Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Ardhi, Maliasili na Utalii Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2019 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2019

Hon. Ester Amos Bulaya

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Ardhi, Maliasili na Utalii Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2019 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2019

MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ili nami niweze kuchangia katika taarifa za kamati ambazo ziko mbele yetu. Kwanza kabisa nichukue fursa hii kumshukuru Kiongozi wa Kambi Rarmi ya Upinzani kwa kuniamini na kuniteua kuwa Mnadhimu wa Kambi Rasmi ya Upinzani. Hii inaonesha ni namna gani chama chetu kinavyotoa fursa kwa wanawake kushika nyazifa mbalimbali.v
Mheshimiwa Spika, kwanza nianze kwenye taarifa ya Kamati ya Kilimo, Mifugo na Maji. Mheshimiwa Spika, mosi, ningependa Mheshimiwa Waziri wa Maji akija kujibu anieleze. Mradi wa maji wa Bunda umechukuwa mda mrefu sana, na tatizo kubwa lilikuwa ni ufisadi wa
mkandarasi aliyekuwa anaendesha mradi ule ambao sasa hivi ni takribani miaka 12 na mradi bado haujakamilika.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri Mkuu alifanya ziara mkoa wa mara na akapata taarifa mbalimbali kuhusiana na mkandarasi huyu Nyakirang‟anyi aliyepewa kuhudumia mradi wa maji ambayo chanzo chake ni Jabeu.

Mheshimiwa Spika mkandarasi yule Waziri Mkuu aliamuru TAKUKURU imkamate kuhusiana na ufisadi unaofanyika kwenye mradi wa Bunda. Kama haitoshi Mheshimiwa Rais alifanya ziara Mkoa wa Mara na kwenye Jimbo la Bunda Mjini akaelekeza mkandarasi yule akamatwe na akafunguliwa kesi ya kuhujumu uchumi.

Cha ajabu, mkandarasi yule ameongezewa mkataba tena ili kumalizia mradi Bunda; kwa ajabu. Yaani mtu amefanya madudu yote, Waziri Mkuu amesema Rais ameenda amesema bado tu Wizara mnampa tenda mwizi ambaye tayari mlisha declare wenyewe kwamba huyu mtu ni mwizi na amechelewesha huu mradi. Ilifikia kipindi account zake zote zikafungwa, Wizara kipindi cha Maghembe kikamkopesha pesa mwizi; leo tena mnampa tenda? Kwenye moja ya mkataba wake ilikuwa pia aanze kujenga vituo, hajajenga mpaka sasa hivi; mnamuongezea tena mkataba kwa ajili ya kusambaza mtandao wa maji?

Mheshimiwa Spika, haya si maneno yangu nikiongea kitu nina uhakika nacho nakuona mdogo wangu unatikisa kichwa, nina uhakika nacho.

Mheshimiwa Spika, niliongea na kiongozi mmoja mkubwa Wizarani; akasema tumeona tumuongezee mkataba ili amalize; Mara mia kuvunja mkataba wa wizi mkampa mtu mwingine; alizoiba zinatosha ili wananchi wa Bunda wapate maji safi na salama huu mradi ni wa muda mrefu na kuchelewa kusuasua kwa mradi huu na nyie pia mnapata hasara. Ningependa nipate majibu sahihi kwanini mmerudia kumpa mkataba mwizi ambaye aliwekwa ndani na nyie mnasema ni Serikali safi mnashughulika na mafisadi, huyu fisadi mmemuongezea mkataba tena.

Mheshimiwa Spika, ningependa nizungumzie kidogo suala la pamba. Sisi wananchi wa Kanda ya Ziwa vitu tunavyovitegemea ni uvuvi ufugaji na kilimo cha pamba. Tangu nimeingia Bunge hili huu ni mwaka wa tisa kilio kikubwa cha wananchi wanaolima pamba ambacho Serikali ya Chama cha Mapinduzi kimeshindwa kutatua ni mbegu, bei, dawa ya kuulia wadudu na kulipa wakulima kwa muda mwafaka; imekuwa ni tatizo kubwa. Kama pamba ingewekewa utaratibu mzuri ingeleta fedha nyingi za kigeni, ingesaidia kumaliza matatizo mengine na kukuza uchumi wa taifa letu; lakini leo zao la pamba limeshuka. Sasa tunashindwa kuweka mikakati dhabiti ya kusaidia zao la pamba alafu tunakuja na maamuzi ya zima moto.

Mheshimiwa Spika, unakumbuka ilivyoletwa mbegu ambayo haina ubora hatima yake Serikali ilikimbizana kulipa fidia ya mabilioni ya shilingi. Kama tungefanya utafiti wa kutosha tukajua mbegu sahihi wakulima wangepatiwa leo tusingekuwa tunazungumza matatizo ya pamba.

Mheshimiwa Spika, kilimo cha pamba kinaanza mwezi wa kumi na moja lakini hivi tunavyozungumza mpaka leo wakulima hawajalipwa. Huyu mkulima anasomesha watoto, huyu mkulima ana mahitaji mengine. Tukileta takwimu hapa za wakulima wanaodai pamba si sawa, hawa nao ni binadamu. Si mnasema ni Serikali ya wanyonge? Wanyonge ni akina nani kama si hawa wakulima wanaotafuta wanaokopa kuhakikisha hawaombi wanatafuta pesa zao kwa jasho na damu? Hivi leo tukizungumzia mkoa wa Simiyu peke yake wanadai takribani billion nne; hapo bado hatujazungumzia Geita hatujazungumzia Mwanza, hatujaenda Shinyanga haujagusa Mara. Lipeni, na msimu unaanza mwezi wa tano. Jamani kama lilivyo zao la zabibu tegemeo kwa Mkoa wa Dodoma, kama ilivyo korosho tegemeo kwa Mkoa wa Mtwara na sisi wananchi wa kanda ya ziwa tegemeo letu ni pamba.

Mheshimiwa Spika, akisimama Mheshimiwa Raphael Chegeni atazungumzia pamba, akisimama Mheshimiwa Richard Ndassa atazungumzia pamba na nikisimama Ester Bulaya nitazungumzia pamba, akisimama Mheshimiwa Gimbi Masaba, akisimama Mheshimiwa Mashimba Mashauri Ndaki atazungumzia pamba na Mheshimiwa Ester Matiko atazungumzia pamba. Kilio cha pamba kimekuwa kikubwa; inawezekana ninyi Mawaziri hamjui hali halisi iliyoko kule chini.

Mheshimiwa Spika, please fanyeni utafiti wa kutosha msifanye utafiti wa kukurupuka. Fanyeni utafiti wa kutosha, lipeni wakulima kwa wakati ili tuhakikishe zao letu linakua. Kila siku kumekuwa na visingizie lukuki.

Mheshimiwa Spika, hivi vyama vya msingi ni tatizo, kuna rushwa huku. Sasa hivi kumekuwa na malalamiko, na mimi nimepata malalamiko kwenye Jimbo langu Kijiji cha Chagunge. Katibu wa cha msingi amekula pesa ya mkulima takribani milioni tatu.

Mheshimiwa Spika, vilevile havifanyi kazi kwa ufanisi, kuna mazingira ya rushwa. Mtu ili alipwe naye pia lazima atowe kitu kidogo. Tusipokuwa na mifumo mizuri huku juu inaenda kuambukiza uwozo mpaka huku chini, ndiyo maana leo vyama vya msingi navyo havitimizi wajibu wake na havifanyi kazi.

Mheshimiwa Spika, pia kuna tatizo kwenye suala la mizani kwenye vipimo. Tunajuwa inahakikiwa, tunajua; lakini leo hii mkulima anaenda kupima pamba yake, lets say ameweka kwenye shuka, kapeleka kg 15 anaambiwa hii shuka tu peke yake ina uzito wa kg. 3; ni wizi. Fuatilieni, pamoja na kwamba mmefanya uhakiki bado kuna rushwa ndogo ndogo zinamkandamiza mkulima wa pamba.

Mheshimiwa Spika, lakini kuna kitu kingine, nimepewa malalamiko kwa baadhi ya watu ambao wanalipwa. Anasema, anaambiwa ameingiziwa milioni 300…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Ahsante sana.

MHE. ESTER A. BULAYA: …akienda kwenye akaunti anaziona akitoa anakuta milioni 20 wizi na utapeli ukemewe.

Mheshimiwa Spika, ahsante.