Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020

Hon. Daniel Edward Mtuka

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Manyoni Mashariki

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020

MHE. DANIEL E. MTUKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa fursa hii. Nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutupa zawadi ya uhai tumekutana tena safari hii, hii ni bajeti ya nne; tunamshukuru sana Mwenyezi Mungu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nimpongeze jemedari wetu Mheshimiwa Dkt. Magufuli kwa kazi kubwa anayoifanya, kiongozi mahiri, wa kiwango na wa wakati huu. Nipongeze wizara hizi mbili hasa zikiongozwa na Mawaziri mahiri; Mheshimiwa Kapt. (MST) George Mkuchika pamoja na kaka yangu Mheshimiwa Jafo kwa kazi kubwa wanayoifanya pamoja na Naibu Mawaziri wao, Makatibu Wakuu, Naibu Katibu Wakuu na timu nzima katika idara zao katika wizara hizi mbili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia niungane na Mheshimiwa Mbatia leo ni tarehe 12 ni siku ambayo tulimpoteza kiongozi mahiri kabisa, Waziri Mkuu wa zamani Moringe Sokoine. Wote tunaungana naWatanzania wenzetu katika kukumbuka siku hii muhimu ambayo tulimpoteza shujaa wetu, aliweka alama katika nchi hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya utangulizi huu, niseme tu kwamba kwa kuanzia Wizara ya TAMISEMI wanayo kazi kubwa kuwa na trilioni 6.2, asilimia 18 ya bajeti nzima; hili ni fungu kubwa sana. Mnayo kazi kubwa ya kufanya lakini nimpongeze Mheshimiwa Rais, timu ambayo ameiweka nina uhakika wanafanya kazi vizuri na fungu hili najua litapita. Niwaombe Wabunge wenzangu tuwapitishie bajeti hii iliwaende wakafanye kazi. Naiona timu ni nzuri imehamasika watafanya kazi kama ambavyo inatakiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya utangulizi huo, niseme yafuatayo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, niwaombe timu hii ya Wizara na sisi tunawaunga, washughulikie jambo la udhibiti wa ubora hasa majengo na barabara, watusaidie sana. Mheshimiwa Katibu Mkuu yeye niengineer Ndugu Nyamhanga namfahamu, adhibiti sana ubora wa majengo pamoja na barabara. Hizi BOQ fedha hizi ni nyingi, ndipo tunapopigiwa hapa kwenye utaalam; mimi nipo very much concerned hapa kwenye BOQ. Wahandisi wa Wilaya kwenye Halmashauri zetu na Wakurugenzi wasimamie jambo hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie na mimi kama wenzangu ambavyo wamesema natoa shukrani zangu nyingi/kubwa, wametutendea haki sisi Jimbo la Manyoni Mashariki kama Wizara, kabisa. Nimepokea Jimbo hili likiwa limechoka sana katika miundombinu ya elimu na afya lakini hivi ninavyozungumza auheni ni kubwa sana. Tumepokea milioni 900 katika vituo viwili vya afya, bilioni moja katika kuboresha huduma ya maji pale Manyoni Mjini, bilioni 2.2 katika mradi wa vijiji 10 wa maji, milioni zaidi ya 600 katika mradi wa ujenzi wa madarasa hizi fedha za EP4R pamoja na EQUIP na mambo mengi ambayo siwezi kuyataja. Kwa kweli sasa Manyoni naona inakwenda kinyume na zamani ambavyo niliikuta. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninalo tatizo dogo lakini ni kubwa la usimamizi wa fedha hizi, zinakuja nyingi lakini usimamizi bado mimi nauona haupo vizuri. Wanisaidie alizungumza Mheshimiwa Nkamia jana, lakini mwingine amezungumza leo suala la kozi ya viongozi ni muhimu sana na ni msingi kabisa, tunavurugana sana kule. Mbunge anasema hivi na Mkurugenzi anasema hivi badala ya kwenda kwa sauti moja kusimamia mambo haya na fedha hizi za Watanzania tunabaki kuvurugana na fedha na muda vinapotea. Kozi hizi ni muhimu sana, Manyoni tuna shida kidogo ndio maana hata tunadaiwa benki; Madiwani wanadai posho kwa sababu ya mambo haya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nawaomba Mheshimiwa Jafo na timu yake hebu waitazame Halmashauri ya Wilaya ya Manyoni watusaidie, ndiyo maana tupo hapa, hatuwezi kukaa kimya wala kulindana tunataka Watanzania wapate huduma sio kuzozana na kufukuzana na kukimbilia kwamba huyu ana cheo hiki au mimi ni mkubwa, haiwezekani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mfano mzuri, Mbunge anaweza akaenda kufanya mikutano kule kwa wananchi akapokea malalamiko, yale malalamiko Mbunge yeye kazi yake ni kuyapekela sasa kwa wenzake; la Mkuu wa Wilaya nalipeleka kwa Mkuu wa Wilaya na la Mkurugenzi nalipeleka kwa Mkurugenzi. Sasa nikimpeleka asiseme mimi namtuma kazi, ni katika utaratibu wa mgawanyo wa majukumu, mimi napokea kila kitu. Lazima hawa watusaidie sisi, ndio wenye vyombo na watekelezaji, sisi ni wasimamizi; kozi hizi ni muhimu jamani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, upande wa ikama pia tuna shida, upungufu wa watumishi idara ya afya na idara ya elimu kwa kweli bado hali ni ngumu sana, watendaji ni wachache sana, watusaidie sana kwenye hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, TARURA fedha hii haitoshi, vijana wale wana moyo pamoja na kiongozi wao, wana moyo sana. Mimi wamenifungulia vibarabara vitatu pale wananchi wamefurahi sana, tumewaunganisha na vijana wana moyo wa kufanya kazi, lakini hawana fedha. Naungana na mimi na wenzangu waliotangulia angalau ile share ya 70/30 iwe 60/40. Najua TANROAD wana barabara chache lakini zina gharama kubwa sawa lakini ile share ikiwa 40/60 angalau tutapata fedha kule, ndio kwa wananchi kule. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme tu kidogo kuhusu TAKUKURU, wawaongezee fedha, wawape nguvu, wanalinda heshima ya nchi hii.Hawa ndio ma-watchdog tunavyowaita. TAKUKURU bado ni chombo chenye heshima kubwa na nguvu, kama kuna watu wana matatizo wanashughulikiwa, lakini chombo chenyewe kama institution kinabaki bado kina nguvu, wawape hela wakafanye kazi. Naona vijana wale wana mori wa kazi, lakini hawana mafuta hata ya kufanyia kazi, hawana magari na ofisi bado ni chache kwenye Wilaya kule hebu tuwape nguvu walete heshima katika nchi hii. Mheshimiwa Rais tumsaidie analia sana, bado rushwa ipo, ndugu zangu naomba wanisikilizekwa hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho, niseme tu kwamba naunga mkono hoja ya bajeti hizi mbilikwaasilimia mia moja. Ahsante sana. (Makofi)