Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Katiba na Sheria

Hon. Prof. Palamagamba John Aidan Mwaluko Kabudi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kilosa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Katiba na Sheria

WAZIRI WA MAMBO NJE NA USHIRIKIANO WA AFRIKA MASHARIKI: Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote nianze kuunga hoja mkono iliyoletwa mbele yetu na Dkt. Augustine Maiga, Waziri wa Katiba na Sheria ambaye amewasilisha hii hoja kwa umahiri mkubwa kabisa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ningependa kuchangia katika maeneo machache ya hoja iliyoletwa kwetu na Balozi Dkt. Maiga. Kwanza kuhusu mashauri ya nje; kama alivyoekeza Mwanasheria Mkuu wa Serikali toka kuundwa kwa Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali mafanikio yetu yamekuwa makubwa. Ndani wiki mbili zilizopita na waliosoma gazeti la Citizen juzi tumeweza kushinda kesi ya Valambhia ambao walikuwa wanaidai mabilioni ya fedha Benki ya Tanzania. Sasa kama alivyoeleza Mwanasheria Mkuu wa Serikali katika kesi ya Sterling Construction, kwanza kampuni hii sio ya Kanada kama ilivyoandikwa kwenye hotuba ya Kambi ya Upinzani. Kampuni hii ni ya Uingereza na kabla ya hapo ilikuwa kampuni ya Italy ambapo deni lake lilinunuliwa na kampuni ya Uingereza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kuwa tumefanya maelewano yote, wao wenyewe kampuni ya Sterling Construction Company waliomba the Supreme Court of Quebec kiwango cha fedha walicholipwa na ile hukumu iwe siri. Kwa hiyo, maagizo ya kwamba hukumu na kiasi cha fedha kilicholipwa iwe siri, hayakuwa maombi ya Tanzania, yalikuwa maombi ya kampuni ya Sterling Construction ya Uingereza na ilikubaliwa na the Supreme Court of Cubec na sisi kuyaweka hadharani itakuwa ni contempt of court, lakini pia itakuwa ni kuvunja uungwana wa maelewano.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme pia walitueleza wazi kwamba mnafanya makosa makubwa sana mara nyingine mnapoyaweka mambo haya wazi kwa sababu mna kesi na watu wengine na si ajabu wakijua kiwango ambacho ninyi mmetupa na wao wanaweza wakakidai au kikaleta maswali mengi. Kwa hiyo suala hilo ni wazi ni maombi ya Sterling na uzuri hukumu wa Jaji wa Canada ambaye kwanza alianza kwa kutupa pole ya askari wetu kule Congo kuuawa alieleza wazi. Kwa hiyo sio Serikali ya Tanzania ni Sterling Quebec lakini kiwango kilicholipwa siku wakikubali taarifa hiyo iwe wazi, ni kidogo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la uteuzi wa Majaji, ningependa suala hili nieleze kabisa, Majaji wote walioteuwa, wameteuliwa na Mheshimiwa Rais kwa ushauri wa Judicial Service Commision. Nami nichukuke nafasi hii kukupongeza sana wewe ulipokuwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali mwaka 2000 na mwaka 2005 ulileta mabadiliko ndani ya Bunge hili ambayo moja yalipanua na kuongeza divest ya wajumbe wa Judicial Service Commision.

Mheshimiwa Mwenyekiti, unakumbuka kabla ya wewe kuleta hayo mabadiliko ya Katiba, Judicial Service Commision ilikuwa na watu wachache na wote walikuwa kwenye mhimili wa Mahakama lakini ni wewe mwaka 2000 mara ya kwanza na 2005 mara pili uliyefanya mabadiliko makubwa kuishauri Serikali kufanya hivyo, ikiwa ni pamoja na kuboresha haki za binadamu, wewe ukiwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali ulileta mabadiliko hapa Bungeni ambayo yaliondoa clawback clauses zote. Sisi ndio Katiba pekee katika Bara la Afrika inapokuja kwenye haki za binadamu haina clawback clauses, someni ya Kenya, Uganda, Zambia, Zimbambwe na nchi nyingi, lakini kazi hiyo aliifanya Mheshimiwa Andrew John Chenge mwaka 2005 akiwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali. Ndio maana daima nabeba Katiba hii mwisho hapa A. J. Chenge, Mwanasheria Mkuu wa Serikali ndio aliingiza haya mabadiliko. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wapo watu wa umri mdogo humu wanapapukia mambo wasiyoyajua, wangejua tulipotoka wangejua tulipofika. Kwa hiyo ni jukumu letu hawa walio wadogo tuwakumbushe tulikotoka na ndio maana Katiba hii Mheshimiwa Chenge wewe ni miongoni mwa watu walioisaidia Judicial Service Commision. Kwa sababu hiyo basi, uteuzi wa Majaji umebadilika; leo hii Majaji hawatoki katika mhimili wa mahakama tu, wanatoka kwenye vyuo vikuu, wanatoka kwenye Mawakili binafsi na huo upanuzi wa aina ya Majaji wanaoingia, imeongeza ubora wa hukumu lakini pia imeongeza ubora wa utendaji katika Mahakama zetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Rais kwa kutumia mamlaka ndani ya ibara 109(7) na (8) hatoi fadhila, anateua watu wenye sifa na sababu za kuwa Majaji baada ya kuwa amependekezewa na Tume ya Mahakama. Kwa hiyo, nataka nisisitize, Rais hatoi zawadi katika kuteua Majaji. Nami narudia tena kwa ndugu zangu, hakuna kazi ambayo naiogopa na tuwaombee sana Majaji na mkitaka kujua ugumu wa kazi ya kuwa Jaji, kaisomeni Zaburi ya 15 na baada ya hapo muisome Zaburi 51 na Zaburi ya 32. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakishazisoma Zaburi hizo tatu za toba katika kipindi hiki cha kwaresma watawaombe sana Majaji. Si kazi ya kukurupukia ni kazi ya kumwombea mtu huyo aliyopewa kwa sababu amechukua kazi ambayo ni ya Mwenyezi Mungu mwenyewe, yeye pekee ndiye Hakimu wa kweli wengine wote wanajitahidi kufanya hivyo.

Kwa hiyo si kazi kuendelea kuwabeza na ndio maana naunga mkono nchi nyingine ambazo mambo ya mahakama hayajadiliwa kabisa katika Bunge. Sisi tumeruhusu kuyajadili mambo hayo, lakini tuyajadili kwa hekima, kwa kiasi, kwa saburi, lakini kwa unyenyekevu mkubwa maana hatupo katika viatu vya watu hawa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ambalo ningependa kulizungumzia ni suala la Sheria ya Ndoa, sio kweli kwamba Sheria ya Ndoa ya Tanzania ya mwaka 1971 ni sheria kandamizi, ni sheria ya kimapinduzi. Narudia tena Sheria ya Ndoa ya mwaka 1971 ni sheria ya kimapinduzi na nchi nyingine mpaka leo zimeshindwa kutunga sheria ya aina hii. Kwa hiyo tusichukulie suala moja tu la umri wa mtu kuoa au kuolewa likawa ndio kigezo cha kusema sheria hii ni kandamizi. Hata hilo suala la mtu kuoa au kuolewa, mtu akikisoma kwa makini kifungu hicho hakizungumzii msichana tu bali pia kinamzungumzia mvulana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo ndani sheria zetu wapo wavulana wanaoweza kuona chini umri ya mdogo, soma kile kifungu vizuri, kinasema either paties or one of them. Sheria hii ni sheria ya kimapinduzi kwa sababu ndio sheria kwanza mwaka 1971 iliyowakomboa wanawake wa Kitanzania hasa wenye ajira sasa kuweza kwenda kufanya kazi eneo lolote na Tanzania na kupanda vyeo. Kwa sababu kabla ya hapo sheria tulioachiwa na Waingereza ilikuwa mwanamke lazima akae mahali alipo mumewe na hilo liliwanyima wanawake fursa kama akina Dkt. Christine Ishengoma asingeweza kuwa Mkuu wa Mkoa Iringa akamwacha Profesa Morogoro, ilikuwa lazima akae Morogoro.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nisimtolee mfano yeye tu, nitolee mfano sasa mwingine, kwa sababu sheria kabla ya mwaka 1971 Cohabitation maana yake ilikuwa lazima siku zote mlale katika chumba kimoja, lakini leo chini ya sheria hii kwa hiyo habitation pamoja na whatsApp pamoja na simu. Hilo limewakomboa wanawake wa Tanzania kuweza kwenda kufanya kazi maeneo mbalimbali ya nchi. Ni makosa kuita sheria ya namna hiyo ni sheria kandamizi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, katika umliki wa mali hii ndio sheria ya kwanza katika Bara la Afrika iliyotambua kwamba mwanamke aliyeolewa anaweza akamiliki mali kwa jina lake, someni sheria za nchi zingine, hata Uingereza, hata Ujerumani imewachukua miaka mingi mwanamke ndani ya ndoa kuruhusiwa kumiliki mali kwa jina lake. Alimiliki mali kwa jina la mumewe au kwa jina la baba yake. Sisi tuliosoma nje tulishangaa kwamba mwanafunzi wa kike Ujerumani hawezi kupanga chumba mpaka baba yake atie saini ya ile form, hapa wanasaini tu. Hapo tulishangaa kwa kujua wanawake wa Ulaya, wenye sifa sawa na kazi sawa wanalipwa mshahara kidogo kuliko wanaume eti tu ndani ya mwezi kuna siku ambazo hazieleweki kwao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hoja kama hiyo huwezi kuileta hapa, kwamba kuna siku ambazo mwanamke haeleweki na hiyo alipwe mshahara mdogo. Mpaka leo ipo katika nchi Ulaya. Kwa hiyo kuna mambo sheria hii imefanya makubwa ambayo ni vizuri tuyaelewe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu umri wa mtoto kuolewam, hili suala ni suala very sensitive, tukitaka tuliibue tutagombana humu. Uingereza yenyewe mpaka leo umri wa mtoto wa kike kuolewa ni miaka 16, lakini leo wasichana wengi Uingereza hawaolewi kwa sababu ya fursa mbalimbali za elimu na mwamko lakini n I mpaka leo. Ukienda kwenye Sheria ya Kanisa Katoliki kwenye Canon Law, Canon namba 1083 inasema wazi kabisa umri wa msichana kuolewa ni miaka 14, kwa mvulana kuoa ni miaka 16 na hii sio mimi, ni Canon Law ya Kanisa Katoliki ambayo ndani ya vitabu ipo wazi. Kwa hiyo kwa kanisa katoliki binti anaweza kuolewa na miaka 14 mvulana 16, ingawa mamlaka za kidunia zilipo zimeruhusiwa kubadili, lakini mpaka leo Canon Law haijabadishwa kifungu cha 1068 na kifungu 1071 ambacho kilitolewa na baba Mtakatifu Paul wa Sita.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini sitaki kwenda kwenye mifano ambayo daima tunapenda kuitoa kwenye dini ya Kiislam, lakini hata huko kwa madhebebu ya Shafii ni miaka 15; kwa madhehebu ya Hanbali miaka 15 kwa madhebebu Maliki ni miaka 17; kwa madhehebu ya Hanafi ni miaka 12 kwa mvulana, miaka tisa kwa msichana na kwa madhehebu ya Ja’fari, hawa Shia ni miaka 15 na tisa. Tusiende kwenye majadala huo, tuache sheria ilivyo na busara itawale, kwenda kwenye haya tutaingia kwenye mambo ambayo si vizuri kuyaingia kwa sasa. Hata hivyo, nirudie kueleza, Sheria ya Ndoa ya mwaka 1971 tofauti na ilivyoelezwa ni sheria ya kimapinduzi, iliyokuja kwa wakati muafaka na unaostahili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ningependa pia nieleze kuhusu haki za binadamu kwa kifupi. Tumetoka kwenye Baraza la Umoja wa Kimataifa la Haki za Binadamu, Geneva mwezi Februari, tumetoa maelezo kule na baada ya maelezo ya Tanzania, Kamishna wa Haki za Binadamu wa Umoja wa Mataifa kwa kinywa chake ametupongeza kwa utekelezaji mkubwa wa haki za binadamu katika eneo la elimu, eneo la afya, eneo la maji. (Makofi)

WABUNGE FULANI: Aaaaaaa.

MWENYEKITI: Nakuongezea muda kidogo Profesa. (Makofi)

WAZIRI WA MAMBO NJE NA USHIRIKIANO WA AFRIKA MASHARIKI: Mheshimiwa Mwenyekiti, moja na tuliungwa mkono na nchi zote za Afrika, sisi ndio tunaongoza kwa idadi kubwa ya magazeti ambayo yanatoka kila siku ya aina zote na tunamshukuru Mungu kwamba sio sisi tuliyoyabeba magazeti haya kuyapeleka Geneva, tulikuta Umoja wa Kimataifa wanayo magazeti hayo. Walishangaa kabisa uhuru mkubwa tulionao wa haki za magazeti ya risasi yaani wanaojimwaga, yapo, kwa sababu ni diversity, ya muziki yapo na magazeti ambayo ni very critical, yapo. Hata hivyo, pia sisi ndio nchi ya kwanza ambayo magazeti mengi ni magazeti binafsi, magazeti ya Serikali ni mawili tu Dalynews na Habari leolakini magazeti mengine yapo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika vituo vya redio sisi ndio tuna vituo vingi kuliko vyote, vituo vya redio vingi na kwenye vituo vya redio huingilii. Vingi vinaeleza mambo ya nchini. Kwa hiyo Umoja wa Matifa umetuondoa katika tuhuma hizo ambao watu walizipigia kelele, tumechukuliwa ni nchi ya mfano kwa sababu katika Universal Decralation of Human Rights, haijapanga haki, civil and political rights, economic and social rights zipo sawa na sisi tunaongoza katika economic and social rights. Sio tu Afrika lakini pia katika Bara la Afrika na Asia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, yapo maeneo ya kufanyiwa kazi na haya maeneo ya kufanyiwa kazi yanafanyiwa kazi na mahakama. Mwaka huu na mwaka uliopita Mahakama za Tanzania zimetoa land mark decision moja on private investment, judgment ya Court of Appeal kuhusu kesi ya Tigo ambayo watu wengi hawajaisoma ambapo Mahakama ya Rufaa tena, hukumu ya Jaji Mkuu Juma ime-reaffirm the right to private property na kesi hii haikuwa dhidi ya Serikali, ilikuwa kesi ya mfanyabiashara mmoja tapeli aliyetaka kuidhulumu Tigo shares zake, mwaka jana Mahakama ya Rufaa imetoa hukumu muhimu sana inayoeleza uwazi kabisa mipaka ya DPP katika kutekeleza majukumu yake na kumpa mwongozo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka huu Mahakama Kuu imetoa mwongozo katika utoaji wa bail. Sasa mara nyingi watu tunataka majibu ya mkato, badala ya kutaka process ya mahakama iende na baada ya hapo mahakama itoe mwongozo. Baada ya kumweleza Kamishna wa Umoja wa Mataifa kuhusu mambo hayo na kumkabidhi zile judgment, alisema zile judgments zinafaa zitangazwe dunia zima jinsi ambavyo Mahakama za Tanzania zipo mbali katika kufafanua na kusimamia haki za binadamu…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante.

WAZIRI WA MAMBO NJE NA USHIRIKIANO WA AFRIKA MASHARIKI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante na naunga mkono hoja. (Makofi)