Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Maji na Umwagiliaji

Hon. Felister Aloyce Bura

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Maji na Umwagiliaji

MHE. FELISTER A. BURA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kusimama mbele ya Bunge lako Tukufu lakini nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa afya na kwa neema yake aliyotupatia siku ya leo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naishukuru sana Serikali ya Awamu ya Tano kwa shughuli za maendeleo zinazofanyika kwa mkoa wetu na nashukuru kwamba inawajali wananchi wake. Jiji la Dodoma linakua kwa kasi sana na watu wanaongezeka kwa wingi sana na kwa hiyo mahitaji ya maji ni makubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, maeneo ya pembezoni kama Mpunguzi, Mtumba na maeneo mengine hawajapata maji kwa sababu mtandao unaohitajika kule unahitaji fedha nyingi. Sisi kama Jiji tumeomba shilingi milioni 800 kupitia Shirika letu la Maji la DUWASA ili waweze kuchimba visima vya maji katika maeneo ya pembezoni ili viwanda vitakavyojengwa maeneo hayo na ofisi zitakazofunguliwa wasipate shida ya maji. Kwa hiyo, tumeomba shilingi milioni 800 kwa ajili kuongeza visima kwa maeneo ya pembezoni. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni miaka takribani nane au kumi na kila mwaka suala la Bwawa la Farkwa (bwawa la mkakati) linazungumzwa katika bajeti ya Waziri wa Maji na hatuoni jambo linaloendelea katika uchimbaji wa bwawa hili la mkakati. Bwawa hili kama alivyosema Waziri mwenyewe litawasaidia wakazi wa Jiji la Dodoma, Wilaya ya Chemba na Bahi na hasa wakazi wa Bahi ambao ni wakulima wazuri wa mpunga na wakulima hawa wanalisha Jiji la Dodoma na Mkoa wa Singida. Mwaka huu hatuna mchele kwa sababu mvua haikunyesha na bwawa lile halijachimbwa na kila mwaka tunaambiwa ni bwawa la mkakati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaomba sasa ifike wakati bwawa hili lichimbwe liweze kuwasaidia wananchi wa Chemba, Jiji la Dodoma na Bahi. Nia ya Serikali ya Awamu ya Tano ni kumtua mama ndoo kichwani na wananchi ambao mradi huu utapita katika maeneo yao wanauhitaji mkubwa wa maji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie sasa mradi wa Ntomoko. Mradi huu ni wa miaka mingi sana na ni maporomoko ambayo yana maji ya kutosha. DUWASA ambao wamepewa kazi ya kutengeneza miundombinu na kufufua miundombinu iliyochakaa, wameomba shilingi milioni 600 kwa ajili ya kuanza uchimbaji na kutengeneza mradi huu wa Ntomoko.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wananchi wa Ntomoko wamesubiri vya kutosha, wamesubiri miaka na mimi katika Ubunge wangu nimesimama katika Bunge hili mara nyingi nikiomba wananchi wa Ntomoko wapewe maji. Vile vijiji 12 vinavyozunguka mradi huu wa Ntomoko, maji hayajapatikana mpaka leo. Waliohujumu mradi huu na wako mahakamani, lakini kuwepo kwao mahakamani hakumfanyi mwananchi akapata maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niombe sasa Serikali yangu sikivu, wananchi wa pale wapewe maji, wananchi wa Ntomoko wanaona maji yanabubujika pale lakini hawajawahi kupata maji. Nashauri wachimbiwe kisima basi wapate maji kupitia kisima kwa sababu wao hawakula fedha za mradi, waliokula fedha za mradi wanajulikana, kwa nini wasipate maji?

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukisoma ukurasa wa 52 Serikali imesema kwamba vijiji 11 vinavyozunguka mradi huu watapata maji kupitia mradi mkubwa wa bwawa linalotarajiwa kuchimbwa, bwawa hili linachimbwa katika kata gani? Naomba Mheshimiwa Waziri ukija kujibu uniambie bwawa hili linachimbwa katika kata gani na kijiji gani ili hata Mbunge wa Chemba au mimi mwenyewe nitakapokwenda niwaambie wananchi kwamba vuteni subira, bwawa linakuja kuchimbwa hapa katika kijiji Fulani. Hata bajeti, anasema katika mwaka wa fedha 2019/2020, sijaona fedha zilizotengwa kwa ajili ya uchimbaji au usanifu wa bwawa hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nirudi kule kwenye Bwawa la Farkwa kusema kwamba, hata wananchi wa kule Farkwa hawajalipwa fidia. Unasemaje kwamba mradi wa mkakati wakati wananchi hawajalipwa fidia? Niombe wananchi wa Mombosee na Bubutole walipwe fidia ili mradi utakapoanza basi kusiwepo na tatizo lolote la wananchi kudai fidia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, narudi Ntomoko, naomba wananchi wale wakumbukwe walichimbiwe hata kisima. Wananchi wa Ntomoko, Fai na vile vijiji 11 kama nilivyosema Waziri atuambie kwamba bwawa hili linachimbwa katika kata ipi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie suala la maji kule Kondoa. Kondoa tumepewa shilingi bilioni 4 kwa ajili ya visima, visima vimechimbwa, maji yako ardhini lakini hakuna miundombinu. Kwa hiyo, ukimwambia mwananchi kwamba kisima kimechimbwa inawezekana aliona gari likichimba kisima pale lakini, je, maji anayo? Mwananchi anachotaka ni maji, basi tuwajengee miundombinu wapate maji wale wananchi wa Kondoa Mjini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tatizo hilo liko Chilonwa, Wilaya ya Chamwino, visima 12 vimechimbwa maji yapo tena virefu lakini hakuna miundombinu. Kwa hiyo, wanawake bado wanahangaika kilometa 10, 15 kwa ajili ya kutafuta maji. Tunajua Mkoa wa Dodoma ni kame, hakuna maji, maji lazima yatafutwe ardhini. Niombe sana Serikali yetu sikivu maeneo ambayo maji yamekwishachimbwa na yapo sasa miundombinu itengenezwe ili wananchi wapate maji, wanawake na watoto wafanye shughuli zingine waondokane na tatizo la kuamka saa kumi usiku na kuacha shughuli za nyumbani wakienda kutafuta maji. Vijiji vya Deti, Zajilwa, Itiso, Segala, Dabalo, Chilonwa, Nsamalo na Manchali visima vipo na viko visima nane vilivyochimbwa mwaka huu maji yapo lakini hakuna miundombinu na fedha tumeomba.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la uvunaji wa maji limezungumzwa na Wabunge wengi, naomba sasa Serikali yetu kama hatuna uwezo wa kuchimba visima na kutoa maji maeneo ya mbali kwa ajili ya kuwasaidi wananchi wetu, basi Taasisi za Serikali, shule za msingi, shule za sekondari, zahanati, vituo vya afya, tujenge miundombinu ya kuvuna maji ya mvua. Inawezekana kabisa kero ya maji kwa wananchi wetu ikapungua. Naomba Serikali iweke mkakati huo na uvunaji wa maji hauchukui fedha nyingi na Mheshimiwa Waziri na Serikali inajua. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante Mheshimiwa Bura kwa mchango wako.

MHE. FELISTER A. BURA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja. (Makofi)