Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2019 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara na Mazingira Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2019

Hon. Selemani Moshi Kakoso

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mpanda Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2019 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara na Mazingira Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2019

MHE. MOSHI S. KAKOSO - MWENYEKITI WA KAMATI YA KUDUMU YA BUNGE YA MIUNDOMBINU: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa kunipa fursa ya kipekee kupokea michango ya Waheshimiwa Wabunge ambao wamechangia hoja. Wabunge waliochangia wako 16. Kati ya hao, ni Mheshimiwa Julius Kalanga, Mheshimiwa George Lubeleje, Mheshimiwa Bhagwanji Meisuria, Mheshimiwa Miraji Jumanne Mtaturu, Mheshimiwa Vedastus Manyinyi, Mheshimiwa Deogratias Ngalawa, Mheshimiwa Mbaraka Dau, Mheshimiwa Boniphace Getere, Mheshimiwa Susan Kiwanga na wengineo ambao wanafika 16.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hoja za Wabunge waliochangia taarifa hii ni zinazohusu Sekta ya Ujenzi, Sekta ya Uchukuzi na Sekta ya Mawasiliano. Wengi wao wamejikita sana juu ya hoja ya uharibifu wa miundombinu kutokana na mvua kubwa zinazoendelea kunyesha hapa nchini. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Kamati imezingatia hili na kufanya majadiliano katika vikao vyake na Wakala wa Barabara (TANROADS) katika mwaka wa fedha wa 2019/2020, fedha zilizokuwa zimetengwa kwa ajili ya matengenezo ya dharura ni shilingi bilioni 8.2, wakati
gharama za kazi za dharura zimekadiriwa kuwa shilingi bilioni 15 na inaweza ikazidi karibu mara mbili ya kiasi kilichokuwa kimetengwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kamati imeona kuwa fedha za dharura zinazotengwa ni kidogo ukilinganisha na uhitaji uliopo, hivyo kuona haja ya Serikali kufanya mapitio kwa ajili ya kuongeza fedha za dharura ili kusaidia kufanya matengenezo katika maeneo yaliyoathirika na mvua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye hili hili la barabara, Waheshimiwa Wabunge ambao wamechangia wanachanganya barabara zinazomilikiwa na TARURA na zile ambazo zinamilikiwa na TANROADS. Hili ni vyema Waheshimiwa Wabunge wakaliangalia na tutakapokuwa tumekaa kwenye vikao vya Bajeti tukajielekeza zaidi kuitengea TARURA uwezo mkubwa ambao wanaweza wakajenga hizo barabara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ujenzi wa barabara nchini umekasimiwa kwa TANROADS na TARURA. Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS) ina majukumu ya kupanga, kujenga, kukarabati na kutengeneza barabara kuu, barabara za mikoa za Tanzania Bara na Wakala wa Barabara za Mijini na Vijijini. Hizi barabara zinazojengwa na TARURA ni kwa ajili ya kuhudumia barabara za mijini na vijijini ambazo haziko chini ya TANROADS.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Waheshimiwa Wabunge, niliona hili nilieze ili mwangalie zile barabara zinazotugusa ili tujue kwamba tunapochangia zipo barabara ambazo zinamilikiwa na TANROADS ambazo ziko chini yetu na zile ambazo zinamilikiwa na TARURA ambazo ziko Ofisi ya Rais.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivyo, Kamati imekuwa ikiishauri Serikali iendelee kusisitiza kuwa inaunganisha Miji yote Mikuu na Mikoa iliyosalia kama vile Mikoa ya Katavi - Kigoma, Katavi - Tabora, Kigoma – Kagera, Njombe – Makete, Morogoro, Lindi, Mbeya, Makete – Mbeya na barabara za lami ili kufungua fursa za maendeleo katika maeneo hayo. Aidha, Serikali kukarabati baadhi ya barabara za mikoa zilizo katika hali isiyoridhisha na kutokupitika hasa wakati wa mvua na kuathiri shughuli za kiuchumi na kijamii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile Serikali kuendeleza ujenzi wa barabara za lami hasa maeneo yanayochochea uchumi wa Taifa letu kama vile maeneo yenye Miradi mikubwa, vivutio vya utalii, kilimo, viwanda na madini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Waheshimiwa Wabunge, wamezungumzia sana suala la Viwanja vya Ndege hasa Kiwanja cha Ndege ya Musoma ambacho Mheshimiwa Mbunge ameiomba Kamati kwenye mwezi wa Tatu wafike kwenye eneo la Mkoa wa Mara. Katika Bajeti ya mwaka huu 2019/2020 Serikali imetenga fedha za ndani kiasi cha shilingi bilioni 3.5 kwa ajili ya Kiwanja cha Ndege cha Musoma ambacho kitakuwa katika hali ya usanifu na TANROADS ndiyo watakaojenga na wako katika hatua ya kukamilisha maandalizi ya tender kwa ajili ya ukarabati wa kiwanja hicho. Kazi za ukarabati zinatarajiwa kuanza kufanyika mwaka ujao wa fedha wa 2020/2021.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Waheshimiwa Wabunge wamezungumzia suala la kuchelewa kwa mizigo na meli kukaa kwa muda mrefu bandarini. Wabunge wengi wamelizungumzia hili. Hii ni kutokana na ucheleweshaji wa mzigo unaokuja kwenye Bandari ya Dar es Salaam. Tumeshaishauri Serikali iangalie uwezekano wa kukaa na wadau ili waweze kutoa hili tatizo, kwani kutokufanya hivyo vipo viashiria vikubwa ambavyo vitakimbiza Wafanyabiashara waache kuitumia Bandari ya Dar es Salaam. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli Tanzania ni nchi iliyobarikiwa, kwani kijografia hasa katika usafiri wa usafirishaji wa majini na nchi kavu kwani tumepakana na nchi takribani tisa ambazo zinategemea kupitisha mizigo na malighafi. Kamati imeendelea kuishauri Serikali mara kwa mara; pamoja na kuwa katika mazingira mazuri ya kijografia ni muhimu sana kupunguza urasimu na vikwazo mbalimbali ambavyo vinasababisha Wafanyabiashara kuhama kutumia Bandari yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ipo changamoto ambapo na Serikali wamezizungumzia kwamba zipo changamoto kiasi ambazo ni za mawasiliano hasa maeneo ya mipakani. Ni kweli kumekuwepo na changamoto za wananchi wanaoishi maeneo ya mipakani kukosa huduma ya mawasiliano au wakati mwingine kupata huduma ya mawasiliano toka nchi jirani, jambo ambalo siyo sawa na ni hatari kwa usalama wa nchi. Hivyo, Kamati imeendelea kutoa ushauri wa kuishauri Serikali kusimamia jambo hili liweze kufanyiwa maboresho ya maeneo ya mipakani na ikiwezekana kuweka minara yenye nguvu ambayo itawezesha kupata mawasiliano.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ipo michango ya Mbunge mmoja mmoja, siyo rahisi kuipitia yote, lakini kuna baadhi ya maeneo ambayo naweza nikagusa. Mheshimiwa Dau Mbaraka ametoa pongezi za ujenzi wa gati lakini ameelezea juu ya umuhimu wa kujenga boti mpya ya kisasa itakayotoa huduma kwenye eneo la bahari ya hindi kwenda eneo la Mafia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali ilishaanza kulifanyia kazi. Kwa sasa inaendelea na ujenzi wa boti ambayo itatoa huduma kwenye maeneo hayo, lakini amezungumzia suala la minara penye maeneo ya Mafia. Tunavyozungumza hivi, kesho kutakuwa na uzinduzi wa minara kwenye eneo la Mafia. Hivyo, Serikali ilishasikia ombi lake na sisi kama Kamati tumekuwa tukisimamia Mfuko huu ili uweze kutoa maboresho kwenye maeneo mbalimbali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye suala la maboresho ya Viwanja vya Ndege, Kamati imeendelea kutoa ushauri wa kuielekeza Serikali hasa kwenye Viwanja vya Ndege vya Mwanza, Mbeya, Songwe na Dodoma. Eneo hili ni muhimu sana ili kufanya maboresho ya viwanja hivi vya ndege. Viwanja hivi vinatumiwa na Watanzania walio wengi na Kiwanja cha Mwanza kinategemewa kuwa Kiwanja ambacho kitakuwa hub ya kutumika kwenye maeneo ya Afrika Mashariki. Hivyo, tunahitaji Kiwanja kile kifanyiwe ukarabati hasa kujenga Jengo la Abiria na kuweka wigo kwenye maeneo ambayo wananchi wanakatisha kwenye viwanja hivyo vya ndege.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mchangiaji mwingine amezungumzia juu ya umuhimu wa kuboresha reli ya TAZARA. Reli hii ni muhimu sana katika nchi yetu na ni ya kihistoria ambayo imeelekeza wazi kwamba ilikuwa ya uhusiano kati ya nchi mbili ya Zambia na Tanzania na rafiki wa karibu, nchi ya China.

Mheshimiwa Mwenyekiti, reli hii ina changamoto, hivyo tumeishauri Serikali kuhakikisha wanakaa pamoja kati ya Serikali ya Zambia na Serikali ya Tanzania ili kupitia mapitio ya sheria ya kuweka mazingira mazuri yatakayoifanya reli hii iweze kutumika vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine kwenye suala la Reli ya TAZARA ni umuhimu wa kulipa wafanyakazi waliokuwa wanaidai Serikali. Tunaipongeza Serikali, imelipa fedha nyingi kwa wafanyakazi na wanaendelea kulipa wafanyakazi mishahara, lakini bado kuna baadhi ya Watanzania wenzetu ambao wanadai Shirika hili. Hivyo, tunaomba Serikali ipitie na kuangalia umuhimu wa kuwalipa wale wafanyakazi ili kutoa motisha kwa wale wengine waliobaki. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wapo wachangiaji ambao Mheshimiwa Mwakajoka ameelezea kwa nini suala la miundombinu wanapewa fedha nyingi kwa ajili ya Bajeti? Ni ukweli usiopingika, miundombinu inapewa fedha nyingi kwa sababu Serikali ya Awamu ya Tano imetekeleza miradi mingi karibu kila mkoa, hakuna sehemu ambako hakujaonekana mradi ambao unafanyiwa kazi na Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye maeneo tu ya Mkoa wa Songwe ipo barabara inayojengwa kutoka eneo la Mloo kwenda Kilyamatundu mpaka Mkoa wa Katavi. Hiyo barabara ni muhimu sana kwa maendeleo, lakini kuna ukarabati wa barabara ya kutoka Mbeya kwenda Tunduma, hizo ni kazi zinazofanywa na Serikali sambasamba na ujenzi ule wa Songwe ambao utawanufaisha sana wananchi wa Kanda ya Nyanda za Juu Kusini kwa ajili ya kusafirisha mizigo na kutoa fursa mpya ya usafirishaji wa zao la matunda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni mengi ambayo yametekelezwa ambayo Serikali ya Awamu ya Tano imekuwa ikiyafanya. Tunawapongeza Waheshimiwa Wabunge wote walioipongeza Kamati, Serikali kwa kazi ambayo imefanyika na juhudi ambazo zimefanywa na Serikali ya Awamu ya Tano chini ya Rais, Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja ya Kamati hii na ninawashukuru sana Wabunge wote waliotoa mchango wao tunawaahidi kwamba tutaendelea kushirikiana nao kuhakikisha tunafanya maboresho. Tunawapongeza Manaibu Waziri ambao kimsingi wameungana na Kamati na kukubali yale ambayo tumeshauriana nao. Hivyo naamini tukiwa pamoja tutafanya kazi ambayo haitakuwa ngumu na itakuwa na manufaa kwa Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunawashukuruni sana, naunga mkono hoja. (Makofi)

MWENYEKITI: Toa hoja Mheshimiwa.

MHE. MOSHI S. KAKOSO - MWENYEKITI WA KAMATI YA KUDUMU YA BUNGE YA MIUNDOMBINU: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kutoa hoja.

MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naafiki.