Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge na Utawala na Serikali za Mitaa pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Sheria Ndogo

Hon. Angellah Jasmine Mbelwa Kairuki

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Nominated

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge na Utawala na Serikali za Mitaa pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Sheria Ndogo

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU, UWEKEZAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, niungane na Waheshimiwa Wabunge wengine waliounga mkono hoja hii kipekee nipongeze sana Kamati yetu ya Katiba na Sheria kwa kazi nzuri waliyoifanya lakini kwa taarifa nzuri waliyoiandaa nishukuru kwa namna ambavyo wamekuwa wakishirikiana nasi pamoja na Mheshimiwa Waziri mwenzangu Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Bunge, Kazi, Ajira, Vijana na Wenye Ulemavu Mheshimiwa Jenista kwa kweli wamekuwa wakitupa ushirikiano mzuri sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ningependa kuchangia masuala machache la kwanza kuendelea kuwahakikishia Watanzania kwamba kwa upande wa uhamasishaji na kuvutia mitaji ya uwekezaji tunaendelea kufanya jukumu hilo na wawekezaji wamekuwa wanakuja kwa wingi na kwa mwaka uliopita tumeweza kupata takribani uwekezaji wenye mtaji wa zaidi ya Dola Bilioni 2.8 na tunaendelea kufanya hivyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kulikuwa kuna hoja nadhani ya Mheshimiwa Jitu ilijitokeza kwamba tuone namna gani tunaendelea kujenga wawekezaji wazawa zaidi jukumu hilo tunaendelea kulifanya na ukiangalia katika Usajili wa Miradi ile ambayo imesajiliwa katika Kituo cha Uwekezaji Tanzania zaidi ya asilimia 48 ilikuwa ni Miradi ya wazawa na tunaendelea kuhamasisha na tunatoa rai wazawa wengi zaidi ikiwezekana waweze kusajili Miradi yao TIC. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kulikuwa kuna hoja ya kutokuwa na uratibu au kutokuwa na ushirikiano baina ya Wizara na Taasisi nipende tu kusema kwamba tunaendelea kushirikiana vizuri na tutaendelea kuboresha namna ambavyo tunaendelea kuratibu lakini vilevile kushughulikia masuala mbalimbali ya Uwekezaji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kulikuwa kuna hoja ya ucheleweshwaji wa huduma na Kamati imeweza kutoa ushauri mzuri sana ya kuweza kutumia zaidi huduma za kielektroniki nipende kusema tu kwamba tumeanza na kwa kuanzia kwa sasa walau katika Idara yetu ya kazi wameunganishwa katika Mfumo wetu wa Kituo cha kazi kupitia Mifumo ya Vibali vya Kazi na kwa sasa vingi vinatolewa pia kwa mfumo wa elektroniki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile kwa sasa pia tumeandaa mfumo kwa ajili ya kuweza kutoa mrejesho kutoka kwa wawekezaji na wafanyabiashara lakini vilevile kwa Wafanyabiashara wetu na wawekezaji kuweza kutoa malalamiko yao kupitia mfumo wa kielektroniki na ni jukumu ambalo tunashirikiana Ofisi ya Waziri ya Mkuu, CPSF pamoja na Baraza letu la Biashara la Taifa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kulikuwa kuna hoja ya suala zima la utelekezaji wa blueprint nipende tu kuwahakikishia Waheshimiwa Wabunge Ofisi ya Waziri Mkuu kwa kushirikiana na Wizara ya Viwanda na Biashara ambayo ndiyo wamepewa jukumu hili, Wizara ya Viwanda na Biashara tayari wameshaandaa mapendekezo na tunaamini mchakato ndani ya Serikali utakapokamilika basi mapendekezo hayo kwa ajili ya kutunga Sheria ya Uwezeshaji wa Biashara au business facilitation Act yatawasilishwa Bungeni mapema. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile kwa upande wa Sheria yetu ya Uwekezaji ambayo kimsingi tutaupitia upya muundo wa TIC lakini kuangalia masuala mbalimbali ya kitaasisi na namna ambavyo tunashirikiana na Taasisi nyingine. Vilevile mipaka ya Taasisi moja na Taasisi nyingine katika kuvutia na kuhamasisha uwekezaji na masuala mazima ya uratibu wa Uwekezaji nayo ni masuala ambayo tunakusudia kuyaingiza katika Sheria hiyo ambayo itakuja humu bungeni muda si mrefu na tutaomba ushirikiano wenu Waheshimiwa Wabunge. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kulikuwa kuna hoja pia la ukosefu wa miundombinu wezeshi na ya msingi kwa ajili ya uwekezaji ni jambo ambalo tumeliona na ni kweli na tayari tunashukuru Ofisi ya Waziri ya Mkuu kwa kushirikiana na Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa tumeendelea kuzihamasisha halmashauri zetu kutenga maeneo ambayo yatakuwa na miundombinu ambayo inakidhi lakini vilevile miundombinu ya umeme, maji na Mawasiliano maeneo ambayo yatakuwa yamelipiwa fidia hayana mgogoro lakini yaliyopimwa na yaliyopangwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika eneo hili pia ilijitokeza hoja ya ucheleweshwaji wa suala zima la uhavilishaji kutoka katika ardhi ya Kijiji kwenda katika ardhi ya jumla ni eneo ambalo ni kweli limekuwa ni changamoto wakati mwingine Mwekezaji amekuwa akitumia miaka mitatu mpaka miaka minne kwa sababu ya mlolongo ambao unahitajika katika uhavilishaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni hatua ambazo kutokana na mfumo wetu kama Tanzania wa Umiliki wa ardhi, ardhi ya Kijiji ukomo wake kuweza kuiuza ni eka hamsini tu. Kwa hiyo, kwenye hili hatuwezi kuliepuka lakini tunashukuru Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi imeweza kutoa maelekezo kwa halmashauri zote kuweza kuona ni kwa namna gani wataandaa mipango ya matumizi bora ya ardhi ili waweze kuainisha maeneo yanayohitajika kwa uwekezaji na tunaamini halmashauri zetu na vijiji zitakapofanya hivyo basi wataweza kupunguza muda wa uhavilishaji lakini vilevile itatuhakikishia kuwa na uhakika wa ardhi ya uwekezaji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nipende tu kuwatoa hofu Wana Vijiji ukiangalia kwa kila Kijiji kuweka mpango wa matumizi bora ya ardhi kwa takwimu kama nitakuwa sijakosea haizidi kati ya milioni sita mpaka milioni nane. Kwa hiyo, ni muhimu waweze kuona umuhimu wa kutenga fedha kupitia mapato mbalimbali ambayo wanayapata ili kutekeleza jukumu hili ambalo ni la muhimu sana kwa ajili ya kuwa na uhakika wa utatuzi wa Uwekezaji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile kulikuwa kuna hoja ya mwingiliano wa majukumu ya Kitaasisi kama nilivyoeleza kupitia Sheria ile ya Uwezeshaji wa Biashara au business facilitation tunaamini suala hili pia kwa kiasi kikubwa litaweza kuondoka vilevile kwa sasa Serikali inaendelea kupitia majukumu ya baadhi ya Taasisi ili kuona ni kwa namna gani tutaweza kuondoa mwingiliano katika usimamizi vilevile kuona ni kwa namna gani tutaweza kupunguza muda na gharama kwa ajili ya uendeshaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tayari tumeshaanza kwa TBS pamoja na TMDA tutaendelea vilevile kufanya kwa Taasisi nyingine za Serikali. Kulikuwa kuna hoja nyingine kuhusiana na kupunguza tozo tayari ndani ya miaka miwili Wizara ya Fedha na Mipango tuliona hapa kupitia Sheria ya Fedha imeleta zaidi ya tozo 163 kwa mwaka 2017/2018 tozo zaidi 109 ziliweza kufutwa lakini kwa 2018/2019 tozo zaidi ya 54 zimeweza kufutwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii ni hatua nzuri na tunaamini kadri tunavyoendelea na Bajeti ya Serikali basi Wizara ya Fedha na Mipango itakuwa ikiendelea kufanya hatua hiyo muhimu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile kulikuwa kuna hoja ya halmashauri zetu za wilaya pamoja na mikoa kuweza kutumia na kuutekeleza muongozo uliotolewa TNDC katika kufanya majadiliano kati ya Sekta ya Umma na Sekta Binafsi tunashukuru bahati nzuri nimefanya Mikutano kwa kushirikiana na Mawaziri wengine wa kisekta zaidi ya Mikoa saba na tumekuwa tukipata ushirikiano mzuri sana kutoka TNDC vilevile kutoka katika mikoa na halmashauri zetu na wamekuwa wakisisitizwa kuona ni kwa namna gani wanaweza kutekeleza mwongozo huo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru lakini niendelee kuwahakikishia Waheshimiwa Wabunge tutaendelea kuvutia na kuhamasisha Uwekezaji muhimu tu kwa halmashauri zetu Wabunge na wananchi kwa ujumla waweze kutambua manufaa ya Uwekezaji kwa ajili ya Taifa letu nakushukuru. (Makofi)