Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Ardhi, Maliasili na Utalii Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2019 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2019

Hon. Eng. Edwin Amandus Ngonyani

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Namtumbo

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Ardhi, Maliasili na Utalii Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2019 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2019

MHE. ENG. EDWIN A. NGONYANI: Mheshimiwa Spika, kwanza naomba kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa pumzi na kuniwezesha leo kuongea mbele ya Bunge lako Tukufu. Pili nikushukuru sana kwa kunipa furs hii na kwa kweli nitajitahidi kwenda haraka nikiwa kama mmoja kati ya wajumbe wa Kamati ya Kilimo, Mifugo na Maji.

Mheshimiwa Spika, kwanza ningeanza na taarifa ya jumla kwanza nimpongeze sana Mwenyekiti wa Kamati kwa kutuletea mapendekezo saba tu na kwa kweli sekta nzima ya maji ameleta pendekezo moja sekta nzima ya mifugo ameleta pendekezo moja, kilimo pendekezo moja, umwagiliaji pendekezo moja na uvuvi mapendekezo matatu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nikuombe sana na Bunge lako Tukufu mapendekezo hayo tuyapitishe yawe maazimio ya Bunge letu Tukufu ili Serikali iyafanyie kazi. Nafahamu kuna pendekezo moja halijawekwa wazi ni pendekezo la kuhakikisha kwamba maazimio yaliyopitishwa mwaka jana tunaomba Serikali iendelee kuyatekeleza kama tulivyoyapitisha mwaka jana. Mapendekezo hayo ndio yanagusa watu wengi wameyachangia hapa wanadhani kwamba hayapo katika taarifa hii ya Kilimo, Mifugo na Maji lakini kwa sababu tayari yalishafanyiwa maazimio mwaka jana ikiwa ni pamoja na pendekezo ambalo Mheshimiwa Kiruso ameongelea suala la uendelezaji wa malisho. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naunga mkono sana hoja ya kuanza viwanda vinavyotumia mazao ya kilimo, mifugo na uvuvi kama malighafi, hili pendekezo tukilipitisha na Serikali ikilichukulia kwa ukina wake litatusaidia sana katika kuendeleza sekta yetu ya viwanda lakini wakati huo huo kutoa fursa kwa wakulima kupata masoko ya mazao yanayozalishwa na vilevile kuongeza thamani mazao hayo na kwa maana hiyo kuongeza ajira kupitia sekta hizo za viwanda.

Mheshimiwa Spika, vilevile katika suala la umwagiliaji ni muhimu sana na tunaomba sana Serikali itilie mkazo katika kuhakikisha kwamba eneo hili la umwagiliaji linawekewa bajeti ya kutosha ili researchers wetu wanaoshughulikia na masuala ya mbegu ambazo zinagunduliwa na wataalamu wetu katika vituo mbalimbali vya utafiti viweze kuendelezwa na hivyo kupunguza kiwango kikubwa cha mbegu kinachoagizwa kutoka nje. (Makofi)

Mheshimiwa Spia, nafahamu kwa sasa tunaagiza zaidi ya asilimia 60 na kwa kweli sio sahihi kabisa kutegemea kiwango kikubwa cha mbegu kutoka nje. Ningeomba sana Serikali itilie mkazo suala hili la umwagiliaji kwa sababu ni kweli changamoto kubwa kwa sasa haiwezekani kuandaa mbegu kwa kutumia mvua na wakati huo kipindi hicho hicho ndio uzalishaji wa mazao unatakiwa ufanyike.

Mheshimiwa Spika, ni kwa vyovyote vile utakuta mbegu zinazalishwa kwa wakati mmoja na kilimo chenyewe na njia pekee ya kuondokana na hili ni kuboresha umwagiliaji ili mbegu ziweze kuzalishwa kipindi cha kiangazi kisha wakulima wazipate kipindi cha masika tuweze kupanua kilimo chetu na wakulima wetu wapate mbegu bora na waongeze tija katika uzalishaji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ningeomba kuongelea vilevile suala la force account, wapo walioongelea, mimi nina mtizamo tofauti kidogo kwa maana naungana na Kamati lakini wakati huo kuna eneo nataka niliongezee. Kitu cha kwanza niipongeze sana Wizara ya Maji na Serikali ya Awamu ya Tano inayoongozwa na Dkt. John Pombe Joseph Magufuli kwa kweli suala hili la kutumia force account limetusaidia sana limebadilisha uwezekano wa kutekeleza miradi mingi sana ya maji kwa muda mfupi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, miradi mingi ya maji kwa maana ya kwa utaratibu ule wa zamani wa kutumia wakandarasi ilikuwa unatumia fedha nyingi sana, mradi mmoja unatumia fedha nyingi sana lakini kwa namna ambavyo sasa hivi unafanyika fedha zile zinaweza zikafanya miradi mitano hadi sita badala ya mradi mmoja na mfano huo upo katika eneo ambalo natoka Wilaya ya Namtumbo. Nashukuru sana Waziri wa Maji amesitisha mikataba miwili na mingine miwili nayo amerekebisha ili kuhakikisha force account inatumika katika kununua vifaa na wale wakandarasi wanatoa tu labor force peke lakini vifaa vinanunuliwa na Serikali kupitia force account na matokeo yake gharama za mradi zimeshuka sana kwa zaidi ya asilimia 40 na hivyo kuwezesha miradi mingine mingi kuweza kutekelezeka.

Mheshimiwa Spika, napongeza sana hilo vilevile naungana na pendekezo la Kamati na mimi nimeshiriki kutoa hilo pendekezo kwamba tuangalie suala la ajira kwa makandarasi wetu na hasa wale wanaomaliza mafunzo katika vyuo vyetu vya VETA waweze kupata kazi kwa hiyo watumike na hivyo licha ya kutumia hiyo force account ni nzuri itumike lakini wakati huo tuangalie kuingiza na uwezekano wa kuzalisha ajira kwa private sector. Kwa hiyo, nilikuwa naomba na hilo liangaliwe kama ambavyo Kamati imependekeza. (Makofi)

SPIKA: Ahsante sana.

MHE. ENG. EDWIN A. NGONYANI: Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja zote mbili asante sana.