Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 - Ofisi ya Waziri Mkuu

Hon. Angellah Jasmine Mbelwa Kairuki

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Nominated

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 - Ofisi ya Waziri Mkuu

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU (UWEKEZAJI): Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote, nami nichukue fursa hii kumpongeza Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania; Mheshimiwa Makamu wa Rais; Mheshimiwa Rais wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar pamoja na Mheshimiwa Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kutokana na uongozi wao makini na mahiri na kwa namna ambavyo wanaliongoza Taifa letu ili liweze kwenda mbele. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kipekee, napenda pia kuchukua nafasi hii kumshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa imani kubwa ambayo bado anayo kwangu kwa kuniteua hivi karibuni kuwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia masuala ya uwekezaji. Itakumbukwa kwamba Mheshimiwa Rais alipofanya mabadiliko haya ilimpendeza kuweka jukumu la kuratibu, kuhamasisha, kuvutia na kusimamia suala zima la maendeleo ya uwekezaji nchini chini ya Ofisi ya Waziri Mkuu. Kimsingi uamuzi ule ulikuwa na mambo ya msingi matatu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza, ni kwa namna ambavyo yameonesha yeye mwenyewe na Serikali yake inavyotambua umuhimu na mchango mkubwa ambao uwekezaji unao katika ujenzi wa Taifa letu.

Pili, ni imani kubwa ambayo Mheshimiwa Rais yeye mwenyewe anayo kwa sekta binafsi nchini lakini kwa wawekezaji kwa ujumla wake. Tatu, ni usikivu wa Mheshimiwa Rais wetu juu ya kilio cha sekta binafsi na uwekezaji ambacho Mheshimiwa Rais kupitia uteuzi huu ameamua kukisikiliza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa uamuzi huo, Mheshimiwa Rais amethibitisha kwa vitendo kwamba anajali sekta binafsi na wawekezaji. Itoshe tu kusema kwamba utekelezaji wa Mpango wa Kuboresha Mfumo wa Taasisi za Udhibiti kupitia Blueprint; Mpango Jumuishi wa Kuboresha Mazingira ya Biashara ya Uwekezaji nchini na tatu kuteua Waziri mahsusi wa Uwekezaji pamoja na kuhamishia jukumu hili la uratibu chini ya Ofisi ya Waziri Mkuu ni sehemu tu ya mambo mengi ambayo yanaonesha dhamira njema ya Mheshimiwa Rais na Serikali kwa ujumla kwa sekta binafsi na uwekezaji. Hakika mwenye macho haambiwi tazama. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa namna ya kipekee pia napenda kumpongeza sana Mheshimiwa Kassim Majaliwa, Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa hotuba yake mahiri kabisa ambayo imeweka msingi na mwelekeo wa utekelezaji wa majukumu ya Serikali kwa mwaka wa fedha 2019/2020 ambayo baadhi yake kama ambavyo mlisikiliza hotuba ile mwanana kabisa iligusa masuala ya uwekezaji. Pili, napenda sana kumpongeza pacha wangu na dada yangu Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Kazi, Ajira na Wenye Ulemavu), Mheshimiwa Jenista Mhagama pamoja na Naibu Mawaziri, Mheshimiwa Mavunde na Mheshimiwa Ikupa; Makatibu wetu Wakuu, mama Tarishi, mama Mwaluko pamoja na Bwana Massawe na watumishi wote kwa ushirikiano mkubwa ambao wanatupatia katika ofisi hii ya Waziri Mkuu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kipekee kabisa, nichukue nafasi hii kuishukuru sana Kamati yetu ya Bunge ya Kudumu ya Sheria na Katiba kupitia kwa Mwenyekiti wake Mheshimiwa Mchengerwa, Mheshimiwa Najma pamoja na Wajumbe wote wa Kamati hii kwa ushirikiano mkubwa walionipatia na kwa mchango na ushauri wao mkubwa ambao tunaamini utatuletea ufanisi katika majukumu yetu. Mwisho kabisa, napenda kumshukuru sana Mheshimiwa Spika, Naibu Spika na Wenyeviti wote kwa umahiri wao katika kusimamia shughuli za Bunge. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho na si kwa umuhimu na nitakuwa sijatenda haki nisipowashukuru sekta binafsi kwa ujumla na wawekezaji wote kwa namna ambavyo wamewekeza mitaji yao katika kuhakikisha kwamba wanakuza uchumi wetu wa Taifa. Pia kuwapongeza sana TNBC, niwashukuru kipekee TIC ambayo iko chini ya Ofisi yangu, EPZA, TPSF, TCCIA, Balozi zetu za Tanzania nje ya nchi pamoja na CEO Roundtable lakini na Wakuu wa Mikoa wote, Wakuu wa Wilaya, Wenyeviti wetu wa Halmashauri na viongozi mbalimbali na wananchi ambao wameona na kutambua umuhimu wa uwekezaji katika uchumi wa Taifa letu. Niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge na Watanzania, nitaendelea kukutana na wawekezaji na wafanyabiashara ili kuweza kusikiliza kero na changamoto zao mbalimbali kwa lengo la kuzitatua. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kipeke kabisa nimshukuru sana mume wangu mpenzi Balozi Mbelwa Kairuki pamoja na watoto wangu. Zaidi pia viongozi wote na wanachama wa UWT Mkoa wa Dar es Salaam pamoja na Wajumbe wa Baraza Kuu la UWT Taifa kwa namna ambavyo wamekuwa wakinipa ushirikiano pia kunivumilia wakati ninapotekeleza majukumu yangu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri Mkuu, kabla sijajibu hoja za Waheshimiwa Wabunge nianze na maelezo ya jumla kwa kuelezea umuhimu wa uwekezaji ambao upo katika maendeleo ya Taifa lolote ulimwenguni. Kwa hakika wote tunatambua mchango mkubwa wa wawekezaji katika kuongeza ajira, uzalishaji na tija pia kwa namna ambavyo unashiriki katika kuongeza Pato la Taifa, kuleta teknolojia mbalimbali na kuwezesha wananchi na kupunguza umaskini. Ni kutokana na umuhimu huo ndiyo maana Serikali imejipanga kikamilifu kuhakikisha kwamba uwekezaji wa ndani na nje unakua kwa kasi sambamba na kuhakikisha kwamba wananchi wetu nao pia wanaweza kunufaika na uwekezaji huo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kipindi cha miaka 10 nikitolea tu takwimu za mwaka 2008 - 2018, TIC iliweza kusajili miradi takriban 6,596. Napenda kusema kwamba hii si miradi yote ya uwekezaji, iko miradi mingi ya uwekezaji ambayo imeingia nchini na mitaji yake lakini unakuta mingine bado haijasajiliwa TIC. Ni miradi yenye thamani ya zaidi ya Dola za Kimarekani bilioni 79.4 ambapo si kiwango kidogo na umeajiri zaidi ya wafanyakazi 788,547. Tutaendelea kuhakikisha kwamba tunaendelea kuongeza mitaji zaidi kutoka nje lakini zaidi pia kuhakikisha kwamba wawekezaji wetu wa ndani na wenyewe wanashiriki katika uwekezaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, bado tutaendelea kuhakikisha kwamba tunasonga mbele katika tasnia ya uwekezaji kama ambavyo tumetambuliwa na ripoti mbalimbali za Kimataifa za uwekezaji tumepiga hatua, tunaongoza katika nchi za Afrika Mashariki lakini pia katika nchi ambazo zinapendekezwa kuwekeza Afrika Tanzania ni miongoni mwa nchi chache ambazo zimependekezwa katika uwekezaji. Jukumu letu kubwa ni kuhakikisha kwamba wote kwa pamoja tuongeze jitihada ili kuhakikisha kwamba tunaendelea kuvutia wawekezaji zaidi kutoka nje ili waweze kuiona Tanzania kama kituo au nchi bora kwa ajili ya kuweka uwekezaji wao. Hili ni jukumu letu sote Waheshimiwa Wabunge ambao tuna wananchi nyuma yetu, mna Halmashauri ambazo ziko chini yenu mnazoziongoza, tuendelee kuwa mfano na tutoe ushirikiano ili kuhakikisha kwamba wawekezaji wetu wanapokuja basi waweze kuwekeza mitaji yao vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kuhamasisha wawekezaji wa ndani, tunaendelea na mikakati yetu mbalimbali kama Serikali kuhakikisha kwamba tunafanya makongamano ya ndani na nje ya nchi. Pia tunatoa elimu ya uwekezaji kuwawezesha wawekezaji wetu wadogo wadogo nao waweze kupata mitaji ya kuwekeza kutoka katika taasisi za fedha ikiwemo katika Benki ya Kilimo kama ambavyo Waziri wa Mifugo ameeleza lakini pia tutaendelea na mikakati mingine mbalimbali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia pia katika takwimu mbalimbali ukilinganisha na mwaka 2005 ambapo wawekezaji wa ndani walikuwa ni takriban asilimia 25 tu lakini nafurahi kusema kwa sasa wawekezaji wa ndani ni zaidi ya asilimia 72. Tutaendelea kuhamasisha ili kiwango hiki kiweze kukua zaidi ili Watanzania nao waweze kuona manufaa ya uwekezaji na waweze kupata pato kubwa zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ili kufikia malengo yetu kiuchumi kama Serikali, tumeweka vipaumbele au mipango katika kuvutia miradi ya uwekezaji katika sekta ambazo zina tija na zina mchango mkubwa kiuchumi na kwa wananchi. Lengo kubwa la kufanya hivyo ni kuhakikisha kwamba tunaimarisha minyororo ya thamani katika mazao ya kilimo, mazao ya uvuvi pamoja na mifugo lakini pia katika masuala ya madawa ya binadamu, kemikali na bidhaa kwa ujumla ambazo zinatumika kwa wingi nchini lakini pia ambazo zinaajiri wananchi wengi na ambazo zinatumia malighafi zinazozalishwa nchini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitaje vipaumbele vichache ni pamoja na uzalishaji wa mafuta ya kula kwa kutumia mbegu zinazozalishwa. Hili limeelezwa vizuri sana na Waheshimiwa Wabunge wengi sana na ukiangalia tuna upungufu wa zaidi ya tani 320,000. Kwa hiyo, napenda kuwatangazia Watanzania hii ni fursa kubwa ambayo naamini kila moja akijipanga kwa namna ya uwezo wake wa kimtaji tunaweza tukatumia soko hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, uzalishaji wa mbegu. Ukiangalia kwa sasa mbegu zinazozalishwa nchini ni tani 51,000 tu lakini mahitaji ambayo yanaagizwa kutoka nje ni tani zaidi ya 16,000 na mahitaji kwa ujumla wake ni tani zaidi ya 370,000. Kwa hiyo, hapa napo jamani ndugu zangu ni fursa, hebu tuwekeze katika uzalishaji wa mbegu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tatu, ni suala la sukari. Ukiangalia mahitaji ni zaidi ya tani 670,000 kwa sukari ya viwandani pamoja na ya majumbani na tumekuwa tukiagiza kwa kiasi kikubwa nje ya nchi ukilinganisha na kiwango ambacho kinazalishwa hapa. Hapa napo tunaweka mkazo ili tuhakikishe kwamba tunajitosheleza kwa mujibu wa uwekezaji wetu uzalishaji wa ndani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nne, ni uzalishaji wa dawa za binadamu na nafurahi na kushukuru sana kwa namna ambavyo tumeshirikiana na Mheshimiwa Waziri wa Afya katika kuhakikisha kwamba tunachochea, kuhamasisha na kuvutia wawekezaji katika sekta hii ya dawa. Tumeona pale Zegereni viko viwanda vingi ambavyo vimejengwa na wakati wowote vitaanza kuzalisha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tano, ni ujenzi wa miundombinu kwa ajili ya uvuvi wa kisasa pamoja na kuchakata viwanda vya samaki. Vilevile tuna masuala ya vifungashio, ni fursa kubwa na katika korosho tuna tani zaidi ya 230,000 ambazo lazima ziweze kuongezewa thamani kwa kuchakatwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, bila kusahau hoja ya Mheshimiwa mama Kilango, Mheshimiwa Njalu na Waheshimiwa wengi sana ambao walionyesha umuhimu wa kuwekeza katika viwanda vya nguo. Napenda kuwashukuru wote walioongelea suala hili ikiwemo na viwanda vya ngozi, viatu, maziwa, pembejeo pamoja na mbolea tunaiona hoja hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia kwa sasa ambacho Serikali imekifanya kupitia mazao sita ambayo Mheshimiwa Waziri Mkuu na Serikali imeyatamka kama mazao ya kimkakati na pamba ikiwemo ni kuhakikisha kwamba tunaongeza uzalishaji ili wanapokuja wawekezaji katika sekta hii basi waweze kuwa na uzalishaji ambapo watakuwa na uhakika wa malighafi kwa siku 260. Kwa mujibu wa ufanisi wa viwanda unatakiwa uwe na malighafi mfululizo kwa siku takriban 260.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tunachokifanya hivi sasa kwa kushirikiana na Wizara ya Viwanda na Wizara zingine za kisekta ni kuhakikisha kwamba tunaongeza malighafi ili tuwe na malighafi ambazo zitaweza kujitosheleza.

Nawashukuru, tutaendelea kukaa na wadau kuhakikisha kwamba tunaweza kuzitambua kwa kina changamoto ambazo zinawakabili ili kuhakikisha kwamba watakuwa na viwanda ambavyo wamewekeza kwa tija na kuweza kupata faida. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuongezea, pamoja na changamoto zote hizo nilizozieleza, wako wengine ambao malighafi zinawatosheleza lakini bado wana changamoto. Tutahakikisha tunaweka vivutio maalum kwa ajili ya wale watakaowekeza katika sekta hizi ambazo nimezieleza ni za vipaumbele ili kuhakikisha kwamba wanaweza kuendesha viwanda vyao kwa tija na kuweza kutupatia pato zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna masuala kama zipu, vifungo na materials mbalimbali ambazo unakuta zinatumika katika viwanda vya nguo ambavyo kimsingi usipoviondolea kodi inakuwa ni ngumu wao kuzalisha kwa faida. Kama tulivyoelezwa hapa yuko Mheshimiwa nadhani ni Salum Mbuzi mwenye kiwanda cha Jambo Spinning ambaye alituelezea changamoto zake na nimhakikishie kwamba ni maeneo ambayo tunayafanyia kazi ili tuweze kupata suluhu katika suala hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, bila kusahau hoja za uwekezaji katika hoteli, Mheshimiwa Dkt. Kigwangalla amezieleza vizuri. Tutaenda kuangalia masuala ya utalii katika Selous Game Reserve, Kilwa Kivinje, Mafia pamoja na sehemu zingine. Yako maeneo mengi kwa sasa niishie kwenye vipengele hivyo tu na mengi nitaeleza nitakapokuwa najibu hoja za Waheshimiwa Wabunge.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya maneno hayo ya utangulizi, niungane na wote walionitangulia lakini zaidi kuwashukuru sana Waheshimiwa Wabunge wote waliochangia katika suala zima la uwekezaji. Nawashukuru sana kwani natambua nia yenu kama Waheshimiwa Wabunge ni kuona kwamba tunakuwa na mazingira mazuri ya biashara na uwekezaji nchini lakini kuhakikisha kwamba mazingira haya yanaboreshwa na kila siku kuhakikisha kwamba taasisi na Wizara zetu zinaweza kubadilika, kwenda na wakati ili kuhakikisha kwamba kodi, ajira na bidhaa zinaweza kupatikana kupitia uwekezaji tulionao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kabla sijaanza kujibu hoja hizi, nihitimishe kwa kutoa rai kwa mamlaka mbalimbali zihakikishe kwamba zinakuwa wabunifu na kuona namna gani wanaweka mikakati ya kufanikisha uwekezaji nchini kwa kuwa uwekezaji ni suala mtambuka. Ni muhimu wakaonesha kwa vitendo kila Afisa wa Serikali aone ni kwa namna gani anaweza kujenga taswira na mazingira mazuri ya uwekezaji nchini. Kwa kitendo kimoja tu inaweza ikatuondolea wawekezaji wengi sana ambao kuwarudisha itakuwa ni shida. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini mwisho kabisa niwahakikishie katika suala zima la wepesi wa kufanya biashara. Ni suala ambalo kwa kweli nitajikita nalo sana kupitia viashiria vile 11. Niitakaa na Mawaziri wa sekta kwa sekta na menejimenti zao na kuhakikisha kwamba yale yote yaliyoelezwa katika viashiria vya Tathmini ya Benki ya Dunia ambapo kwa mwaka huu tumekuwa nafasi ya 144 kati ya nafasi 190, hii ni nafasi ambayo tulikuwa 2016, 2017 tulishapiga hatua nzuri tukawa 132, hatuwezi kurudi nyuma. Ukiangalia malengo yetu mwaka 2025 ni kufikia nafasi ya 95 katika wepesi wa kufanya biashara. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, niwaombe sana sekta zote mkae mkao mzuri, tutakuja kuketi. Bahati nzuri nimeshawapata wale wathamini wenyewe Benki ya Dunia wako Chile na nina mpango wa kufanya nao video conference wiki hii ambapo wamepanga kunipitisha katika kila kiashiria ni nini hasa wanakiangalia ili kuhakikisha kwamba tunapiga hatua katika wepesi wa kufanya biashara. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kingine ambacho kinaturudisha nyuma, katika kujaribu kupitia ripoti za wepesi wa biashara wa nchi mbalimbali, unaangalia Rwanda, unaangalia Uganda, wanatupita katika rank hiyo. Kwenye uwekezaji tunawashinda, iweje kwenye wepesi wa kufanya biashara hawa watushinde?

Mheshimiwa Mwenyekiti, moja ambalo nimeligundua, ukiangalia katika improvements za reforms ambazo nchi nyingine wamehesabika wamefanya vizuri, moja au mbili tu, inaonekana yako mengi mazuri ambayo tumeyafanya lakini unajikuta wale wanaohojiwa hawayaelezi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, kwenye hili naomba sana, wako Wanasheria wa Kampuni binafsi za kisheria na wako watoa huduma wengine mbalimbali ambao wanapata huduma pia kwenye taasisi zetu, yale mazuri yanayofanywa na Serikali, basi wasisite kueleza maboresho ambayo yamefanywa. Kwa sababu kwa kufanya hivyo, mwekezaji anaangalia pia ranking ambayo nchi inayo katika wepesi wa kufanya biashara, ndipo anaamua pia kwenda kuwekeza. Kwa hiyo, kwenye hili nitaomba sana ushirikiano na ni imani yangu kila mmoja ataweza kubadilika na kutoa ushirikiano kwenye hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, nijibu sasa hoja ambazo zimeelezwa. La kwanza ambalo lilikuwa ni kubwa ni kuboresha mazingira ya uwekezaji kwa ajili ya kuvutia uwekezaji wa ndani na nje ili kuweza kuongeza fursa za ajira na biashara na hivyo kuongeza kipato kwa wananchi wengi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kusema kwamba kama Serikali tunapokea ushauri huu na niendelee kuwahakikishia kwamba, lengo la Serikali ni kuhakiksiha kwamba tunaimarisha mazingira ya biashara ya uwekezaji, kama nilivyoeleza awali ili kurahisisha uanzishaji na zaidi ukuaji wa biashara zetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tutaendelea kuongeza maeneo mbalimbali ya kiuchumi (special economic zones) na kuhakikisha kwamba upatikanaji wa ardhi na kuwa na miundombinu wezeshi ambayo itaweza kuwasaidia wawekezaji wetu kuweza kuwekeza. Pia tutaendelea kufanya vikao vya mashauriano na wawekezaji wetu na wafanyabishara kupitia ngazi mbalimbali za kisekta mikoa na wilaya ili kuzipatia ufumbuzi changamoto mbalimbali ambazo wamekuwa wakizibainisha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kulikuwa kuna hoja ya Msemaji wa Kambi Rasmi Bungeni, ambapo yeye alikuwa haamini kama Serikali au kupitia TIC tumeweza kuvutia zaidi ya miradi 145 mpaka sasa. Napenda tu kumhakikishia Mheshimiwa Mbowe, nimtajie tu chache, kuna Alpha Pharmaceuticals ya Dar es Salaam, ambayo watawekeza zaidi ya Dola za Kimarekani milioni 20 na ajira zaidi ya 40. Tunayo Bio-Sustain Limited ya Singida ambao hawa watakuwa wakichakata mafuta ya alizeti na watawekeza zaidi ya Dola milioni 11 za Kimarekani; tunayo GBRI Business Solution ya Shinyanga; tunayo Kilimanjaro Bio-Chemical Limited ambao watakuwa wanazalisha Ethanol; tunayo KOM Food ya Shinyanga ambao nao wataweza kuchakata alizeti na watawekeza zaidi ya Dola za Kimarekani milioni 20; tunayo pia MW Rice Millers ambao nao pia watawekeza zaidi ya dola milioni 17. Siyo maneno na akiitaka orodha hii kwa kina; na anaweza kwenda kuwatafuta wawekezaji hao ambao wamesajili miradi hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Mbowe pia alitaka kujua mgawanyo wa hizi dola bilioni 1.18. Napenda kumwambia kwamba kwa wawekezaji wa ndani, tunatarajia kwamba watawekeza mitaji ya dola milioni 401.66, lakini kwa upande wa wawekezaji wa nje, watawekeza mitaji ya zaidi ya Dola za Kimarekani milioni 127; na kwa upande wa miradi yenye ubia kati ya wawekezaji wa ndani na nje, watawekeza Dola za Kimarekani milioni 423.75.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho naomba sana wawe na imani. Tunachoki-present hapa ni takwimu na taarifa ambazo ni thabiti na zina ukweli. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tatu, kulikuwa kuna hoja nadhani ya Mheshimiwa Anna Kilango, kulikuwa na Mheshimiwa Mashimba na wengine wengi; ni kwa namna gani tunaendelea kuwalinda wazalishaji wa ndani? Niendelee kuwahakikishia tu kwamba, kupitia mfano wa hatua za kikodi, kupitia Sheria ya Fedha ya Mwaka 2018, iliongezwa kodi kwa wale wanaoagiza mafuta mafuta ya kula kutoka nje ya nchi. Kwa yale ambayo ni ghafi, kuna kodi ambayo ilianzishwa ya takriban asilimia 25 na kwa mafuta ambayo yamechakatwa ilianzishwa kodi ya zaidi ya asilimia 35.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile tumeendelea kudhibiti uingiaji wa mafuta ya kula kutoka mipakani. Lengo kubwa ni kuhakikisha kwamba tunalinda viwanda vyetu vya ndani na tutaendelea kufanya hivyo na kuhakikisha kwamba tunakuja na hatua nyingine za kikodi ili kulinda viwanda vyetu vya ndani pia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kulikuwa kuna hoja nyingine kuhusiana na mifugo, kuona ni kwa namna gani tunaweka vivutio vya kodi kama nilivyoeleza kule mwanzo. Kwenyewe pia kupitia Sheria ya Fedha, waliweza kupunguziwa kodi ya makampuni na hili lilifanyika kupitia viwanda vya ngozi, pamoja na viwanda vya madawa vipya. Badala ya kulipa Corporate Tax ya asilimia 30, wao kwa sasa wanalipa Corporate Tax ya asilimia 20 tu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile kwenye kodi ya ongezeko la thamani kwa upande wa mitambo na vifaa vya viwanda hivyo na kwenyewe pia kodi hizi ziliondolewa. Tunaweza kuona kwa kiasi kikubwa Serikali inaweza kuweka jitihada katika kuhakikisha kwamba viwanda vinalindwa, lakini kuweza kuwapa nafuu wawekezaji waliowekeza katika sekta hizo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kulikuwa kuna hoja ya kuendelea kuhakikisha kwamba tunafanyia maboresho sera yetu pamoja na sheria. Niendelee kuwahakikishia Waheshimiwa Wabunge, tayari tumeshafanya tathmini ya mazingira ya uwekezaji na tumeshabainisha maeneo ambayo ni muhimu yanayohitaji kufanyiwa mapitio ili kuboresha mazingira haya ya uwekezaji. Kufuatia tathmini hiyo, tutakuja sasa na Sera mpya ya Uwekezaji ambayo sasa hivi imeanza kufanyiwa mapitio, tayari tumeshaanza mchakato wa kupata timu ya watalamu ambao wataendesha zoezi hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande wa Sheria ya Uwekezaji na yenyewe kwa kiasi kikubwa tutaifanyia marekebisho ili kuhakikisha tunaondoa vikwazo vilivyopo, ikiwemo na kuwa na vivutio vipya katika sekta mbalimbali maalum kama nilivyozieleza huko awali. Pia kuona ni kwa namna gani suala zima la upatikanaji wa ardhi kwa ajili ya wawekezaji, suala zima la miundombinu wezeshi kwa ajili ya wawekezaji na kuondoa changamoto mbalimbali za kitaasisi ili kuhakikisha kwamba tunakuwa na mazingira ambayo ni shindani kwa ajili ya uwekezaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tayari tumeshafanya tathmini na kuandaa blueprint kama nilivyoeleza kule mwanzo na masuala yote muhimu ambayo yamekuwa yakikwamisha uwekezaji yalishabainishwa na hata wahusika ambao wanatakiwa kutatua changamoto hizo wanajulikana. Ni suala ambalo kupitia mpango kazi ule jumuishi ambao niliusema, pindi tu utakapokuwa tayari, basi hili nalo litaweza kuondolewa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hayo, pamoja na kwamba mpango kazi jumuishi unaandaliwa, lakini tayari yako maeneo ambayo yameshaanza kufanyiwa kazi. Kama ambavyo tumemsikia Mheshimiwa Mavunde ambavyo ameeleza, pia sasa hivi wanapita sheria ile namba moja ya mwaka 2015, kuweza kuona wanaweza kuleta ufanisi kiasi gani katika masuala mazima ya vibali vya ajira pamoja na taratibu nyingine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile ukiangalia katika masuala ya tozo, kwenye sekta tu pekee ya kilimo; nawapongeza sana Wizara ya Kilimo, kwa kuwa tayari, kuweza kuondoa zaidi ya tozo 114, siyo jambo dogo. Kwa hiyo, naomba tu Wizara nyingine, badala ya kuona wanataka maduhuli makubwa, hebu tuangalie kikapu kikubwa zaidi. Tutakapochangia katika Mfuko Mkuu wa Hazina, naamini mengi yataweza kufanyika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naendelea kuwaomba Mawaziri wenzangu, kila mmoja aweze kupitia tozo ambazo zinaweza zikapunguwa; nampongeza Mheshimiwa Ummy naye pia anajiandaa kupunguza tozo mbalimbali kupitia TFDA. Nampongeza Mheshimiwa Jenista kupita OSHA zaidi ya tozo tano wameweza kufuta; lakini pia Wizara ya Madini, waliokuwa wenzangu tukiwa nao zaidi ya tozo tisa ziliweza kuondolewa katika uzalishaji wa chumvi. Naamini Serikali itaendelea kufanya hivyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho, kwa kumalizia hoja chache, napenda tu kusema kwamba kwa upande wa zao la chikichi, ukiangalia tumeweka kipaumbele pia katika zao hili. Tayari kupitia TIC zaidi ya hekta 13,000 zimetengwa katika Mkoa wa Kigoma kwa kutambua kwamba zao hili ni la muhimu na la kipaumbele na kuhakikisha kwamba tunakuwa na mafuta ya kupikia ya kutosha na hii ni malighafi muhimu sana kama nilivyoeleza katika maelezo yangu ya utangulizi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kulikuwa kuna hoja za Mheshimiwa Shangazi kuhusiana na namna ya kulinda mazao ya wakulima, hususan katika kuondoa parking fees, landing fees pamoja na kuondoa tozo mbalimbali katika cold-rooms. Ni hoja nzuri na ninaamini kwa kuwa tulitembelea Rungwe pamoja na Hai na Mheshimiwa Waziri wa Fedha na Mipango, naamini kupitia Task Force ile ni eneo ambalo atakuwa ameliangalia ili kuona ni kwa namna gani wanaweza kulinda mazao au bidhaa ambazo zinaweza kuharibika kama nyanya, matunda na mbogamboga kupitia regime ya kodi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho kabisa, napenda kuwashukuru sana Waheshimiwa Wabunge wote waliochangia kwa kuzungumza pamoja na maandishi. Niwahakikishie hoja zote, endapo kuna nyingine ambazo hatujazijibu, tumezipikea, tutazinakili na tutaweza kuwawasilishia majibu, kila mmoja ataweza kupata.

Mheshimiwa Mwenyekiti, zaidi, kwa kuwa nina mwezi mmoja tu katika ofisi hii, niendelee kuwaomba sana ushirikiano wa dhati kabisa na tutakuja katika maeneo yenu ili kuweza kutembelea uwekezaji katika sekta mbalimbali. Tunaomba mtupatie ushirikiano. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuwasilisha. (Makofi)