Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Ardhi, Maliasili na Utalii Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2019 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2019

Hon. Dr. Hamisi Andrea Kigwangalla

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nzega Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Ardhi, Maliasili na Utalii Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2019 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2019

WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, ahsante, nianze kwanza kwa kuwapongeza Wenyeviti wa Kamati zote mbili ambao wametoa hoja hapa Bungeni leo hii. Lakini niishie palepale alipoishia Mheshimiwa Mpina kwamba Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, aliteuliwa na Mwenyezi Mungu mwaka 2015 kuja kuwafuta machozi Watanzania. Na yeye kwa mamlaka aliyopewa na Mwenyezi Mungu akaunda Serikali ambayo ina mtazamo huo na ambayo inaendelea na zoezi la kuwafuta machozi Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwenye Sekta ya Uhifadhi – wewe ni shahidi – Serikali ya Dkt. Magufuli imewafuta machozi wafugaji ambao walikuwa na migogoro mikubwa na maeneo ya hifadhi. Imewafuta machozi wakulima ambao walikuwa wanaishi bila amani ndani ya mipaka ya nchi yao kwa kuwa wamejikuta wapo katika maeneo ya hifadhi.

Mheshimiwa Spika, leo hii migogoro baina ya wananchi na sisi wahifadhi imepungua sana, na yote hii ni kutokana na utendaji na uongozi mahiri wa Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli. Mheshimiwa Rais ametutuma twende kwa niaba yake tukawafute machozi hawa wananchi. Hatuwezi kukaa ofisini tukategemea tutaweza kutatua migogoro inayowasibu wananchi bila kufika site. Iwe tutaonekana ni watendaji na sio watunga sera ama wasimamizi wa sera, potelea mbali, Cha muhimu tumewafuta machozi wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, katika miaka hii minne ya uongozi wa Dkt. Magufuli, mapato kwenye Sekta ya Utalii yamekua kutoka trilioni 3.8 mwaka 2015 mpaka trilioni zaidi ya 6.5 mwaka 2018. Idadi ya watalii imeongezeka kutoka milioni moja mwaka 2015 mpaka milioni moja na nusu mwaka 2018, matarajio yetu ni kwamba tutakapokuwa tunatoa takwimu za mwaka 2020 ambapo Mheshimiwa Rais, Dkt. Magufuli na Serikali yake watakuwa wanamaliza muhula wa kwanza wa uongozi wa taifa letu, tuwe tumefikisha idadi ya watalii milioni mbili.

Mheshimiwa Spika, na mafanikio haya yamechangiwa na vitu vingi, na mtu atakayebeza kwa kiongozi wa aina yangu sipaswi kumjibu hata kidogo kwa sababu nitaanza ku-question uwezo wake, uelewa wake na uzoefu wake kwenye sekta hii, jambo ambalo kwa heshima niliyonayo na ninayopenda kumpa Mbunge mwenzangu, sipendi kulifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, katika miaka hii minne ya Mheshimiwa Dkt. Magufuli, tumeweza kudhibiti mapato yanayotokana na Sekta ya Utalii kwa kiasi kikubwa kwa kupitia kutengeneza mfumo fungamanishi wa kukusanya mapato ujulikanao kama MNRT Portal ambayo sasa inaendelea kuwekezwa kwenye taasisi zote ambazo zinakusanya mapato kwenye Sekta ya Uhifadhi na Utalii kwa ujumla wake. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini pia tumeweza kuendeleza na kukuza jitihada zetu za kutangaza vivutio vya utalii ikiwemo kutumia maonesho maarufu kama Karibu Kili Fair, Karibu Kusini ambayo ilifana sana, kwao na Mheshimiwa Mch. Msigwa kule, na sasa tunaanzisha maonesho mapya ya Kanda ya Ziwa yajulikanayo kama GLITE (Great Lakes International Tourism Expo) ambayo yatakuwa yakifanyika Mwanza kwa mara ya kwanza mwaka huu mwezi wa sita. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini sambamba na hiyo tumekuwa tukitumia watu mashuhuri kutangaza vivutio vya utalii. Watu mashuhuri wapo ndani ya nchi na nje ya nchi, kwa malengo ya kukuza utalii wa ndani lakini pia wa nje ya nchi. Wamedhihakiwa hapa wasanii ambao tumekuwa tukiwatumia kutangaza vituo vya utalii. Sipaswi kuwajibia lakini ninapenda nieleze kwa ufupi tu concept ya kutumia influencers ama watu mashuhuri kwenye kutangaza katika zama hizi za sasa.

Mheshimiwa Spika, mfano msanii mmoja kama Diamond Platnumz, Nasibu Abdul. Ana wafuasi milioni 8.6 kwenye akaunti yake moja ya Instargram, anajulikana Tanzania kwa kiasi kikubwa, anajulikana Afrika Mashariki, Afrika yote na nchi mbalimbali huko duniani, na hivi ninavyozungumza hapa anafanya tour ya kutangaza muziki wake, kuuza muziki wake nchi za Ulaya, baada ya kumaliza tour nchi za Afrika.

Mheshimiwa Spika, mtu huyu anafuatiliwa kwa ukaribu sana na kwa raha za vijana ambao ni chini ya miaka 35, anafuatiliwa kwa ukaribu kuliko hata mimi na Mheshimiwa Mch. Msigwa. Maana yake akiweka kivutio cha utalii ama experience ambayo ameipata akiwa kwenye kivutio fulani cha utalii maana yake takribani watu milioni 8.6 wana fursa ya kufikiwa na huo ujumbe, na huo ujumbe atakaouweka katika ukurasa wake utadumu kwa muda mrefu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, na kizazi ambacho tunaki-target katika zama za sasa, hususani ukiwa kiongozi visionary ni kwamba tunawatazama watoto wetu, wadogo zetu na vizazi vitakavyokuja kwa sababu sisi hatuna tradition ya kwenda kutalii, hatuna tradition ya safari na vitu kama hivyo. Sasa ili tuweze kuwafikia kizazi hicho, hatuwezi kupenyeza ujumbe wa vivutio tulivyonavyo kwenye television, kwenye magazeti na all these other traditional media, ni lazima tutumie new media ambapo ndipo watoto wetu, wadogo zetu wapo huko.

SPIKA: Malizia Mheshimiwa Waziri.

WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, tukubaliane tu kwamba watoto wa sasa hivi wanatumia mitandao ya kijamii kupata taarifa zaidi kuliko chombo chochote kile kingine cha habari. Kwa hiyo, kwa maana nyingine wanawafuatilia hawa watu mashuhuri. Kwa hiyo, tukiwatumia hawa tuna uhakika taarifa zitafika kwa walengwa kwa haraka zaidi na kwa uhakika zaidi kuliko tukitangaza kwa kutumia njia hizi ambazo tumezizoea. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nakushukuru na ninaunga mkono Hoja za Kamati zote mbili. Ahsante. (Makofi)