Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali kwa Mwaka 2019 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kwa Mwaka 2019

Hon. Leah Jeremiah Komanya

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Meatu

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali kwa Mwaka 2019 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kwa Mwaka 2019

MHE. LEAH J. KOMANYA: Mheshimiwa Naibu Spika, nikushukuru kwa kunipatia nafasi. Pia nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa kibali niweze kuchangia katika hoja hizi mbili.

Mheshimiwa Naibu Spika, nishukuru kwa kipindi chote nilichokuwa Bungeni katika awamu hii nimeweza kuhudumu Kamati ya Hesabu za Serikali za Mitaa. Mengi nimejifunza, mengi nimeyaona kumekuwa na mabadiliko katika halmashauri zetu katika utendaji kazi. Kumekuwa pia na mabadiliko katika usimamizi wa miradi, miradi imeongezeka tofauti na tulivyokuwa tunaanza.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia Halmashauri katika kujinasua katika ukusanyaji wa mapato pia kumekuwepo na miradi ya kimkakati. Niipongeze Serikali ya Awamu ya Tano, Serikali ya Chama cha Mapinduzi chini ya uongozi wa Mheshimiwa Dkt. Magufuli kwa kuziwezesha Halmashauri zetu kupata miradi mikubwa ya kimkakati kwa mfano soko la Job Ndugai hapa Dodoma, stendi ya basi, soko la Morogoro na miradi mingine iliyopo katika mikoa mingine. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuwepo kwa miradi ya mikakati kutatengeneza sasa mazingira ya kuwezesha ukusanyaji mzuri wa kodi kwa ajili ya Halmashauri. Kubwa pale niombe kuwepo na mikakati mizuri ya uendeshaji ili kuwe na tija katika ukusanyaji wa mapato na tija katika kutoa huduma kwa wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kufuatia ripoti yetu kumekuwa na tatizo kubwa upande wa mafao ya watumishi, tofauti na tulivyokuwa tunaanza Kamati hakukuwa na matatizo ya michango ya watumishi katika mifuko yao ya mafao lakini kwa sasa kasi inakuwa kubwa sana ya mafao ya watumishi kutokupelekwa katika mifuko yao hususan kwa watumishi wa Halmashauri wanaolipwa na mapato ya ndani. Naomba hili kama Mwenyekiti wa Kamati alivyosoma jambo hili likemewe kabisa kwa sababu michango ni midogo lakini riba inaenda kuongezeka kwa kasi kubwa mpaka inazielemea Halmashauri kuweza kulipa mafao hayo na kusababisha watumishi wanaostaafu kupata shida.

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda pia nichangie upande wa Halmashauri kutokukusanya kikamilifu mapato yao. Katika taarifa zetu Halmashauri nyingi zimeshindwa kufikia malengo ya ukusanyaji wa mapato kutokana na sababu mbalimbali za kimiundombinu na hali ya hewa. Moja ya sababu zilizotajwa ni uduni wa mtandao wa mawasiliano (internet) kwa kutumia zile mashine zetu za kukusanyia mapato. Sisi kama Kamati Halmashauri nyingi zilizofika katika Kamati zilionekana mapato hayakuweza kuwasilishwa Halmashauri wakati wa ukaguzi wa CAG, lakini baadaye yalionekana lakini pia yalisababisha kushuka kwa asilimia ya ukusanyaji wa mapato.

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na changamoto zilizo katika mashine hizi, sababu hii haimuondoi Mweka Hazina wa Halmashauri ya Wilaya kusimamia ukusanyaji wa mapato kwa kufuata sheria na kanuni za fedha za Serikali za Mitaa. Kwa sababu misimu ya ukusanyaji wa mapato inajulikana, unajua ni msimu gani upo juu lakini Mweka Hazina amekaa tu ofisini eti anasubiri mtandao usome. Kuna vigezo vingi vya kuangalia, anaweza kuangalia kwenye taarifa ya mapato na matumizi, anaona haipandi lakini umekuwa kama ni mwanya wa fedha hizi kutumika kwa matumizi mengine kabla hazijafikishwa Halmashauri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niipongeze Serikali kupitia TAMISEMI imeweza kutoa mashine za kukusanyia mapato 7,227 ambazo zimewekewa udhibiti zaidi na mashine hizi zinaonekana pia hazitakidhi mahitaji ya Halmashauri zilizopo. Ushauri wangu napenda kutokana naupungufu uliopo katika mashine zilizopo sasa hivi, Serikali ifanye utaratibu wa kuzitoa katika mzunguko zile mashine kwa sababu zifuatazo:-

Kwanza hazijulikani ziliponunuliwa, hakukuwa na mzabuni mmoja kwa hiyo udhibiti wa hizi mashine haukuwepo. Kuendelea kuwepo katika mzunguko zinaendelea kukusanya fedha ambazo haziingii katika mapato ya Halmashauri.(Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia kupitia mashine hizi mpya zilizoletwa zitasababisha sasa kuwe nacontrol ya mnunuzi Halmashauri fulani atajulikana POS yake iko Halmashauri fulani. Kwa hiyo, ushauri mkubwa ziondolewe katika mzunguko.(Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kama wenzangu walivyochangia nataka kuchangia kuhusu madai ya watumishi wa Halmashauri zetu za Serikali. Pamoja na juhudi zinazofanywa na Serikali za kulipa madeni ya watumishi lakini kumekuwepo na malimbikizo makubwa ya madeni ya watumishi katika halmashauri zetu. Kwa mfano, Halmashauri ya Chamwino kwa madai ya watumishi ni shilingi bilioni 1.3; Sumbawanga bilioni 1.3; na Halmashauri ya Meatu bilioni 1.5. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na kuwa Serikali inafanya uhakiki, ushauri wangu ambao nataka kuutoa, kama kuna watumishi ambao hawastahili kulipwa basi taarifa zirudishwe ili Halmashauri ziweze kupunguza katika madeni yaliyopo katika hesabu zao. Pia, Serikali iwe na mkakati wa makusudi wa kulipa madeni ya watumishi. Ushauri mwingine madeni mengine yanasababishwa na mishahara kwa ajili ya ule mfumo wa Lawsonuidhinishaji wake ni mdogo, kwa hiyo inasababisha kutengeneza malimbikizo ya mishahara ambayo hayastahili yangeweza kulipwa katika mishahara kusiwepo na usumbufu wa watumishi kudai madeni yao.

Mheshimiwa Naibu Spika, madeni yanayotokana na watumishi kukaimu kwa muda mrefu yamekuwa ni mengi hususan kwa watumishi wasio na barua za kutoka TAMISEMI ndio wanatengeneza madeni hayo.

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na hayo nashukuru kwa mazuri yanayofanywa. Nakushukuru na naunga mkono hoja. (Makofi)