Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020

Hon. Janet Zebedayo Mbene

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Ileje

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020

MHE. JANET Z. MBENE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ya kuchangia hotuba ya Wizara hizi mbili muhimu sana. Nianze kwanza kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutujaalia siku njema, lakini vilevile nataka kuwapongeza sana Waheshimiwa Mawaziri wa Wizara hizi mbili, Manaibu Waziri, Makatibu Wakuu na watendaji wote wa Wizara hizi muhimu sana kwa mustakabali na maendeleo ya nchi yetu. Hizi ni Wizara ambazo unaweza ukasema ni pacha; moja inasimamia Utumishi na Utawala Bora, nyingine inasimamia utekelezaji wa miradi ya maendeleo katika ngazi ya halmashauri na miji yetu. Kwa hali hiyo, kuna haja kubwa sana ya kuhakikisha kuwa kwanza zinawezeshwa kifedha, lakini vilevile kimfumo na pia kwa watumishi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeanza hivyo kwa sababu tunapozungumzia utumishi na tunaposikia michango yote ya Wabunge ikilalamikia watumishi na upungufu wake nafikiri kuna haja sasa ya kuchukua hatua ya makusudi ya kimkakati ya kujaza hizi nafasi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna tatizo kubwa la watumishi katika Wilaya zetu hasa kwenye sekta ya afya, kwenye sekta ya elimu, kwenye sekta ya maji yaani karibu kila sehemu ina matatizo ya upungufu wa watumishi. Mimi binafsi katika wyangu nia upungufu mkubwa sana wa Walimu katika shule za msingi na shule za sekondari, lakini hasa hasa katika shule za sekondari ni Walimu wa sayansi. Tuna tatizo kama alilolisema Mheshimiwa Maghembe kuwa sehemu nyingine ni kujaza nafasi tu za watu ambao wameondoka aidha kwa kustaafu, au kwa kufa, au kwa kuhama. Sasa hili ni jambo ambalo naamini halipaswi kuchukua mlolongo mrefu kama vile ambavyo tunavyongojea vibali vya ajira mpya labda nisahihishwe kuwa hivyo sivyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile nitakuwa mtovu wa shukurani kama sikutoa shukurani zangu kwa jinsi ambavyo wilaya yetu imepatiwa fedha ya kumalizia hospitali ya wilaya ambayo Awamu ya Nne tulipata fedha kwa ajili ya kuianza na sasa hivi tumepata bilioni moja na milioni mia tano kwa ajili ya kuimalizia. Naamini fedha hii itatosha kumalizia hospitali, itajenga nyumba za Wauguzi na vilevile kumalizia miundombinu yote iliyokuwa inahitajika, nawashukuru sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nashukuru kwa kupata fedha ya vituo vya afya viwili vikubwa na tumeahidiwa kingine cha tatu, lakini niombe tupate na cha nne kwa sababu wilaya yangu mimi ina tatizo la miundombinu migumu; milima, mabonde na umbali kati ya kata moja kwenda nyingine. Hii kwa vyovyote vile inasababisha umbali kuwa mkubwa na bila kuwa na zahanati za kutosha hata vituo hivi vya afya vinaweza visisaidie.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikija kwenye zahanati; tulikuwa tumeweka kwenye bajeti yetu milioni 200 kwa ajili ya kukarabati maboma ya zahanati saba ambayo ilishapitishwa kuwa zitakuwepo, lakini ghafla tukaja kuambiwa tuziondoe katika bajeti yetu kwa sababu zinapelekwa Mbozi na Songwe. Hii imetuathiri sana kwa sababu haya maboma ya zahanati yameshafikia mahali pazuri kumaliziwa na hizi fedha tulikuwa tumeshazitarajia kwa sababu zilikuwa zimeshakubaliwa sasa kuja kuziondoa tu juu juu hivi zinatuathiri sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilivyosema Wilaya yangu miundombinu ni migumu, usipokuwa na zahanati hata ya kuanzia tu kumtibu mwananchi kufikia vituo vya afya ni tatizo hasa wakati wa mvua. Naomba sana Wizara ya TAMISEMI mliangalie hilo na mturudishie ile shilingi milioni 200 ambayo mlikuwa mmeitoa wakati tayari tulikuwa tumeshakubaliana kuwa itakuwepo katika ceiling zetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile napenda kushukuru kwa fedha iliyotolewa kwa Daraja la Mwalisi ambalo linaunganisha Wilaya yangu na Mgodi wa Kiwira. Hili daraja litatusaidia kwa sababu ilibidi kutoa makaa ya mawe na kuyapitishia Kyela na huko ilikuwa ni Wilaya nyingine of course na ilikuwa inaleta gharama kubwa na usumbufu kutokana na umbali wake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda pia kuzungumzia suala la TASAF. TASAF imekuwa msaada mkubwa sana kwa nchi nzima na hata kwa Wilaya yangu. Nataka niombe vile vijiji 21 kati ya 71 ambavyo havijaingizwa katika mpango huu basi na vyenyewe viweze kuingizwa kwa sababu faida zake zimeonekana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kidogo nataka niongelee suala zima la TAKUKURU au masuala mazima ya ufisadi au rushwa. Tunashukuru kuwa imeanzisha Mahakama ya Ufisadi lakini kiwango cha watu wanaopelekwa pale cha bilioni moja ni kikubwa sana, mafisadi wengi sana wanaachwa hapa chini hawawezi kufikia Mahakama hiyo kwa sababu hawajatuhumiwa kwa kiwango hicho kikubwa. Kiwango hiki kingepunguzwa kidogo mafisadi au watuhumiwa wengi zaidi wangeweza kufikiwa na rushwa ikapungua lakini bado rushwa ipo na inalalamikiwa sana, tusijidanganye. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ndiyo juhudi zinafanywa lakini bado rushwa nyingi ni tena inafanywa waziwazi katika taasisi zilezile ambazo zimekuwa zikilalamikiwa siku zote Polisi barabarani, Mahakama na sehemu zinazotoa huduma za afya na hata elimu. Naomba sana tusielegeze kamba rushwa bado ipo, wanagundua misemo mipya, ohoo, sijui kula samaki gizani, kuna maneno yanayotumika ambayo hayatufurahishi kwa sababu rushwa inaondoa haki za kimsingi za watu wa kawaida. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nataka kuzungumzia suala la watumishi. Watendaji wakubwa katika taasisi mbalimbali wanahitaji kupata mafunzo ya kutosha ya uongozi. Tulikuwa na vyuo vyetu vilikuwa vinatoa elimu hiyo lakini najua sasa hivi tuna Uongozi Institute, napenda sana kuona mpango mkakati wa jinsi gani ya kuwapeleka watendaji hawa kwenda kujifunza kwa sababu pamoja na kuwa ni viongozi wa taasisi mwenendo hauoneshi ile leadership ambayo inategemewa kwa viongozi wa ngazi hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna jambo lingine ambalo linaanza kuzoeleka la Watendaji Wakuu wanaopata nafasi kuhamishwa kwenye taasisi aliyokuwa mwanzo kuanza kutengeneza himaya zao, wanaondoka na watu wao wote waliokuwa nao kwenye taasisi moja wanawahamishia kwenye taasisi nyingine na kuleta sasa tabaka za waliokuwepo na waliokuja, hii inaleta chuki na inavunja moyo wale waliokuwepo. Mimi nafikiri suala hapa ni kujenga taasisi imara siyo kujenga Watendaji Wakuu wa taasisi imara. Kwa hiyo, naomba hili pia liangaliwe la huu mtindo watu kuhama na ma-secretary wao na viti na meza za maofisini kama vile wanahama nchi.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. JANET Z. MBENE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana, naunga mkono hoja. (Makofi)