Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017- Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji

Hon. Vedasto Edgar Ngombale Mwiru

Sex

Male

Party

CUF

Constituent

Kilwa Kaskazini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017- Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji

MHE. VEDASTO E. NGOMBALE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Pia nachukua nafasi hii kumshukuru Mwenyezi Mungu na kwa mara nyingine tena kwa namna ya kipekee niwashukuru wapiga kura wa Jimbo la Kilwa Kaskazini. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze na suala zima la uwekezaji wa viwanda katika mazao ya bahari. Mikoa ya Kusini ambayo inapakana na Bahari ya Hindi haina viwanda vinavyosindika mazao ya bahari.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tukumbuke kwamba Mikoa ya Kusini inapitiwa na mkondo wa Kilwa (Kilwa Channel), mkondo ambao unafanya eneo la Kilwa na Mikoa ya Kusini liwe ni miongoni mwa maeneo machache yanayozalisha samaki kwa wingi. Kwa bahati mbaya kabisa mpaka leo baada ya miaka zaidi ya 54 ya Uhuru hatuna kiwanda cha kusindika mazao ya bahari.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mkoa wa Lindi pia unapakana na Mto Rufiji na delta za Mto Rufiji. Delta za Mto Rufiji zimetokana na Mto Rufiji ambao unatiririsha mboji nyingi kutoka Mikoa ya Bara. Maeneo haya yanasababisha bahari hii ya kusini iwe maarufu kwa uzalishaji wa kamba. Tunazalisha kamba wengi, lakini kwa bahati mbaya hatuna kiwanda cha kusindika mazao ya bahari. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kama hiyo haitoshi, sisi watu wa Mikoa ya Kusini tuna mazingira wezeshi ambayo yanaweza kupelekea kuanzishwa kwa kiwanda katika maeneo yetu. Tuna barabara nzuri ya lami, tuna umeme wa uhakika unaotokana na gesi, lakini tuna ardhi ya kutosha. Kwa mfano, katika Jimbo langu maeneo ya Miteja pale, pana ardhi ya kutosha inayowezesha kuanzishwa mchakato wa kuanzishwa kiwanda, lakini kwa bahati mbaya hatuna kiwanda.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kutokana na hilo sasa wavuvi wetu kutokana na kukosa hilo bado wanajihusisha na ku-preserve samaki kwa njia ya kukausha, zile njia za kijima kwamba sasa inalazimika wakaushe ili wapate ng‟onda. Bado tunawafanya wavuvi waendeshe shughuli zao katika njia za kijima.
Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme ukianzia maeneo ya Moa - Tanga mpaka Msimbati - Mtwara, kuna viwanda viwili tu vya kusindika mazao ya samaki. Hii haitengenezi ustawi wa wavuvi wetu wa maeneo ya mikoa ya Kusini. Sasa naomba commitment ya Serikali kwamba Mheshimiwa Waziri atakapokuja atuelekeze ana mpango gani wa kujenga kiwanda cha kusindika mazao ya bahari katika maeneo ya mikoa ya Kusini? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine, niende moja kwa moja kwenye suala zima la uwekezaji katika kilimo cha muhogo. Nilipata kumsikia Mheshimiwa Waziri akisema kwamba Serikali sasa imewezesha kutuletea wawekezaji wa China na wamechagua eneo la mikoa ya Kusini hususan katika Jimbo langu la Kilwa Kaskazini kwamba wataanzisha kilimo cha mashamba makubwa ya mihogo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hilo, naipongeza sana na nichukue fursa hii kuwakaribisha wawekezaji hao, waje, maeneo yapo, tuna ardhi ya kutosha, watu wapo na kwa bahati nzuri sasa tuna umeme huu wa REA. Kwa hiyo, wazo la uwekezaji wa kilimo cha muhogo liende sambamba na kujenga kiwanda cha kusindika mazao ya muhogo. Bila kumung‟unya maneno, napendekeza kiwanda hicho kijengwe katika Jimbo langu katika Tarafa ya Njinjo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, niende kwenye suala zima la kiwanda cha kuzalisha mbolea Kilwa Masoko maeneo ya Kilamko. Wakati harakati za kusafirisha gesi zinaanza kutoka maeneo ya Kilwa kuja Dar es Salaam, kati ya ahadi zilizotolewa na Serikali ya Chama cha Mapinduzi wakati wa mfumo wa chama kimoja mwishoni mwa miaka ya 1980 ni kwamba gesi ile ije Dar es Salaam lakini watu wa Kilwa waliahidiwa kujengewa Kiwanda cha Mbolea maeneo yaa Kilamko. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, mpaka sasa ninavyozungumza, hakuna kiwanda zimebakia hadithi. Kilichotokea ni kwamba, watu wa TPDC walichukua zaidi ya hekari 800 maeneo ya Kilwa Masoko na hawajaziendeleza mpaka leo. Kinachotokea sasa ni kwamba wao walisema watawalipa fidia watu 28 tu. Toka mwaka 1989 walipochukua maeneo hayo mpaka leo ninavyozungumza, kuna zaidi ya watu 1,000 wako pale. Kwa hiyo, watu wa TPDC wamekuja lakini kwa msimamo wa kwamba wao watafidia watu 28 tu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naitaka Serikali ihakikishe kwamba wakati wa mchakato wa kujenga kiwanda kama mlivyotuahidi, wakati tunakumbuka maumivu makubwa ya kuondokewa na gesi yetu kwenda Dar es Salaam, tuwakumbuke pia wale wananchi ambao wapo katika eneo lile. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine la muhimu ni kwamba sasa hivi sisi watu wa mikoa ya Lindi na maeneo ya Kilwa ni wazalishaji wakubwa wa zao la ufuta. Wilaya ya Kilwa peke yake inazalisha zaidi ya tani 25,000 za ufuta, lakini mpaka leo bei ya zao la ufuta inasuasua kwa sababu hatuna kiwanda cha kusindika mazao ya ufuta. Sijapata kusikia kama kuna kiwanda cha kusindika mazao ya ufuta. Ninaona tu kwamba Serikali inaendelea ku-entertain kwamba zao la ufuta lisafirishwe kama zao ghafi kitu ambacho kinawaumiza wakulima wetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nipate maelezo ya Mheshimiwa Waziri atakapokuja atuambie Serikali ina mkakati gani wa kuhakikisha sasa zao hili la ufuta linapata viwanda vya usindikaji ndani ya nchi? Nashukuru, ahsante.