Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Elimu, Sayansi, Teknolojia na Ufundi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.

Hon. Mashimba Mashauri Ndaki

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Maswa Magharibi

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Elimu, Sayansi, Teknolojia na Ufundi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.

MHE. MASHIMBA M. NDAKI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Nakushukuru kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia bajeti ya Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze pia kwa kuwapongeza Mheshimiwa Waziri Profesa Ndalichako na Naibu Waziri mama Engineer Stella, lakini pia nimpe pole kufiwa na mama yake, Mungu aendelee kumtia nguvu katika wakati huu mgumu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, niende moja kwa moja kwenye kujadili hotuba ya Mheshimiwa Waziri na nianze na eneo la ada elekezi. Nilikuwa najiuliza kuna tatizo gani mpaka tuanze na ada elekezi? Tatizo hili linamgusa nani? Na nilikuwa najiuliza, wanaopeleka kwenye shule hizi za binafsi ni akina nani? Si Mawaziri, sio Makatibu Wakuu, sio Makamishna, sio Wabunge na watu wengine wakubwa wakubwa?
Sasa Mheshimiwa Waziri anapoileta hapa au tunapoiona, mimi najiuliza pia je, hii sio conflict of interest? Kwa sababu wanaopeleka watoto kwenye shule hizi ambazo sasa zinatakiwa zipewe ada elekezi ni watu walio na uwezo mkubwa kifedha. Na kama tutakubali ada elekezi kwa shule hizi za binafsi maana yake tunatafuta unafuu wa wakubwa na kama watapata unafuu hawa wakubwa kwenye shule hizi za binafsi basi tusahau shule zetu za Serikali kuboreshwa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, shule za Serikali ni nyingi kuliko shule za binafsi. Kama zingekuwa ni bora zingeweza kuchukua watoto wote wanaofaulu kwenda sekondari, kidato cha kwanza mpaka cha nne, kidato cha tano mpaka cha sita na hizi shule za binafsi zingekosa wateja. Lakini sasa kwa nini shule hizi za binafsi zinachukua watoto wetu? Ni kwa sababu shule zetu za Serikali tunazitelekeza, miundombinu yake mibovu, walimu wachache, ndiyo hawa hatuwalipi vizuri, ndiyo hawa ambao Wabunge wanalalamika hapa hawapandishwi madaraja na ndiyo hawa ambao wakitaka pesa ya nauli kwenda likizo hapewi. Lakini kwenye shule hizi hayo yote wanapewa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kwa nini huyu mwalimu asifundishe vizuri? Kwa nini huyu anayemiliki shule binafsi anapolipa pesa hii asitengeneze miundombinu mizuri ya madarasa? Nyumba za walimu na mambo mengine? Kwa hiyo. Mheshimiwa Waziri mimi ningekuomba tu ungekuja na mkakati mahsusi kwa ajili ya kuboresha shule zetu za Serikali, tunazo kuanzia ngazi ya kata, kata zote zina sekondari, vijiji vyote vina shule za msingi. Sasa hizi zinatakiwa ziboreshwe. Tuwe na walimu ambao wako motivated, tuwe na madarasa yanayotosha, tuwe na vitabu vinavyotosha, mazingira kwa ujumla kwenye shule zetu yawe bora. Hizi shule za binafsi watapunguza wenyewe ada zao. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu kama shule za Serikali zimekuwa nzuri, zinatoa kile wanachotaka wazazi naniatapeleka mtoto wake shule ya binafsi akalipe laki tano, akalipe milioni au ngapi? Sasa nimesikia kwenye majibu ya Mheshimiwa Waziri alipokuwa anaulizwa swali wakati mmoja kwenye Bunge hili, akasema; tunatafuata namna ya kuzitofautisha hizi ada kulingana na shule hizi za binafsi. Sasa nikawa najiuliza pia tunataka kurudi kule kwenye matabaka ambayo Mwalimu Nyerere aliyakataa? Kuna shule za wenye hela, shule za wasio na hela, shule za weusi, shule za weupe. Mimi nafikiri itatuletea matatizo. Suala la ada elekezi tungeliacha, kwa walioamua kuanzisha hizo shule waziendeshe kwa gharama hizo watakazoweza, kama wanashindwa wazifunge.
Niende kwenye suala lingine la pili. Elimu ya msingi bure. Naipongeza Serikali yangu kwa mkakati wake wa elimu bure. Elimu bure imesaidia kuchukua watoto waliokuwa wanafichwa kwa sababu ya michango mbalimbali na ada mbalimbali zilizokuwepo kwenye shule za msingi na shule za sekondari na matokeo yake kwenye shule za msingi uandikishaji umeongezeka. Sisi kwenye Mkoa wetu wa Simiyu uandikishaji ni 123%; kwenye Wilaya yangu ya Maswa asilimia 130 na kitu. Watoto wengi wameandikishwa na hivyo tunaamini watoto wengi watapata elimu kuanzia ya msingi na hata ya sekondari. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini sasa kutokana na kuongezeka huku kuna tatizo la miundombinu kwenye shule zetu za msingi na shule zetu za sekondari. Hatuna madarasa ya kutosha, hatuna nyumba za walimu za kutosha, hatuna vyoo vya kutosha. Aidha, kwenye shule za sekondari maabara zetu hazijakamilika na mahali pengine bado yameanzishwa tu maboma yakaishia hapo na Serikali ilipoanzisha tena mchango wa madawati ndio basi kabisa habari ya maabara imesahauliwa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nilikuwa ninamsihi Mheshimiwa Waziri kwamba hebu tujaribu kuja na mkakati unaoeleweka kuhusiana na mapungufu haya.
Waheshimiwa Wabunge, wengi wameelezea habari ya mapungufu haya kwa hiyo, hiki ni kielelezo kwamba, kila mahali kuna tatizo kubwa la upungufu wa madarasa, nyumba za walimu, ofisi za walimu, vyoo; upungufu huu ni mkubwa. Tunajitahidi na Halmashauri zetu, lakini ni vizuri Wizara hii kwa sababu, ndio Wizara mama na ndio yenye kuelekeza ubora wa elimu kwenye nchi yetu waje na mkakati ni kwa namna gani tunatatua tatizo hili kwa sababu, tumekazana na habari ya madawati, lakini najiuliza madawati haya yanawekwa wapi? Juani kwenye mti? Kwa sababu madarasa hayapo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, shule yangu moja ina darasa la kwanza mpaka la saba ina madarasa matatu tu, shule ya Zawa! Lakini tunapeleka madawati pale ambayo tumechangishana kule. Najiuliza tunaenda kuyaweka wapi?
Mheshimiwa Mwenyekiti, walimu wetu ambao pia wana madai chungu nzima kama walivyosema wenzangu hawana nyumba za walimu na hasa kwenye Jimbo langu shida ni kubwa sasa matokeo yake napata allocation ya walimu anakaa miaka mitatu anaomba uhamisho ahame kwa sababu, nyumba za walimu hazipo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ni vizuri Serikali ikaja na mkakati ni kwa namna gani mkakati unaoeleweka ni kwa namna gani unatatua mapungufu haya ambayo tumeyataja hapa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga…