Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Maji na Umwagiliaji

Hon. Edward Franz Mwalongo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Njombe Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Maji na Umwagiliaji

MHE. EDWARD F. MWALONGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa fursa hii ili niweze kuchangia katika hoja hii ya Wizara ya Maji ambayo iko mbele yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote nitoe pongezi nyingi sana kwa Serikali yetu ya Chama cha Mapinduzi kwa kazi nzuri inayofanya. Nikisema juu ya Mheshimiwa wetu Rais, Dkt. John Pombe Magufuli, alifanya ziara katika Mkoa wa Njombe na pale Njombe Mjini alituahidi kwamba kuanzia Septamba mkandarasi atakuwepo site kwa ajili ya maji ya Mji wa Njombe. Nikushukuru sana Mheshimiwa Waziri na wewe mwenyewe ulithibitisha mbele ya Mheshimiwa Rais kwamba mkandarasi atakuwepo Njombe kwa ajili ya mradi wa maji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niombe sana jambo hilo litekelezwe kwa sababu Mji wa Njombe unakua kwa kasi na una shida kubwa sana ya maji. Kwa kuwa shida ile ni kubwa na shida yenyewe inasikitisha kwa sababu Njombe kila bonde lina maji ya mwaka mzima sasa tunapokuwa na mji hauna maji na mabondeni kuna maji o hapo masikitiko yanaongezeka zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, viongozi wetu wa Wizara ya Maji kwa maana ya Waziri, Naibu Waziri na Watendaji wote wa Wizara ya Maji tunawapongeza sana. Wanafanya kazi nzuri, ni wasikivu na wanachukua hatua pale tu ambapo tunakuwa tumeshawaeleza matatizo yaliyopo katika Majimbo yetu na kadhalika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande wa Njombe, nimshukuru sana Mheshimiwa Naibu Waziri na Mheshimiwa Waziri. Mheshimiwa Waziri umeingilia Mradi wa Igongwi ambao unaleta shida sana katika Jimbo la Njombe Mjini na nakushukuru sana kwa sababu kasi inakwenda vizuri. Niwaombe wenzangu kule Jimboni, Mkurugenzi wa Halmashauri ya Mji, Mhandisi wa Maji na Mwenyekiti wangu wa Halmashauri wafanye haraka kadri ya maelekezo yako ili kusudi tuweze kumruhusu tena mkandarasi wa Lot One ya Igongwi ili vijiji vinavyoangukia katika mradi huo viweze kupata maji ambavyo Vijiji vya Uwemba, Njomlole, Luponde pamoja na Kitulila. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Jimbo la Njombe kiko kijiji kinaitwa Lugenge katika Kata ya Lugenge, kina mradi ambao umekadiriwa kusaidia zaidi ya vijiji sita. Mradi huu ulikuwa ni wa miezi tisa lakini mpaka hivi tunavyoongea una miaka saba haujakamilika. Mheshimiwa Naibu Waziri unakumbuka tulifika katika kile kijiji na tuliona ule mradi, mkandarasi alituahidi kwamba ndani ya miezi mitatu atakuwa amefikisha maji kwenye tenki hadi dakika hii ninavyoongea mkandarasi yule hajamudu kazi ile.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimwombe sana Mheshimiwa Waziri mtusaidie wananchi wa Lugenge wapate maji. Miundombinu ya usambazaji na matenki ya Vijiji vya Lugenge, Kiyaula, Kisilo, Ihalula na Otalingolo yalishakamilika lakini miundombinu ya kuleta maji kutoka kwenye chanzo mpaka leo haijakamilika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, moja ya tatizo kubwa tunalopata kwenye miradi ya maji, kadri nionavyo mimi hatuna mipango kwa maana ya Halmashauri kuwa na mpango wa maji wa Halmashauri kwamba tunatekeleza mradi upi, kwa ajili ya kijiji kipi, kwa gharama zipi na tukimaliza huu tunaenda upi. Niombe sana sasa Wizara itoe hayo maelekezo kwamba kila Halmashauri sasa iwe na mpango kwa maana kwamba kuwe na usanifu wa kila kijiji ili kuwezesha vijiji viweze kupata maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Jimbo langu la Njombe Mjini kuna Vijiji kama Mtila, Lusitu, Idihani, Idunda, Ihanga, Uliwa, havina dalili kabisa ya kupata maji ya bomba. Niombe sasa Serikali isaidie kutoa maelekezo kwa Halmashauri kusudi vijiji hivi vifanyiwe usanifu, viwekewe mipango ya maji ili tujue kabisa kwamba katika utekelezaji wa mipango yetu ya maji vijijini ni lini itatekelezwa na kwa gharama zipi ili kusudi tunapowaeleza wananchi kwamba tuna jitihada ya kuleta maji hapa, wawe wanafahamu kwamba ni kweli jitihada ya kuleta maji inafanyika kuliko unasema kwamba una jitihada ya kuleta maji lakini hata usanifu haujafanywa, haijulikani ni lini maji yatapelekwa mahali hapo na ni nani atafanya kazi hiyo. Niombe sana jambo hilo liweze kufanyika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunalalamika sana juu ya miradi ya maji lakini tatizo kubwa ambalo tunaliona sisi kama wawakilishi wa wananchi na hasa hasa katika Jimbo langu la Njombe Mjini ni tatizo la usanifu. Unaona kabisa kwamba usanifu umefanyika hasa hasa ile miradi ya vijiji 10, mimi katika Jimbo langu kuna mradi wa Vijiji vya Ngalanga na Utengule, usanifu umefanyika katika mazingira ambayo hayana maji na mkandarasi amepewa kazi ya kutekeleza ule mradi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, naye katika utekelezaji wake anatekeleza kwa viwango vya chini sana. Anaweka mabomba ambayo hayawezi kuhimili pressure, unajiuliza ni nani hapa mwenye mapungufu, ni Mhandisi wa Maji wa Halmashauri, ni msanifu aliyesanifu mradi au mkandarasi? Hakuna teknolojia rahisi kama ya maji, inabidi wataalam wetu huko Wizara ya Maji watafakari na wajiulize kwamba ni kweli wanastahili kuendelea kutoa huduma katika Wizara hiyo? Kwa sababu haiwezekani teknolojia rahisi inashindwa kutoa huduma. Hivi kama leo tungefanya mabadiliko tukasema Wizara ya Maji ndiyo iwe Wizara ya Ujenzi, ina maana madaraja yangebomoka siku ya pili yake, barabara zingebomoka siku ya tatu yake, tungekuwa hatuna huduma kabisa. Teknolojia rahisi kama ya maji tunashindwa kweli kusafirisha maji yawafikie wananchi na tunaona Serikali inatoa fedha nyingi sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niombe sana, wataalam wa Wizara ya Maji wakishirikiana na Wahandisi wa Wizara ya Maji walale kwenye taaluma zao, wafanye kazi kitaalam. Sisi ni wanasiasa lakini tunafika mahali tunaona kabisa kwamba usanifu uliofanywa siyo sahihi kabisa lakini wao kwa vigezo vyao vya utalaam wanasema hivi ndiyo inavyotakiwa, kwa kweli inasikitisha sana. Mimi najua kabisa Waziri, Naibu Waziri na Katibu wetu Mkuu mko makini sana, hebu waangalieni hawa wataalam, kweli wana moyo wa dhati wa kuwasaidia Watanzania wapate maji?

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine tunalo tatizo sana la watengenezaji wa vifaa vya mabomba. Watengenezaji wa vifaa vya mabomba wamekuwa wakiingia katika mitego ya gharama wakishirikiana na Maafisa Manunuzi katika maeneo mengine lakini wakati mwingine wanaingia kwenye mitego ya gharama wakishirikiana na wakandarasi. Mkandarasi BOQ inamuambia bomba labda la PN9 lakini kwa sababu bomba la PN9 ni la gharama kwa hiyo mkandarasi anaongea na mwenye kiwanda, mwenye kiwanda yuko tayari kugonga muhuri wa PN9 kwenye bomba la PN6 ama PN5 matokeo yake ule mradi unakuwa unavujisha maji mara kwa mara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, na kama tunavyosema kwamba tujali viwanda vya ndani, naomba Serikali na sisi Wabunge tusimame pamoja tuwaambie wenzetu wanaotengeneza vifaa vya mabomba kama kweli wanataka tuendelee kuwaunga mkono ili kusudi uzalishaji wa vifaa vyao vya maji viweze kununuliwa na vitumike kwa wananchi basi wawe waaminifu, wakweli na wawe wanatengeneza vitu ambavyo ni imara kwa sababu haiwezekani Serikali itoe fedha nyingi wananchi hawapati huduma, yaani haiwezekani kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo niombe sana, inafika mahali wakati mwingine mkandarasi anakwambia kabisa ni bora nikaagiza bomba kutoka nje ya nchi ni nafuu kuliko kununua ndani. Kwa hiyo, ina maana sasa hata kumuunga mkono huyo mzalishaji binafsi haisaidii kitu. Kwa hiyo, niombe sana kama itawezekana kwenye upande wa usanifu, Serikali iangalie sana kwenye usanifu pamoja na engineering cost kwa sababu hapa mahali pawili ndipo ambapo wakandarasi pamoja na watu wa manunuzi pamoja na consultants wanacheza na gharama za miradi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuangalie mbinu ya pekee ambayo inaweza ikasaidia. Kama inawezekana kabisa, tunao wahandisi katika idara mbalimbali za Serikali, tunao wahandisi wa Jeshi wako Mzinga, wako Suma JKT, tuwe tunawashirikisha kuona hizi engineers cost ziko sahihi kweli kwa sababu bila kufanya hivyo tunamuachia mhandisi na mtu wa manunuzi wanaweka ile engineers cost matokeo yake mradi unakuwa na gharama kubwa halafu unakuwa hautekelezi lakini ukishaona kwamba mahali panapoingia nafsi ya ulafi maana yake hata ufanisi wa kazi unashuka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo naunga mkono hoja na nampongeza sana Mheshimiwa Waziri. (Makofi)