Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 - Ofisi ya Waziri Mkuu

Hon. Zuberi Mohamedi Kuchauka

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Liwale

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 - Ofisi ya Waziri Mkuu

MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa nichukue fursa hii kumpongeza Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. John Joseph Pombe Magufuli kwa uongozi wake mahiri katika kuzisimamia rasilimali za nchi yetu ili ziweze kuwanufaisha wananchi wa nchi hii bila kujali tofauti ya itikadi, dini, kabila, rangi na mipaka ya kikanda. Ama kwa hakika kwa namna Serikali ya Awamu ya Tano inavyotekeleza Ilani ya Uchaguzi ya CCM ni Serikali ya kupigiwa mfano.

Mheshimiwa Mwenyekiti, miradi ya kielelezo inayotekelezwa nchini ni kielelezo tosha cha kuonesha dhamira ya Rais ya kuona Tanzania mpya, Tanzania ya uchumi wa kati na Tanzania ya viwanda. Miradi kama reli ya SGR, umeme wa maporomoko ya Rufiji, ununuzi wa ndege, ujenzi wa viwanja vya ndege, ujenzi wa barabara za juu Jijini Dar es Salaam, ujenzi wa Hospitali za Wilaya na vituo vya afya, ni mifano michache ya Tanzania mpya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu vitambulisho vya wajasiriamali, naomba visigawiwe kwa idadi sawa kwa kila Wilaya. Ziko Wilaya ambazo zina wajasiriamali wachache, Wakuu wa Wilaya wanalazimika kuwakopesha watu ambao hawana uwezo wa kupata hata hiyo Sh.20,000 na kuwa kero kwa wananchi wanyonge kwani Mkuu wa Wilaya analazimika kumaliza hivyo vitambulisho vya wajasiriamali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu sheria au kanuni za uendeshaji ni bora zikafanyiwa mapitio kwani zingine tayari zimepitwa na wakati. Mfano kwenye zile Halmashauri zinazoongozwa na upinzani, Diwani akikiuka kanuni fulani, Mwenyekiti ana madaraka ya kumtoa nje au adhabu nyingine lakini inapotokea Mwenyekiti amevunja kanuni, kanuni au sharia hizo hazisemi chochote. Kwa namna hii baadhi ya Wenyeviti wanajifanya Mungu watu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sheria ya wazee ni jambo muhimu sana. Ni muda mrefu sasa suala hili limekuwa likisemwa bila utekelezaji. Katika Wizara ya Afya hasa hospitali zetu nyingi, kuna vibao vyenye maneno kama “mpishe mzee” lakini ni mzee gani huyu tunayemzungumzia? Hivyo, umefika wakati sasa sheria hii ikaletwa hapa Bungeni ili hawa wazee wakatambuliwa na sheria.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wilaya ya Liwale ni ya zamani sana ina umri wa miaka 43 lakini haina jengo hata moja la kuitambulisha Wilaya hiyo. Mfano, haina jengo la Mkuu wa Wilaya; jengo la Mahakama ya Wilaya; jengo la Polisi Wilaya na jengo la Hospitali ya Wilaya. Taasisi zote hizo nilizozitaja, zinatumia majengo ya iliyokuwa Tarafa ya Liwale Mjini ndiyo walirithi majengo hayo na kwa kuwa ni ya Tarafa yanashindwa kukizi mahitaji ya ofisi hizo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye Ilani ya CCM ya 2015-2010 barabara za Nachingwea - Liwale na Nangurukuru - Liwale zimeelezwa kuwa ni miongoni mwa barabara zitakazofanyiwa upembuzi na usanifu wa kina. Hivyo, naomba kwa bajeti hii jambo hili litekelezwe. Sambamba na hili, Mikoa ya Morogoro na Lindi bado haijaunganishwa kwa barabara za kiwango cha lami.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sheria ya maliasili kuhusu kifuta machozi kwa waathirika wa majanga yanayotokana na wanyamapori kama vile kuliwa mazao yao au kujeruhiwa nashauri ifanyiwe marekebisho. Bora sasa waathirika wakapewa fidia badala ya kile kinachoitwa kifuta machozi ambacho hakitolewi kwa wakati, sheria hii imepitwa na wakati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naishauri Serikali kuongeza kasi ya ulipaji wa madeni kwenye taasisi zake. Zipo taasisi zinazoshindwa kujiendesha kwa kukosa mitaji, kwani fedha zao nyingi ziko Serikali Kuu (Hazina). Yako Mashirika na taasisi zinazoidai Hazina fedha nyingi kiasi cha Mashirika hayo kushindwa kujiendesha. Pia, taasisi zingine zingefutiwa madeni yaliyopitwa na wakati na hayalipiki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sekta ya kilimo inaajiri wananchi wengi sana. Kwa hiyo, Serikali inatakiwa kuipa kipaumbele sana. Hapa mkazo mkubwa uwe kwenye utafutaji wa masoko na uwekezaji katika uchakataji wa mazao ya kilimo. Wakulima wengi hivi sasa wanashindwa kuchagua wajikite na mazao gani kwani bei za mazao zimekuwa zikibadilika mwaka hadi mwaka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mfano, mwaka huu korosho zikishuka wakulima wanahamia kwenye ufuta. Mwaka unaofuata ufuta ukishuka, wakulima wanahamia kwenye mbaazi na mbaazi zikishuka wanahamia kwenye alizeti. Hivyo, nashauri Serikali ijikite kwenye kuimarisha masoko. Hii ndiyo changamoto kubwa sasa kwenye kilimo kuliko hata changamoto za pembejeo.