Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020

Hon. Othman Omar Haji

Sex

Male

Party

CUF

Constituent

Gando

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020

MHE. OTHMAN OMAR HAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuzungumzia mishahara na maslahi katika utumishi wa Umma. Watumishi Serikalini wanakatishwa tamaa na maisha. Hii ni kutokana na kipato cha mishahara, hakikidhi mahitaji yao.

Mheshimiwa Naibu Spika, punguzo la 11% hadi 9% linatekelezwa kwa wafanyakazi wenye mishahara ya kima cha chini. Kodi kubwa hadi kufikia asilimia 30 inaendelea kukatwa kwa wafanyakazi wenye mishahara ya kima cha juu. Wafanyakazi sasa hulazimika kutafuta kipato cha ziada kwa njia nyingine, jambo ambalo linaweza kuathiri uzalishaji na kupunguza pato la Taifa.

Mheshimiwa Naibu Spika, lingine ni kuhusu ajira katika utumishi wa Umma. Hotuba ya Mheshimiwa Waziri haijatueleza kiwango cha Watumishi wa Umma ambao wameajiriwa, lakini kuna taarifa kwamba kwa kipindi cha kuanzia mwaka 2015 - Desemba, 2018 takribani vijana 594,300 waliomba ajira Serikalini, lakini ni vijana 6,554 sawa asilimia 1.1 pekee ndio waliopata ajira. Kwa mujibu wa Kamishna Mkuu wa Mamlaka ya Mapato (TRA) ya Desemba 10, 2018, taasisi yake ina upungufu wa wafanyakazi 1,930 ambapo athari yake ni ucheleweshwaji wa ukusanyaji wa kodi. Baadhi ya Wilaya wameshindwa kufungua ofisi na Serikali inakosa mapato.

Mheshimiwa Naibu Spika, lingine ni mpango wa kunusuru kaya masikini. Wazee wetu walio wengi ni masikini na Serikali yetu ilijipiga kifua kuwa watatoa shilingi bilioni 66.5 kwa ajili yao. Inasikitisha kuona Serikali hii inajisifu kuwa inatetea wanyonge (Serikali ya wanyonge) kwamba tokea ilipoingia madarakani (2015) mpaka tarehe ya leo imetoa shilingi bilioni 1.35 kati ya shilingi bilioni 4.35 zilizotolewa tokea kuasisiwa kwa mpango huu hapo mwaka 2013/2014.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu utawala bora, Tanzania ni miongoni mwa nchi 16 za Afrika na ndiyo nchi pekee Afrika Mashariki iliyokataa kutia saini na kuridhia Mkataba wa Umoja wa Afrika unaohusu demokrasia, uchaguzi na utawala bora (ACDEG). Mkataba huu unalenga kuchochea mijadala miongoni mwa wadau wanaotetea utawala bora na demokrasia Barani Afrika. Kama haitoshi, Tanzania pia imejiondoa katika makubaliano ya kuondokana na kasumba ya kuendesha mambo kwa siri kati ya Serikali na wananchi wake.

Mheshimiwa Naibu Spika, hatua ya Tanzania kujitoa katika mpango wa uendeshaji wa shughuli za Serikali kwa uwazi na ukweli (Open Government Partnership) inazua wasiwasi kuhusu utekelezaji wa Sera ya Uwazi. Kutokana na hatua hizo, inaonyesha kwamba Tanzania imekusudia kuendeleza kuminya demokrasia na uhuru wa watu wake kutoa maoni.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuwasilisha.