Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020

Hon. Grace Sindato Kiwelu

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020

MHE. GRACE S. KIWELU: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa nafasi. Nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa uhai na kuweza kusimama mbele ya Bunge lako Tukufu kuchangia machache.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kupongeza hotuba zetu zote mbili za Kambi ya Upinzani. Zimeeleza mambo mengi mazuri na tunaishauri Serikali kuzingatia yale yote yaliyoelezwa na kambi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kutoa pole kwa Wabunge wenzetu, Mheshimiwa Freeman Aikael Mbowe pamoja na Mheshimiwa Esther Matiko ambao walikaa gerezani kwa siku 104 kwa kunyimwa haki yao ya dhamana. Nimpongeze Jaji Rumanyika kwa kuweza kuona hilo na kutoa haki na hata leo wako nje kwa dhamana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kumwambia Mwenyekiti wetu wa Chama, Mheshimiwa Freeman Aikael Mbowe, tunakupongeza kwa uimara wako, pamoja na yote ambayo unafanyiwa umeendelea kuwa imara na wewe ndiwe Mwenyekiti wetu…

MBUNGE FULANI: Atabaki kuwa juu.

MHE. GRACE S. KIWELU: Najua wako ambao wanaumia kwa ajili ya wewe kuwa Mwenyekiti lakini utaendelea kuwa juu. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kuchangia kuhusu Tume huru ya Uchaguzi. Najua wengi watatushangaa ni kwa nini tunazungumzia Tume hii lakini kitanda usichokilalia huwezi kujua kunguni wake. Sisi tunayo maumivu tuliyoyapata kwa sababu ya Tume hii ya Uchaguzi kutokuwa huru. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika nchi ambazo mfumo wake ni wa kupata viongozi kwa mujibu wa sheria kwa kupigiwa kura, viongozi wengi wameanza kudharau wapigakura wao na tumeona wakifanya maamuzi bila kujali wanawaathiri vipi wapigakura wao. Tumefanya maamuzi mengi bila kujali waliotupa dhamana ya kutuleta humu ndani wanataka nini. Wanafanya haya kwa sababu wanajua Tume wameimiliki, si huru, wanafanya maamuzi bila kujali mawazo ya wananchi wao ambao ndiyo wamewapa dhamana ya kuwaleta humu. (Makofi)

T A A R I F A

MHE. GRACE S. KIWELU: Mheshimiwa Mwenyekiti, niwaambie akina mama wa Kinondoni kwamba Mbunge wao hana heshima kwa akina mama ambapo mama yake amemzaa yeye na kuweza kuwa kiongozi leo. Wabunge wanawake wa CHADEMA tumechaguliwa kama walivyochaguliwa Wabunge wengine wa Viti Maalum kwa kufuata taratibu na kanuni za chama chetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niendelee, tumeshuhudia mabadiliko makubwa sana sasa hivi ya uteuzi wa Wakurugenzi wa Wilaya umeacha kufuata taaluma, taratibu na sheria zilizokuwa zinafanyika hapo awali lakini sasa hivi kigezo namba moja ni kuwa kada wa Chama cha Mapinduzi. Kibaya zaidi tunakwenda kwenye chaguzi za Serikali za Mitaa ambazo tunajua Tume haina muundo mpaka chini, wanakwenda kuchukua watu kutoka TAMISEMI, sasa kwa muundo huu ambao Awamu ya Tano umeanza nao wa kuchagua Wakurugenzi sifa zao wawe makada wa Chama cha Mapinduzi, tunawaambia mapema kwamba, kama walivyosema wenzangu jana kwamba hatutakubali kudhulumiwa, wakatende haki kwa wote.

Mheshimiwa Mwenyekiti, najua haki hii haitatendeka kwa sababu walishaonywa na Mkuu wa Nchi kuwa wasipomtangaza mgombea anayetokana na chama tawala akatafute kazi nyingine na kauli hii haijawahi kufutwa mpaka leo. Kwa maana hiyo, Wakurugenzi, Maafisa Kata ambao wako kwenye kata zetu zinazokwenda kufanya uchaguzi watakwenda kwa maelekezo ya Mheshimiwa Rais. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa tunataka TAMISEMI ituambie hawa Maafisa Kata walioletwa pamoja na Wakurugenzi, wana haki kweli ya kuendelea kuwa wasimamizi wa uchaguzi wakati wanakwenda kufuata maelekezo ambayo walishapewa na Mkuu wa Nchi? Ndiyo maana tunaendelea kulalamika na kusema kwamba Tume hii si huru tunataka Tume huru itakayozingatia haki za wapigakura. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeona uhuni uliofanyika kwenye chaguzi za marudio, watu wamepora maboksi na kwenda kujaza kura na kurudisha kwenye vituo wakisaidiwa na Polisi. Pia tumeona kwenye vituo vya kupigia kura, mawakala tuko ndani tunaheshabu kura lakini Mapolisi wanabandika matokeo nje, wanaingia kuchukua maboksi ya kura. Halafu mnatuambia hii ni Tume huru, kwa kweli Kambi ya Upinzani na wapinzani wote bado tunaendelea kudai Tume huru ya Uchaguzi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niende kwenye suala la ma- DC na Wakuu wa Mikoa. Mimi ninatoka Mkoa wa Kilimanjaro, sina tatizo na Mkuu wangu wa Mkoa, anafanya kazi zake vizuri, anatimiza wajibu wake kuleta maendeleo kwa wananchi wake. Nina tatizo na Mkuu wa Wilaya ya Hai, DC Sabaya. Huyu kabla ya uteuzi wake alikuwa Diwani Kata ya Sambasha, Halmashauri ya Arusha DC, kwa Chama cha Mapinduzi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, DC huyu ameletwa Wilaya ya Hai, anasema anakuja kupambana na Mheshimiwa Mbowe. Namwambia hana ubavu wa kupambana na Mheshimiwa Mbowe. Amekuwa akiingilia shughuli za vyama vya siasa, pia mmeona akiwa anawabughudhi wawekezaji. Tunajua Ma-DC na Wakuu wa Mikoa ni wanasiasa, lakini tunajua ziko sheria na taratibu zilizowekwa kwa ajili ya kuwawesha kufanya kazi zao. (Makofi)

Mheshimiwa Sabaya amekuwa akikamata viongozi wetu wa chama kuzuia wasifanye vikao, tuna chaguzi zinaendelea chini za chama, Mheshimiwa Sabaya hataki vikao vifanyike, lakini amekuwa akimsumbua Mwenyekiti wa Halmashauri kwa kumbambikizia tuhuma za uongo. Nampongeza Mwenyekiti wa Halmashauri, ni mwanamke na yuko imara kweli kweli. Amekuwa akiwalazimisha Wenyeviti wetu wa Vijiji na Vitongoji kusaini barua za kujiuzulu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii siyo haki na siyo kazi aliyotumwa kufanya Hai. Ametumwa akashirikiane na wananchi wa Hai kuleta maenendeleo na siyo vinginevyo. Kama ni mwanasiasa, kwanza atekeleze kazi zake, akimaliza ndiyo akafanye siasa ya chama chake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie suala la kushuka kwa mapato kwa Halmashauri zetu. Halmashauri nyingi nchini zimeshindwa kukusanya mapato kutokana na vyanzo vingi vikubwa vya mapato kuchukuliwa na Serikali Kuu. Hii imesababisha Halmashauri zetu kushindwa kuleta maendeleo na ile mipango waliyokuwa wamepanga kushindwa kufanyika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa naitaka Serikali, yale mapato ambayo waliyokuwa wanakusanya, ni wakati muafaka sasa kurudisha kwenye Hamashauri zetu ili ziweze kujiendesha, kwa sababu kutakuwa hakuna maana kuanzisha Halmashauri ambazo zinashindwa kujiendesha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, yako mambo madogo madogo ambayo yalikuwa yanafanywa kutokana na hayo mapato ya ndani ikiwemo ujenzi wa vyoo, kulipa bill za maji na umeme, lakini yameshindwa kufanyika mpaka sasa. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)