Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hotuba ya Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania wakati wa Kufungua Bunge la Kumi na Moja

Hon. January Yusuf Makamba

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Bumbuli

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Hotuba ya Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania wakati wa Kufungua Bunge la Kumi na Moja

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS (MUUNGANO NA MAZINGIRA): Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa fursa hii. Naanza moja kwa moja kwa kutoa pongezi kwa hotuba nzuri aliyoitoa Rais wetu mpendwa, hotuba ambayo imetoa dira na mwelekeo wa Tanzania mpya. Kwa kauli ya hotuba ile na vitendo vilivyofuatia baada yake, tunaanza kuiona kabisa safari ya kupata Taifa jipya. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, safari hii haitakuwa nyepesi, itakuwa ngumu, tutajaribiwa njiani, tutakejeliwa, tutakebehiwa, tutatiwa mashaka kuhusu mwenendo wetu, kuhusu mwelekeo wetu, lakini napenda kuwasihi Waheshimiwa Wabunge na Watanzania wote kwamba tumuunge mkono Mheshimiwa Rais. Unapotaka kutengeneza keki ya mayai au chapati za mayai ni lazima upasue mayai. (Makofi)
Mheshimwa Naibu Spika, zamani kulikuwa na dawa zimeandikwa shake well before use, lazima utikise ndipo unywe dawa, ndipo ifanye kazi. Kwa hiyo, mitikisiko hii inayotokea ni sehemu ya kujenga Taifa jipya na wala watu wasipate mashaka wala wasiwasi kwamba nchi yetu inaelekea katika mwelekeo ambao sio wenyewe. Tulifika mahali tulihitaji Rais wa aina hii na tumempata na tumuunge mkono. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa nizungumze kuhusu Zanzibar. Uchaguzi ni mchakato wa kikatiba na ni mchakato wa kisheria. Wakati tulipoamua kuingia kwenye Mfumo wa Vyama Vingi, tulibadilisha Katiba yetu, tukatengeneza taasisi zitakazotusaidia kuendesha uchaguzi wa ushindani na sheria ambazo zitatusaidia kuendesha siasa ya ushindani.
Kwa upande wa Zanzibar, Katiba ya Zanzibar Ibara ya 119 iliweka Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar ambayo ilipewa majukumu na mamlaka ya namna ya kufanya na ikapewa uhuru mkubwa. Vilevile ikatungwa Sheria Na. 11 ya mwaka 1984 na ikabadilishwa mara kadhaa ili kukidhi mahitaji ya siasa ya ushindani.
Mheshimiwa Naibu Spika, Sheria ya Uchaguzi ya Zanzibar Kifungu cha 5(a) kinasema kwamba; “Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar ina jukumu la usimamizi wa jumla wa mwenendo wa uchaguzi.” Maana yake ni nini? Maana yake ni kwamba Tume imepewa nguvu na Mamlaka ya Kikatiba na Kisheria kufuta matokeo ya uchaguzi pale inapojiridhisha kwamba sababu na kasoro zilizojitokeza kwenye uchaguzi haziwezi kutoa matokeo yanayoakisi utashi wa watu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, mamlaka ya Tume kuhusu kufuta uchaguzi wa Zanzibar hayana mashaka yoyote; hayana mashaka ndani ya Katiba, wala ndani ya sheria. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, Tume ilitoa sababu nane za kufuta matokeo. Sababu mojawapo ikiwa ni malalamiko ya vyama vya siasa; ikiwa ni mgombea mmoja kujitangaza kwamba ameshinda ambapo ni kinyume kabisa na sheria, jambo ambalo lingeweza kupelekea machafuko na mtafaruku. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, Tume ilikaa katika Mkutano wake wa tarehe 28 Oktoba, 2015 na kupitisha uamuzi wa kufuta matokeo yale.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye Katiba ya Zanzibar upo utaratibu wa Tume kufanya maamuzi. Ibara ya 119(10), kwamba Tume itakapokaa maamuzi yake ni halali anapokuwepo Mwenyekiti au Makamu na wajumbe wengine wanne. Vilevile Sheria ya Uchaguzi ya Zanzibar inatamka kwamba kanuni, maelezo na matangazo yote ambayo Tume ina mamlaka ya kutunga au kutoa, yatahesabika kwamba yametungwa kisheria kama yamewekwa sahihi na Mwenyekiti wa Tume au Mkurugenzi wa Uchaguzi. (Makofi)
Tangazo lililotolewa na Mwenyekiti wa Tume ya Uchaguzi wa Zanzibar kufuta matokeo kwa mujibu wa Sheria ya Uchaguzi ya Zanzibar ni tangazo halali kisheria. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, vile vile baada ya hapo tangazo lile, kama invyohitajika kwenye Katiba, liliwekwa kwenye Gazeti la Serikali kama hati ya kisheria namba 130 kwenye GN Namba 6587 ya tarehe 6 Novemba, 2015. Kwa hiyo, mjadala wa mamlaka ya Tume ya Uchaguzi kuhusu kufuta matokeo yale haupaswi kuwepo kwa sababu mamlaka yale inayo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, tarehe 21 Januari , 2016 Tume iliamua na kutangaza tarehe ya kurudiwa kwa uchaguzi. Kama Katiba inavyoelekeza katika Ibara ya 119 (10) kwamba maamuzi ya Tume ili yafanyike, ni lazima akidi itimie na lazima wengi wakubaliane na uamuzi ule.
Katika kikao cha Tume cha tarehe 21 mwezi wa Kwanza cha kuamua kutangaza kurudiwa kwa uchaguzi, akidi ilitimia na wengi walikubaliana na uamuzi ule. Kwa hiyo, uamuzi ule ni halali kisheria na Kikatiba. Katiba ya Zanzibar inasema kwamba hakuna mwenye mamlaka, hata Mahakama ya kuhoji au kuchunguza maamuzi yanayotolewa na Tume kuhusu uchaguzi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, wote tunajua kwamba uamuzi ule ulikuwa halali. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nchi yetu lazima iendelee kuwa nchi ya amani, ni lazima iendelee kuwa nchi ya utulivu na msingi wa amani na utulivu ni kuheshimu Katiba na sheria ambazo tumezitunga sisi wenyewe. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine linalozungumzwa ni kwamba kama matokeo ya uchaguzi ulioendeshwa na Tume Zanzibar yamekubalika na kwamba kama tuna Wabunge kutoka Zanzibar humu, iweje basi uchaguzi wa Zanzibar uharibike na matokeo yafutwe? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, chaguzi zile ni mbili tofauti, zimefanyika kwa Katiba mbili tofauti, Tume mbili tofauti, sheria mbili tofauti, madaftari mawili tofauti, utaratibu wa kuhesabu kura tofauti, wasimamizi tofauti, hata wino kuna wino wa NEC na wino wa ZEC. Kwa hiyo, haishangazi wala haistaajabishi kwamba uchaguzi mmoja ukaharibika mwingine ukawa halali. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kinachounganisha chaguzi hizi mbili ni kitu kimoja tu ni kwamba zilifanyika siku moja, lakini chaguzi hizi ni tofauti. Hoja kwamba kama uchaguzi huu ulikwenda sawa na mwingine siyo sawa, haina mashiko. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kuwasihi wenzetu ambao wameamua kutafuta suluhu hii kwa nje ya Katiba na nje ya sheria, wanakosea na kwamba hakuna miongoni mwetu ambaye ana uwezo wala mamlaka ya kuiamrisha Tume ifanye kingine nje ya Katiba na nje ya sheria. Viongozi wa nchi yetu akiwemo Rais wetu, wamefanya jitihada kubwa na za kutosha kuhakikisha kwamba nchi yetu inaendele kuwa ya amani na kwamba maamuzi haya ya Tume ambayo hatuna mamlaka nayo, hayapelekei katika vurugu na mtafaruku. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, wajibu wa kulinda amani na umoja wa nchi yetu ni wajibu wa viongozi wa kisiasa. Maamuzi ambayo viongozi wa kisiasa wa Zanzibar watayachukua, kama yatakuwa ni maamuzi ya kusababisha vurugu na fujo na mtafaruku, basi damu ya Watanzania itakuwa mikononi mwao.
Sisi kwa upande wa Chama cha Mapinduzi na kwa upande wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, wajibu wetu ni kuhakikisha kwamba nchi yetu ianendelea kuwa ya amani, utulivu na usalama. Tunao wajibu wa kuheshimu maamuzi ya Tume na hicho ndicho tutakachofanya. Hatuna mamlaka ya kuiamrisha Tume ifanye vinginevyo kinyume na utaratibu wake. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, niliona niseme hayo. Yapo mengine yamezungumzwa yakiwemo masuala ya bomoa bomoa, tutayazungumza wakati wa michango ya kuchagia kwenye Mpango. Nashukuru sana kwa nafasi hii. (Makofi)