Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020

Hon. Mwita Mwikwabe Waitara

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tarime Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020

NAIBU WAZIRI OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. MWITA M. WAITARA): Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana. Hoja ni nyingi lakini nitajaribu kupitia zile ambazo nitaweza ndani ya muda huo na nyingine kila Mheshimiwa Mbunge ambaye ametoa mchango wake kwenye eneo hili tutampa majibu ikiwezekana kwa maandishi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna hoja katika michango ya Waheshimiwa Wabunge ilikuwa inazungumzia Watumishi wa Umma ambao wanakaimu kwa muda mrefu. Naomba tuwahakikishie Waheshimiwa Wabunge kwamba hoja hii tumeipokea, tunatoa maelekezo kila ngazi ya Serikali za Mitaa wakusanye taarifa zao wazilete ili wale watu ambao wanakaimu kwa muda mrefu na wanakidhi vigezo, basi waweze kuthibitishwa kazini ili waweze kufanya kazi kwa umakini zaidi.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la pili, tunafajamu kwamba tuna upungufu wa wahandisi katika Halmashauri zetu, ni kweli, wahandisi wengi walipelekwa TARURA, lakini jambo hili limeshachukuliwa na Serikali linafanyiwa kazi ili tupate wahandisi hasa wa majengo na waweze kusimamia miradi mbalimbali ambayo kwa kweli kwa awamu hii ya tano miradi mingi Serikali imepeleka fedha ujenzi wa vituo vya afya, nyumba za viongozi wetu wa Wilaya na mikoa. Kwa hiyo, hili jambo limechukuliwa litafanyiwa kazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, wakati wa mchango wa Mheshimiwa Mbunge mmoja, alijaribu kutoa maelezo ya kupotosha ya elimu msingi bila malipo. Naomba niseme tu kwa watanzania wote na Waheshimiwa Wabunge kwamba kwa kweli kama kuna jambo kubwa ambalo Mheshimiwa Rais Dkt. John Pombe Magufuli amefanya, ni maamuzi thabiti ya kuruhusu elimu msingi bila malipo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kumekuwa na wanafunzi wengi waliopata fursa ya kusoma na gharama imekuwa ikiongezeka. Tumepanda kutoka shilingi bilioni 249 sasa mwaka huu wa fedha tunaozungumza ni shilingi bilioni 288 elimu msingi bila malipo. Hili siyo jambo la kubeza, ni jambo la kumpongeza Mheshimiwa Rais na Watanzania wana macho wanaona; na masikio na nina uhakika wataendelea kumuunga mkono katika eneo hilo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna madai yamezungumzwa hapa ya Waheshimiwa Madiwani na Wenyeviti wa Serikali za Mitaa. Jambo hili limesemwa kwa upana na uzito. Tumelichukua Ofisi ya TAMISEMI linafanyiwa kazi na baada ya muda siyo mrefu sana litapata muafaka na naamini kwamba kero hiyo itakuwa imeondoka. Kwa hiyo, linafanyiwa kazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, mchangiajie ambaye amemaliza sasa hivi amezungumza kama wengine ambavyo wamesema habari ya madarasa, nyumba na mambo mbalimbali ya miundombinu ya elimu, lakini ukweli ni kwamba Serikali ya Awamu ya Tano ya Chama cha Mapinduzi imejitahidi sana kuboresha miundombinu ya elimu. Changamoto nyingi ilikuwa tunajaribu kuboresha maeneo haya.

Mheshimiwa Naibu Spika, mwaka 2019 kwa mfano, tulikuwa na shida ya magari, hapa tunafanya mchakato wa kununua magari 26; kila mkoa Maafisa Elimu wa Mikoa watapata magari mapya kabisa ili waweze ku-move kutoka eneo moja kwenda lingine kusimamia suala zima la elimu.

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile katika bajeti hii ambayo tumezungumza tutanunua magari 40 tena ambayo yataelekezwa kwenye ngazi ya elimu sambamba na kujenga nyumba za Wakuu wa Mikoa, Wakuu wa Wilaya na Makatibu Tarafa. Ukiangalia kwenye kitabu cha Mheshimiwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI utaona imezungumzwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia tumejenga madarasa 4,400, matundu ya vyoo zaidi ya 8,000, maabara 22, tumepeleka fedha mwezi wa Pili hapa shilingi bilioni 29; tupo kwenye mchakato wa kupeleka shilingi bilioni 34 kwenda sasa kukamilisha maboma ya shule za msingi. Zaidi ya maboma 2,000 yatafanyiwa kazi hiyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kumekuwa na hoja hapa ambazo zimezungumzwa, naomba niseme tu, mwingine alisema nitaje uwezo wangu, nisiwe nachangia kama Naibu Waziri. Nijibu na nianzie hapa hapa nazungumza.

Mheshimiwa Naibu Spika, demokrasia ambayo inazungumzwa katika nchi hii mimi siielewi. Mheshimiwa Msigwa sijui kama yupo humu ndani. Mheshimiwa Msigwa wakati anagombea Uenyekiti wa Kanda, walienda wakaondoa wagombea wa CHADEMA akabaki peke yake. Pamoja na hayo, walipowaondoa alienda akapata kura asilimia 48 za hapana. Huyo ndio Mheshimiwa Msigwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hapa mlimsikia Mheshimiwa Mwenyekiti wa Kambi Rasmi ya Upinzani anazungumza kwamba leo mafisadi ambao wamekamatwa kudhulumu Taifa hili, leo anasema waondolewe wasichukuliwe hatua. Huu ndiyo ulikuwa wimbo wao wa siku zote. Kwa kweli katika mazingira haya hatuwezi kukubaliana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, unaweza ukaona, hivi Mkuu wa Majeshi ambaye anaangalia ulinzi wa nchi hii, hutaki atoe kauli juu ya ulinzi wa nchi hii kweli! Kama kuna chokochoko ndani za kichochezi, anaachaje? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Selasini ni Mjumbe wa Kamati ya Utawala na TAMISEMI, amekuwa kwenye vikao vyote vya Wakuu wa Mikoa na Wakuu wa Wilaya, naomba nimpongeze Mheshimiwa Selasini, ametoa michango mizuri sana. Wakuu wa Mikoa ambao walikuwa na matatizo ambao hatukatai, tumezungumza nao, tumetoa maelekezo na wamebadilika. Alikuwa na malalamiko ya Mfuko wa Jimbo, tumeongea na Mkurugenzi, imeisha. Haya mambo ya jumla jumla hayatakubalika. Kama kuna mtu ana kesi specific, case by case alete tuchukue tuifanyie kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Chuo chetu cha Hombolo kimetoa semina kwa mafunzo mbalimbali. Niseme kwamba Serikali ya Chama cha Mapinduzi ipo kazini na kwa kweli siasa ni kupambanisha hoja siyo vioja. Tumeshuhudia kwenye Bunge hili, wenzetu wana vioja, CCM wana hoja, chapeni kazi. Huo ndiyo ukweli na Watanzania wanaona.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mfano, inawezekanaje Mbunge anasema patachimbika. Hivi hao Watanzania mnaowazungumzia, ni hawa tunaokaa nao sisi au nyie ndio mnajua! Kama patachimbika, mtakuwepo, tutakuwepo. Huu mchezo dakika 90 haziishi, hao Watanzania tupo nao wote. Kwa hiyo, maneno kama hayo ya kuchochea watu, kuandaa kifujofujo, Serikali haiwezi kuruhusu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunataka tupate hoja za wanasiasa makini kama akina Mheshimiwa James Mbatia, wanatoa hoja hapa mtu unafurahi, akina Mheshimiwa Selasini na wengine. Wale ambao hawataki kufanya siasa kwa vyama hivi; leo amekuja Prof. Pierre Lumumba, anasema Magufulification of Africa, yaani Rais wa Tanzania, John Pombe Magufuli anakuwa reffered Afrika nzima. Huyu ni Rais wa mfano. Miradi ambayo ameitoa ni ya kimkakati. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Chama cha Mapinduzi mna huruma sana. Miradi pale Rombo tumepeleka, Iringa inajengwa lami, Tarime kuna mpango wa kimkakati, soko liko pale zaidi ya shilingi bilioni kadhaa, Majimbo yamepewa fedha mbalimbali, watumishi wamepelewa; mnataka nini ndugu zangu wa upinzani? Mnataka mpewe nini? Gunia la chawa! (Kicheko/Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nilitaka niwashauri ndugu zangu wa Upinzani kwa kazi hii inayofanyika ya Chama cha Mapinduzi, ilitakiwa tupange vizuri namna ya kutoa hoja. Mahali pa kukosoa ukosoe vizuri, wala siyo kutukana… (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)