Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020

Hon. Timotheo Paul Mnzava

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Korogwe Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

3

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020

MHE. TIMOTHEO P. MNZAVA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ya kuweza kuchangia. Awali ya yote, nitumie nafasi hii kwanza kabisa kumshukuru Mungu mwingi wa rehema aliyenijalia uzima na kuweza kuwepo humu ndani leo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitumie nafasi hii kumpongeza kwa dhati kabisa Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kazi kubwa anayoifanya kutuletea maendeleo watu wa nchi ya Tanzania. Pia nitumie nafasi hii kumpongeza Mheshimiwa Waziri wa TAMISEMI na Waziri wa Utumishi wanafanya kazi kubwa na wasaidizi wao wote kwenye Wizara, tunaona kazi wanayoifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kipekee kabisa niruhusu nimpongeze Mheshimiwa Rais kwa jambo moja kubwa ambalo amelifanya kwenye nchi yetu. Baada ya kuingia kwa Serikali ya Awamu ya Tano Mheshimiwa Rais amekuja na namna tofauti ya kuwapata Wakurugenzi Watendaji wa Halmashauri za Wilaya, Halmashauri za Miji, Majiji na vile vile Makatibu Tawala wa Wilaya na watumishi wengine wa maeneo mengine, tofauti na utaratibu uliokuwa umezoeleka mwanzoni. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo hili limetusaidia kuondoa utendaji wa mazoea kwenye Halmashauri zetu. Kama kuna mtu ambaye analipiga vita, atakuwa na matatizo, lakini tunaojua tunaona kwamba jambo hili limetusaidia sana kupunguza urasimu na mazoea kwenye Halmashauri ndani ya nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nichangie kwenye eneo la afya. Mheshimiwa Waziri wa TAMISEMI, tunaishukuru sana Serikali sisi watu wa Korogwe. Mlichukua Hospitali ya Wilaya ya Korogwe ikaenda Halmashauri ya Mji lakini mmetupa shilingi bilioni 1.5 kutengeneza Hospitali ya Wilaya na inajengwa pale Makuyuni na ujenzi umeanza. Tunaishukuru sana Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lazima tukumbuke jambo moja, unapotoa shilingi bilioni 1.5 kwa ajili ya ujenzi wa Hospitali ya Wilaya au shilingi milioni 400 au 500 kwa ajili ya kituo cha afya halafu gharama za kuingiza umeme kwenye hospitali shilingi milioni 200, gharama za kuingiza maji shilingi milioni 150 na hakuna fedha nyingine nje ya hiyo inayotoka, hiyo shilingi bilioni 1.5; inatupunguzia majengo ambayo tungeweza kujenga kwenye hospitali hizi za wilaya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaiomba TAMISEMI itusaidie kukaa na Wizara nyingine kama ya Nishati na Wizara ya Maji. Sisi Korogwe alipokuja Mheshimiwa Waziri wa Maji nilimwomba kutusaidia kusogeza huduma ya maji kwenye hospitali ya wilaya tunayoijenga sasa hivi na alikubali. Bado tunapata shida kwenye upande wa umeme na zaidi ya shilingi milioni 190. Naomba sana Mheshimiwa Waziri aangalie namna ya kuwasiliana na Wizara nyingine kuweza kutusaidia kwenye jambo hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeona kwenye kitabu humu ndani Mheshimiwa Waziri ametengea Korogwe shilingi milioni 200 kwa ajili ya kituo cha afya Kerenge, tunakushukuru sana. Wewe ulikuja Korogwe unajua shida iliyokuwa Korogwe kulingana na eneo la kujenga hospitali ile ya wilaya, pamoja na shilingi milioni 200 kwa ajili ya Kituo cha Afya cha Kerenge.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunavyo vituo vya afya vingine vitatu Korogwe. Mwaka wa fedha uliopita hatujapata fedha yoyote kwa ajili ya kituo cha afya. Kuna Vituo vya Afya vya Bungwe na Kituo cha Afya Magoma, vina hali mbaya. Ni vya muda mrefu. Mwaka 2018 aliyekuwa Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya TAMISEMI anayeshughulika na afya, mama yangu Zainab, alikuja Korogwe na aliwaahidi watu wa Korogwe kwamba watapata shilingi milioni 500 kwa ajili ya ukarabati na upanuzi wa Kituo cha Afya cha Bungu. Kwenye kitabu hiki sijaona.

Mheshimiwa Mwenyekiti, namwomba sana kaka yangu, Ubunge wenyewe ndiyo kwanza nimekuja juzi, namwomba, Kituo cha Afya cha Bungu chonde chonde tusaidie tupate hela tukatanue kile Kituo cha Afya. (Makofi/ Kicheko/Kigelegele)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumze kidogo upande wa TARURA. Kwanza tuwapongeze TARURA, wanafanya kazi nzuri. Pamoja na changamoto za kibajeti, lakini wanajitahidi wanafanya kazi nzuri. Sisi Korogwe tuna Jimbo kubwa, jiografia yetu ni kubwa na siyo nzuri. Hela tunayotengewa ukilinganisha na maeneo mengine havilingani. Tunaomba mtupe kipaumbele watu wa Korogwe. Mwaka wa fedha uliopita tumetengeneza barabara 11 tu tena ni kwa vipande, lakini ziko barabara muhimu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pale tunapojenga hospitali ya wilaya alipokuja Mheshimiwa Waziri, ukiangalia kwa upande wa juu kuna mlima, ndiyo inapatikana Tarafa ya Bungu. Ili ile hospitali ya wilaya iweze kuwa na faida kwa watu wa Tarafa ya Bungu ya mlimani, iko barabara inaitwa Makuyuni - Zege - Mpakani, Kwemchai – Makuyuni lazima itengenezwe. Bajeti ya kuitengeneza ni zaidi ya shilingi milioni
140. Kabla ya bajeti hii, nimekwenda TARURA zaidi ya mara tatu, nimekwenda ofisini kwa Mheshimiwa Waziri zaidi ya mara nne nikiwaomba ili hospitali ile ya wilaya iweze kutusaidia watu wa Korogwe. Tusaidieni barabara hizi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna barabara ya kwenda Kizara; huko mahali mvua ikinyesha kuna eneo la Kizara na Foroforo ni kisiwani kwa sababu barabara ni mbovu. TARURA ukizungumza nao kwamba matengenezo yanahitajika; wanasema yanahitaji hela nyingi na hela tunayopewa ni ndogo, tunawaomba muwaongezee TARURA hela iweze kutusaidia kufanya hii kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia tumekuwa na shida kwenye upande wa madaraja. Ukiangalia hela wanayopewa watu wa TARURA kutengeneza barabara inakuwa ngumu sana kwa wao kutengeneza madaraja. Ninalo daraja kule Korogwe linaitwa Daraja la Mswaha, ni zaidi ya shilingi milioni 180 kutengeneza lile daraja, lakini utakuta TARURA wanapewa shilingi milioni 400 kwa mwaka mzima wa fedha. Hawawezi kutengeneza daraja kama hilo. Wananchi wanapata shida, wanapata taabu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lipo daraja kule kwa Lukongwe, liko daraja linalotuunganisha watu wa Korogwe na wenzetu wa Bumbuli kule Mbagai, yamesimama kwa muda mrefu, wananchi wanashindwa kuvuka, wanapata shida ya kupita kwa sababu ya hela ndogo ambayo wanapata watu wa TARURA. Mheshimiwa Waziri, nakuomba sana hebu tuangalieni, ili ile hospitali iweze kuwa na faida, tusaidie kwenye hizo barabara. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, natambua kwamba Serikali imeweka msimamo. Yapo maelekezo kwamba hakuna kutoa maeneo mapya ya utawala; lakini kuna Halmashauri ya Mji wa Mombo imepewa Mamlaka ya Mji Mdogo tangu 2004. Miji mingine yote iliyopewa Mamlaka ya Miji Mdogo pamoja na Mji wa Mombo ilishakuwa Halmashauri za Wilaya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, siyo tu kwa ajili ya kupewa muda mrefu, jioghrafia ya Korogwe Vijijini ni ngumu. Mheshimiwa Waziri ndiyo maana hata kwenye eneo la kujenga hospitali tulipata shida kwa sababu ya aina ya jiografia ya Wilaya ya Korogwe. Pamoja na hayo maelekezo ya Serikali, naomba sana muangalie uhalisia wa jiografia za Wilaya zilivyo, ukubwa wa wilaya zilivyo kuweza kutafuta maeneo mapya ya utawala kwenye maeneo ya nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, limezungumzwa jambo hapa kuhusu Ofisi za Wakuu wa Wilaya kuingilia Ofisi za Halmashauri. Zimepigwa kelele nyingi sana. Natambua kwamba Ofisi za Wakuu wa Wilaya zimeanzishwa kwa mujibu wa sheria. Sheria ya Tawala za Mikoa, ukisoma kifungu cha 13 (1) na (2). Ukisoma kile kifungu cha 14, kinasema Mkuu wa Wilaya ndio principle representative wa Serikali na wanasema all executive functions zitafanywa na Mkuu wa Wilaya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lazima tujue tunasema Rais wetu ana sehemu tatu; kwanza, ni mkuu wa nchi; pili, ni mkuu wa Serikali; tatu, ni Amirijeshi. Mkuu wa Wilaya na Wakuu wa Mikoa ndio Wawakilishi wa Mheshimiwa Rais. Wanaonjaonja na haka kaharufu. Huwezi ukawa Mkuu wa Wilaya ukaona kwenye Halmashauri ndani ya Wilaya yako, Halmashauri inafanya vitu vya ovyo halafu ukaviacha. Ni lazima ufuatilie.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi ni mashahidi. Ziko Halmashauri ambazo Wakuu wa Mikoa walizuia ziara za Madiwani za zaidi ya mamilioni ya shilingi na wakasaidia kuokoa hela za wananchi. Tunachokitaka hapa ni tuweke tu utaratibu mzuri wa namna gani hawa Wakuu wa Wilaya watashiriki kuzisimamia vizuri hizi Halmashauri zilizokuwa chini yao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, najua kwamba TAMISEMI mlitoa Waraka Na. 2 wa 2010, unaonyesha ushirika wa Ofisi za Wakuu wa Wilaya kwenye Halmashauri. Kuna mahali kuna upungufu kwenye ule waraka. Unasema Katibu Tawala wa Wilaya ambaye ndiye technical person kwenye Ofisi ya Mkuu wa Wilaya; naomba ni-declare interest, kabla sijawa Mbunge nilikuwa Katibu Tawala wa Wilaya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Waraka unasema, ataingia kwenye vikao vya SMT, unasema ataingia kwenye Baraza la Madiwani, lakini kikao cha kila mwezi cha kufanya maamuzi ni Kamati ya Fedha. Katibu Tawala wa Wilaya haingii, anapata wapi taarifa za kumpelekea Mkuu wa Wilaya ili kujua wapi pana shida aweze kuingia hapo? Naomba sehemu hii ifanyiwe marekebisho. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile Makatibu Tawala wa Wilaya na Makatibu Tarafa wamesahaulika. Yako maeneo Katibu Tawala wa Wilaya anakuwa MC wa kusherehesha kwenye shughuli wanapokuja wageni. Hii kitu siyo sawasawa. Naomba wapewe heshima yao, naomba wakumbukwe na wasaidiwe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiiti, ukienda kwenye Halmashauri za Upinzani kwa mfano, ziko Halmashauri ambazo Mabaraza ya Madiwani yanataka kufanya maamuzi kinyume hata na maelekezo ya Serikali, kinyume hata na sera za nchi. Huwezi ukaacha Mkuu wa Wilaya au Mkuu wa Mkoa kuingilia kwenye Halmashauri za namna hiyo. Ni lazima uingie. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nizungumze kidogo kwenye eneo la utawala bora. Kwanza nilimsikia ndugu yangu, baba yangu Mheshimiwa Ally Saleh asubuhi alisema, ni kweli tuna uhuru, kila mtu ana uhuru na uhuru upo kwenye Katiba…

MHE. RAPHAEL J. MICHAEL: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MHE. TIMOTHEO P. MNZAVA: Mheshimiwa Mwenyekiti, Katiba hii inayotoa huo uhuru, kwa mujibu wa haki za binadamu…

MWENYEKITI: Taarifa.

MHE. TIMOTHEO P. MNZAVA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba ulinde muda wangu

T A A R I F A

MHE. RAPHAEL J. MICHAEL: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kumpa taarifa mzungumzaji kwamba siyo wajibu wa Wakuu wa Mikoa wala Wakuu wa Wilaya kuingilia Halmashauri. Ofisi za Mkuu wa Mkoa na Mkuu wa Wilaya kazi yao ni kuIshauri Halmashauri. Kwa hiyo, wao hawana hiyo mamlaka wanayotaka kupewa na Bunge lako Tukufu.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Mnzava.

MBUNGE FULANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MHE. TIMOTHEO P. MNZAVA: Mheshimiwa Mwenyekiti, siipokei hiyo taarifa.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Mnzava kwanza pokea hiyo taarifa ya mwanzo.

MHE. TIMOTHEO P. MNZAVA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza siipokei hiyo taarifa kwa sababu sheria iko wazi kwamba Wakuu wa Wilaya na Wakuu wa Mikoa ndio wenye jukumu la kusimamia; na hiyo iko kwa mujibu wa sheria siyo kwa matakwa ya mtu. Huwezi kusimamia, halafu mtu unayemsimamia afanye mambo ya ovyo halafu usiingilie, haiwezekani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakwenda kwenye utawala bora. Ibara ya 30(2) inaweka utaratibu wa hizo haki tunazozisema. Unaposema huna haki ya kusema, una haki ya kukusanyika; ibara hii imetoa mwanya kwa nchi kutengeneza Sheria ya Kusimamia Utaratibu huo. Huwezi ukakusanyika kama hali ya usalama inahatarishwa, huwezi ukakusanyika kama kuna jambo haliendi vizuri. Hiyo ni katiba na hakuna katiba inayovunjwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeona hoja ya mama yangu, namheshimu sana mama yangu Mheshimiwa Ruth Mollel, kuna hoja mbili kwenye ukurasa wake wa 17 na 18 kwenye hotuba yake, anasema TAKUKURU iache kupeleka watu Mahakamani…

MBUNGE FULANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MHE. TIMOTHEO P. MNZAVA: …mpaka itakapoweza kupata ushahidi wa kutosha.

MBUNGE FULANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MHE. TIMOTHEO P. MNZAVA: Pia anasema kwamba kushindwa kwa kesi nyingi za TAKUKURU mahakamani ni ishara…

MBUNGE FULANI: Mheshimiwa mwenyekiti, umenipa ruhusa au!

MWENYEKITI: Taarifa kuhusu nini? Kwa sababu anazungumza kitu ambacho kiko kwenye kitabu.

MBUNGE FULANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, si kawaida kupiga taarifa!

MWENYEKITI: Ananukuu kitabu kilichoelezea. Hebu endelea Mheshimiwa Timotheo.

MBUNGE FULANI: Mheshimiwa mwenyekiti, taarifa.

MHE. TIMOTHEO P. MNZAVA: Mheshimiwa Mwenyekiti, anasema kwenye kitabu chake kwamba kushindwa kwa kesi nyingi za TAKUKURU Mahakamani ni ishara kwamba kesi hizo siyo za haki.

Mheshimiwa Mweyekiti, sisi tutakuwa nchi ya ajabu kweli. Hivi ni lazima kila anayeenda Mahakamani ashinde? Hilo ni swali l a kwanza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine hebu tuulizane, hivi ni nchi gani ambayo eti mpaka ushahidi wote ukipatikana ndiyo unaenda kumpeleka mtu Mahakamani. Hili ni jambo endelevu, wakati mwingine unaweza ukamkamata mtu, ukampeleka mahakamani…

MBUNGE FULANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MHE. TIMOTHEO P. MNZAVA: Ukaendelea kuafuta ushahidi…

MWENYEKITI: Mheshimiwa Mnzava, malizia.

MHE. TIMOTHEO P. MNZAVA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naipongeza TAKUKURU, nataka waendelee kufanya kazi vizuri…

MBUNGE FULANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MHE. TIMOTHEO P. MNZAVA: …waimarishe Kitengo cha Uchunguzi, waimarishe Kitengo cha Prosecution ili wafanye kazi nzuri kwa ajili ya kutetea nchi yetu na kupingana na mafisadi wanaoifisadi nchi yetu. (Makofi)