Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 - Ofisi ya Waziri Mkuu

Hon. Jenista Joackim Mhagama

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Peramiho

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 - Ofisi ya Waziri Mkuu

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU, SERA, BUNGE, KAZI, VIJANA, AJIRA NA WALEMAVU: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nichukue nafasi hii kwanza nimshukuru sana Mwenyezi Mungu, mwingi wa rehema kwa kutujalia sisi Wabunge wote afya njema na kuweza kukutana jioni hii ya leo, tunamshukuru sana Mwenyezi Mungu.

Mheshimiwa Naibu Spika, vile vile nikupongeze sana wewe mwenyewe binafsi kwa kweli unaongoza Bunge hili kwa umahiri mkubwa sana sana na ni mfano mzuri wa viongozi wanawake katika Taifa letu, hongera sana. Pia upeleke salamu zangu za shukrani kwa niaba ya Ofisi ya Waziri Mkuu kwa Mheshimiwa Spika kwa kazi nzuri anayoifanya kuliongoza Bunge letu akisaidiana na Wenyeviti wa Bunge, mnafanya kazi kubwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, siwezi kuanza kuhitimisha hoja hii bila kumpongeza Rais wetu Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Ndugu zangu Waheshimiwa Wabunge Mheshimiwa Rais huyu kwa kweli amejipambanua kuwa Rais shupavu anayeaminiwa na kutumainiwa na Watanzania wengi na hasa wanyonge. Kwa kweli nchi yetu imepata jembe, imepata Mheshimiwa Rais mahiri kabisa; na tumeshuhudia kwa muda mfupi maendeleo yamekuwa makubwa sana. Kwa pamoja naye nimpongeze sana Makamu wa Rais mama yetu Samia Suluhu Hassan, lakini ninaomba kwa dhati ya moyo wangu nimpongeze na kumshukuru sana Mheshimiwa Kassim Majaliwa Majaliwa, Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, upande wangu na watendaji wote ndani ya Ofisi ya Waziri Mkuu, tunamwona Mheshimiwa Waziri Mkuu kama kioo na kiongozi mahiri anayeweza kutuongoza vyema ndani ya Taasisi yetu. Mheshimiwa Waziri Mkuu naomba upokee shukrani zangu za dhati kwa uongozi wako ambao umetufanikisha, umenifanikisha mimi na wenzangu kufika katika hatua hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kweli mwenye macho haambiwi tazama, hawa viongozi wetu wakubwa niliowataja hapo juu wameweza kulipatia Taifa hili maendeleo makubwa sana kwa kipindi kifupi cha takriban miaka mitatu. Tumeona maendeleo makubwa kwenye Sekta ya Ujenzi, barabara, madaraja, meli, reli, miundombinu ya maji, afya, elimu na mambo mengine mengi kadha wa kadha. Serikali ya Awamu ya Tano chini ya usimamizi wa viongozi hawa imefanya mabadiliko makubwa na jitihada hizi tuziunge mkono Watanzania wote pamoja na sisi Wabunge wote wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nichukue nafasi ya pekee kumkaribisha ndani ya Ofisi ya Waziri Mkuu, dada yangu mpenzi Mheshimiwa Angella Jasmine Mbelwa Kairuki, Waziri mwenye dhamana ya Uwekezaji, nina imani naye kubwa, tutashirikiana sana, ni Waziri mchapakazi, mwanamke wa mfano, Mheshimiwa Angellah karibu sana.

Vilevile naomba nichukue nafasi hii kuwatambua na kuwashukuru sana Manaibu wangu wawili; Mheshimiwa Anthony Peter Mavunde na Mheshimiwa Stella Ikupa, vijana hawa wasomi, wenye weledi, wazalendo, waaminifu na wachapakazi, kwa kweli wamekuwa ni nguzo kubwa sana sana katika kazi zangu na ni mhimili mkubwa kwangu. Nawashukuru sana sana Makatibu Wakuu wote watatu ndani ya Ofisi ya Waziri Mkuu, Wakuu wa Taasisi, Wakurugenzi na watendaji mbalimbali ndani ya Ofisi ya Waziri Mkuu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nisisahau kabla sijaenda mbele niwashukuru wapigakura wa Jimbo la Peramiho, Mwenyezi Mungu awape baraka kwa kuendelea kunijali na kunipa imani. Nawashukuru pia watoto wangu, vilevile niombe tu kuwaomba Ndugu zangu wana Peramiho, mwezi Novemba mwaka huu habari ni ileile, hakuna kulala na mwakani mwaka 2020 matokeo ni yaleyale hakuna kupunguza. Kwa hiyo nawashukuru sana wapigakura wangu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tusingeweza kufika hatua hii sisi kama Ofisi ya Waziri Mkuu bila juhudi za Kamati ya Katiba na Sheria inayoongozwa na Mwenyekiti Ndugu yangu Mheshimiwa Mohamed Omary Mchengerwa na Mheshimiwa Najma Murtaza Giga na Wajumbe wa Kamati wamefanya kazi kubwa; pia Kamati ya UKIMWI inayoongozwa na kaka yangu Mheshimiwa Oscar Rwegasira Mukasa na dada yangu Mheshimiwa Jasmine Tisekwa na Wajumbe wa Kamati. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mfuko wa Jimbo uko pia ndani ya Ofisi ya Waziri Mkuu, hivyo basi, nimshukuru sana Mwenyekiti wa Kamati ya Bajeti Mheshimiwa George Simbachawene na Ndugu yangu Mashimba Mashauri Ndaki na Wajumbe wote wa Kamati kwa kazi kubwa na miongozo na ushauri walionipatia. Kazi hii inafanyika kwa kutumia kanuni ya 99(2) ambacho kinaniruhusu sasa kukaa hapa mbele ya meza yako ili mwisho wa hotuba yangu lakini, mwisho wa hotuba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu, tuombe fedha za kutekeleza majukumu mbalimbali ya Ofisi ya Waziri Mkuu. Hivyo basi, nitaanza kujibu baadhi ya hoja za Waheshimiwa Wabunge na zile ambazo tutashindwa kuzijibu kwa siku hii ya leo tutazijibu kwa maandishi.

Mheshimiwa Naibu Spika, nianze na mambo mahususi ambayo pia ni mambo ya jumla, Waheshimiwa Wabunge wengi wameunga mkono na kupongeza sana bajeti yetu, lakini wakimpongeza sana Mheshimiwa Waziri Mkuu, hata hivyo, baadhi ya Waheshimiwa Wabunge wametilia shaka Ofisi ya Waziri Mkuu na utendaji kazi wake kama kweli umetekeleza majukumu yake sawasawa. Kwanza, naomba niwakumbushe Waheshimiwa Wabunge uwepo wa Mheshimiwa Waziri Mkuu ni kwa mujibu wa Katiba Ibara ya 52 mpaka Ibara ya 57 ya mwaka 1977; Mheshimiwa Waziri Mkuu ndiye mratibu na msimamizi mkuu wa utekelezaji wa shughuli na mipango yote ya Serikali, Wizara na Taasisi zote.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, kwanza ni lazima tujue Mheshimiwa Waziri Mkuu hajajiweka mwenyewe, amewekwa kwa mujibu ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Hata hivyo, wote tumeshuhudia ni kwa kiasi gani Mheshimiwa Waziri Mkuu huyu amekuwa mchapakazi na ametekeleza majukumu yake kisawa sawa kweli kweli. Mheshimiwa Waziri Mkuu ameweza kufanya ziara takriban katika mikoa yote nchi nzima ya Tanzania kwenye wilaya zote, kwenye halmashauri zote.

Mheshimiwa Naibu Spika, niseme tu, suala la msingi hapa siyo idadi ya ziara zilizofanywa na Mheshimiwa Waziri Mkuu, ziwe ziara fupi ama ziara ndefu ama ziara zilizofanywa na viongozi wa kitaifa; suala la msingi hapa ni yale matokeo ya ziara hizo zilizofanywa na viongozi wakubwa wa kitaifa na Mawaziri na Viongozi wengine wote ndani ya Serikali ya Awamu ya Tano. Jambo la kwanza, Mheshimiwa Waziri Mkuu ziara zake na viongozi wengine wa kitaifa zimeweza kurudisha nidhamu na uwajibikaji kwa watumishi wa umma katika nchi nzima ya Tanzania, lakini ziara hizo zimezaa matunda ya kuongezeka kwa kasi ya utekelezaji wa miradi ya huduma za jamii, ikiwemo, elimu, afya, maji, miundombinu ya barabara, umeme na kadhalika na sisi ni mashahidi.

Mheshimiwa Naibu Spika, ziara hizi na Mheshimiwa Waziri Mkuu halali na ziara hizo, zimeweza kuongeza tija kwenye mazao ya kilimo na hasa mazao ya biashara ya kimkakati, Mheshimiwa Waziri Mkuu tunakupongeza sana. Ziara hizo zimeweza kuimarisha ukusanyaji wa mapato ndani ya Serikali za Mitaa na Serikali Kuu. Nitoe tu wito kwetu sisi Waheshimiwa Wabunge na Watanzania wote tuanze kulipa kodi kwa hiari bila shuruti. Pia ziara hizi zimeimarisha hali ya usalama, amani na utulivu nchini na kuongeza mshikamano wa kitaifa na umoja wa kitaifa.

Mheshimiwa Naibu Spika, nalisema hili kwa ushahidi mkubwa, juzi nilikuwa Mkoa wa Songwe kwenye shughuli za Mwenge wa Uhuru na shughuli za Mwenge wa Uhuru mwaka huu zilifanyika kwenye eneo la Mloo ambalo pale Mheshimiwa Mbunge wake ni wa CHADEMA, lakini wananchi wote walionesha ushirikiano bila kujali chama, bila kujali itikadi za vyama, dini zao wala makabila. Sasa unaona tu ni kwa namna gani nchi hii amani na utulivu viko sawasawa na wananchi wanaendelea kushikamana pamoja na kujenga umoja wa kitaifa. Niwaombe Waheshimiwa Wabunge wenzangu tuwe mawakala wa amani na utulivu katika Taifa letu la Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, yako masuala yamezungumzwa hapa kuhusu Bunge letu la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Waheshimiwa Wabunge wengine wanatia shaka na wanalalamika kwamba Bunge hili limeshindwa kutekeleza majukumu yake sawasawa na yako maneno mengi ambayo yamekuwa yakitafsiri kazi na mwenendo mzima wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Bunge hili la Kumi na Moja. Hata hivyo, nitaeleza mifano michache ya kuonesha ni kwa kiasi gani Bunge hili limefanya kazi ya kutukuka.

Mheshimiwa Naibu Spika, mpaka leo ninaposimama mbele yako Waheshimiwa Wabunge hawa wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania wameshaiuliza Serikali yao maswali yasiyopungua 2,653, lakini wameshauliza maswali ya nyongeza yasiyopungua 8,202, ni kazi nzuri imefanywa na Waheshimiwa Wabunge hawa. Maswali hayo yalikuwa yanataka kuwa na uhakika wa uwakilishi wa wananchi katika kufuatilia Mpango wa Taifa wa Maendeleo, bajeti za Serikali, ahadi za viongozi wetu na utekelezaji wa ilani ya uchaguzi.

Mheshimiwa Naibu Spika, hapa nataka kusema kitu kidogo ukiangalia maswali hayo yote yasiyopungua 10,000 na kitu, ukijumlisha maswali ya nyongeza na maswali ya msingi, yanaonesha hawa Waheshimiwa Wabunge ambao ni wawakilishi wa wananchi wametumwa nini na wananchi wao kuja kuliuliza Bunge na kuiuliza Serikali. Maswali haya kipaumbele kiliwekwa kwenye Sekta ya Maji, Umeme, Afya, Elimu na Miundombinu. Imeletwa hoja ndani ya Bunge hili katika bajeti hii kwamba, kipaumbele cha wananchi wa Tanzania ni Katiba pendekezwa, Katiba iliyopendekezwa ambayo inatarajia kubadilisha Katiba tuliyonayo sasa, Waheshimiwa Wabunge wengi wamesisitiza kwamba hicho ndiyo kipaumbele cha wananchi kwa sasa.

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka kuliarifu Bunge lako Tukufu maswali yaliyoulizwa humu ndani ambayo yanatokana na kero za Watanzania, yameletwa na wawakilishi wa Watanzania, Wabunge nimesema hapa yanafika kama maswali 10,000 na kitu, lakini katika maswali hayo 10,000 na kitu maswali yaliyoletwa na Waheshimiwa Wabunge hawa wakiwakilisha mahitaji ya Watanzania yaliyokuwa yanadai Katiba mpya na Tume Huru ya Uchaguzi ni maswali mawili tu kati ya maswali hayo 10,000 na kitu. Hapa nataka kusema nini?

Mheshimiwa Naibu Spika, hoja yangu hapa, naendelea kusisitiza kama kweli sisi ni wawakilishi wa wananchi, maswali tunayoyaleta Bungeni yanaashiria mahitaji ya Watanzania, basi mahitaji ya Watanzania kwa sasa ni maji, umeme, afya, elimu, miundombinu, utawala bora, masuala ya wafanyakazi na mambo mengine yanayohusiana na maeneo niliyoyasema hapa. Hivyo basi, suala la Katiba mpya, suala la Katiba pendekezwa, suala la Tume ya Uchaguzi kwamba haitendi haki, kwa maswali yetu sisi wenyewe Waheshimiwa Wabunge, hayo siyo maeneo ya kipaumbele kwa Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Bunge hili limefanya kazi kubwa, limetunga Sheria mbalimbali, limeridhia mikataba, limetengeneza maazimio mbalimbali mpaka tunapofika siku hii ya leo Bunge letu Tukufu limeshatunga Sheria mpya zisizopungua 44, lakini zimefanya mabadiliko ya Sheria mbalimbali takribani kama zizopungua 95. Nirudi pale pale, haitoshi kusema tumetunga, tumefanya mabadiliko ya Sheria hizo zote nyingi, tumetunga Sheria hizo zote mpya, hizo Sheria zinaakisi nini katika mahitaji ya Watanzania na nchi nzima ya Tanzania.

Mheshimiwa Naibu Spika, nitasema Sheria chache kama mfano tu wa kazi nzuri iliyofanywa na Bunge letu Tukufu. Moja kwa mfano tumefanya marekebisho ya Sheria ya kudhibiti na kupambana na dawa za kulevya Na.5 ya mwaka 2015 (The Drugs Control Enforcement Act)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya uwepo wa Sheria hii; uingizaji na matumizi ya dawa za kulevya katika nchi yetu ya Tanzania kwa kazi nzuri iliyofanywa na Waheshimiwa Wabunge imekwenda mpaka asilimia 90, udhibiti na uingizaji wa dawa umedhibitiwa kwa asilimia 90 ndani ya Taifa letu. Nashangaa kama kazi hizi nzuri hatutazisema na kujisemea sisi wenyewe Waheshimiwa Wabunge na Bunge letu, basi kwa kweli hatujitendei haki.

Mheshimiwa Naibu Spika, Bunge hili pia limetunga Sheria ya kutambua kwa mfano, Dodoma kuwa Makao Makuu ya Nchi ya Tanzania, kitu ambacho kilikuwa kinaliliwa na Watanzania wengi. Vilevile tumefanya marekebisho ya Sheria ya Uhujumu Uchumi, Sura Na. 200 na Sheria hii imetusaidia sana kudhibiti ufisadi katika Taifa hili, kwa hiyo ni lazima tujipongeze. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Sheria nyingine nzuri ambayo lazima niiseme ni marekebisho ya Sheria ya ununuzi wa umma ambayo imesaidia sana kutengeneza mfumo wa kielektroniki wa kufanya procurement (The Tanzania National Electronic Procurement System). Hiyo imepunguza ubadhirifu kwenye manunuzi ya umma, kwa hiyo tunajipongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, Bunge hili limetunga Sheria ya Ubia kati ya Sekta ya Umma na Sekta Binafsi Na.9 ya mwaka 2018 na Sheria hiyo imezaa nini? Inakwenda kuzaa mradi muhimu sana wa ujenzi wa reli, Mtwara - Mbamba Bay
- Mchuchuma na Liganga. Sheria hii mpya ya PPP inakwenda kuzaa ujenzi wa reli ya Tanga Mwambani, Arusha, Musoma, ujenzi wa kipande cha barabara ya treni cha Tanga - Arusha, lakini na barabara nyingine kutoka Dar es Salam – Chalinze - Morogoro. Kwa hiyo unaona ni kwa kiasi gani hili Bunge ambalo wengine wanabeza kwamba haliwezi, halijafanya kazi nzuri limewezaji kufanya kazi nzuri kwa kiasi hicho?

Mheshimiwa Naibu Spika, yako mambo mengine mazuri tu kwa mfano Azimio la Mkataba wa Kuanzisha Kamisheni ya Bonde la Mto Songwe ambalo baadaye litatuletea kuwa na bwawa kubwa la maji la ubia ambalo litazalisha umeme, huduma za viwandani na mahitaji ya nyumbani.

Mheshimiwa Naibu Spika, vile vile Bunge hili nimeridhia mkataba wa eGA mkataba kati ya Serikali ya Uganda na Tanzania kuhusu bomba la mafuta, ni Bunge hilihili. Mkataba huo tija yake unaenda kuzaa ajira zisizopungua 10,000 kwa vijana wa Tanzania wakati wa ujenzi, lakini baada ya hapo ajira takriban 1,000 zitapatikana katika kuendesha mradi huo. Mikoa nane, Kagera, Geita, Shinyanga, Tabora, Singida, Dodoma, Manyara, Tanga itanufaika na mradi huo, Wilaya 24 na Vijiji 134 vyote vinanufaika na mradi huo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, naomba niseme kwa kweli Ndugu zangu Waheshimiwa Wabunge ukiacha hapo Ofisi ya Waziri Mkuu imeridhia Mkataba wa Kimataifa wa Vitambulisho vya Mabaharia Na. 185 wa mwaka 2003 na imeridhia pia Mkataba wa Kimataifa wa Kazi za Ubaharia wa Shirika la Kazi Duniani (Maritime Labour Convention) ya mwaka 2016. Mikataba hii imeweza kuongeza fursa za ajira kwa Mabaharia wa Kitanzania kwenye meli za ndani na meli za nje ya nchi, imeweza kuleta mafunzo fursa za mafunzo ya kitaalam, lakini imeongoza viwango vya kazi za staha kwa Mabaharia wetu. Kwa hiyo, kazi hizo zote zimefanywa na Ofisi ya Waziri Mkuu uratibu na usimamizi na zimetufikisha mahali pazuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine ambalo lilizungumzwa na Waheshimiwa Wabunge, ni suala la uwezeshaji wananchi kiuchumi. Jambo hili lilizungumzwa sana eneo la local content kwa maana ya ushiriki wa Watanzania katika kumiliki uchumi wa Taifa lao. Ofisi ya Waziri Mkuu imekamilisha kazi ya msingi sana ya kutengeneza Mwongozo na tunaamini Mwongozo huu utawezesha wadau kutambua wajibu na majukumu yao katika kushiriki kwenye suala zima la kuhakikisha Watanzania na wao wanapata ajira katika miradi yote inayozalishwa katika Taifa letu, lakini vilevile masuala ya ununuzi kama wa bidhaa, ununuzi wa huduma na mambo mengine watanzania pia wanaweza kushiriki.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kupitisha Mwongozo huo, mwamko ni mkubwa kweli kweli, naomba nitoe mifano michache, wakati tulipomaliza kuandaa Mwongozo huu wa local content tumefanya utafiti na tumegundua yafuatayo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mfano, kwenye mradi mkubwa wa uwekezaji wa daraja ya Mfugale, daraja la Mfugale lilitoa ajira 616, Ndugu zangu Waheshimiwa Wabunge kwa sababu ya Mwongozo huo kati ya ajira 616 ajira 589 zilichukuliwa na Watanzania na ilikuwa ni asilimia 95 ya ajira zote. Hiyo haitoshi, lakini ununuzi wa bidhaa mbalimbali ambazo zilitumika katika ujenzi wa huo mradi ulitaka makampuni 28 ndiyo yaende yakafanye ununuzi wa hizo bidhaa. Napenda kuliarifu Bunge lako Tukufu kati ya makampuni hayo 28, makampuni 24 yote yalikuwa ni makampuni ya Watanzania, makampuni ya wazawa na ilikuwa ni asilimia 85 ya makampuni yote. Makampuni matatu tu ndiyo yalikuja kutoka nje na kampuni moja ilikuwa ni ya ubia.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo hilo linaendelea kusimamiwa na Ofisi ya Waziri Mkuu, ni hivyo hivyo hata kwenye barabara za juu za Ubungo, mpaka sasa ajira ya Watanzania ni asilimia 89, kwenye mradi wa SGR, asilimia ya Watanzania kwenye ajira katika mradi huo ni asilimia 93, mradi huo wa SGR kuna sub-project ndani ya mradi huo na ndani ya mradi hiyo sub-project imetoa ajira 1,129 za Watanzania na wageni ni 152 tu.

Mheshimiwa Naibu Spika, hii ni mifano michache, tunayo mifano mingi sana ambayo Ofisi ya Waziri Mkuu inafuatilia na tukipata muda tutaiweka hapa. Naomba niwaambie Ofisi ya Waziri Mkuu inafanya kazi kukuza ajira kwa kutumia miradi ya kimkakati ambayo inaendeshwa na Serikali ya Dkt. John Pombe Magufuli na msimamizi wake akiwa ni Waziri Mkuu wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Miradi hiyo ni pamoja na Salender Bridge na umeme Rufiji. Kwa hiyo, ndugu zangu Waheshimiwa Wabunge hatutakiwi kubeza mambo haya yanayofanywa na Serikali yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, suala lingine lilizungumzwa sana hapa na Wabunge wachache ilikuwa ni Ofisi ya Msajili wa Vyma vya Siasa. Kumekuwa na hali ya upotoshaji na ninaomba niseme ya upotoshaji kwamba hali ya kisiasa ni tete na ni mbaya na demokrasia inaminywa. Mimi naomba nilihakikishie Bunge lako Tukufu kwamba hali ya demokrasia katika nchi yetu ni shwari na ni tulivu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hatuwezi kabisa kufananisha hali ya siasa na demokrasia katika nchi yetu na mataifa yanayotuzunguka ambayo tumekuwa tukiona na kushuhudia hali jinsi ilivyo huko. Niwaombe Waheshimiwa Wabunge, viongozi mbalimbali wa vyama vya siasa kama mnaona kuna tatizo hebu tujaribu kusaidiana, kushauriana na kukaa kwenye meza moja kujadiliana na kutatua matatizo yetu kwa pamoja. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nasema hivyo kwa sababu gani? Hapa tumeshuhudia viongozi wa vyama wakihama kutoka chama kimoja kwenda chama kingine. Kama hali ya kidemokrasia na siasa ingekuwa siyo nzuri, unapata wapi raha ya kuhama kutoka chama kimoja kwenda kingine? Hiyo ni dalili tosha kwamba hali yetu kisiasa hapa ni nzuri. Hiyo ni sababu tosha inamfanya mtu awe huru. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waitara aligombea mwaka 2015 kupitia CHADEMA leo Mbunge wa Chama cha Mapinduzi ni kwa sababu ya utulivu wa kisiasa na demokrasia. Mheshimiwa Nyalandu alishinda Chama cha Mapinduzi leo amehamia CHADEMA ndiyo mambo hayo hayo ya utulivu. Mheshimiwa Lowassa aligombea Urais kupitia CHADEMA leo amerudi CCM, utulivu huo wa demokrasia. Ndugu yetu Maalim Seif alikuwa CUF kindakindaki lakini leo yuko ACT-Wazalendo, huu ndiyo uhuru. Waheshimiwa Wabunge tuko shwari, anayetaka kuhama ahame, anayetaka kubaki abaki, safari ya siasa na demokrasia inaendelea, taratibu na sheria zifuatwe tu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini niseme kama ni masuala ya uchaguzi hakuna chama ambacho kilikataliwa kuweka mgombea na kushiriki kwenye uchaguzi. Hatukuwahi kusema hivyo na tumeendelea kusimamia kuona kwamba kila chama kinaendelea kupata haki. Nirudie kusema kama haki haipatikani vipo vyombo vya sheria vitatusaidia kupata haki. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ninayo mifano, wako watu ambao walihisi kwamba haki zao zimepotea. Nitatoa mifano miwili na mifano hiyo inatupelekea kuthibitisha kwamba ukiona kwenye demokrasia na hali ya siasa nchini haiko sawa nenda Mahakamani utapata haki tu. Mfano wa kwanza, tarehe 22 Februari, 2019 Mheshimiwa Ally Saleh alishinda kesi dhidi ya Bodi ya Wadhamini wa Chama cha CUF kwenye Mahakama Kuu, iliamuliwa na jopo la Majaji na alishida. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tarehe 18 Machi, 2019, Mheshimiwa Lipumba alishinda na akatambulika yeye ni Mwenyekiti halali wa Chama cha Wananchi (CUF). Haki hii haikupatikana Bungeni wala mahali popote ilipatikana Mahakamani. Leo nimemsikia hapa Mheshimiwa Bwege nampongeza sana amesema sisi CUF sasa ni chama kimoja, wamoja, ni kitu kimoja hatutaki mgogoro lakini kama watu wasingekwenda Mahakamani mgogoro wa Chama cha Wananchi CUF usingekwisha na mpaka leo ungeendelea kuwa ni mgogoro mkubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niviombe vyama vya siasa kuendelea kutii Sheria ya Vyama vya Siasa. Lengo la sheria yetu ni kufanya hivi vyama viwe ni taasisi. Kwa mfano, leo Maalim Seif alivyohama kama chama chake cha CUF kisingekuwa taasisi ingekuwa shida lakini kwa sababu ni taasisi ndiyo maana na leo Mheshimiwa Bwege amesema sisi ni CUF moja kwa sababu chama ni taasisi. Sheria hii inataka vyama viwe taasisi na visiwe vyama vya mtu mmoja kwamba mtu mmoja ndiye anakiendesha chama yeye peke yake. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini tunataka vyama hivi kupitia Sheria yetu ya Vyama vya Siasa tuendelee kuondoa chuki, ubaguzi wa dini, vitendo vya vurugu, kulinda amani na utulivu na ustawi wa Taifa hili, sisi wote ni Watanzania. Niendelee tu kutoa wito kwa wenzangu wote na viongozi wote wa vyama kutii sheria bila shuruti. Hilo ni jambo zuri na litaendelea kudumisha umoja wetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kulikuwa na hoja Tume ya Taifa ya Uchaguzi siyo huru, watendaji wake siyo huru, muundo wake siyo huru, jambo hili limesemwa sana. Mimi hapa leo ni Yohana Mbatizaji tu naandaa mapito ya Mheshimiwa Waziri Mkuu mwenye Wizara yake atakuja kusema zaidi hapa. Nataka niseme jambo moja, Tume ya Uchaguzi imewekwa kwa mujibu wa Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Ibara ya 74(1) na Sheria ya Taifa ya Uchaguzi, Sura 343 na kifungu cha 4(1) kinaeleza sifa ya Wajumbe wa Tume ya Taifa ya uchaguzi.

Mheshimiwa Naibu Spika, nitatoa sifa za Wajumbe wawili tu kwanza kwenye Bunge hili kwa siku ya leo. Mjumbe wa kwanza ni Mwenyekiti wa Tume ya uchaguzi, sifa yake, anatakiwa awe Jaji wa Mahakama Kuu au Mahakama ya Rufaa, tena amefanya kazi hiyo ya Ujaji kwa miaka isiyopoungua 15 na Makamu Mwenyekiti wa Tume hivyo hivyo. Wajumbe wa Tume sifa zao zinatokana na kifungu cha 4(1) kwenye Sheria, Sura 343.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nijiulize kidogo, kwa namna hiyo ya aina na sifa za Wajumbe wa Tume ya Uchaguzi na hasa hao Viongozi Wakuu (Majaji) na jinsi wanavyopatikana na Majaji hawa nimetoa mfano hapo mbele ndiyo hao hao wamehusika kutoa haki hata kwa vyama ambavyo ni vya upinzani, leo hii tunasemaje kwamba Tume hii ya Uchaguzi siyo Tume halali, haitendi haki? Naomba kwa kweli hebu tujaribu kujiuliza zaidi na tuendelee kuiunga mkono Tume yetu ya Uchaguzi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ziko hoja hapa zimesemwa kwamba Wakurugenzi wa Halmashauri wanatuhumiwa wao ni wanachama wa Chama cha Mapinduzi, walikuwa ni wagombea wa Ubunge kwenye Majimbo kupitia Chama cha Mapinduzi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunazo Halmashauri 185 lakini humu ndani kuna Wabunge 392. Ukichukua Wabunge 392 ukasema hawa Wakurugenzi wote ndiyo waligombea ukagawa kwa hiyo 185 ina maana kila Halmashauri ina Wakurugenzi wawili na 1.18, sasa huo uhalali sijui unapatikana wapi.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini jambo lingine kubwa, suala la uumini wa chama kwa kiongozi yoyote liko katika moyo wake na linatawaliwa na Sheria za Utumishi wa Umma. Naomba niseme kidogo, humu ndani ya Bunge letu wako Wabunge walikuwa ni wafanyakazi katika taasisi mbalimbali za Serikali lakini leo ni Wabunge kupitia vyama vya upinzani. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, iko mifano tu wengine walikuwa mpaka Viongozi Waandamizi, Makatibu wakuu wa Wizara lakini wametoka na leo ni Wabunge wakiwakilisha vyama vingine. Tuna uhakika gani kwa tuhuma hii kwamba hawa Wakurugenzi wote niliowasema 185 eti ni waumini wakubwa wa Chama cha Mapinduzi? Naomba tukubali kwamba Tume ya Uchaguzi inaongozwa na Katiba, Ibara ya 74 na naomba muamini kwamba uchaguzi utakuwa huru na wa haki kama tulivyoingia, tutaendelea kuingia na Tume itaendelea kutusimamia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Tume ya Uchaguzi imeshafanya kazi kubwa, imeshafanya uhakiki wa vituo vya kupiga kura 37,814, kati ya vituo hivyo 407 viko Zanzibar. Imeshafanya majaribio ya vifaa vya kuboresha daftari kwenye Wilaya mbili Kisarawe na Morogoro. Imeshafanya maandalizi ya kuhakikisha kwamba kanzidata ya Daftari la Kudumu la Wapiga kura iko tayari na mifumo mingine yote iko tayari. Serikali imeshatenga bajeti kwenye MFUKO MKUU wa Serikali kwa ajili ya kuboresha Daftari vilevile kwa ajili ya Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2020. Nawahakikishia Waheshimiwa Wabunge tuko salama, maandalizi yako salama, uchaguzi utafanyika kwa amani, tusiwe na wasiwasi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kulikuwa na hoja moja ililetwa na Mheshimiwa Bulembo kuhusu suala la kibali cha ajira ya wageni kwa mwekezaji mmoja. Naomba hii hoja nisiijibu kwa sababu mwaka jana hoja hii ilivyotolewa, eneo ambalo lilitakiwa lifanyiwe kazi na Ofisi ya Waziri Mkuu tumeshalikamilisha. Ombi la kibali cha mwekezaji huyu kuwa raia wa Tanzania limekwenda Uhamiaji, mwenye mamlaka ya kuzungumza jambo hili ni Waziri wa Mambo ya Ndani. Kwa hiyo, naomba niliache nisitolee ufafanuzi suala hili, Waziri wa Mmabo ya Ndani ndiye mwenye mamlaka ya kupitia sheria na kujua huyu mwekezaji kama atapewa uraia ama hawezi kupewa uraia.

Mheshimiwa Naibu Spika, kulikuwa na hoja kuhusu namna gani Serikali yetu imeshirikiana na taasisi nyingine kuwawezesha wananchi kiuchumi kupitia programu mbalimbali. Nikuhakikishie kwamba tumekuwa na miradi ndani ya Ofisi ya Waziri Mkuu, kwa mfano, Mradi wa Miundombinu ya Masoko na Huduma za Kifedha Vijijini (MIVARF) umefanyakzi nzuri sana Bara na Visiwani. Mradi huu umewafikia wakulima wadogo wakiwemo wafugaji, wavuvi, wafanyakazi na umetoa mikopo kwa watu mbalimabli, umewawezesha wajasiriamali na wafanyabiashara wadogo wadogo vijijini, asasi za kifedha, vyama vya msingi vya ushirika na asasi zinazojishughulisha na usindikaji wa mazao.

Mheshimiwa Naibu Spika, yako mambo machache nitayasema hapa kama ni matunda ya mradi huu ndani ya Ofisi ya Waziri Mkuu ambao umeongeza nguvu kwenye bajeti ya Wizara ya Kilimo. Kazi nyingine zilizofanywa na mradi huu ni pamoja na ukarabati wa barabara. Jumla ya kilomita 1,076.6 zimekarabatiwa pande zote mbili za Muungano na zimeweza kurahisisha sana usafirishaji wa mazao ya wakulima. Mradi huu umejenga na kukarabati maghala 35 ambayo yamekwishakukamilika na maghala sita yanaendelea kukarabatiwa. Vilevile wakulima wameweza kuunganishwa na huduma za fedha, zaidi ya shilingi milioni 300 zimekopeshwa kwa wakulima hao kupitia mpango wa Stakabadhi ya Mazao Ghalani.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye eneo hili la ukarabati na ujenzi wa maghala, asilimia 40 ya wanawake katika maeneo hayo wameweza kunufaika na kuweka mazao yao katika maghala hayo. Mradi umejenga masoko 16 na matokeo yake programu hii ya ujenzi wa masoko imerahisisha wakulima kuwaunganisha na wafanyabiashara na kuuza mazao yao na Halmashauri zimeweza kuongeza mapato.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini mradi huu umeweza kutoa ruzuku za mashine na mitambo ya usindikaji wa mazao ili kuongeza thamani ya mazao. Kazi hiyo imefanyika vizuri, mashine takribani 34 zimeweza kusimikwa kwenye maeneo mbalimbali ndani ya nchi yetu ya Tanzania Bara na Visiwani. Kwa hiyo, kazi hiyo pia imefanyika kwa kiasi kikubwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, mradi umeweza kuwajengea uwezo wazalishaji katika kuzalisha na kutafuta masoko na kuwaunganisha na masoko. Vilevile mradi umeweza kuongeza Mfuko wa Huduma za Fedha Vijijini kupitia asasi za kifedha. Pia mradi kabla haujafungwa umeanzisha Mfuko wa Dhamana yaani Guarantee Fund kwa ajili ya ubunifu kwa kushirikiana na Benki ya Maendeleo ya Kilimo. Shughuli hii Mheshimiwa Waziri Mkuu ataizundua muda siyo mrefu. Niwaombe Waheshimiwa Wabunge baada ya uzinduzi wa jambo hili tuungane pamoja ili kuhakikisha kwamba tunaitendea haki programu hii iweze kuwafikia wananchi wengi zaidi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kulikuwa na hoja kwamba baadhi ya wanachama wa Chama cha CUF wamehamia ACT-Wazalendo na kuonekana kwamba Serikali inatumia nguvu kupitia Msajili wa Vyama vya Siasa ili kukikandamiza Chama cha ACT. Waheshimiwa Wabunge, naomba tu niwaambie, Msajili haangalii chama hiki kikubwa, kidogo, kikoje yeye anafuata sheria na utaratibu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niendelee tu kusema Waheshimiwa Wabunge, nguvu ya chama pia inapimwa pia na idadi ya Wabunge ndani ya Bunge la Jamhuri la Muungano wa Tanzania. Sasa sisi wote tutajiuliza kama ACT- Wazalendo inaweza ikamtikisa Msajili ama kuitikisa Serikali nzima kwa sababu kiongozi mmoja ama wanachama fulani wamejiunga na Chama cha ACT-Wazalendo. Sisi wote nadhani tunaweza tukatafakari na tukapata majibu labda nisiendelee kusema zaidi ya hapo na jambo hili liko tu wazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, zimetolewa hoja kuhusu utendaji wa Mifuko ya Hifadhi ya Jamii. Naomba kukubaliana na Waheshimiwa Wabunge liko eneo bado halijakaa vizuri kwenye mifuko hii. Naomba kuwahakikishia kwamba Serikali kupitia Ofisi ya Waziri Mkuu tutajitahidi, tunachotaka ni kuhakikisha michango inafika kwenye mifuko kwa wakati, wastaafu wanafanyiwa uhakiki, ulipaji wa mafao unafanyika kwa wakati, usumbufu kwa wastaafu unaondolewa haraka sana. Wakurugenzi mko hapa naomba mnisikilize vizuri na kwa kweli tutaendelea kuchukua hatua kama haya tunayoendelea kuyaagiza hayatekelezwi na sisi kama Serikali hatutakuwa tayari kubeba dhamana yenu na ninyi ndiyo wenye wajibu wa kuyasimamia haya yote na kuhakikisha kwamba wastaafu hawaendelei kupata shida, wanaendelea kupata maisha mazuri hata baada ya kustaafu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kulikuwa na hoja ya Serikali kutumia nguvu nyingi kama Polisi wakati wa kusimamia uchaguzi. Najua iko sheria inasimamiwa na Wizara ya Mambo ya Ndani atakapokuja Waziri atatoa maelezo. Naamini kabsia suala la msingi hapa ni kufuata sheria bila shuruti. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hoja hizi ni nyingi kweli kweli lakini kwa sababu muda unapingana nami, niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge maswali yaliyobakia tutayajibu kwa maandishi, nawashukuru sana kwa michango yenu. Naomba kuunga mkono hoja, ahsanteni sana kwa kunisikiliza. (Makofi/ Vigelegele)