Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge na Utawala na Serikali za Mitaa pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Sheria Ndogo

Hon. Lolesia Jeremia Maselle Bukwimba

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Busanda

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge na Utawala na Serikali za Mitaa pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Sheria Ndogo

MHE. LOLESIA J. BUKWIMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi ili nami niweze kuchangia katika taarifa hizi za Kamati. Kwanza nianze kipekee kabisa kuwapongeza Wenyeviti wote pamoja na Wajumbe wa Kamati hizi kwa kazi kubwa ambayo imefanyika. Kusema ukweli mmechambua vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujikita zaidi katika Kamati ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa kuhusu shughuli zake za utekelezaji katika mwaka uliopita. Kabla sijaanza, nitoe kabisa shukrani za dhati kwa Mheshimiwa Rais kwa sababu tulikuwa na changamoto kubwa sana katika upande wa Sekta ya Afya lakini Serikali kupitia Mheshimiwa Rais ameweza kutupatia hospitali ambayo itajengwa katika eneo la Mji Mdogo Katoro, pia ni hospitali ambayo ni ya Umoja pamoja na Uselesele. Hii yote ni kwa ajili ya utekelezaji wa shughuli mbalimbali za maendeleo katika Serikali za Mitaa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme kwamba kwa kweli Serikali inafanya mambo makubwa sana hasa katika Serikali za Mitaa. Wote tumeshuhudia jinsi ambavyo mambo mengi yamefanyika. Siku za nyuma ilikuwa ni changamoto kubwa sana katika Sekta ya Afya, lakini kwa kweli kwa sasa hivi tunaona jinsi ambavyo Serikali inafanya mambo makubwa sana kupitia TAMISEMI. Tumeona katika Sekta ya Afya lakini pia katika Aekta ya Elimu Serikali imeendelea kutekeleza mambo mengi kwa kushirikiana na wananchi. Yote haya nina kila sababu ya kuweza kushukuru na kuipongeza Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo ambalo nilitaka kulizungumza hapa ni suala kubwa kuhusu barabara ambazo ziko chini ya TARURA. Kamati imezungumzia vizuri sana katika ukurasa wa tisa wa taarifa hasa ya Kamati ya Utawala wa Serikali za Mitaa kuhusu utekelezaji wa ujenzi wa barabara kupitia TARURA. Ni kweli kwamba barabara za TARURA zina changamoto kubwa sana na nilikuwa ninaomba kama ambavyo Kamati imeshauri, kwamba kutokana na ufinyu wa bajeti kwa bajeti zilizopita na mwaka huu tumeshuhudia kwamba kuna mvua nyingi sana ambazo zinaendelea Tanzania nzima.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa naomba Serikali katika bajeti ijayo kama ambavyo Kamati imesema kwamba waangalie uwezekano mkubwa wa kuweza kuongeza bajeti hasa katika TARURA ili kuweza kushughulikia barabara ambazo imekuwa ni changamoto kubwa sana. Tukiangalia kila sehemu katika nchi yetu ya Tanzania mvua zinanyesha kwa wingi lakini pia barabara hazipitiki kwa kiasi kikubwa, madaraja yamebomeka. Kwa hiyo, nilikuwa naomba Serikali sasa pengine iangalie sana suala hili la TARURA.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeshuhudia, nami pia nikiangalia kwenye Jimbo langu ninaona kabisa kwamba bajeti za TARURA zinakuwa ni kidogo barabara za TARURA ni nyingi, lakini bajeti inayotengwa ni kidogo. Kwa hiyo, kama Mbunge nilikuwa naishauri Serikali iangalie suala hili kwa sababu barabara ndiyo kiungo kikubwa katika maendeleo ya jamii katika maeneo yetu ya vijijini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaona jinsi ambavyo mwananchi hawezi kusafiri kutoka point moja kwenda point nyingine. Kama barabara haipo kwa kweli changamoto inakuwa ni kubwa. Kwa hiyo, naomba sana kama ambavyo Kamati imesema, tuombe TARURA iongeze bajeti ya kutosha ili kuweza kuboresha barabara za mijini na vijijini ili hatimaye tuweze kuona utekelezaji na uboreshaji wa huduma mbalimbali za kijamii katika maeneo yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile katika upande wa TAMISEMI tumeshuhudia jinsi ambavyo Serikali inajenga Hospitali na Vituo vya Afya vilivyoboreshwa; tunaipongeza sana. Nilikuwa naomba sasa katika bajeti ijayo pengine Serikali iangalie umuhimu wa kuongeza watumishi katika sekta hasa ya Afya ambapo tuna upungufu mkubwa sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikiangalia katika sehemu mbalimbali Waheshimiwa Wabunge wengi hapa wanalalamikia kwamba kuna upungufu mkubwa wa watumishi, ikiwemo pia kwenye halmashauri yangu kwakweli kuna upungufu mkubwa sana ambapo wanahitajika zaidi ya watumishi 200 katika Seta ya Afya.

Kwa hiyo nilikuwa ninaomba pengine Serikali kwa kuwa imeboresha zaidi katika miundombinu hasa kwa kujenga vituo vya afya na hospitali, nilikuwa naomba katika bajeti zijazo iangalie uwezekano wa kuangalia suala zima la kuhakikisha watumishi wanapatikana wa kutosha ili sasa tuweze kuhakikisha kwamba huduma sasa inaboreshwa vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kipindi hiki wananchi wanahudhuria kliniki au kwenye vituo vya afya, lakini kwa sababu ya wingi wa watu unakuta watumishi wanakuwa wachache, na hatimaye kunakuwa na changamoto kubwa sana katika utoaji wa huduma.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo Serikali imeboresha kwa kiasi kikubwa, imeongeza dawa za kutosha; na ukiuliza hata sasahivi vijijini watu wanafurahia sana huduma kwa kiasi kikubwa. Juzi nilikuwa napigiwa simu naambiwa hata ukienda katika hospitali ya Rufaa ya Wilaya na hata ile ya Mkoa tumeshuhudia kwamba wazee wametengewa sehemu maalum kwa ajili ya kupewa huduma. Kwa kweli huduma zimeboreshwa vizuri, lakini tu ni mpungufu madogo hasa katika upungufu wa watumishi katika maeneo mengi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile pamoja na sekta ya afya, napenda tu kuomba mimi binafsi kwenye jimbo langu tumeshuhuda Mheshimiwa Rais ametoa maelekezo kwamba kila halmashauri ihamie kwenye maeneo yao ya utawala. Sisi katika halmashauri yetu, ofisi yetu ya halmashauri imehamia Nzela, ambako kidogo ni mbali kiasi kwamba baadhi ya wananchi ndani ya halmashauri wanapata shida kubwa sana katika kuzifikia huduma hizi katika halmashauri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo nitumie fursa hii kuiomba Serikali pia iangalie changamoto hizi. Najua inazifanyia kazi, lakini naomba sasa iharakishe jambo hili, ipitie hizi halmashauri ambazo zimefanya maamuzi ya kuhamia kwenye maeneo yao ya utawala kuangalia kama kuna changamoto ili hatimaye kuweza kuzirekebisha.

Nilipokuwa jimboni kwakweli maeneo mengi hasa vijijini watu wamekuwa wakiniulizia sana kuhusu suala hili, hasa la kuhamishiwa Halmashauri Nzela; ambako sasahivi zaidi ya kilometa 100 wananchi wanahangaika kwenda kufuata huduma. Hili pengine pia limechangia hata mapato kushuka, kwa sababu wengine wanajiuliza niende kweli, nikaandikiwe kibali Nzela kule halafu nije nilipe mapato. Kwa hiyo kumekuwepo pia changamoto kubwa sana katika suala hilo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu nimepata nafasi nilikuwa naomba tu Serikali iweze kuliangalia suala hili hasa kwangu kwa sababu watu wengi sana wanapata changamoto, kama ilivyofanya katika Halmashauri ya Lindi, Mkoa wa Lindi pamoja na Mkoa wa Morogoro, iweze kufanya marekebisho basi na kwenye mikoa baadhi kama halmashauri yangu ya Geita basi Serikali iangalie itusaidie, itupatie halmashauri mpya. Kama hakuna uwezekano huo basi Serikali iangalie namna utaratibu mzuri ili wananchi waweze kupata huduma kwa karibu kwa sababu lengo la Serikali ni kuona kwamba wananchi wanapata huduma kwa karibu zaidi kuliko kwenda kufuata huduma mbali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo ninaunga mkono hoja kwa ajili ya Kamati hizi. Najua mambo mengi mazuri yamezungumzwa, nikiamini kwamba Serikali inasikiliza na kuweza kuyafanyia kazi yaliyobakia. Ahsante sana.