Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Bajeti Kuhusu Shughuli Zilizotekelezwa na Kamati hiyo Katika Kipindi cha Mwezi Februari, 2019 Hadi Januari, 2020 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma Kuhusu Shughuli Zilizotekelezwa na Kamati Hiyo Katika Kipindi cha Mwezi Februari, 2019 Hadi Januari, 2020

Hon. Jitu Vrajlal Soni

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Babati Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Bajeti Kuhusu Shughuli Zilizotekelezwa na Kamati hiyo Katika Kipindi cha Mwezi Februari, 2019 Hadi Januari, 2020 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma Kuhusu Shughuli Zilizotekelezwa na Kamati Hiyo Katika Kipindi cha Mwezi Februari, 2019 Hadi Januari, 2020

MHE. JITU V. SONI: Mheshimiwa Mwenyekiti, niwapongeze Wenyeviti wote wawili kwa kutuletea taarifa nzuri, lakini pia na kamati kuchambua kazi walizofanya ndani ya mwaka mzima. Ni taarifa ambazo zinatupa dira lakini kuna maeneo ambayo tungependa kuchangia ili kuboresha zaidi ili na wao katika Kamati zao waendee kuishauri Serikali ili kufanya mabadiliko makubwa zaidi na tuweze kupata mafanikio makubwa zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitachangia Kamati zote mbili. Moja, naomba nichangia kwa upande wa Kamati ya Bajeti. Nishukuru kwamba taarifa yao kwa sehemu kubwa inaonesha kazi ambazo zilipangwa na ambazo wamefanya, lakini bado naomba niendelee kusisitiza Kamati iendelee kuifanyia kazi sekta nzima ya kilimo kwa mapana yake; kilimo, mifugo na uvuvi kwa sababu ndio inachangia kwa 27% kwenye pato la Taifa, lakini ukuaji wake bado ni 4.3%. Bado ni mdogo sana, tulitegemea sekta ya kilimo ukuaji wake ungekuwa angalau 20% au 30% kutokana na watu wengi kuwa huko.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hiyo yote inatokana na kutokuwekeza kwenye Sekta ya Kilimo. Pia, siyo kuwekeza tu kwa Serikali au kuweka labda fedha ya kutosha na bajeti zilizopangwa, yaani budget approval na zile disbursed kuendana sawa kwenye fedha za maendeleo, lakini bado kuna changamoto nyingi ambapo Kamati hii ya Bajeti pamoja na Kamati ya Uwekezaji inaweza kutusaidia kwa kuhakikisha kwamba ile blueprint for regulatory authorities yaani reforms zile ziletwe haraka, kwasababu kwa mwendo tunaoenda, bado itatuchukua labda miaka mitano au kumi kufikia huko.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kilimo hakiwezi kukua kwa sababu bado kuna kodi, tozo na ada nyingi sana ambazo zinazuia sekta hiyo kukua. Tunaondoa kitu kimoja kwa mwaka wakati ilitakiwa viondolewe vitu zaidi ya 50 au 60 ambavyo itafanya Sekta ya Kilimo kukua sana. Moja kwa wale ambao ambao wamesajiliwa kwenye sekta ya kilimo ni kuwa rasmi (formal sector). Wale ambao wana kampuni wanalipa kodi, ada, tozo nyingi sana ambapo yule ambaye hajasajiliwa (informal sector) halipi chochote zaidi ya ushuru; kama ni ushuru, ni ushuru wa mazao. Hiyo inafanya wengi waondoke kwenye formal sector na kurudi kwenye informal sector.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano, kwenye taarifa nzima utaona Sekta ya Kilimo, kwa mfano horticulture ambayo inaingiza zaidi ya dola milioni 680 kwa mwaka, hiyo bado hujajumuisha mboga mboga na matunda ambayo yanauzwa humu nchini ambayo ni zaidi ya mazao mengine yote au bidhaa yoyote nyingine yoyote inayozalishwa nchini, lakini sekta hiyo inachukuliwa kama ni sekta isiyokuwa rasmi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa ili sekta hii iweze kuwa na nguvu zaidi, ni vizuri zile kodi, tozo, ada na ushuru mbalimbali ambazo ndiyo kikwazo zingeendelea kuondolewa. Nami napendekeza, ili tuendelee kuwa vizuri kwenye umwagiliaji, mitambo ile ya kuchimba mabwawa ya maji ingeondolewa kodi, kwa sababu bidhaa wanayozalisha huwezi kutoza kodi ya VAT. Kwa hiyo, wale wakileta hawapati ile exemption kutokana na mitaji (Capital goods). Kwa hiyo, bado kwa wao hiyo kodi inakuwa ni kubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sekta nyingine, kwa mfano, ya madini au ya viwandani, akileta hiyo bidhaa wao hawajali. Wanalipa hiyo kodi kwa sababu au watapata hiyo exemption on capital goods kwa sababu bidhaa zao ziko vatable watasamehewa. Sasa kwenye Sekta ya Kilimo, hiyo haipo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa tumesamehe kwa mfano kwenye majokofu, kwenye cold rooms kwa ajili ya horticulture, lakini tungeenda mbali zaidi, hiyo hiyo gari ndiyo inatumika kwenye maziwa na samaki. Kwa hiyo, wangeangalia kwa mapana yake. Ni vizuri Wizara ya Fedha, Wizara ya Kilimo, Wizara Mifugo zote zikae pamoja na kuangalia kwa mapana yake. Pia nyingine hazipo Wizara ya Fedha. Unakuta tozo na ada mbalimbali zipo katika taasisi mbalimbali kwa mfano OSHA iko sekta nyingine, fire, yote haya wanalipwa kwenye Sekta ya Kilimo. Ndiyo maana hata tukiondoa kodi yote kwa upande wa Wizara ya Fedha ikawa sifuri, bado hizi nyingine zikitozwa bidhaa ya nje bado itaendelea kuwa bei rahisi na hatutaweza kuendeleza kilimo hapa Tanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ni vizuri kwenye Sekta hii ya Kilimo na Mifugo Serikali ingekaa na Wizara nyingine zote wahakikishe kwamba ile blueprint for regulatory authorities, ile reform ifanyike haraka; na kwenye bajeti hii tunatarajia itakuja vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia Serikali iangalie kwamba watakuwa wanapata indirect taxes. Siyo lazima upate direct tax, tuangalie indirect tax ambayo itafanya Serikali ipate mapato makubwa zaidi na huduma kwa wananchi itaongezeka sana. Vile vile coordination baina ya Wizara moja na Wizara nyingine zote, jambo hilo pia lazima lifanywe vizuri na ninaamini Kamati hii ya PIC inaweza ikatusaidia kwa kuunganisha pamoja na Kamati zote ili chini ya Waziri wa Uwekezaji, jambo la uwekezaji wa ndani na wa nje yote iende sambamba

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukirudi pia kwa upande wa uwekezaji, nashauri kwa mfano kwenye shirika letu, kama tulivyopendekeza Serikali iwekeze, tunaipongeza kwamba TTCL sasa inafanya vizuri, lakini mngeiongezea mtaji wa kutosha. Kwa sababu leo kampuni binafsi ambayo wanachukua data kutoka TTCL na kuuza kwa wateja ambao ni raia wa kawaida, ni vizuri TTCL pia ingepata mtaji wa kutosha nao waendelee kusambaza mawasiliano, data pamoja na voice ili iweze kuwa na nguvu kama tulivyosema kwa upande wa NIC.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sheria nyingi ambazo ziliunda haya mashirika zimepitwa na wakati. Ni vizuri zingeangaliwa upya ili zifanyiwe marekebisho ili mashirika haya pia yaweze kuwa na mchango mkubwa katika pato la Taifa lakini pia wananchi kuendelea kupata huduma vizuri zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mbali na hiyo, kama nilivyosema kule kwenye Sekta ya Kilimo, ni vizuri tukaangalia bajeti ambayo imekuwa approved na bajeti ambayo inakuwa disbursed bado haijakaa vizuri. Ni muhimu wakaangalia nini kitapunguza gharama ili uzalishaji wa ndani uweze kukua na viwanda vya ndani viweze kukua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo ukiagiza viwanda vidogo vidogo ya vya thamani ya shilingi milioni 10, 20 au 30, vinatozwa kodi kama kawaida na wakati wa kuingiza hawapati ule msamaha wa capital goods ambayo ingesaidia viwanda hivi vidogo na Watanzania wengi wangeweza kuwekeza huko kwa sababu umeme umeenda katika maeneo mengi, pongezi kwa Serikali. Hiyo ingetusaidia kuwa na viwanda vidogo ambapo bidhaa zinazoenda viwandani zingekuwa zinatoka kwenye sekta ya kilimo, mifugo, uvuvi na ingetusaidia sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine muhimu ambalo Kamati inaishauri Serikali ni suala hili la informal sector na formal sector. Leo hii tumeona informal sector inaendelea kukua na hiyo ni kutokana na kwamba formal sector ndiyo wanakamuliwa, wanatozwa kodi, ada, tozo na ushuru mbalimbali ambayo inawafanya wengi sasa kukata tamaa na wengi sasa wanarudi kuwa informal sector. Lengo la Serikali ni kuwa na formal sector ambayo ni strong.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lengo la kuwaandikisha hawa walipa kodi kuongeza wigo ni muhimu sana kwa sababu wengi wakilipa, Serikali itaweza kupunguza kodi na ushuru mbalimbali ili jambo hili liweze kufanikiwa. Ombi langu ni kwamba Serikali ikubali kuunda taasisi moja, Tanzania Regulatory Authority ambayo taasisi zote hizi zitakuwa chini yake ili sasa mfanyabiashara alipe mara moja halafu sasa huko ndani wanagawana ili tuweze kudhibiti watu kwenda kudai fedha na kupiga faini za ajabu ajabu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya hayo, naomba nishukuru na kupongeza Kamati zote mbili kwa kazi nzuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana.