Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Ardhi, Maliasili na Utalii Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2019 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2019

Hon. Jumaa Hamidu Aweso

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Pangani

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Ardhi, Maliasili na Utalii Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2019 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2019

NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Spika, awali ya yote nikushukuru sana kwa kunipa nafasi hii. Kwa namna ya kipekee nimpongeze sana sana Mheshimiwa wa Kamati yetu ya Mifugo pamoja na Maji Mheshimiwa Mahmoud Mgimwa pamoja na wajumbe wake wamekuwa wakifanya kazi kubwa na nzuri sana ya kutushauri sisi Wizara yetu ya Maji, wamekuwa msaada na wala hawakuwa kikwazo.

Mheshimiwa Spika, ninachotaka kuwahakikishia Watanzania na Waheshimiwa Wabunge, sisi kama viongozi wa Wizara ya Maji hatutokuwa kikwazo kwa Kamati yetu katika kuhakikisha tunaleta maendeleo makubwa sana katika sekta yetu ya maji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimesimama hapa kujibu hoja chache sana. Moja, kuhusu hoja ambayo imetolewa na Mheshimiwa Mbunge wa Mchinga kaka yangu Hamidu Bobali kuhusu suala zima la uvunaji wa maji ya mvua, kwamba lita zitakazozidi elfu 20 unatakiwa ulipie; nataka niweke sawa taarifa. Kwa mtu ambaye anavuna maji ya mvua lita zaidi ya elfu 20 hatakiwi kulipa chochote kama anatumia matumizi ya nyumbani. Hata kama ikitokea anatumia kwa matumizi mengine, ada yake ni shilingi laki moja tu lakini hii yote ni katika kuhakikisha tunalinda na kutunza vyanzo vyetu vya maji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hoja ya pili, imezungumzwa hapa na dada yangu ambaye ninamheshimu sana, Mheshimiwa Ester Bulaya, kuhusu suala zima la mradi wa maji wa Bunda. Nimeshtuka kidogo akiwa kama Mnadhimu kutoa taarifa ambazo binafsi zimenishtusha sana. Nikiri kwamba Mheshimiwa Waziri Mkuu alifika Bunda na akatoa agizo kutokana na athari ya baadhi ya miradi ya maji iliyokuwa ikisuasua na hata baadhi ya wataalam wetu, kwa maana ya kushirikiana kuhujumu miradi ya maji.

Mheshimiwa Spika, yule mkandarasi Nyakirang‟anyi alikamatwa na hatua ambazo tulizichukua sisi kama Wizara; tukasema mradi ule tunaukamilisha kwa kutumia wataalam wetu wa ndani. Fedha ambazo zilitakiwa kukamilisha mradi ule zilitakiwa kiasi cha shilingi milioni 375 lakini wataalam wetu wa ndani wa Mamlaka ya Maji na Usafi wa Mazingira Musoma wamefanya kwa force account kwa shilingi milioni 200 na mradi umekamilika mwezi Desemba mwaka jana, Mheshimiwa nakupa taarifa hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, na mimi kama Naibu Waziri wa Maji nimeshafika na Waziri amekwishafika, na nipo tayari kwenda kuongozana na wewe Bunda kukuonesha kazi nzuri ya Ilani ya Chama Cha Mapinduzi ilivyotekelezwa katika eneo lako la Bunda. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lingine ambalo ninataka kusema, nataka nimjibu Mheshimiwa Mbunge kaka yangu Mheshimiwa Haonga. Wakati mwingine unapojenga hoja hebu jiridhishe basi kidogo kazi zilizofanywa. Amezungumza kwamba kazi ya miradi ya maji, sisi pale katika Jimbo lake tuna mradi wa milioni 550 tumeshalipa pesa zaidi ya milioni 500. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tumeshapeleka fedha ambazo tumepata kupitia fedha za P4R zaidi ya bilioni 119 ambazo zimetengwa kwa mikoa 17 na Halmashauri 86 ikiwemo Halmashauri ya Mbozi ya Mheshimiwa Haonga zaidi ya bilioni 1.3 kwa ajili ya kutekeleza miradi ya maji.

Mheshimiwa Spika, kubwa Serikali ya Awamu ya Tano inaendelea kutekeleza miradi ya maji maeneo yote bila ya ubaguzi wowote. Sisi kama viongozi wa Wizara ya Maji hatulali, usiku na mchana katika kuhakikisha tunaisimamia na kuifuatilia miradi yetu ya maji ili wananchi waweze kupata huduma ya maji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ninachotaka niwaambie wakandarasi na wataalam wa maji vipo vitu vya kuchezea, ukishiba unaweza kucheze kidevu ama tumbo lako, kwa maana ya kitambi; lakini kwa yeyote ambaye atakayetaka kuchezea miradi ya maji, sisi hatupo tayari tutashughulikiana ipasavyo katika kuhakikisha tunajenga nidhamu katika miradi yetu ya maji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tangu Wizara ya Maji ianze kutekeleza miradi ya maji kwa kutumia Programu ya Maendeleo ya Sekta ya Maji, tangu 2006 mpaka sasa tumeshatekeleza miradi 2,450. Hata hivyo Mheshimiwa Rais Dkt. John Pombe Magufuli tangu aingie 2015 mpaka Desemba mwaka jana tumeshatekeleza miradi 1,423. Miradi 792 imekamilika na miradi 600 ipo katika hatua mbalimbali ya utekelezaji, na tumeshajipanga katika kuhakikisha miradi hii inakamilika kwa wakati ili azma ya Mheshimiwa Rais ya kumtua mwanamama ndoo kichwani, kwa maana ya asilimia 85 ya upatikanaji vijijini na asilimia 95 ya maji mijini.

Mheshimiwa Spika, tuna miradi mikubwa ambayo itaongeza hali ya upatikanaji wa maji. Leo ukienda Arusha mradi wa zaidi ya bilioni 520 unatekelezwa, ukienda Orkasmet pale zaidi ya bilioni 30 mradi unatekelezwa. Ukienda Longido zaidi ya bilioni 16 ya mradi umekamilika, Tabora, Igunga, Nzega zaidi ya bilioni 600 ule ni mradi wa standard gauge/Stierglers mfano katika kuhakikisha tatizo la maji na vijiji zaidi ya 102 vitaweza kupatiwa huduma hii ya maji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nataka niwaambie Waheshimiwa Wabunge pia katika Miji 28 na …

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Ahsante sana, malizia Mheshimiwa Waziri.

NAIBU WAZIRI WA MAJI: …ambapo tumepewa fedha zaidi ya dola milioni 500. Nataka niwape taarifa kwamba kibali tumeshapata vya Exim Bank, tunajipanga katika kuhakikisha tunatangaza tenda ile ili mkandarasi apatikane ili azma ya Mheshimiwa Rais kwa maana ya miji 28 miradi ile inatekelezwa na wananchi waweze kupata huduma ya maji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana, asante sana. (Makofi)