya ni kubwa, anahitaji kufanya kazi ya ziada kusimamia miradi mingi ambayo inakuja katika Mkoa wetu wa Tabara. Niombe sana tuweze kuangalia namna ya kusaidia.

Mheshimiwa Naibu Spika, bado inahitajika nguvu kubwa katika eneo la afya. Sisi katika Jimbo la Igalula tumejenga vituo zaidi ya vitano lakini tumepata fedha za kituo kimoja cha afya. Nina hakika katika bajeti hii inayokuja tutaendelea kuangalia nguvu hizi za wananchi na kuongeza fedha na zaidi ili ziweze kusaidia kuondoa tatizo la afya kwa wananchi wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka nimalizie, kwa miradi ambayo inafanyika katika maeneo yetu, mimi nitoe mfano wa mwisho, katika barabara tumepokea zaidi ya bilioni mbili za barabara zetu za ndani katika Jimbo la Igalula, kwa nini tusiishukuru Serikali yetu ya Awamu ya Tano kwa kazi kubwa ambayo inaifanya. Tumepata zaidi ya bilioni 149 za kujenga barabara ya lami ya Chaya - Nyahua ya kilomita 189 ambayo inakaribia kwisha, ni lazima tuendelee kuishukuru Serikali kwa kazi nzuri ambayo inaifanya na tunazidi kuwapa moyo kwamba Wabunge wenu wa CCM tunaona kazi ambayo inafanyika na tunazidi kuwatia moyo kwamba wanafanya kazi nzuri sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niunge mkono hoja na ahsante sana. (Makofi)