Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 - Ofisi ya Waziri Mkuu

Hon. Oran Manase Njeza

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbeya Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 - Ofisi ya Waziri Mkuu

MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kuipongeza Serikali ya Awamu ya Tano kwani katika kipindi cha miaka mitatu iliyopita imefanikiwa kuleta mageuzi ya kiuchumi na kijamii katika nchi yetu hususan Jimbo la Mbeya Vijijini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kushauri Serikali kupitia Wizara mpya ya Uwekezaji kuendelea kuhamasisha na kuvutia wawekezaji kutoka nje na ndani. Nchi yetu imejaliwa rasilimali mbalimbali yakiwemo madini. Katika Wilaya ya Mbeya kuna madini ya niobium ambayo ni adimu sana na mahitaji yake ni makubwa kwa viwanda vya vyuma, mabomba ya mafuta, injini za ndege na hata vifaa vya kielektroniki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napendekeza TIC, EPZ na Wizara ya Madini waweke mkakati wa kuvutia wawekezaji katika viwanda vya vyuma na niobium ambayo yanaweza kusaidia kupunguza gharama na hasa pesa za kigeni kwa kuagiza vyuma toka nje ya nchi. Kutokana na miradi mingi ya ujenzi wa madaraja, bomba la mafuta, SGR na vivuko, kiwanda cha niobium kitakuwa msaada mkubwa kupunguza gharama na pia kuwezesha nchi yetu kuuza madini yetu ambayo yameongezwa thamani na kwenda moja kwa moja kwa walaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kutokana na azma yetu ya Tanzania ya viwanda, kuna mahitaji makubwa ya mafundi mchundo (technicians) na mafundi wasaidizi (artisans). Kwa vile Taasisi ya Maadilisho iliyopo Irambo, Mbeya DC ina miundombinu ambayo ni under-utilized, napendekeza Serikali (Wizara ya Afya) iruhusu shule hii ibadilishwe matumizi na kuwa chuo cha ufundi kwa Kanda nzima ya Mikoa ya Kusini Magharibi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Halmashauri ya Mbeya ina changamoto kubwa za barabara na viongozi wa kitaifa walitoa ahadi za ujenzi wa barabara zifuatazo kwa kiwango cha lami, napendekeza ahadi hizo zitekelezwe. Barabara hizo ni Mbalizi – Shigamba – Isongole; barabara ya Mbalizi – Makongolosi na barabara ya Isyonje - Kikondo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Serikali iimarishe usimamizi wa soko la zao la pareto. Pia nashauri liwe mojawapo ya mazao ya kimkakati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na jitihada za kupeleka maji vijijini katika Jimbo la Mbeya bado upatikanaji wa maji ni changamoto kubwa hasa Kata ya Mjele na Mji Mdogo wa Mbalizi. Naomba Serikali itimize ahadi za kutatua kero hii kubwa ya maji katika Jimbo la Mbeya Vijijini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.