Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 - Ofisi ya Waziri Mkuu

Hon. Joseph Leonard Haule

Sex

Male

Party

CHADEMA

Constituent

Mikumi

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 - Ofisi ya Waziri Mkuu

MHE. JOSEPH L. HAULE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kuweza kuchangia hoja hii ya Ofisi ya Waziri Mkuu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, mafao ya wafanyakazi wa iliyokuwa Kilombero Sugar Company ambayo mwaka 1999 ilibinafsishwa kwa mwekezaji wa Illovo. Wafanyakazi zaidi ya 3,000 ambao walifanya kazi kwa weledi mkubwa walishastaafishwa mwaka 1999 – 2000. Kampuni ya Kilombero Sugar ilipobinafsishwa mpaka sasa wanapigwa danadana kuhusu mafao yao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi kama Mbunge nilishafanya jitihada za kuwaleta wawakilishi wa wazee hawa mpaka kwa Waziri Jenista Mhagama, lakini mpaka leo bado hawajapatiwa ufumbuzi wa malipo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nilileta mara kadhaa swali la msingi hapa Bungeni, lakini cha kustaajabisha swali hili limekuwa haliletwi kabisa kwenye order paper, jambo ambalo linatupa wasiwasi kwamba, Serikali haina majibu ya swali lao kwamba ni ni lini watu hawa maskini watalipwa mafao yao?

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama hilo halitoshi, Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt.John Pombe Magufuli alipofanya ziara kwenye uzinduzi wa barabara ya Kidatu – Kilombero, nilimwomba atusaidie ili wafanyakazi hawa ambao wengi wao wameshakuwa watu wazima sana na wengine wameshatangulia mbele za haki, bila kulipwa stahiki zao kitu ambacho kwa kweli kinawafanya waishi kwenye maisha duni sana huku wengine wakiwa hawana hata uwezo wa kuhudumia familia zao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa masikitiko makubwa kabisa, Mheshimiwa Rais ambaye aliwapa moyo sana wananchi hawa kwa kuwaambia kuwa atahakikisha wanapata stahiki zao na atazungumza na Mawaziri husika lakini mpaka leo wananchi hawa bado hawajapata majibu yoyote na hawajui leo yao wala kesho yao. Namwomba sana Waziri akija kwenye majumuisho ya hoja yake, atupe majibu; Je, ni lini hasa waliokuwa wafanyakazi 3,000 wa Kilombero Sugar Company watalipwa mafao yao?

Mheshimiwa Mwenyekiti, wafanyakazi wa Serikali waliopunguzwa na baadaye kurudishwa kwenye zoezi la vyeti feki; kuna idadi kubwa sana ya watumishi katika Wilaya ya Kilosa ambao walipunguzwa kwenye zoezi la vyeti feki, lakini baadaye wakaonekana wanastahili kuendelea na kazi lakini mpaka sasa hawajalipwa pesa zao walizokuwa wanastahili, kupokea kipindi walipokuwa Watendaji wa Vijiji, Walimu, Watumishi wa Afya, Madereva na kadhalika. Nakumbuka Waziri wa Utumishi alisema, watu wote waliosimamishwa kimakosa watalipwa stahiki zao, ningependa kujua, je, watumishi hawa wa Serikali watalipwa lini?

Mheshimiwa Mwenyekiti, bajeti ya TARURA ni ndogo sana, lakini pia TARURA wanafanya kazi yao ya kutengeneza barabara za ndani ya Halmashauri ya Wilaya ya Kilosa kwa kusuasua sana, kwa mfano, barabara ya Ruaha Mbuyuni – Malolo – Kibakwe ambayo ni muhimu sana kwa wakulima wetu na kwa umuhimu huo pia, barabara hii inaunganisha Mikoa ya Morogoro – Iringa na Dodoma. Tuliomba ipandishwe hadhi ili ihudumiwe na TANROAD lakini mpaka sasa barabara hii inaharibika sana na kuna kipindi haipitiki kabisa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara ya muhimu ya Ulaya – Madizini – Malolo – Kibakwe pia ni muhimu sana inayounganisha Mikoa ya Morogoro – Iringa na Dodoma, lakini imekuwa haipitiki hasa kipindi kama hiki cha masika, naomba sana waifikirie ili iweze kuhudumia wananchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kumekuwa na kusuasua sana kwa zoezi la uunganishwaji wa nishati ya umeme kwenye Jimbo la Mikumi, ningependa kujua; je, ni lini Serikali itaweka umeme kenye barabara kuu ya Tanzania – Zambia hasa maeneo ya kona za Msimba, Ng’apa na kadhalika ambapo panaunganisha na maeneo ya Ruaha Darajani lakini umeme unapita juu na kushindwa kuunganishwa umeme kwenye maeneo yao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nimeshauliza mara kadhaa hapa Bungeni kuhusu jimbo letu lenye sifa kubwa ya utalii, lakini maeneo mengi ni ya giza. Je, ni lini Serikali itakamilisha ahadi yake ya kuwaunganishia umeme wananchi wa Kata za Vidunda, Ulelingombe, Malolo, Wedo
– Kisanga, Zombo, Ulaya, Mhenda, Tindiga, Mbamba, Kiduhi, Tambukareli, Kikwalaza, Munisagala, Dodoma Isanga, Udung’u Mgogozi, Chabi, Kielezo, Gezaulole, Dinima na kadhalika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Jimbo la Mikumi tumekuwa na matatizo makubwa sana ya mawasiliano ya simu. Mfano, barabara ya TANZAM (Tanzania – Zambia), pale maeneo ya Msimba, Iyovi na Ng’apa kumekuwa kuna ajali nyingi sana na sehemu hii ina kona kali nyingi sana na ajali nyingi sana zimekuwa zinatokea, lakini jambo baya kabisa ni kuwa, maeneo haya kuanzia Msimba mpaka Ruaha Mbuyuni hakuna mawasiliano yoyote yale ya simu na hakuna umeme kabisa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niiombe sana Serikali ilitupie jicho la huruma eneo hili ambapo wasafiri wengi sana wa ndani ya nchi na wengi wa nje ya nchi wanapata matatizo mbalimbali lakini hawawezi kuwasiliana na wenzao na kusubiri kudra za Mwenyezi Mungu tu. Pia, katika Jimbo la Mikumi kwenye Kata za Vidunda, Malolo, Tindiga, Kisanga, Kilangali, Ulelingombe, mabwerebwere na eneo la muhimu kabisa la katikati ya Hifadhi ya Mikumi ambalo ni muhimu sana kwa watalii na linaongeza sana pato la Taifa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ujenzi wa tuta la Mto Miyombo/Bwawa la Kidete; nashukuru sana Ofisi hii ya Waziri Mkuu kwa kuwa mara nyingi wamekuwa wakitusaidia pale tunapopata maafa ya mafuriko kwenye Wilaya yetu ya Kilosa na Jimbo la Mikumi. Kubwa ni kupasuka kwa kuta za Bwawa la Kidete ambalo Serikali kila siku imekuwa ikituahidi kuwa, imetenga pesa kwa ajili ya kujenga bwawa hili muhimu la Kidete kuzuia mafuriko hayo. Pia, kingo za Mto Miyombo zimezidiwa na wingi wa maji na mvua inapozidi, maji hufurika kwa wananchi na kuleta maafa. Naomba majibu ya Serikali, ni lini itajenga Bwawa la Kidete na lini itajenga tuta la Mto Miyombo?