Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali kwa Mwaka 2019 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kwa Mwaka 2019

Hon. Felister Aloyce Bura

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali kwa Mwaka 2019 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kwa Mwaka 2019

MHE. FELISTER A. BURA: Mheshimiwa Naibu Spika, nichukue fursa hii kukushukuru sana kwa kunipa nafasi hii adimu ya kuchangia katika Bunge lako Tukufu. Pia nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa afya aliyonijalia siku ya leo.

Mheshimiwa Naibu Spika, nichukue fursa hii kuipongeza sana Serikali ya Awamu ya Tano wa usimamizi wa matumizi ya fedha za umma. Kabla ya Serikali ya Awamu ya Tano tulikuwa tunaona kurasa ripoti ya PAC na ripoti ya LAAC zilikuwa na kurasa zaidi ya 100, lakini kwa sasa ukiangalia taarifa iliyoletwa na Kamati hizi mbili unaona jinsi matumizi yalivyodhibitiwa na Serikali na fedha za umma zinatumika ipasavyo. Ukitaka kushuhudia hali hiyo Bunge lako Tukufu lilitoa maazimio kwa Serikali na maazimio hayo yametekelezwa kwa kiasi kikubwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, nitoe tu mfano kwamba, Serikali imeboresha mfumo wa ulipaji kwa Mfuko Mkuu wa Serikali, lakini Serikali pia imeboresha mfumo wa ulipaji mishahara, kuondoa mishahara hewa, vile vile akaunti jumuishi Serikali imeboresha. Kamati yetu kipindi kilichopita tuliiomba Serikali kuona namna ya ukusanyaji wa madeni na hasa madeni ya SUMA JKT ambayo ilikopwa na watu binafsi. Tumeona mpaka mwezi wa sita mwaka 2018, Serikali imeweza kukusanya bilioni saba na milioni mia tisa. Pia tumeona madeni chechefu ya TIB
yameanza kukusanywa. Hii inaonesha jinsi Serikali ilivyo makini sasa kusimamia matumizi ya fedha za umma, naipongeza sana Serikali ya Awamu ya Tano. Serikali pia imehakikishia Kamati kwamba itaendelea kuzingatia Sheria ya Bajeti na kwa utekelezaji wa shughuli mbalimbali za umma.

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na hayo CAG ameona upungufu kwa mashirika aliyokagua kati ya mashirika 150 amekagua mashirika 122, lakini kati ya mashirika hayo aliyokagua ameona upungufu, kama walivyosema wenzangu lakini nianze na STAMICO.

Mheshimiwa Naibu Spika, STAMICO CAG ameshindwa kutoa maoni yake kutokana na kasoro ambazo ni kubwa zilizoonekana katika shirika hili. Katika shirika hili la STAMICO shirika limepata hasara ya bilioni mbili na milioni 387 na hasara hii imetokana na nini, hasara hii imetokana na kutojumuishwa taarifa ya makampuni tanzu ya STAMICO. STAMI Gold Limited na Kyelwa Tin Company ambayo hesabu jumuishi ya mashirika haikujumuishwa kwenye taarifa ya hesabu ya STAMICO. Pia hali halisi ya madeni ya mashirika haya, lakini hali halisi ya madeni ya STAMICO, pia uwekezaji wa bilioni 33 ya uwekezaji STAMICO katika kampuni hizi sio wa uhalisia.

Mheshimiwa Naibu Spika, STAMICO haijafanya tathmini ya uwekezaji au ya makubaliano yake kati yake na Tanzania One Mining na kama ni uendeshaji wa pamoja au kama ni joint venture. Kwa hiyo haya yamefanya CAG asitoe maoni. Niiombe Serikali imeweza kudhibiti mambo mengi kwa mashirika ya umma imeweza kudhibiti matumizi mabaya kwa mashirika ya umma na hata kwa halmashauri zetu itupie jicho STAMICO na kusimamia haya ambayo CAG ameyaona kwa STAMICO. Pia STAMICO iliweka asilimia 10 ya uwekezaji kwa kampuni ya Itetemia, STAMICO haijawahi kupata faida stahiki. Kwa hiyo niiombe Serikali iangalie namna ya kuisaidia STAMICO.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia tulikagua National Housing, National Housing kazi yake ni kujenga na kuuza majengo hapa nchini na imejenga majengo mengi katika halmashauri zetu, lakini kuna uwekezaji uliofanywa pale Kawe, uwekezaji wa nyumba 711 kwa site ya kwanza. Hata hivyo, mpaka sasa ule uwekezaji umesimama na umesimama kwa sababu Shirika la Nyumba la Taifa halina fedha za kuendesha ile miradi, lakini pia tumeona miradi ya pale eneo la Victoria pia kuna miradi mikubwa ambayo National Housing ilianza kujenga ni vitega uchumi lakini mpaka sasa miradi ile imesimama.

Mheshimiwa Naibu Spika, nina wasiwasi kwamba wale wakandarasi waliokuwa wanajenga zile nyumba watakuja kuleta hasara kwa National Housing kwa sababu watadai fedha. Wamesimama ujenzi sio kwamba wao wameshindwa kazi, wamesimama ujenzi kwa sababu hakuna fedha za kuendeleza ujenzi. Kwa hiyo wao wanahesabu kila siku faida, kila siku hasara wanayoipata kila siku wanachaji kwa National Housing na hizi fedha National Housing walizikopa sio kwamba ni za kwao na kule walikokopa kila siku riba inaingia.

Mheshimiwa Naibu Spika, niiombe Serikali iamue kukwamua National Housing tusiache lile shirika letu zuri ambalo limefanya kazi nzuri kwa muda mrefu likapata hasara ambayo haitaweza kumudu kulipa na tumeona kama Serikali haitawasaidia bilioni 99 kwa ripoti ya CAG tuliyoipata watatakiwa kuwalipa wakandarasi.

Mheshimiwa Naibu Spika, nizungumze pia juu ya TPA au juu ya bandari tumeona hali halisi ya bandari ilivyo. Nawashukuru na kuwapongeza kwamba walitoa gawio Serikalini bilioni 168, walitoa Serikalini, nawapongeza sana, lakini kitu ambacho ni shida pale ni usimikaji wa mifumo ya uendeshaji na usimamizi wa shughuli za bandari. Bandari ni shirika ambalo tunalitegemea kuisaidia Serikali katika mapato, lakini kama mifumo haieleweki na mifumo yenyewe imeshagharimu bilioni 57 lakini mpaka leo haijakamilika. Niiombe Serikali isaidie na kuisimamia bandari ili mifumo hii ikakamilike kwa wakati.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna suala la UDOM, UDOM waliingia mkataba na Bima ya Afya kwamba Bima ya Afya wajenge Hospitali ya Benjamini Mkapa na mimi kama mwakilishi wa wananchi wa Dodoma naishukuru sana Serikali kwa ujenzi wa hospitali ya Bima ya Afya, wengi wanapata huduma pale na huduma inayopatikana pale maeneo mengine inawezekana haipatikani. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, BIMA waliambiwa na Serikali kwamba watapewa dhamana ya Serikali kufidia lile deni mpaka leo dhamana ya Serikali haijatoka. Mimi nilidhani ni kitu rahisi tu kwa Serikali kutoa dhamana ya kwake kwa mfuko wa Bima ya Afya. Kwa hiyo, niiombe Serikali, deni hili linazidi kukua kwa sababu ni muda mrefu sasa na mimi kama mkazi wa Dodoma naishukuru sana Serikali kupata hospitali ya Benjamin Mkapa. Lakini basi watoe dhamana kwa ule mfuko maana mfuko huu ni mfuko unaowatibu wenye uwezo na wasio na uwezo.

Mheshimiwa Naibu Spika, nikushukuru sana. Naipongeza sana Serikali ya Awamu ya Tano kwa kusimamia vizuri matumizi ya fedha za umma na kwa kuchukua hatua za haraka pale ambapo inaonekana kwamba kuna ufujaji wa pesa. Naunga mkono ripoti za Kamati zote mbili. (Makofi)