Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Katiba na Sheria

Hon. Susan Anselm Jerome Lyimo

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Katiba na Sheria

MHE. SUSAN A. J. LYIMO: Mheshimiwa Mwenyekiti,Wizara hii ndiyo yenye kusimamia haki na utawala wa sheria zilizowekwa na vyombo mbalimbali vya maamuzi. Katiba ndiyo Sheria Mama na hivyo ni muhimu mno Wizara hii kutekeleza majukumu yake kwa weledi na bila ubaguzi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni wazi katika kipindi hiki tunashuhudia jinsi Katiba yetu na sheria halali zinavyokiukwa. Mfano, tumeona na kusikia matamko yasiyofuata kabisa Katiba, Sheria na Kanuni yakitolewa hadharani tena bila woga, kama vile zuio la mikutano ya hadhara kwa vyama vya siasa wakati Sheria ya Vyama vya Siasa inaruhusu nakutokulipa watumishi wa Serikali annual increments na ama nyongeza ya mishahara iliyo kisheria eti kwa kigezo fedha zinaenda kwenye miradi mikubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vitendo vya ukiukwaji washeria siyo tu vinakomoa wapinzani bali kutia doa nchi yetu ambayo ilionekana kama nchi yenye amani na utulivu na nchi ya kipekee (unique).Ieleweke kwamba bila haki hakuna amani wala upendo. Hivyo basi, tuna kila sababu ya kusimamia haki, Katiba nasheria ili nchi yetu iwe na amani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna matukio mbalimbali yanayoashiria Ofisi ya Taifa ya Mashtaka haifanyi kazi zake vizuri ama kwa makusudi ama kwa hofu. Baadhi ya mambo tunayoyalalamikia ni pamoja na kutekwa kwa mfanyabiashara maarufu Mohamed Dewji, kupotea kwa Ben Saanane, Azory, kupigwa risasi kwa Mbunge Mheshimiwa Tundu Lissu na kupotea kwa Mwenyekiti wa Halmashauri ya Kibondo na kadhalika. Pamoja na matukio haya na mengine mengi Ofisi hii ya Mashtaka na Mkurugenzi wake amekuwa kimya kwa kutochukua hatua licha ya malalamiko mengi ya ndugu, jamaa na wananchi kwa ujumla.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na kuwa hakuna anayeweza kutengua uteuzi wa Mheshimiwa Rais ila yeye mwenyewe, hasa tukijua ni suala la kikatiba lakini pale inapoonekana waziwazi kuwa kuna mazingira yanayoonesha teuzi zinakuwa fadhila kwa jambo lililofanyika, tuna kila sababu ya kushauri. Wote tunajua Viongozi wa Kambi ya Upinzani akiwemo Mheshimiwa Mbowe wako kwenye Shauri Na.112 la 2018. Shauri hili linadhaminika lakini Hakimu wa Mahakama ya Kisutu aliwanyang’anya dhamana na kupelekwa mahabusu Segerea kwa siku 104 (zaidi ya miezi mitatu).

Mheshimiwa Mwenyekiti, kilichonishangaza ni Hakimu huyu kupandishwa cheo na kuwa Jaji wa Mahakama Kuu. Hata kama alikuwa amefikia kupandishwa cheo mtu yeyote ataamini ni fadhila kwa kuwa muda ulikuwa mfupi mno. Hata hivyo, rufaa ya Mahakama ya Rufaa na Mahakama Kuu ilidhihirisha kuwa Hakimu huyo alikiuka utaratibu na hivyo dhamana ikawa wazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, haki kucheleweshwa ni haki kunyimwa. Wote tunajua wananchi wengi hawajui sheria lakini pia kesi nyingi zinachukua muda mrefu huku mahabusu wakiendelea kusota rumande. Mfano, kuna watu wamekaa rumande kwa miaka hadi sita bila kuhukumiwa na kwa sheria zetu hata mtuhumiwa akihukumiwa, ule muda aliokaa rumande hauhesabiki. Huu ni unyama na ukatili. Tunaishauri Serikali iliangalie suala hili ili watuhumiwa wasikae mahabusu kwa muda mrefu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho, naiomba Serikali ijenge Mahakama za Mwanzo na za Wilaya ili haki ziweze kupatikana kwa wakati na kuwaondolea wananchi usumbufu wa kwenda mbali kutafuta haki zao.