Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Bajeti Kuhusu Shughuli Zilizotekelezwa na Kamati hiyo Katika Kipindi cha Mwezi Februari, 2019 Hadi Januari, 2020 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma Kuhusu Shughuli Zilizotekelezwa na Kamati Hiyo Katika Kipindi cha Mwezi Februari, 2019 Hadi Januari, 2020

Hon. Mashimba Mashauri Ndaki

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Maswa Magharibi

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Bajeti Kuhusu Shughuli Zilizotekelezwa na Kamati hiyo Katika Kipindi cha Mwezi Februari, 2019 Hadi Januari, 2020 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma Kuhusu Shughuli Zilizotekelezwa na Kamati Hiyo Katika Kipindi cha Mwezi Februari, 2019 Hadi Januari, 2020

MHE. MASHIMBA M. NDAKI – MWENYEKITI WA KAMATI YA KUDUMU YA BUNGE YA BAJETI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa tena nafasi ili niweze kuhitimisha hoja yangu ambayo iliwekwa Mezani kwako asubuhi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hoja ya Kamati ya Bajeti imechangiwa na Wabunge tisa; Mheshimiwa Dkt. Sware Semesi, Mheshimiwa Mbaraka Dau, Mheshimiwa Jitu, Mheshimiwa Adadi Rajabu, Mheshimiwa Mussa Mbarouk, Mheshimiwa Martha Umbulla, Mheshimiwa Shally Raymond, Mheshimiwa Joseph Kakunda na Waziri wa Fedha na Mipango - Mheshimiwa Dkt. Mpango.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niende moja kwa moja kwenye hoja zilizosemwa na Waheshimiwa Wabunge, kwa sababu muda wangu ni kidogo sana hapa. Mheshimiwa Dkt. Sware aliongelea kuhusu VAT kwenye miradi ya World Bank, kuiwezesha NFRA, uwekezaji kwenye Sekta ya Kilimo na uwekezaji kwenye Shirika la TTCL.

Mheshimiwa Mwenyekiti, masuala yote hayo tumeyazungumza kwenye Kamati na pia kwenye taarifa yetu tumeyaonesha. Kwa mfano, kipengele cha 12 - Mapendekezo ya Kamati; 12:3, 12:5 NFRA ukurasa ule wa saba kipengele cha 3:2 na Sekta ya Kilimo tumeizungumza sana hasa ukurasa ule wa saba kipengele cha 3:1.

Mheshimiwa Mwenyekiti, inawezekana kuwa ukuaji wa uchumi ungechochewa zaidi na Sekta ya Kilimo, lakini pia sekta ambazo Serikali imewekeza zaidi zinachangia kwa sehemu kubwa sana kwenye kilimo. Kwa mfano, Sekta ya Ujenzi inachangia kwa sehemu kubwa sana kwa sababu mimi naamini sekta hizi huwezi kuziweka peke yake zikawa na faida kwenye uchumi, lakini zina faida kilimo pia kwa sababu ya namna ya mwingiliano wa kilimo pamoja na sekta ambazo Serikali iliwekeza sana. Hata hivyo, bado kuna umuhimu kwa Serikali kuwekeza zaidi kwenye suala hili la kilimo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Mbaraka Dau aliongelea masuala ya TRA kufikia shilingi trilioni 1.9, nami naungana naye kuipongeza TRA kwa sababu kwa kweli wamefika kiwango ambacho ni kikubwa na kwa kweli ni cha kupigiwa mfano. Huwezi kudharau jambo hili. Shiligi trilioni 1.9 ni kiwango kikubwa, ingawa kweli bado jitihada zinatakiwa kufanyika, lakini ni kiwango kikubwa kabisa ambacho tunahitaji kutambua. Nasi kama Kamati tumetambua hilo na kwa kweli wamefanya jitihada mno. Kwa muda wa nusu mwaka makusanyo ya nchi kwa ujumla ni asilimia 95 nukta, sikumbuki sawa sawa lakini ni asilimia 95. Sasa makusanyo ya namna hii kwa mtu yeyote kwa kweli lazima apongeze.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia Mheshimiwa Dau amezungumzia upotevu wa mapato yasiyo ya kodi, lakini bado Kamati inaendelea kusisitiza pia kwamba kuhusiana na suala hili na tunatambua kwamba mapato kweli yanapotea hasa kwenye bandari zinazoitwa bubu; sasa kwenye Kamati pia tulisisitiza sana kwamba suala hili liangaliwe vizuri kwa sababu ni muhimu sana kuziangalia hizi bandari bubu. Bahati nzuri mwaka 2019 tulipitisha bajeti ya kumruhusu Waziri anayehusika na Wizara hii kuweza kuzitambua bandari bubu. Kwa hiyo, ni suala tu la Serikali sasa kuona ni kwa namna gani wanaweza wakazitambua baadhi ya bandari bubu ili kuweza kupunguza upotevu wa mapato ya Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Dau alizungumzia pia ukusanyaji wa kodi ya majengo, naye alisema hakuwa ameona kwenye taarifa yetu, lakini kwa kweli kwenye taarifa yetu suala hili tulizungumza na kwenye mapendekezo kipengele kile cha 12:9 tulilitaja vizuri na naamini Mheshimiwa Dau atakuwa ameona pia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia alizungumza juu ya mfumo wa stamps za kieletroniki (ETS). Kamati inaipongeza Serikali sana kwa kuja na mfumo huu madhubuti ambao tunaweza kusema umetoa real time data, yaani kwa makusanyo yanayokusanywa kwa wakati ule ule na lakini pia kuziba mianya ya upotevu wa mapato. Mfumo huu umeonyesha matokeo chanya na hivyo Serikali haina budi kuangalia sehemu nyingine pia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuanza na mfumo huu mwanzoni kabisa, Kamati ilitaarifiwa kwamba Serikali wanaanza na vinywaji vile vikali, lakini wanaendelea kuweka ETS kwenye viwanda vile vinavyozalisha vinywaji baridi; maji, soda na kadhalika. Nadhani pia Serikali wataangalia ili kwenda kwenye bidhaa zaidi ya hizo za vinywaji peke yake kwa sababu katika Kamati tuliona pia pengine labda wanaweza wakaenda mpaka kwenye cement na bidhaa nyingine ili mradi tu kuhakikisha kwamba kodi inayotokana na bidhaa hizo ambazo tunaweza kuweka ETS, basi kodi hiyo ipatikane kwa urahisi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia alizungumza juu ya mchango wa hisani ya jamii (social responsibility). Mheshimiwa Dau alisema kule kwake kuna mtu mmoja anachangia shilingi milioni mbili nadhani kwa mwaka na alikuwa anaona pengine hicho ni kiwango kidogo. Sasa ipo Sheria ya Mapato Na. 332 ambayo inazungumza juu ya suala hilo. Kwa hiyo, ni muhimu sheria hii ikafuatwa ili kwamba wananchi wanaozunguka eneo hilo ambalo mwekezaji yupo na wenyewe waweze kufaidika na kitu hiki kwa sababu kipo kwenye sheria zetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mchangiaji mwingine ni Mheshimiwa Jitu Soni, yeye aliongelea kuhusu masuala ya Sekta ya Kilimo na Blue Print. Kamati inaipongeza Serikali kwa hatua iliyochukua hasa katika kuondoa tozo mbalimbali ikiwa ni pamoja na zile alizokuwa akizitaja Mheshimiwa Jitu. Bado tunasisitiza Blue Print kwa sababu bado ipo kwenye mchakato wa kufanyiwa kazi, basi Serikali iharakishe kufanyia kazi suala hili ili wananchi na wafanyabiashara kweli wawe na mazingira mazuri ya kufanyia biashara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia alizungumzia kuhusiana na Serikali ione umuhimu wa kusimamia Sekta ya Kilimo na kuondoa vikwazo vya kikodi katika sekta hii. Suala hilo limezungumzwa pia na Wabunge wengine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna suala la TTCL ambalo Mheshimiwa Waziri pia amelizungumzia. Tunashukuru kwamba Serikali imekubali kwamba TTCL inahitaji kuwezeshwa. Kwa kweli inahitaji kuwezeshwa hasa katika suala la minara. Tunashukuru kwamba Serikali inakubaliana na pendekezo tuliloliweka kwa sababu tayari wameshakutoa ruhusa ili waweze kukopa kama Mheshimiwa Waziri alivyosema.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi pia tulikubaliana kwamba TTCL hawapaswi kununua minara mitumba, baada ya maelezo yanayohusiana na sheria tuliyoiweka sisi wenyewe. Kwa hiyo, hatukubaliani na suala hilo, lakini bado tunasisitiza kwamba Serikali ione umuhimu wa kuiwezesha TTCL ili iweze kufanya kazi zake vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Balozi Adadi Rajab ameongelea masuala ya miradi ya Liganga na Mchuchuma na pia mradi wa General Tyre. Tumesisitiza kwenye taarifa yetu kuhusiana na miradi hii ya kimkakati ambayo ipo kwenye Mpango wa Maendeleo wa Miaka Mitano kwamba miradi hii basi Serikali iharakishe namna ya kuitekeleza kwa haraka iwezekanavyo kwa sababu ina tija na ina faida kwa nchi yetu. Kwa hiyo, Serikali iangalie tu ni kwa namna gani inaweza ikaharakisha uanzishwaji wa miradi hii ili iweze kuwasaidia wananchi na kulisaidia Taifa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tulikuwa tu na reservations zetu kwenye mradi wa General Tyre ule wa Arusha kwa sababu tuliona ni kama mipango yake haiendi sawa sawa na pengine wawekezaji waliokuwa wameshapatikana tayari, Kamati ilikuwa inaona kama wawekezaji hao hawajawa serious kiasi cha kutosha kuweza kuanzisha au kufufua kiwanda hiki cha General Tyre. Kwa hiyo, tulitoa tahadhari kwa Serikali kwamba iwe makini inapokaribisha hawa wawekezaji ili kuona kama wanaweza wakafanya kazi hiyo au watashindwa kufanya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Mbarouk aliongelea masuala ya mapato na vyanzo vya Halmashauri kwa mazingira ya biashara. Ni kweli tumekubaliana, lakini mapato na vyanzo vya Halmashauri amezungumzia; lakini ukijaribu kuangalia kuhusu mapato ya Halmashauri kwenye taarifa ambayo tumewasilisha mbele yako, mapato ya Halmashauri yamepanda. Sasa sijaelewa Mheshimiwa Mbarouk anapozungumza mapato au vyanzo vya mapato ya Halmashauri alikuwa anamaanisha mapato ya aina gani? Kuhusu suala la mazingira ya biashara tunakubaliana naye kwa sababu pia tumelizungumza kwenye taarifa yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Martha Umbulla aliongelea masuala ya Deni la Taifa, mfumuko wa bei na NFRA. Mimi nakubaliana naye na sisi tumezungumza kwenye taarifa yetu kwamba suala la Deni la Taifa inabidi liangaliwe kwa sababu ukuaji wake ni ule wa nje. Ni wale wakopeshaji wa nje, sio wakopeshaji wa ndani. Sasa wakopeshaji wa nje wana mambo yao. Sasa ni vizuri kuliangalia kwa makini sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu mfumuko wa bei tulizungumza pia tukashauri Serikali iangalie mfumuko wa bei pamoja na riba zinazotolewa na mabenki yetu ili kuona uwiano wa hivi vitu viwili kama tunaweza kubadilisha au kusahihisha riba zinazotolewa na mabenki yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la NFRA Mheshimiwa Mama Umbulla tunakubaliana kabisa kwamba NFRA lazima iwezeshwe kifedha na kimtaji kwa sababu hivyo ilivyo sasa hivi inakua ni ngumu sana wao kununua chakula au mahindi hasa wakati mahindi yamekuwa kwa wingi kwa wakulima wetu, hasa ukizingatia kwamba suala la chakula ndiyo linalosaidia kupunguza mfumuko wa bei zaidi linapokuwa ni zuri. Sasa likiachwa linaelea, siyo vizuri sana kwa sababu italeta shida kwenye mfumuko wa bei. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Shally Raymond aliongelea mwenendo wa riba pamoja na gharama za mabenki. Mheshimiwa Joseph Kakunda, aliongelea mfumo wa uwajibikaji wa watumishi Serikalini uangaliwe namna ya kuwa na huo mfumo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia Mheshimiwa Kakunda alizungumzia juu ya utokaji wa fedha za mfuko wa jimbo zipangiwe mwezi Januari. Yaani kazi zake zipangwe mwezi Januari, zikija tu ziende kwenye miradi moja kwa moja. Suala hili nadhani linahitaji mjadala mkubwa, kwa sababu ni kweli zikija zinaweza zikaenda kwenye miradi, lakini nadhani mfuko wa Jimbo kazi yake ni kuchochea au kuhamasisha maendeleo, sio kumaliza miradi iliyoanzishwa na Halmashauri husika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kmahitaji ya Jimbo yanabadilika mara kwa mara, sasa yakipangwa moja kwa moja kuanzia Januari halafu yaje yatekelezwe mwezi wa Kumi au wa Kumi na Moja pesa zinapokuja, inaweza kabisa wakati huo ikawa mahitaji yamebadilika yamekuwa mengine na kwa hiyo utekelezaji wake ukawa ni mgumu. Kwa sababu mfuko huu uko chini ya Waheshimiwa Wabunge, nadhani wanaelewa maana yake, pesa zake hizi zinapokuja kwenye Majimbo yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Kakunda ndio alikuwa wa mwisho kuchangia. Labda suala la VAT kwenye miradi linafanyiwa kazi na Serikali na Serikali imekubali…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Malizia Mheshimiwa.

MHE. MASHIMBA M. NDAKI – MWENYEKITI WA KAMATI YA KUDUMU YA BUNGE YA BAJETI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi kumaliza hoja yangu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sasa kutoa hoja kwamba Bunge lako Tukufu likubali maoni, ushauri na mapendekezo ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Bajeti. Ahsante sana. (Makofi)

MHE. PAULINE P. GEKUL: Mheshimiwa Mwenyekiti, naafiki.