Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge na Utawala na Serikali za Mitaa pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Sheria Ndogo

Hon. Jitu Vrajlal Soni

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Babati Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge na Utawala na Serikali za Mitaa pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Sheria Ndogo

MHE. JITU V. SONI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana, awali ya yote naomba nichukue fursa hii kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa afya na kunipa fursa ya kuchangia leo lakini nitumie fursa hii kwa kuzipongeza Kamati zote tatu kwa kuwasilisha report ya Mwaka ambayo imeeleweka vizuri sana na tumeona maoni yao na tunaunga mkono kwa asilimia kubwa maoni yao waliyotoa lakini kuna baadhi ya meneo ningependa kuchangia ili tuweze kuboresha vizuri zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, moja; nilikuwa naomba Kamati ya Sheria Ndogo lakini pia Kamati ya Sheria wakati wanapofanya mapitio katika Sheria mbalimbali kwa sababu sasa tunatumia teknolojia basi wawe wanaweza kuweka na Bunge liangalie utaratibu wa sisi kupata hizo Sheria mbalimbali wanazopitia kwa sababu kipindi wao wanapitia Sheria hizo na Kanuni na sisi tuko kwenye Kamati zingine tunafanya shughuli zingine. Lakini kama kuna eneo ambalo ninahitaji kuja kuchangia basi niweze kujua ni lini itakuwa ni sehemu ya kupatia taarifa vizuri niweze kupitia hizo Sheria lakini ombi langu moja na nimekuwa nikilisema mara nyingi Bungeni; Sheria zote ziwe online ambazo ziko updated, Sheria na Kanuni. Leo tukitaka kufanya marejeo yoyote hizi Sheria ni ngumu kuzipata na nyingi haziko updated kwenda na wakati lakini pia Kanuni mbalimbali pia zote ziwe updated, ziwe online ili iwe rahisi kwetu sisi kupata.

Mheshimiwa Mwenyekiti, na moja katika mifano naweza kutoa; kipindi nimehangaika kuleta hapa Sheria ile na kuleta kwenye Kanuni, suala la force account tulichukua miaka minne kwa sababu kupata tu nyaraka zile mbalimbali hazikuwepo. Nimshukuru Mheshimiwa Chenge kama siyo yeye, bado hili jambo la force account ingekuwa bado ni ndoto kwetu na yeye amesaidia kutoa kwenye archive yake zile document na leo sifa kubwa ya mafanikio ya Serikali yetu ni kwa kutumia force account.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, lingine ni suala la upande wa uwekezaji kwa Waziri wa Uwekezaji pamoja na timu yake; wanafanya kazi kubwa na nzuri lakini bado naona kuna Sheria mbalimbali ambazo zinawapa ugumu wa kufanyakazi. Leo siyo kweli kwamba ni one stop center, bado changamoto ziko nyingi. Leo vibali vingi ambavyo viko pia TIC, kwa kupata tu vibali vile vya muwekezaji wa class A hatuzungumzii yule mfanyakazi ni nani lakini yule wa Class A tu bado inasumbua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa mtu amewekeza ana jengo lake lina thamani labda ya ghorofa 10 lakini baada ya miaka miwili au mitatu kupata ile Class A anahangaika kupata ile permit ya labor, bado aende kule kupata resident permit sasa mngeunganisha na ingekuwa rahisi kwamba mtu amewekeza hivi yule ukimnyima permit, hiyo mali yake inakwenda kwa nani? Lakini mbali na hilo, kuna biashara nyingine nyingi tu ambazo zimeendelea kufungwa na zimeendelea kudorora kutokana na watu kunyimwa vibali.

Leo kwa mfano; kwenye sekta ya hotel; unapomnyima mpishi wa aina mbalimbali kama ni Mchina au kama ni M-mexico unapowanyima vibali na wale watu wanakwenda kula pale kutokana na aina ya yule mtu kufanya hiyo kazi, unapomnyima kibali leo chakula kinapikwa na Jitu ambaye hajui kupika chakula Kichina kweli ni jina tu la Kichina lakini ile ladha na nini haipo. Tuangalie kwamba wale wakiwepo biashara kiasi gani inaongezeka na tunayo mifano mingi tunaweza kuwapa biashara zilizofungwa, kudorora kabisa kwa ajili ya watu kunyimwa vibali.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Sheria ya TIC inasema vile vibali vitano vya mwanzo yaani hamtamuhoji yule Muwekezaji kwa sababu hata akileta Ndugu yake, amemleta pale ili asimamie kwa ajili ya imani na kuwa na uaminifu na yule Mtu. Sasa tunapoanza kuhoji mambo mengine ya kwamba je, hiyo kazi inaweza kufanywa na Mtanzania na haiwezi kufanywa kwenye uaminifu hakuna cha Utanzania hata mimi na Ndugu yangu wote Watanzania hatuaminiani kwa hiyo inaweza kuwa Mtu mwingine ambae ninamuamini anaweza kuwa anasimamia ile mali kuliko Ndugu yangu ambae anaweza kunirusha sasa ni vizuri haya mambo tuyaangalie. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini huko zamani kwenye incentives kulikuwa na mambo mengi leo hayo yote hayapatikani. Kwa mfano; tukitaka kuwekeza kwenye sekta ya kilimo na ndiyo hiyo katrika kila mchangu wangu hapa naisemea. Leo sekta ya kilimo bidhaa yake yote siyo veritable kwa hiyo sisi tukitaka exemption kwenye capital goods hatuwezi kupata hata tukiwa kwenye TIC hatuwezi kupata kwa sababu VAT on deferment bidhaa zetu hazipo veritable kwa hiyo tunanyimwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini ya pili; unaambiwa ni lazima VAT kiwango kile kiwe ni milioni 10 na kuendelea. Milioni 10 ina maana ile bidhaa ni zaidi ya milioni 50 sasa capital goods kwa Watanzania ambao wanaanzisha viwanda vidogo vidogo kama haikufika hiyo milioni 10. Je, hawana haki ya kupata hiyo VAT on deferment hata kama bidhaa yao iko veritable? Kwahiyo, Sheria hizo zinafanya watu wengi wanaona kama TIC ni sehemu tu nyingine ya kupata vibali vingine vingi zaidi. Ni vizuri lengo la kuanzisha TIC, lengo la kuanzisha Wizara ya Uwekezaji ni kuangalia mahali tuwe na one stop center na sisi tukisema mbali na TIC, local content ni wangapi wamewekeza Watanzania TIC? Ni vizuri pia Watanzania wa kawaida wajue fursa zilizopo ili na sisi wengine ambao ni Watanzania tupate hizo fursa kupitia hizo incentives za TIC na tuweze kuwekeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini lingine naomba nichangie kwa upoande wa Serikali za Mitaa, kwa upande wa TARURA; ni vizuri tungeendelea namna ya kuongeza bajeti ya TARURA lakini pia Waziri akae, TARURA ni agency inayojitegemea pamoja na TANROADS lakini matatizo mengi tunayoyapata barabarani sasa hivi katika barabara za vijijini ni matokeo ya athari za kujengwa kwa barabara za TANROADS.

Sasa ni vizuri wale wawili wakae kwa pamoja ili waweze kutatua na kusaidia katika kuboresha amzingira mbalimbali huko chini lakini TARURA mngeruhusu kazi nyingi angalau isiyozid milioni 200 zifanywe kwa mfumo wa force account. Force account leo hii barabara inayopangiwa milioni 30 au 40 huko kijijini itachongwa kilometa mbili au tatu, Morum wataweka mita 500 na labda kujenga culvert moja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kupitia force account tunaweza kutengeneza Kilometa 10 yote iliyojazwa vizuri kwasababu kukodisha mitambo yote kwa siku moja haizidi milioni tisa. Sasa tukienda kwa mfumo huo kwa force account, barabara nyingi amabzo ni za milioni 30 tutaweza kutengeneza sehemu kubwa na hasa kipindi hiki ambayo karibu barabara zote zimeharibiwa na mvua, kwa kutumia force account tutaweza kutengeneza barabara nyingi zaidi huko vijijini kwa hiyo, nilikuwa naomba muiruhusu TARURA kwa kipindi hiki iweze kufanya hivyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia jambo lingine ni vizuri suala la blueprint, ili uwekezaji uendelee kukua wa ndani na wa nje, blueprint bidhaa ya Kitanzania kama isipokuwa na bei ambayo itakuwa ya ushindani ndani na nje, bado bidhaa za nje zitaendelea kutawala ndani ya masoko yetu. Ni vizuri suala hili lisije kidogo kiodgo, lije kwa wakati mmoja ni sawa na mtu ukitaka kupona malaria lazima uchomwe sindano ya Quinine, hivyo hivyo itakuwa na madhara mengi, mapato yanaweza kushuka kwa mwaka mmoja lakini long run tutakuwa na mapato mengi zaidi na ajira kwa watu wengi zitaongezeka kwa hiyo jambo hili la blueprint ninaomba sana lifanyiwekazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande wa Utawala Bora; nilikuwa naomba nikushauri kwamba Kamati iendelee kusisitiza customer charter iendelee kuhimizwa katika Idara zote, katika Taasisi zote za Serikali ili kila mmoja aweke wazi customer charter yake. Lakini humo humo nilikua naomba sasa tumeingia kwenye mfumo wa kidigitali na kielektroniki, kila mtu anapopeleka barua au nyaraka apewe risiti ya kielektroniki ya ku-acknowledge kwamba barua tumepokea tarehe hii na nyaraka fulani ili haya mambo ya kusumbuana Mwaka mzima hupewi majibu hayatakuwepo, mtu unakuwa na ushahidi kwamba vitu vyangu vimepokelewa na yote haya ambayo yanatakiwa kufanyiwa kazi uwe na ushahidi kwa sababu unaweza kuacha barua baada ya mwaka unaambiwa barua yako haijulikani mahali ilipo zaidi ya wewe kusainiwa kwenye kile kitabu chako ambacho siyo ushahidi wa uhakika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, kila Taasisi itoe acknowledgement ya barua au nyaraka ambazo watakuwa wanapokea ili twende na numbering na kila first come, first save ndiyo iwepo. Hiyo ndiyo italeta Utawala Bora na huduma nyingi zitaendelea kupatikana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo naomba nishukuru, ninaomba Kamati zote zinafanyakazi zao vizuri lakini haya mambo tukiyasimamia vizuri nina uhakika kwamba katika Utawala Bora lakini pia hii ya TARURA itafanya vizuri lakini kwenye uwekezaji hilo ndiyo eneo pekee na ndiyo maana Mheshimiwa Rais ameunda tena Wizara hii ya Uwekezaji ili kuweza kupata uwekezaji wa ndani na nje na tuweze kupata mafanikio makubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimpongeze Waziri wka kazi kubwa anayofanya lakini ni vizuri semina hizi pia msitutolee sisi Wabunge tu, nendeni mkatoe Wizara ya Fedha kwa sababu changamoto ya Wizara zote ziko Wizara ya fedha. Kwa hiyo, naomba huko Wizara ya fedha mtuite hata sisi tutakuja kutoa hiyo semina tukawasaidia changamoto na experience ambazo tunapata kutoka huko kwa raia na kwa Wananchi kwa sababu ndiyo wawakilishi wao, nina uhakika hizi zote tutaweza kuzitatua na tukapata mafanikio na tusiangalie kupata mapato ya moja kwa moja. Inawezekana usipate direct tax lakini indirectly ukawa unapata mara 10 ya hiyo na ajira kwa Watanzania ikawa ni kubwa zaidi. Kwa hiyo ni vizuri tukaangalia hayo.

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa Jitu.

MHE. JITU V. SONI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru wka nafasi uliyonipa, lakini nizipongeze Kamati zote tatu, naunga mkono hoja zote, ahsante sana. (Makofi)