Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Elimu, Sayansi, Teknolojia na Ufundi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.

Hon. Stella Ikupa Alex

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Elimu, Sayansi, Teknolojia na Ufundi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.

MHE. STELLA I. ALEX: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi hii. Awali ya yote napenda kumshukuru sana Mwenyezi Mungu kwa ajili ya ulinzi, rehema na fadhila zake kwangu pamoja na familia yangu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, pia napenda niitumie nafasi hii kumpa pole sana Mheshimiwa Naibu Waziri Engineer Stella Manyanya kwa kuondokewa na mama yake mpendwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, vile vile naomba niitumie tena fursa hii kuipongeza Serikali yangu ya Chama cha Mapinduzi kwa jinsi ambavyo imetekeleza kwa haraka sana ahadi yake ya elimu bure kuanzia darasa la kwanza mpaka kidato cha nne. Kama tunavyofahamu kwamba, hata mbuyu ulianza kama mchicha, pamoja na changamoto zilizopo lakini Serikali yetu inastahili kupewa pongezi kwa jinsi ambavyo imefanya na kwa jinsi ambavyo inaendelea kutatua changamoto ambazo zimejitokeza ikiwemo changamoto ya madawati.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niongelee tatizo la ufaulu wa msomo ya sayansi, biology pamoja na mathematics. Mheshimiwa Waziri kwenye hotuba yake ameliongelea hili, lakini naomba niongelee kwa msisitizo. Kweli kumekuwa kuna tatizo kubwa la ufaulu wa masomo haya kwa watoto wetu, tatizo ambalo linasababishwa na Walimu lakini pia ukosefu wa maabara pamoja na vifaa.
Mheshimiwa Naibu Spika, naishauri Serikali kwa upande wa Walimu, iangalie watu ambao wanakwenda kuchukua course ya Ualimu, wawe ni wale watu ambao wamefaulu sana katika haya masomo yaani chemistry, biology na physics. Inakuwa inatia simanzi sana kuona kwamba Mwalimu ambaye labda yeye alipata ā€žDā€Ÿ lakini ndiyo huyo anayekwenda kusoma Ualimu wa physics au Ualimu wa chemistry. Kwa hiyo, naishauri sana Serikali iliangalie hili.
Mheshimiwa Naibu Spika, pia naomba niongelee suala zima la ukosefu wa maabara pamoja na vifaa katika hizi maabara. Inatia simanzi sana kuona kwamba vyumba vipo, lakini vifaa vya maabara hakuna tatizo ambalo linapelekea wanafunzi kufundishwa theory, lakini baadaye inabidi aende akafanye practically, vifaa hamna vya kumwezesha mwanafunzi huyu kufanya hizi practical, mwisho wa siku anaingia kwenye chumba cha mtihani anakutana na swali hata ambalo ni rahisi la titration anashindwa kufanya, anakutana na kifaa kama test tube, anashindwa kugundua kama hiki kifaa kinaitwa test tube.
Kwa hiyo, niiombe sana Serikali iliangalie hili, iangalie uwezekano mkubwa wa kuweka vifaa kwenye hizi maabara zetu.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba pia niongelee suala zima la changamoto ya elimu kwa wanafunzi ama watoto wenye ulemavu. Changamoto ziko nyingi sana, lakini naomba niongelee changamoto chache kwa sababu ya muda. Kuna changamoto kubwa ya Walimu kwa watoto hawa wenye ulemavu. Changamoto hii ni ya muda mrefu na ni changamoto kubwa. Niiombe sana Serikali kwa habari ya Walimu wa kundi hili maalum, wawachukue wale Walimu ambao wana uweledi wa kuwafundisha watoto hawa ndiyo ambao wakachukue course hii ya kufundisha watoto wenye ulemavu.
Mheshimiwa Naibu Spika, pia niiombe Serikali itoe motisha kwa sababu kiukweli kufundisha makundi maalum ni kazi. Kwa hiyo, itoe motisha kwa maana ya pakages za mishahara ziwe kubwa tofauti na Walimu wa wanaofundisha watoto wengine. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, pia naomba niongelee suala zima la changamoto ya miundombinu kwa watoto wenye ulemavu ama wanafunzi wenye ulemavu. Changamoto hii ni kubwa kuanzia primary school mpaka vyuoni. Naomba nitolee mfano mdogo wa Chuo Kikuu cha UDOM, hiki chuo ni kipya, kimejengwa miaka ya hivi karibuni, lakini cha kushangaza miundombinu yake si rafiki kwa wanafunzi wenye ulemavu. Kwa hiyo, niiombe Serikali iangalie suala zima la kuboresha miundombinu kwa wanafunzi ama watoto wenye ulemavu.
Mheshimiwa Naibu Spika, vile vile kuna changamoto ya uhaba wa shule za haya makundi maalum. Shule ni chache sana ukilinganisha na uhitaji. Kwa mfano, unaweza ukakuta labda shule inapatikana Dar es Salaam, lakini mtoto yuko Mtwara, ama yuko Mwanza ama yuko mahali ambako panakuwa hapana shule, inakuwa ni ngumu sana kwa sababu tuelewe kwamba wazazi wengi wenye watoto hawa wana kipato cha chini. Kwa hiyo, inakuwa ni ngumu mzazi huyu kumleta mtoto wake shule halafu aje amfuate, ukizingatia kwamba pia kulikuwa kuna ile pesa ambayo inatolewa kwa ajili ya kumwezesha mzazi mwenye mtoto mwenye ulemavu kuweza kumpeleka mtoto wake shuleni, hizi pesa siku hizi hazitolewi tena.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, niiombe sana Serikali izirudishe hizi pesa, iwapatie wazazi wenye watoto wenye ulemavu pamoja na walezi ili waweze kusafiri kuwapeleka watoto hawa kwenye maeneo ambayo yana shule maalum. Pia niiombe Serikali kuboresha sana hizi shule ambazo zipo kwenye maeneo, kwamba watakapoziboresha hizi shule katika maeneo husika, itaondoa huu usumbufu wa wazazi kusafiria huduma hii ya shule kwenda mbali.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niongelee suala zima la changamoto ya vifaa saidizi kwa watoto wenye ulemavu. Unaweza ukakuta kwamba mtoto ana uwezo wa kwenda shule, wa kusoma lakini sasa changamoto yake aidha ni wheel chair au ni brail au ni vifaa vingine vinavyofanana na hivyo. Changamoto hii ni kubwa sana na inawafanya watoto wengi washindwe kwenda shule kwa sababu ya ukosefu wa hivi vifaa saidizi.
Mheshimiwa Naibu Spika, niiombe Wizara ya Elimu, ishirikiane na TAMISEMI pamoja na Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Bunge, Kazi, Ajira, Vijana na Walemavu kuwabaini watoto ambao kweli wana uhitaji wa hivi vifaa saidizi na waweze kupatiwa hivi vifaa tofauti na sasa hivi, vifaa hivi vinaweza vikawa vinatolewa lakini haviwafikii wale walengwa, kwa maana kwamba utakuta mtu yule aliyenacho ndiye anaongezewa, kwamba mtu ambaye ana uwezo wa kupata hiki kifaa ndiye huyo ambaye anapewa tena.
Mheshimiwa Naibu Spika, zoezi hili la utambuzi linawezekana kabisa kwa sababu mimi mwenyewe binafsi nimeshawahi kufanya hilo zoezi. Ni juzi tu hapa nilimtumia Mwenyekiti wangu wa Serikali za Mitaa, nikamwambia kwamba naomba nifahamu idadi ya walemavu waliopo kwenye mtaa huu pamoja na changamoto zao na ilikuwa ni within a week yule Mwenyekiti wa Serikali za Mitaa alinipatia orodha ya hawa watu wenye ulemavu pamoja na changamoto zao. Kwa hiyo, naiomba sana Wizara ya Elimu ishirikiane na Ofisi ya Waziri Mkuu inayoshughulikia Bunge, Sera, Ajira na Walemavu pamoja na TAMISEMI kuwabaini watoto hawa na kuweza kuwapatia hii huduma. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba pia niongelee suala la hivi Vyuo vya VETA. Kumekuwa kuna ongezeko kubwa la ombaomba wenye ulemavu pamoja na tegemezi. Niiombe sana Serikali, ili kupunguza hili wimbi la ombaomba wenye ulemavu, iwasaidie kwa kuwawezesha kusoma katika hivi vyuo vya VETA ikiwezekana iwe ni bure kabisa ili waweze kupata ujuzi wa kuweza kumudu maisha yao. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, pia naomba niongelee na niiombe Serikali kwa habari ya suala zima la lugha ya alama. Kumekuwa kuna changamoto kubwa ambayo tumekuwa tukiiongea kila siku, uhitaji wa Wakalimani wa lugha za alama, lakini nashauri kwamba lugha hii ya alama ifundishwe kama somo mashuleni, kwa maana kwamba mtoto huyu ambaye anasoma sasa hivi darasa la kwanza, anafika form six, ndiye mtoto ambaye tunamtegemea kwamba aje kuwa Daktari amuhudumie mtu ambaye ni kiziwi, aje kuwa ni Polisi, aje kuwa ni Nesi ambaye atamzalisha mtu ambaye ni kiziwi. Pia itasaidia hata kwenye jumuiya zetu kwamba unakutana na mtu ambaye ni kiziwi, lakini kwa sababu ulishasoma hii lugha ya alama inakuwa ni rahisi ku-communicate naye.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba pia niongelee suala zima la Mfuko wa Watu Wenye Ulemavu ambao ulianzishwa kwa Sheria namba 9 ya mwaka 2010. Mfuko huu upo lakini umekuwa hautengewi fedha wala haupatiwi fedha. Niiombe Serikali sana kwamba sasa umefika wakati Mfuko huu utengewe na kupatiwa pesa, pesa hizi zitasaidia kwa habari ya mahitaji ya watoto wenye ulemavu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nimalizie kwa kuongelea msongamano wa watoto kule Buhangija. Kule kumekuwa kuna msongamano mkubwa wa hawa watoto, naishauri Serikali kwamba ifanye kuwatawanya kwa yale maeneo ambayo yako safe ambapo kwa mfano, kama Dar es Salaam, Arusha, Kilimanjaro ni mikoa ambayo iko safe ambayo haijaripotiwa na haya matukio ya mauaji.
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema haya, naomba niunge mkono hoja. Ahsante sana.