Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 - Ofisi ya Waziri Mkuu

Hon. Oran Manase Njeza

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbeya Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 - Ofisi ya Waziri Mkuu

MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa kunipa hii fursa nami nichangie katika bajeti muhimu Ofisi ya Waziri Mkuu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza naanza kwa kumpongeza Mheshimiwa Waziri Mkuu, kwa kasi kubwa anayoifanya kuhakikisha kuwa Serikali yetu inaendeshwa na kuleta ufanisi katika maeneo yote ili uwepo ufanisi katika kuwaletea wananchi maendeleo ya kiuchumi na pia ya kijamii. Napenda pia kuwapongeza Mawaziri wote na watendaji wote wa Wizara hii na bila kusahau kumpongeza Mheshimiwa Rais kwa kazi kubwa aliyoifanya ya kuleta transformation (mageuzi) makubwa kwa nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa ajili ya muda labda napenda niorodheshe machache tu aliyofanya nikianzia kwenye Jimbo langu. Kwenye suala la umeme tulikuwa na vijiji 10 tu mwaka 2015 lakini leo tuna asilimia karibu 80 ya vijiji vinavyokaribia 200. Angalia ni mafanikio ya aina gani ambayo yamepatikana katika kipindi hiki kifupi. Pia tunategemea hizi kata mbili zilizobaki nazo zitakamilishwa ndani ya miaka hii miwili. Tunashukuru sana kwa utendaji wa Wizara na Mheshimiwa Rais kwa maagizo yake yeye mwenyewe ambayo yametufanya Mbeya Vijiji tukafanya vizuri kwenye nishati. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ni suala la afya. Katika Wilaya yetu ya Mbeya tulikuwa hatuna Hospitali ya Wilaya na katika Miji mikubwa kama Mbalizi tulikuwa hatuna hata kituo cha afya lakini katika kipindi hiki cha miaka mitatu tumeweza kufanikiwa kujenga vituo vya kisasa vitatu katika Kata za Ilembo, Ikukwa na Santilia. Kwa kuongezea, tumepata na pesa kwa ajili ya kujenga Hospitali ya Wilaya. Tunaishukuru sana Serikali, kwa kweli hayo ni mageuzi makubwa sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hilo tuishukuru vilevile Serikali kwa kuweza kuifikiria Mbeya Vijijini kutuletea Chuo Kikuu cha Afya. Chuo hiki kitakuwa sehemu ya Chuo Kikuu cha Muhimbili ambacho nategemea katika mikakati kitaanza kufanya kazi hivi karibuni. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la elimu nalo tumefanya vizuri sana, imeirudisha Mbeya katika zile nafasi zake muhimu. Kwa mwaka huu Mbeya iko kwenye nafasi 10 bora na kitaaluma maeneo yote tumefanya vizuri mno. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye jimbo langu tumeweza kuongeza shule tatu za sekondari na shule moja ya high school. Katika hizo shule tatu, tuna shule ya wasichana ya bweni ambayo imejengwa na wananchi lakini tumepata msaada kidogo wa Serikali. Kwa hiyo, tunaishukuru sana Serikali kwa hilo na tunategemea waendelee tena kuipa msukumo elimu kwa vile ndiyo msingi wa maendeleo ya nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye miundombinu Serikali imetufanyia mengi mazuri ikiwemo barabara lakini bado tuna changamoto kubwa kwenye barabara zetu za Mbeya Vijijini. Kama alivyosema mwenzangu aliyotangulia tuna tatizo la TARURA. TARURA wanafanya kazi vizuri lakini bajeti yao ni ndogo. Bajeti ya matengenezo ya dharura hakuna, sasa kwa maeneo ya mvua nyingi kama Mbeya Vijijini wanatengeneza barabara leo, madaraja yote unakuta yameondolewa na mafuriko, hawana namna ya kutusaidia. Tunaiomba Serikali iangalie namna gani itaboresha bajeti ya TARURA. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye suala la maji, Wizara ya Maji pamoja na Serikali kwa ujumla wamefanya kazi kubwa kwa Halmashauri yetu ya Wilaya ya Mbeya. Mheshimiwa Waziri na Mheshimiwa Naibu Waziri wamekuja wao na wameweza kusukuma na tumekamilisha miradi ya vijiji karibu zaidi ya 10. Tumekamilisha miradi ya Mbawi, Jojo, Haporoto na Idimi na sasa hivi tunakamilisha vijiji kwenye Kata za Igale na Izumbwe lakini bado tunahitaji maboresho kwenye Mji Mdogo wa Mbalizi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye suala la kilimo ambacho ndiyo msingi wa kila kitu, kwa kweli pamoja na juhudi za wananchi lakini bado tuna changamoto kubwa za masoko. Naiomba Serikali ijaribu kuangalia ni namna gani itaboreshe masoko ya mazao yetu. Kwenye kahawa, pareto na hata mahindi hatufanyi vizuri. Pamoja na matumizi ya mbolea napo hatuko vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naiomba Serikali iangalie namna gani tutumie malighafi tulizonazo hapa nchi kwa ajili ya kuanzisha viwanda vya pembejeo. Chokaa inazalishwa sana hapa nchini lakini ni muhimu sana kama sehemu ya pembejeo. Chokaa inasaidia kutibu ardhi kwa vile ina calcium na magnesium ambayo inasaidia ardhi yetu iliyochoka ili mbolea iweze kutumika vizuri. Ukiweza kufanya application ya chokaa udongo utakuwa vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye suala la kahawa, juzi tulikuwa na Mkutano wa Wadau wa Kahawa na niishukuru sana Bodi ya Kahawa iliandaa mkutano mzuri sana, tukaangalia changamoto nyingi sana. Kitu ambacho nimekipenda ni mkakati wa kuboresha soko la kahawa ambalo napenda msisitizo uwe kwenye direct export, wananchi waweze kuuza kahawa yao moja kwa moja nje ya Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile na uanzishwaji wa hiki chombo kipya kinaitwa Tanzania Commodity Exchange Market (TMX) inaweza kutusaidia kutuokoa katika janga kubwa ambapo kahawa yetu ni nzuri lakini bei yake ni ndogo ukilinganisha na wenzetu wa jirani. Kwa mfano tu, kahawa ya Kenya arabica wenzetu katika kipindi hiki wanauza mpaka dola 200 kwa kilo 50 sisi ni chini ya dola 100 pamoja na kahawa yetu kuwa nzuri kuliko yao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile tuna pareto, nashangaa ni kwa nini haijaingizwa katika mazao muhimu ya kimkakati. Tanzania sisi tunaongoza Afrika kwa kulima pareto na ni wa pili duniani. Sasa zao kama hili la kimkakati ni kwa nini limesahauliwa na fursa bado zipo za kuweza kuzalisha pareto nyingi, mahitaji ni zaidi ya tani 20,000 na uzalishaji duniani ni chini ya tani 10,000. Tanzania pamoja na kuwa wa pili na wa kwanza Afrika tunazalisha tani 1,000 tu. Katika zao hili nalo naomba suala la masoko liweze kutiliwa maanani ili wananchi waweze kupata faida ya uzalishaji wa pareto.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa Njeza, muda wetu hauko rafiki.

MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja. (Makofi)