Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020

Hon. Leah Jeremiah Komanya

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Meatu

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020

MHE. LEAH J. KOMANYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi nami niweze kutoa mchango katika hoja za Wizara hizi mbili. Kwanza nipende kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kuweza kunipa kibali chake na kuniwezesha kusimama mbele kuweza kutoa mchango. Pia nipongeze kazi nzuri inayofanywa na Mawaziri wote wawili na wasaidizi wao kazi zao ni nzuri tunaziona kwa vitendo, maneno wanayoyatoa hapa katika Bunge ndivyo kazi inavyofanyika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze mchango wangu kwa kuongelea idadi kubwa ya Wakuu wa Idara wanaokaimu kwa muda mrefu bila kuthibitishwa katika nafasi hizi. Kumekuwa na idadi kubwa sana ambayo ikiongezeka siku hadi siku ya Wakuu wa Idara katika Halmashauri zetu wanaokaimu kwa kipindi kirefu bila kuthibitishwa. Nakubaliana na kwamba zoezi la uchunguzi ni muhimu sana ili kuweza kupata wakuu wa idara. Zoezi hili limekuwa likichukua muda mrefu sana. Ningependa kutoa ombi katika idara inayohusika kuwepo na muda maalum hata kama mtumishi ana mambo mengi anatakiwa kuchunguzwa kuwepo na muda maalum kwamba itachukua miezi mingapi kuchunguzwa kama hana matatizo mengi itachukua kipindi gani, kuwe na time frame.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nasema hivyo kwa sababu gani Kamati ya LAAC tumetembelea halmashauri nyingi kwa mfano, Halmashauri ya Manispaa ya Bukoba Wakuu wa Idara wanaokaimu sita, Bukombe sita, Mbogwe sita, Ngara wanne kwa kigezo kwamba wanasubiri kufanyiwa vetting. Hii inapunguza ufanisi kwa wakuu wa idara kwa sababu wanaona hawana uhakika na kesho yao. Mara nyingi imekuwa ikitokea anakaimu mpaka mwaka mzima mwisho wa siku analetwa mkuu wa idara mwingine kutoka sehemu nyingine. Hii inavunja moyo sana kwa sababu upande wa Serikali bajeti ya mishahara ya wakuu wa idara ipo kwa kila halmashauri, kinachochelewesha ni suala la vetting, naomba kuwe na timeframe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo kuna upungufu mkubwa sana wa wahandisi wa majengo katika wilaya zetu kwa sababu wahandisi wengi wameenda TARURA. Kwa hiyo kazi za majengo zimekuwa zikifanywa na ma-local fundi bila kuwepo na ufuatiliaji wa wahandisi wa halmashauri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nishukuru na kupongeza kazi nzuri sana inayofanywa na mradi wa TASAF pamoja na MKURABITA. TASAF inafanya kazi nzuri sana na wananchi wetu wanapata fedha, wasio na uwezo na wengi imewasiadia pia kuanza kujiongezea biashara ndogondogo. Naomba nishauri, fedha hizi zimekuwa zikiletwa halmashauri na kuingia katika kapu kuu la halmashauri, hivyo kupelekea fedha nyingine kutumika kwa matumizi yasiyotarajiwa na kuchelewesha utekelezaji wa shughuli za TASAF.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa lengo la Serikali la kudhibiti akaunti nyingi, lakini naomba kwa fedha hizi za wafadhili zingepewa special account kwa sababu mwisho wa siku utekelezaji wa miradi unachelewa na baadaye wanapata hoja za ukaguzi. Hofu yangu ni kuweza kuleta shida kwa wafadhili wetu. Katika Wizara hii hii kuna mradi pia wa MKURABITA, zote ziko chini ya Wizara ya Utumishi. Hata hivyo, MKURABITA wenyewe wamekuwa wakisubiri tu fedha kutoka kapu kuu la Mfuko Mkuu wa Hazina wakati TASAF wanaandika maandiko na kuweza kupata ufadhili. Mwanzo MKURABITA walikuwa wanaandika maandiko na kupata ufadhili, sasa sielewi tatizo limekuwa lipo upande gani. Nashauri pia katika Wizara ya Utumishi katika OPRAS zao kiwe kigezo pia cha kuangalia kwa nini hawa wameshindwa kutafuta namna ya kujipatia fedha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mchango wangu pia naomba nichangie vigezo vinavyotumika katika kupata fedha za EP4R katika halmashauri zetu. Kigezo kikuu kimekuwa kikitumika ili halmashauri zipate fedha kwa ajili ya kujenga madarasa, maabara na shughuli zingine, ni Mwalimu kuhudumia darasa lenye wanafunzi 40 hadi 50. Kigezo hiki katika halmashauri zetu ni changamoto kubwa sana kwa kuwa Halmashauri zinatofautiana mazingira. Nashauri vigezo hivi vingekuwa categorized kwa halmashauri kwa mfano manispaa na majiji zikawa na vigezo vyake na halmashauri za wilaya zikawa na vigezo vyake. Bila kufanya hivyo fedha nyingi zitakwenda sana kwenye Halmashauri za Majiji na Manispaa kwa sababu wenyewe wanakidhi vigezo vya Mwalimu kuhudumia wanafunzi 40 hadi 55. Katika halmashauri za wilaya kigezo hiki ni kigumu. Ombi langu kwa Serikali ziwapelekee Walimu wa kutosha hizi halmashauri ama ziwahamishe kule walikojaa na kuletwa ambako kuna upungufu wa Walimu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata kama halmashauri zitapewa zile asilimia 10 za msawazisho wa ikama fedha hii haitoshi kwa sababu, kwa mfano, Halmashauri ya Wilaya ya Meatu asilimia 10 inayoletwa inaweza ikafanya msawazisho kwa Walimu 10 ikawahamisha, lakini na hiyo siyo solution…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)