Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Azimio la Bunge la Kumpongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli kwa kuchaguliwa kuwa Mwenyekiti wa SADC na kuendesha vyema Mkutano wa 39 wa Jumuiya hiyo

Hon. Shamsi Vuai Nahodha

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nominated

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Azimio la Bunge la Kumpongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli kwa kuchaguliwa kuwa Mwenyekiti wa SADC na kuendesha vyema Mkutano wa 39 wa Jumuiya hiyo

MHE. SHAMSI VUAI NAHODHA: Mheshimiwa Spika, naunga mkono Azimio la Bunge la kumpongeza Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kuwa Mwenyekiti wa SADC. Nina sababu tatu za kuunga mkono Azimio lililoko mbele yetu. Kwanza Azimio hili linatukumbusha historia ya ukombozi Kusini mwa Bara la Afrika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mtakumbuka mwaka 1960 mpaka 1980 Baba wa Taifa, Mwalimu Nyerere aliwaongoza viongozi wenzake kuunda Umoja wa Nchi zilizo mstari wa mbele kwa ukombozi Kusini mwa Afrika na hatimaye kuundwa kwa Jumuiya ya SADC. Viongozi hao ni Agostinho Neto wa Angola, Marehemu Khama wa Botswana, Keneth Kaunda wa Zambia, Samora Machel wa Msumbiji na Mzee Robert Mugabe wa Zimbabwe. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Baba wa Taifa aliitumia ardhi ya Tanzania rasilimali alizotujalia Mwenyezi Mungu katika kuendeleza mapambano ya kudai uhuru Kusini mwa Afrika. Pamoja na umasikini wa Tanzania Baba wa Taifa alijitahidi na kutoa mchango mkumbwa sana, lakini kwa bahati mbaya wako baadhi ya watu wanadhani kwamba mchango alioutoa Baba wa Taifa katika kupigania uhuru haulingani na hadhi anayopewa Baba wa Taifa katika baadhi ya nchi Wanachama. Ni matarajio yangu kwamba kufanyika kwa mkutano huu katika ardhi aliyozaliwa Baba wa Taifa kutatukumbusha historia iliyo tukufu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pili azimio hili linatukumbusha kwamba ajenda ya ukombozi Kusini mwa Afrika na Afrika kwa ujumla bado haijakamilika. Waafrika tusipokuwa makini, siku moja tusishangae, ukoloni mamboleo unaweza kurudi katika Bara la Afrika. Ni wajibu wetu tufanye kila linalowezekana tushirikiane kulinda uhuru huu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tatu, Azimio hili linasisitiza juu ya umuhimu wa nchi za SADC kuendeleza awamu ya pili ya agenda ya mapinduzi na Uhuru wa Kiuchumi katika Jumuiya hii ya Afrika ya Mashariki. Kwa kuwa harakati za kupigania uhuru katika awamu ya kwanza ziliratibiwa katika Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, ni matarajio kwamba awamu ya pili ya mapambano ya Uhuru wa Kiuchumi yataratibiwa tena hapa Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sisi kama Wabunge na kama wawakilishi wa Watanzania, ni matarajio yetu kwamba Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania hataongoza mapambano haya ya ukombozi wa kiuchumi. Nalisema hili kwa sababu ipo dhana na hata Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wakati wa Mkutano alisema wazi kwamba yapo baadhi ya Mataifa wanachama wa SADC yanafanya biashara kubwa zaidi na nchi zilizoko nje ya Jumuiya kuliko zinazofanya ndani ya Jumuiya. Nafikiri jambo hili halikubaliki hata kidogo. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)

SPIKA: Ahsante sana.

MHE. SHAMSI VUAI NAHODHA: Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo, naunga mkono Azimio la Bunge. (Makofi)