Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020

Hon. George Malima Lubeleje

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mpwapwa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020

MHE. GEORGE M. LUBELEJE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia hoja hizi mbili; TAMISEMI pamoja na Utumishi na Utawala Bora. Kwanza kabisa nawapongeza Waheshimiwa Mawaziri wote wawili, Waziri wa TAMISEMI, Waziri wa Utumishi, Manaibu Mawaziri, Wakuu wa Vitengo na Makatibu Wakuu kwa kazi nzuri wanayofanya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze na suala la Mapato ya Serikali za Mitaa. Mapato ya Serikali za Mitaa ndiyo uhai wa Halmashauri za Wilaya, Miji, Manispaa na Majiji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mapato haya yanasaidia sana kulipa Watendaji wa Vijijiā€¦

MWENYEKITI: Utulivu ndani ya Bunge tafadhali. Kuna Senator anatoa mchango wake.

MHE. GEORGE M. LUBELEJE: Mheshimiwa Mwenyekiti, mapato haya yanasaidia sana kulipa Watendaji wa Vijiji wale ambao wameajiriwa na Serikali za Mitaa, mapato haya vilevile yanasasaidia kulipa posho za Madiwani, Wenyeviti wa Vijiji pamoja na Wenyeviti wa Vitongoji na Mitaa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli Halmashauri zetu zilikuwa na vyanzo vingi vya mapato, lakini bahati mbaya sana vyanzo vingi vimechukuliwa na Serikali. Vyanzo hivi ndiyo vingesaidia sana kuongeza mapato katika Halmashauri zetu. Kwa mfano, hivi karibuni TRA wamechukua kodi ya majengo. Mimi sipingi, lakini ule utaratibu kwamba wakusanye mwaka mzima, miezi 12, halafu ndipo wazigawie Halmashauri. Hili kwa kweli mimi sikubaliani nalo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu Halmashauri zina miradi na miradi ile inaendelea mwaka mzima. Sasa fedha ikae TRA mwaka mzima halafu baadaye ndiyo Halmashauri ziweze kupata hizo fedha. Kwa hiyo, nilikuwa namshauri Mheshimiwa Waziri wa TAMISEMI, hili mngeliangalia upya angalau miezi sita Halmashauri ziweze kupata mgao wa fedha zao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la pili, ni kuhusu barabara. Naipongeza sana TARURA, inafanya kazi nzuri sana, lakini changamoto kubwa ya TARURA ni fedha. Tumeishauri Serikali kwamba hii asilimia 30 haitoshi, kwa hiyo, waongezwe angalau ifike asilimia 40. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara za Vijijini ni muhimu sana kwa ajili ya kusafirisha mazao na kusafirisha abiria. Kwa hiyo, naishauri sana TAMISEMI ijitahidi sana kuongeza fedha kwa ajili ya Wakala wa Barabara Vijijini na Mjini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri amefika Mpwapwa na kuona barabara ya kutoka Gulwe, Berege, Chitemo, Mima, Chazima mpaka Igoji moja mpaka Seluka. Amepita hii barabara; barabara hii mbaya sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, bajeti ya mwaka 2018 ambayo inaendelea sasa, tulitengewa shilingi milioni 148. Barabara ile inahitaji zaidi ya shilingi bilioni moja ili iweze kutengenezwa kwa kiwango cha matengenezo makubwa. Sasa naomba sana mwongeze fedha kwa ajili ya matengenezo ya barabara ile pamoja na barabara ya kutoka Mima kwenda Mkanana. Vilevile Mkanana Mheshimiwa Waziri, pamoja na kwamba mmesitisha kugawa maeneo ya Utawala, lakini Mkanana iko milimani kilometa 35 kutoka mlimani kuja Makao Makuu ya Kata ambayo ni Chitemo. Kwa hiyo, namwomba sana Mheshimiwa Waziri wa TAMISEMI kwamba Mkanana nao wapate Kata yao. Nitashukuru sana kwa hilo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu mambo ya TASAF na MKURABITA. TASAF wanafanya kazi nzuri sana, imesambaa nchi nzima. Ombi langu Viongozi wa TASAF ni kwamba, Kamati ya Utawala na Serikali za Mitaa, tumeshatoa mapendekezo kwamba lengo la TASAF Awamu ya Tatu ni kuboresha au kunufaisha kaya masikini, lakini sasa kuna baadhi ya maeneo tumegundua fedha hizi zinakwenda kwa watu wenye uwezo. Tumeagiza chombo kinachohusika, wote ambao wameorodheshwa kwenye daftari waondolewe, kwa sababu wana uwezo, hawawezi wakapata fedha za TASAF.

Mheshimiwa Mwenyekiti, fedha za TASAF tunasaidiwa na Wafadhili na Wafadhili wakigundua kwamba kaya masikini hawapati, wanapata wananchi ambao wana uwezo, wanaweza kuleta maamuzi ambayo yatatuletea matatizo makubwa sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, MKURABITA ni kurasimisha mali, kwa mfano mashamba. Kuna Kijiji changu pale Jimbo la Mpwapwa kinaitwa Inzomvu MKURABITA walipima mashamba, baada ya kupima mashamba, hawakujenga ile Ofisi ya Masijala na ule mradi haujakamilika. Namwomba Mheshimiwa Waziri wa Utumishi, afike kijiji kile, wanalalamika sana, akajibu yeye mwenyewe hoja. Mimi siwezi kukosa kura za pale kwa sababu mradi wa MKURABITA haujatekelezwa, hapana. Namwomba sana Mheshimiwa Waziri aende akawaambie yeye mwenyewe kwamba kwa nini mradi ule umekwama? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ni kuhusu upungufu wa watumishi. Kuna upungufu wa watumishi hasa kwenye Sekta ya Afya. Wilaya ya Mpwapwa ina upungufu wa watumishi katika Sekta ya Afya zaidi ya 450. Kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri, atusaidie tupate watumishi wa kutosha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho ni Bodi ya Mikopo Serikali za Mitaa. Bodi ya Mikopo Serikali za Mitaa, ni chombo cha Serikali za Mitaa, ni chombo cha Halmashauri. Chombo hiki, wadau wakubwa ni Halmashauri na ndiyo wanakichangia hiki chombo. Kulikuwa na mpango wa kuanzisha Benki ya Maendeleo ya Serikali za Mitaa. Sasa Mheshimiwa Waziri: Je, mpango huu umefika wapi? Kama mpango huu haupo, basi Halmashauri ziruhusiwe kukopa kama zamani ili kujenga masoko, barabara, stendi na mambo mengine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, naunga mkono kwa asilimia mia moja. Ahsante sana. (Makofi)